NILIJIUNGA NA DINI YA SHETANI
ONYO: Wakubwa tu, kuanzia Miaka 18, ndio wasome hii Hadithi
Sehemu Ya 9
ILIPOISHIA:
Niliposikia kuna meditation ya mshumaa, shauku ndani ya moyo wangu iliongezeka maradufu, nikawa nasubiri nione inavyofanywa.
Baada ya dakika chache, tulielekezwa wote kuutazama ule mshumaa uliokuwa unawaka katikati yetu, tukaambiwa tusipepese macho na kuelekeza akili zote kuutazama mshumaa ule. Aliyekuwa anatoa maelekezo alisisitiza kuwa tutazame ile sehemu ya juu iliyokuwa inawaka, akasema tukishautazama kwa dakika kadhaa, atatoa ishara maalum ambapo wote tutatakiwa kufumba macho.
Tulianza kuutazama mshumaa ule huku kila mmoja akipumua kwa uhuru, ukimya wa ajabu ukatanda mle ndani. Nilikuwa makini kuhakikisha sikosei hata kidogo, nikawa nautazama ule mshumaa huku nikiwa na hamu kubwa ya kuona kitakachotokea.
Baada ya kuuangalia kwa dakika kadhaa, nilianza kuona hali ambayo nilishindwa kuitafsiri. Watu wote waliokuwa mle ndani sikuwaona tena, nikawa nahisi kama nilikuwa peke yangu chumba kizima, jambo ambalo halikuwa kweli. Baada ya muda, yule aliyekuwa anatoa maelekezo alitoa ishara kama alivyokuwa ameeleza awali, watu wote tukafumba macho.
Kingine kilichonishangaza ni kwamba hata baada ya kufumba macho, niliendelea kuuona ule mshumaa ukiwaka kupitia kile ambacho baadaye nilielezwa kuwa ni jicho la tatu.
Nilitulia katika hali ile kwa muda mrefu, nikaanza kujihisi kama nahama kifikra kutoka pale nilipokuwa nimekaa na kwenda sehemu ambayo siijui.
Sikuona kitu chochote zaidi ya giza nene huku ule mshumaa ukizidi kufifia kabla ya kupotea kabisa kwenye fikra zangu. Nikawa naendelea kuvuta pumzi ndefu na kuzitoa kupitia mdomoni mwangu.
Nikiwa kwenye hali hiyo, mara nilianza kuona picha ya nyumbani kwetu Tukuyu, nikawa naiona nyumba yetu jinsi ilivyo kutoka pande zote. Niliiona kutokea juu, kutoka kushoto, kulia, mbele na nyuma kisha nikajihisi kama nimeingia ndani.
Nikawa nawaona baba na mama wakiwa sebuleni wanatazama runinga.
Nikawaona pia ndugu zangu wengine wakiendelea na kazi zao za kawaida pale nyumbani, kimoyomoyo nikawa natabasamu kwani licha ya ukweli kwamba nilikuwa mbali sana na nyumbani, kiakili nilikuwa nimefika.
“Na huo ndiyo mwisho wa meditation ya mshumaa kwa leo,” nilisikia sauti ikisema, nikashtuka sana kiasi cha kuwashtua watu waliokuwa pembeni yangu. Kilichofanya nishtuke ni kwamba tayari nilishakuwa kwenye ulimwengu mwingine kiasi cha kusahau kabisa kwamba nilikuwa nafanya meditation.
Nilijiona kama nipo nyumbani Tukuyu kumbe katika hali halisi nilikuwa pale kwenye kile kituo, Kimara Kona jijini Dar es Salaam. Nilijifikicha macho huku nikijihisi aibu kwa jinsi nilivyokuwa nimeshtuka, nikawa nawatazama kwa macho ya wizi wale watu niliokuwa nimekaa nao ambao wote walikuwa wakinitazama.
“Haya sasa umefika muda wa kila mmoja kutueleza katika hii safari yetu ya meditation ameona nini. Tunaanza na ndugu yetu mgeni, naona umeshtuka kuliko kawaida, hebu tuambie umeona nini,” alisema yule kiongozi huku akinioneshea ishara mimi. Nilijiumauma kidogo kisha nikaanza kueleza nilichokiona.
Karibu wote walicheka sana walipogundua kilichonifanya nishtuke kiasi kile, zoezi la kila mmoja kueleza alichokiona likaendelea mpaka wote walipoisha. Nilichokibaini ni kwamba, japokuwa wote tulikuwa tumekaa sehemu moja, wakati wa meditation kila mmoja alisafiri kivyake na kwenda sehemu tofautitofauti.
Baada ya kumaliza zoezi lile, tuliekezwa kuwa muda wa kuendelea na masomo ya kawaida ya utambuzi ulikuwa umewadia, yule kiongozi akatuelekeza kuwa kila mmoja aelekee kwenye darasa lake. Watu wote wakainuka na kuelekea kwenye madarasa yaliyokuwa mlemle ndani ya jengo.
