MWANAFUNZI ATOWEKA NYUMBANI BAADA YA KUKATALIWA ASIHAME SHULE – WAZAZI WAOMBA MSAADA KUMTAFUTA
KENYA: Stephanie, mwanafunzi wa darasa la 10 katika Shule ya Upili ya Wasichana ya Sacred Hearts Kyeni, alitoweka mnamo Aprili 28, wakati tu wenzake walipokuwa wakiripoti shuleni.
Akiongea na TUKO.co.ke, mamake Stephanie aliyehuzunika, Cecily Wangari, alisema bintiye alitoweka mara mbili katika muda wa chini ya wiki moja.
Alieleza kwamba Stephanie alikuwa ameonyesha nia ya kuhamisha shule, lakini familia ilisita kuruhusu mabadiliko hayo.
Muda mfupi baadaye, alitoweka lakini baadaye akapatikana Murang’a.
“Kwa mara ya kwanza alitoweka mnamo Aprili 28 lakini akapatikana Murang’a nyumbani kwa nyanyake. Alimwambia kwamba angempa pesa za kurejea nyumbani tukichunguza suala lake la shule,” Cecily alisema.
Kwa kusikitisha, kijana huyo alikaa kwa siku mbili nyumbani kwa nyanya yake na kuondoka wakati yeye hayupo, akiacha familia yake ikiwa na wasiwasi tena.
Cecily alisema tangu wakati huo wamewasilisha ripoti ya mtu aliyepotea lakini bado hawajampata. Pia wameanzisha upekuzi mkali kimwili na mtandaoni, lakini bado hajulikani aliko.
“Hatujui alipo, na tunatamani sana kumtafuta, tafadhali nisaidie kumtafuta mtoto wangu, na popote alipo arudi nyumbani,” alisema.
Zaidi ya wiki tatu baadaye, msichana mdogo bado hayupo.
Familia yake imeomba msaada, ikimtaka yeyote aliye na taarifa kuhusu mahali alipo kuripoti katika kituo cha polisi kilicho karibu au kuwasiliana nao.
Chanzo: TUKO