Nilibabaika kidogo kwani sikujua mimi napaswa kuingia darasa gani, nikaelekezwa kuwa nilitakiwa kwenda kwenye darasa la wanafunzi wanaoanza masomo kama mimi, nikaenda kuungana na wenzangu kadhaa kisha mwalimu akaanza kufundisha.
Kabla ya kuendelea na kipindi, tulitambulishana tena kisha wakawa wanakumbushana walichojifunza kipindi kilichopita.
“Somo la leo linahusu uchawi, tutajifunza maana ya uchawi, jinsi unavyoweza kukupata na jinsi ya kujikinga,” alisema mwalimu huku akiandika ubaoni kwa kutumia ‘marker pen’.
Nilikaa vizuri kwenye kiti changu na kuanza kusikiliza kwa umakini huku nikiandika dondoo muhimu kwenye kijitabu changu kidogo.
“Uchawi ni kitu gani? Hili ni swali gumu sana kuliko unavyofikiri. Tumezoea sana kusema kuna uchawi au hakuna lakini mtu anapotuuliza huo uchawi ni kitu gani ndipo tunapogundua kuwa tumekuwa tukizungumzia kitu ambacho hatukijui.
“Je, uchawi ni kuwa na vifaa ambavyo mtu anaweza kuvitumia kutengeneza nguvu yenye kuweza kusafiri na kwenda kumdhuru amtakaye? Je, uchawi ni uwezo wa mtu kuweka sumu kwenye maji au chakula na watu wakafa polepole au ghafla?
“Je, uchawi ni mbinu ambazo mtu anaweza kuzifanya na kusababisha mwingine afukuzwe kazi bila sababu ya msingi? Je, ni uwezo wa mtu kumghilibu mke au mume wa mwenzake hadi akatoka kwenye ndoa yake halali?
“Uchawi unatajwa sana kwenye matukio mengi kama kuugua, kufukuzwa kazi, kufa, kuachwa na mpenzi, mke au mume, ajali na mambo mengine kama hayo lakini je, tunaujua huo uchawi?” alisema mwalimu na kuanza kutuuliza mmojammoja tueleze jinsi tunavyoufahamu uchawi.
Kila mmoja alieleza alivyokuwa anaufahamu uchawi lakini nilichobaini, wengi hawakuwa wakijua ni kitu gani zaidi ya kuonesha hofu juu ya jambo hilo. Hata
mimi nilikuwa miongoni mwa wasiojua chochote, kilichonisaidia ni kwamba
nilishawahi kusoma kwenye kile kitabu changu kilichoandikwa na marehemu
Munga.
Baada ya majadiliano, kila mmoja akiwa ameshaeleza japo kwa kifupi alivyokuwa anaujua uchawi, mwalimu alitutaka sote tutulie ili atueleze jambo ambalo hatukuwa tukilijua, akaanza: “Neno uchawi limekuwa likitumika
na kuhusishwa na mambo mengi yanayotokea katika maisha ya kila siku
ya mwanadamu kwa karne nyingi sana.
Inaaminika kuwa uchawi ulikuwepo duniani hata kabla ya kuzaliwa kwa Kristo.
“Katika vitabu vitakatifu, uchawi umezungumziwa mara nyingi na umekuwa ukihusishwa na matukio mengi. Maneno kama pepo wachafu, mizimu na matambiko kila yanapotumika, huwakilisha uchawi.
“Licha ya kuwa dhana hii ni kongwe na imekuwepo kwa miaka mingi, bado
kumekuwa na ugumu mkubwa katika kuelezea huo unaoitwa ‘uchawi’ ni
kitu gani hasa. Sote hapa tumekuwa tukilisikia sana neno hili ‘Uchawi’ na
bila shaka tumeshashuhudia matukio ambayo tuliambiwa na tukaamini kuwa
yamesababishwa na uchawi.
“Uchawi umekuwa ukihusishwa katika matukio kama vifo, mtu kuugua ugonjwa wa ajabu, kupata ajali katika mazingira ya kutatanisha, kufukuzwa kazi, kuugua kichaa, ndoa kuvunjika, kuachwa na mpenzi, kutopea kwenye tabia hatarishi kama ulevi au matumizi ya madawa ya kulevya, kufeli mitihani, kufilisika, biashara kudorora na kufa.
“Katika maeneo ambayo mpaka leo imani hii bado inapewa nguvu, uchawi
umekuwa ukitajwa karibu katika kila tukio linalotokea. Ni nadra sana kusikia jambo fulani limetokea au limempata mtu bila ya uchawi kutajwa. Katika maeneo kama Bagamoyo, Tanga, Sumbawanga, visiwani Zanzibar na sehemu nyinginezo, imani hii bado imekuwa ikipewa nguvu kubwa sana
katika jamii.
“Pamoja na kuwa uchawi umekuwa ukitajwa katika mambo mengi kwa maelfu
ya miaka, bado ni wachache sana kati yetu wanaoweza kueleza kwa ufasaha maana ya uchawi.
“Wengi wetu tumeendelea kuamini, kuogopa na kuzungumzia juu ya kitu ambacho hatukifahamu kabisa. Wataalamu wengi wamekuwa wakijaribu
kwa miaka mingi kufanya utafiti juu ya maana, asili na namna uchawi
unavyofanya kazi.
“Licha ya jitihada hizo za kuutafuta ukweli juu ya uchawi kuanza karne nyingi zilizopita, mpaka leo bado hakuna majibu ya kuridhisha juu ya uchawi. Tumezoea sana kusema kuna uchawi au hakuna uchawi, lakini tunapoambiwa tuelezee huo uchawi ni kitu gani, wengi huwa tunashindwa kutoa majibu.
“Hapa niliwapa nafasi ya kila mmoja kueleza namna anavyoufahamu uchawi lakini wenyewe mmeshuhudia mlivyokuwa mnajikanyaga. Hii ni kwa sababu uchawi hupimwa kwa matokeo na siyo sifa nyingine.
“Tunasema huu ni uchawi kwa sababu tumeona jambo fulani likitokea au kufanyika kwa njia ambayo hatuwezi kuielezea, au katika namna ambayo
hatukuitegemea, njia ambayo hatuwezi kuielezea au kwa njia ambayo inaashiria
ubaya au uhasidi. Nje ya matokeo, hakuna uchawi.
“Huwezi kukuta uchawi ukiwa umetundikwa au ukiwa umewekwa mahali, bali unaweza kuuona ukifanya kazi. Kama utakuta hirizi, tunguri au mapembe yenye manyoya mahali, huwezi kusema huo ni uchawi, bali ni vifaa ambavyo hutumika kwa shughuli mbalimbali. Vinaweza kuwa vinatumika kwa uchawi au kwa shughuli nyingine lakini siyo kwamba vyenyewe vinaweza kuwa uchawi.
“Kwa kuwa uchawi umekuwa ukitajwa karibu katika kila jambo tangu karne nyingi zilizopita, ni dhahiri kuwa kweli upo na unafanya kazi. Lakini kwa nini ufanye kazi kwenye maeneo yote hayo?
Kwenye kufa, kuugua, kufilisika, kupoteza hamu ya tendo la ndoa, kuishiwa nguvu za kiume, kushindwa kufanikiwa maishani na kila mahali? Ni kwa sababu ni matokeo na siyo kitu halisi tunachoweza kukishika au kukiona na kusema huu ndiyo uchawi.
“Uchawi ni matumizi mabaya ya nguvu zisizoonekana, zinazozalishwa na
binadamu kutaka kumuonea, kumtishia na kumdhuru binadamu mwingine. Nguvu hizi huzalishwa kwa mawazo, vitendo na kauli.
“Baada ya kuzalishwa, nguvu hizi hurushwa kwenda kwa mtu au kitu kilichokusudiwa na zinapomuingia mhusika, husababisha madhara makubwa
yanayoonekana na yasiyoonekana.
“Ni ukweli usiopingika kuwa kuna idadi kubwa ya binadamu wenye uwezo
wa kuzalisha nguvu zenye uwezo wa kuwadhuru wengine. Inawezekana
anayezalisha nguvu hii mbaya yenye kudhuru (uchawi) akawa anajua
anachokifanya, lakini pia kuna wakati mtu anakuwa hajui kuwa anazalisha nguvu mbaya inayodhuru.
“Kwa asili, kila binadamu ana uwezo wa kuzalisha nguvu kutoka ndani yake, na
anaweza kuishi kwa sababu yuko ndani ya nguvu. Mawazo yetu yanazalisha nguvu, kauli zetu zinazalisha nguvu na matendo yetu yanazalisha nguvu.
“Kuna watu ambao wana nguvu za moja kwa moja ambazo wamezaliwa nazo,
wakati wengine wana nguvu za kunuiza ambazo huwa wanajifunza.
“Nguvu yoyote inayozalishwa na binadamu inaweza kuwa katika sura ya
uharibifu au uadilifu. Inategemea ni nguvu gani na lengo la kuizalisha ni ipi. Nguvu tunazozizalisha zina matokeo ambayo tunaweza kuyathibitisha.
“Nguvu zisizoonekana ambazo ndizo zenye nguvu kubwa kuliko zinazoonekana hujibainisha kwa matokeo yake. Kwa leo tuishie hapa, kuna yeyote mwenye swali?” aliuliza mwalimu, sote tukabaki tukitazamana mle darasani. Nilianza kuhisi kama kichwa kinaniuma kwa aliyoyasema,
nikashusha pumzi ndefu na kuanza kutafakari.
Sehemu Ya 10
ILIPOISHIA:
“Panda magari ya kwenda Temeke, yale yenye mistari ya kijani, mwambie kondakta akushushe kituo kinachoitwa Chang’ombe Maduka Mawili, ukishuka tembea kwenda mbele hatua kadhaa, utaona bango limeandikwa Path Society mkono wako wa kushoto.
Ukiingia muulize mtu yeyote utaratibu wa pale, naamini watakusaidia,” alisema yule mwalimu, nikamshukuru na kumuahidi kuwa nitajitahidi kufanya hivyo. Siku kadhaa baadaye, nilipata upenyo wa kutoka, nikaaga pale nyumbani kwamba naenda Kariakoo kununua nguo, nikaruhusiwa na moja kwa moja nikaianza safari ya kuelekea Chang’ombe.
SASA ENDELEA…
“Konda nishushe maduka mawili!” nilisema kwa sauti kubwa.
“Sogea mlangoni na nauli yako mkononi,” alijibu kwa sauti ya kilevi, nikawaomba abiria wenzangu wanipishe, nikasogea mlangoni. Baada ya muda gari likapunguza mwendo na kusimama, nikamlipa konda nauli na kuteremka.
Akilini mwangu nilitegemea nikishuka nitayaona maduka mawili makubwa kama kituo hicho kilivyokuwa kinaitwa lakini haikuwa hivyo. Kilikuwa ni kituo cha kawaida, upande wa pili wa barabara kukiwa na shughuli mbalimbali zinaendelea.
Nilianza kujiuliza hicho kituo cha Path Society kipo upande gani? Kumbukumbu zangu zilinifanya nizingatie maelekezo niliyopewa na yule mwalimu, nikatembea mita kadhaa mbele na kutazama upande wangu wa kushoto. Nilijikuta nikitabasamu baada ya kuona bango kubwa.
“Ndiyo hapa, siamini kama nimefika. Hakuna mtu anayenijua atakayeniona tena nikiingia wala kutoka, lazima nifikie hatua ya juu sana ya kujitambua na hakuna mahali pengine ninapoweza kupata maarifa hayo zaidi ya hapa,” nilijisemea huku nikitembea kwa hatua fupifupi.
“Karibu kijana, karibu sana,” mwanamke wa makamo alinipokea kwa bashasha tele, akanishika mkono na kuanza kuniongoza kuelekea ndani. Bila shaka aliniona kuwa mgeni wa mazingira yale kwa jinsi nilivyokuwa nababaika.
“Leo ndiyo mara yako ya kwanza kuja hapa?”
“Ndiyo mama.”
“Unaitwa nani na unatokea wapi?”
“Naitwa Mkanwa Sebastian au Saba kama wengine wanavyoniita. Natokea
Tukuyu lakini kwa sasa naishi Kimara.”
“Ooh! Karibu sana, jisikie upo nyumbani,” alisema na kuniongoza moja
kwa moja mpaka upande wa nyuma wa jengo lile, kulipokuwa na madarasa. Alimfanyia ishara mwalimu aliyekuwa anafundisha kwenye moja kati ya yale madarasa, akatoka nje na kumsikiliza ambapo alinitambulisha kwake kisha akaondoka na kutuacha mimi na mwalimu.
“Karibu ndani ujiunge na wenzako,” alisema mwalimu na kunishika mkono, nikaingia darasani na kwenda kukaa sehemu niliyoelekezwa kukaa. Mle ndani kulikuwa na watu wengi, wakubwa kwa wadogo, Wazungu kwa Waafrika, Waarabu kwa Wahindi na wanawake kwa wanaume. Nilibaki nimepigwa na butwaa kwani sikutegemea kukutana na watu kama wale nao wakijifunza elimu ya utambuzi.
“Tumepata mgeni, anaitwa Mkanwa na tutakuwa tukijifunza naye mambo mbalimbali kuanzia leo. Karibu sana Mkanwa,” alisema mwalimu, nikaitikia kwa sauti ya kutetemeka:
“Ahsante.”
“Ok, tunaendelea na mada yetu kama ilivyoandikwa ubaoni,” alisema mwalimu
huku akioneshea mahali palipokuwa pameandikwa THAMANI YA BINADAMU.
Mwalimu aliendelea kueleza kuwa watu wengi wanashindwa kuishi kama walivyokusudiwa kuishi kutokana na tatizo la kushindwa kutambua thamani zao.
Nilivutiwa sana na mada ile, nikakaa vizuri kwenye kiti na kutega masikio kwa umakini wa hali ya juu, mwalimu akawa anaendelea kufundisha kwa staili ya mazungumzo.
“Ni ukweli ambao unashangaza kwamba binadamu walio wengi duniani hawafahamu wao ni akina nani au wao ni nini hivyo wanaishi maisha yaliyogubikwa na giza na kushindwa kufahamu thamani zao.
“Utafiti wa kitaalam unaofanywa na watu mbalimbali umebaini kuwa watu wengi wamekuwa na uelewa mkubwa kuhusu vitu mbalimbali kama vile kompyuta, magari na mashine za aina mbalimbali lakini hawafahamu chochote kuhusu wao.
“Hii ndiyo sababu kubwa inayomfanya binadamu awe kiumbe wa ajabu. Nitakapokwambia kuwa karibu asilimia sabini na tano ya watu wote wanaoishi
duniani leo hii, hawajifahamu wala kutambua kuwa wao ni akina nani, au wao ni nini, hivyo wanaishi gizani, bila shaka utabisha. Kwa haraka haraka huwezi kuelewa ninazungumzia nini.
“Labda kabla ya kufika mbali zaidi niwaulize wote ambao mpo ndani ya hili darasa; wewe ni nani? Wewe ni nini na maisha ni nini? Hili ni swali ambalo ukiweza kulijibu basi haumo kati ya wale asilimia sabini na tano wasiojielewa wao ni nini na wanaoishi gizani.
“Tunaanza na mzee pale mbele kisha kila mmoja ataeleza anavyofahamu kuhusu yeye na thamani yake,” alisema mwalimu na kuanza kutusimamisha mmoja baada ya mwingine mle ndani. Majibu waliyokuwa wanayatoa watu wengi mle ndani, yalinishangaza hata mimi. Ni kweli watu wengi walikuwa hawajui wao ni nini na thamani yao ni ipi zaidi ya kuishia kutaja majina yao, kazi zao au elimu walizokuwa nazo.
Mwalimu alipofika kwangu, aliniruka kwa maelezo kuwa kwa sababu nilikuwa nimeikuta mada njiani, bado nisingeweza kulijibu swali lile kwa ufasaha. Japokuwa nilikuwa na uelewa kwa kiasi fulani, nilikubaliana naye na kunyamaza kimya, wenzangu wakaendelea kujikanyaga.
Baada ya kila mmoja kujieleza kwa kadiri alivyokuwa anajielewa, mwalimu alihitimisha kwa kutuuliza tumejifunza nini kutokana na majibu ya kila mmoja.
Tukiwa bado tunajiumauma, mzee mmoja wa makamo aliingia na kwenda kukaa nyuma kabisa. Nikamuona mwalimu akisalimiana naye kwa ishara kisha akakatisha mada aliyokuwa anaifundisha na kuanza kumuelezea yule mzee kwa kifupi.
Alichokisema juu yake kilimsisimua karibu kila mtu mle ndani, tukageuka wote na kumtazama kwa macho tofauti, tukidhani huenda hakuwa binadamu wa kawaida.
Alituambia kuwa yule mzee alikuwa amefuzu mafunzo ya utambuzi na kwamba alikuwa amefikia hatua ya kuwa na uelewa na nuru kubwa kama waliyokuwa nayo mitume mbalimbali waliowahi kutokea miaka ya nyuma.
Alitueleza kuwa alianza kujifunza mafunzo ya utambuzi akiwa na umri mdogo na kwamba hata kufanya meditation alianza akiwa bado kijana mdogo na kwamba alizingatia masomo yake yote, hatua kwa hatua mpaka akafikia hatua ile.
Kwa kumtazama hakauwana tofauti yoyote na sisi kimwili ingawa kiakili na kiroho alikuwa alikuwa zaidi ya binadamu wa kawaida. Alitusabahi kwa ishara kisha mwalimu akaendelea kueleza mambo mbalimbali yaliyokuwa yanamhusu mzee yule wa makamo.
“Msimuone hivi, hapo alipo anaweza kufanya chochote na kikatokea bila wasiwasi,” alisema mwalimu huku akimsogelea, mkononi akiwa na glasi tupu ya maji. Akamkbidhi ile glasi huku sote tukiwa na shauku kubwa ya kutaka kuona ataifanya nini.
“Mzee tunajifunza kuhusu sisi, nimejaribu kuwauliza wanafunzi wangu lakini hakuna aliyeweza kunijibu vizuri. Nataka uwaoneshe kwamba akili zetu zina nguvu kiasi gani kwa kutumia glasi,” alisema mwalimu huku akimtaka yile mzee asimame.
Kweli alitii, akainuka na glasi yake na kusogea nayo hadi mbele ya darasa, kwa sauti ya upole, iliyotulia kabisa akatuambia kuwa akili zetu zina uwezo wa kufanya chochote tunachokitaka maishani mwetu. Akasema wengi tunaishi maisha ya chini, ya kifukara na yaliyojaa dhiki kwa sababu tumeshindwa kuzitumia akili zetu vizuri.
Akatuambia kua yeye anaweza kuivunja glasi kwa kuitazama tu. Kila mtu mle darasani aliguna kuonesha kutokubaliana na alichokisema. Hata mimi nilidhani anatufunga kamba kwani sikuwahi kusikia hata siku moja mtu anavunja glasi kwa macho yake.
“Najua mtabisha kwa sababu hamjui kuwa akili zenu zina nguvu kiasi gani. Ngoja niwaoneshe kisha mwalimu ataendelea na somo la leo,” alisema yule mzee huku akiweka glasi mezani, akasogea nyuma hatua kadhaa na kukaa juu ya meza akatuambia tumfuatilie kwa makini alichokuwa anakifanya.
Aliikazia macho ile glasi kwa dakika chache, hakupepesa macho wala kutingishika, baada ya takribani dakika tatu kupita sote tukashuhudia glasi ile ikipasuka vipandevipande kama iliyodondoshwa kutoka juu au iliyopigwa na kitu kizito. Vipande vya chupa vikatawanyika juu ya meza.
Hakuna aliyeamini kilichotokea, wengi tulifananisha tukio lile namazingaombwe lakini akatuambia kwa sauti ya upole kuwa lile ni dhihirisho la jinsi akili zetu zilivyo na nguvu kubwa ya kufanya chochote tukitakacho. Baada ya hapo alirudi kwenye kiti chake, akakaa na kutulia kimya kama mwanzo. Tulibaki tumepigwa na butwaa.
Mwalimu akaendelea kutufundisha: “Binadamu ameumbwa akiwa na uwezo mkubwa sana wa nguvu ambayo haionekani kwa macho. Nguvu hii huzalishwa katika mfumo wa kufikiri (mawazo ) ambayo wataalamu wameshindwa kueleza kwa ufasaha huwa inazalishwa katika sehemu gani ndani ya mwili wa binadamu.
“Wapo walioamini kuwa nguvu hii huzalishwa katika ubongo ingawa walishindwa kuthibitisha hilo. Wapo walioamini kuwa nguvu hii huzalishwa kwenye moyo, wengine wakaamini kuwa huteremshwa kutoka kwa Mungu inmgawa nao hupata kazi kubwa kuthibitisha kile wanachokiamini, huku wengine wakiamini nguvu hiyo hutoka kwenye mizimu ya watu waliokufa zamani.
“Hatutakiwi kupuuza wala kudharau imani ya mtu, tunapaswa kuheshimu kila mmoja anachoamini kuhusu yeye na maisha lakini kwa wakati huohuo kutafuta ukweli mkubwa zaidi ambao utatuweka huru. Tunapozungumzia nguvu yamawazo tunazunhgumzia kitu rahisi sana kuliko tunavyofikiri.
“Kila mtu yupo kama alivyo na anaishi kama anavyoishsi kwa sababu akili na mfumo wamawazo yake ndiyo umeamua aweje na aishije. Ni sahihi kabisa kusema wewe mwenyewe ndiye anayechagua awe nani na aishi maisha gani, bila kuhjali kama anajua au la.
“Katika ila kitu kinachotokea maishani mwetu, kiwe kizuri au kibaya lazima kipitie kwanza kwenye mfumo wa kufikiri I(katika nguvu ya mawazo) ndipo kitafsiriwe na kupokelewa na maumbile, mwisho ndiyo kitokee kitu halisi.
“Binadamu waliogundua vitu kama ndege,mashine, kompyuta, magari, ndege na mambo mengine ambayo muda mwingine huwezikuamini yamegunduliwa na binadamu, walipitia katika mfumo huu.
Nguvu ilianzia katika mfumo wa kufikiri (nguvu ya mawazo) kisha nguvu hiyto ikapokelewa na na maumbile na kuingizwa katika nguvu kuu (universal power) kisha kile amvbacho kilifikiriwa na kubuniwa hutokea na kuwa kitu halisi.
“Huu ni uthibitisho wa kutosha kuonesha jinsi ambavyo mawazo na fikra za binadamu zinaweza kuzalisha nguvu kubwa zenye uwezo wa kufanya chochote kama anayezitumia anafahamu anafanya nini. Mfano hgalisi tumeona jinsi mzee wetu alivyovunja glasi kwa macho.
Wengi tumekuwa tukiishi katika maisha ambayo hatuyapendi, yanayotuumiza , yaliyojaa kila aina ya kadhia lakini bado tumeshindwa kutoka na kuishi maisha tunayoyataka kwa kuwa kuwa tumeshindwa kutumia vizuri nguvu ambayo tayari imo ndani yetu.
“Unaishi kimaskini kwa sababu ndiyo aina ya maisha uliyochagua, bila kujali kama ulikuwa unajua unachokifanya katika kuchagua maisha yako.
“Hakuna kitu kinachotokea kwa bahati mbaya kama wengi wetu tunavyoamini. Huwezi kuwa na maisha mazuri kwa kuwa umebahatisha wala kuwa na maisha mabaya kwa sababu una bahati mbaya bali kwa sababu injini yako (nguvu yamawazo ) ndiyo iliyochagua uishije. Wote waliojenga nyumba nzuri, wanaondesha magari ya kifahari, wenye familia bora na wenye utajiri mkubwa hawakubahatisha kuwa hivyo bali waliamua.
Hata wewe leo ukiamua kufanikiwa, unaweza kabisa, ni suala la kuamua tu, hakuna miujiza, uchawi wala kutoa kafara katika hili. Tatizo la watu wengi duniani ni kukosa maarifa,” alisema mwalimukwa kujiamini kisha akariuhusu kama kuna yeyote mwenye swali aulize.
Kila mmoja alivuta pumzi ndefu na kukaa vizuri, tukawa tunatazamana huku kila mmoja akiwa na shauku ya kutaka kusikia mwenzake akiuliza swali. Cha ajabu, hakuna aliyenyanyua mkono kuuliza chochote, tukawa tumepoa kama tuliomwagiwa maji ya baridi.
Mwalimu aliuliza zaidi ya mara tatu kama kulikuwa na na mtu aliyekuwa na swali lakini hakuna aliyejibu.
“Kama hakuna mwenye swali basi somo letu kwa leo linaishia hapa, kwa yeyote ambaye anahitaji kujua kitu chochote anaruhusiwa kuuliza wakati wowote lakini kwa sasa, naomba wote tutoke nje kwani chumba hiki kitatumiwa na wanafunzi wanaojifunza meditation,” alisema mwalimu, wanafunzi wakainuka huku kila mmmoja akiwa kimya.
Ni dhahiri kuwa somo tulilofundishwa siku ile lilitufanya wengi tubaki tunajiuliza maswali mengi ambayo hayakuwa na majibu ya moja kwa moja kuhusu ubinadamu, nguvu, maisha na mafanikio.
“Mwalimu samahani, mimi nataka kujifunza meditation,” nilimwambia mwalimu wakati wanafunzi wengine wote wakiwa wameshatoka darasani.”
“Unataka breath, mantra au light?” aliniuliza swali ambalo ambalo lilikuwa gumu sana kwangu kwai sikuwa nikijua kuwa kuna aina na madaraja tofauti ya meditation. Ilibidi niwe mkweli kuwa nilikuwa na mwanga kidogo kuhusu meditation lakini sikujua chochote kuhusu aina zake.
“Ulijifunzia wapi?” aliniuliza tena, ikabidi nimwambie kuwa nimejifunza mwenyewe kupitia kitabu nilichokuwa nimekinunua lakini pia nilipata uzoefu mdogo baada ya kuhudhuria darasa la Jitambue, Kimara Kona.
“Kwa hiyo bado hujui meditation?”
“Ndiyo, nilimjibu haraka nikitegemea ataniambia basi kaa humu uwasubiri wenzako lakini haikuwa hivyo. Alinielekeza kuwa wale waliokuwa wanataka kuingie mle darasani ni wanafunzi ambao wamefikia ngazi ya pili ya meditation ambayo kwa kitaalamu huitwa tahajudi ya maneno au mantra.
Sehemu Ya 11
“Inabidi ujifunze kwanza namna ya ukaaji, kutuliza akili, kuvuta na kutoa hewa na mambo mengine muhimu, ukishajua utaanza na hatua ya kwanza ya tahajudi ya pumzi (breath) na ukifuzu ndiyo utaruhusiwa kuungana na hawa wanaofundishwa humu darasani,” alisema mwalimu huku akinielekeza nikaonane na mwalimu mwingine aitwaye Bonifasi ambaye angenifundisha wapi pa kuanzia.
Ilibidi nitii nilichoambiwa, nikatoka mpaka nje na kwenda kukutana na mwalimu Bonifasi ambaye alikuwa akizungumza na wanafunzi wengine, nje ya darasa.
‘Shikamoo mwalimu,” nilimsabahi, akaitikia na bila kupoteza muda aliniuliza kama na mimi nilikuwa miongoni mwa wanafunzi wa tahajudi ya pumzi.
Nilimjibu ndiyo, akaniambia nimfuate. Tukapanda ngazi na kuingia kwenyejengo lingine, nikiwa na wanafunzi wenzangu saba ambao nao walikuwa wakitaka kufundishwa.
“Vueni viatu hapo mlangoni,” alisema mwalimu Bonifasi, sote tukafanya kama tulivyoelekezwa. Baada ya hapo tuliingiampaka ndani ambapo tulikuta ukumbi mkubwa ukiwa umetandikwa mazulia ya sufi. Akatuelekeza tukae chini na kukunja miguu kisha kutulia kama wafanyavyo waumini wa madhehebu yenye asili ya mashariki ya mbali.
Tulijipanga na kutengeneza kama nusu duara, tukaanza kwa kuelekezwa namna ya kukaa vizuri kwa ajili ya tahajudi. Kilichonishangaza ni kwamba wengi walianza kushindwa hatua ile yakwanza ya namna ya kukaa.
“Miguu inauma sana mwalimu, mimi siwezi,” alilalamika mwanafunzi mmmoja kwa sauti ya juu, hali iliyofanya wote tucheke.
“Hiyo ni kwa sababu ya utaratibu mbovu wa vyakula, Ndiyo maana hapa tunawafundisha wanafunzi wetu kupendelea kuwa ma- vegetarian,” alisema mwalimu Bonifasi. Mwanafunzi mmoja akauliza:
“Mavegetarian ndiyo nini?”
“Ni watu ambao hawali nyama kwenye milo yao badala yake wanakula mimea na nafaka za asili kama mboga za majani, matunda na kadhalika. Watu wanaopendelea kula nyama ya mbuzi huwa wanapatwa na tatizo la kushindwa kukunja miguu wakati wa tahajudi kama wewe, bila shaka na wewe ni miongoni mwao,” alisema mwalimu Bonifasi, huku akimtazama yule mwanafunzi mwenzetu aliyekuwa analalamikia maumivu ya miguu.
“Ni kweli, mimi napendelea sana nyama ya mbuzi ya kuchoma, hata leo wakati najiandaa kuja huku nilikula kiasi.”
“Haitakiwi kwani binadamu tumeumbwa kula mimea, nafaka, namatunda na si nyama, ndiyo maana hatampangilio wetu wa meno (dental Formula) unatofautina na wa wanyama wanaokula nyama. Baada ya kusema hivyo, mwalimu alituambia kuwa kama tuna tatizo kama la mwenzetu la kushindwa kukunja miguu, basi tunyooshe lakini tujitahidi kufanya mazoezi na kuzingatia mlo ili tumudu kukaa katika mkao ule kwa muda mrefu.
“Kwa kawaida, ukishakaa kwenye mkao huu, unaanza kuvuta punzi ndefu na kuzitoa, akili zako zote ukiwa umezielekeza kwenye pumzi na hakikisha mawazo yako hayafikirii kitu kingine chochote.
Taratibu utaanza kuonamabadiliko kama hivi, kisha utafanya hivi kwa na kutuliakwa muda wa kuanzia nusu saa hadi saa moja,” alisema mwalimu huku akituonesha kwa vitendo namna ya kufanya meditation. Hakuna siku ambayo nilifurahi kama hiyo kwani nilikuwa na hamu kubwa ya kufahamu namna ya kufanya meditation kwa ukamilifu.
Mwalimu akarudia kwa mara ya pili kutuelekeza kisha akatutaka wote tujaribu. Nikakaa na kutulia kisha nikaanza kufuatisha maelezi yake. Kiukweli nilijihisi hali ambayo siwezi kuielezea.
Nilirudia zaidi ya mara tatu kufanya zoezi lile, mara kwa mara mara nilikuwa naangalia muda niliokuwa nautumia. Kwa kuwa ilikuwa mara yangu ya kwanza kufanya tahajudi kikamilifu, nilikuwa sivuki zaidi ya dakika kumi na tano.
Baada ya kumaliza, niliaga na kuwa wa kwanza kutoka darasani kwani nilitaka niwahi kurudi nyumbani. Niliogopa kwenda kusababisha matatizo mengine nyumbani kwa baba mkubwa.
Nikaagana na mwalimu na kuwaacha wanafunzi wengine wakiendelea kufanya tahajudi. Nilitoka hadi nje ya jengo lile, nikashangaa kuona kuwa muda ulikuwa umekwenda sana.
Harakaharaka nikawa natembea kuelekea kwenye kituo cha daladala. Nikiwa naendelea kutembea kwa kasi nilishtuka baada ya kusikia gari likinipigia honi nyuma yangu, jirani kabaisa na pale nilipokuwa nimesimama.
Nilishtuka na kupandwa na hasira kwani nilikuwa nikitembea pembeni kabisa ya barabara, nikahisi ananiletea dharau kwa sababu natembea kwa miguu, nikasogea sehemu ya kioo cha dereva na kutaka kuanza kukwaruzana naye.
Mara kioo kilishushwa, nikakutana na sura ya mwanamke wa makamo ambaye alitabasamukisha kuniomba radhi kwa kilichotokea. Nilimjibu kwa kutingisha kichwa kisha nikawa nataka kuendelea na safari yangu.
Akaniita na kuanza kuniuliza nilikuwa naelekea wapi kwani nilionesha kuwa na haraka sana.
“Nimechelewa kurudi nyumbani, nataka kuwahi.”
“Kwani unaishi wapi?”
“Kimara Kona.”
“Ooh! Mimi mwenyewe naelekea hukohuko, ingia ndani ya gari twende, nitakufikisha hadi nyumbani kwenu,” alisema yule mwanamke huku akiendelea kutabasamu. Nilimtazama usoni kwa sekunde kadhaa kisha nikakubali kupanda kwenye lake lake la kisasa aina ya Murano.
Nilitaka kupanda siti siti ya nyuma lakini akaniambia nipande mbele, nikatii na kukaa pembeni yake, safari ikaanza. Kwa muda wa kama dakika tano kila mmoja alikua kimya, baadaye akauvunja ukimya na kuanza kuniuliza.
“Unaitwa nani?”
“Mkanwa.”
“Kama nimekuona ukitoka kwenye kile kituo cha elimu ya utambuzi pale ,maduka mawili Chang’ombe, kwani na wewe unajifunza masomo ya utambuzi?”
“Ndiyo.”
“Kwa nini unajifunza utambuzi?”
“Napenda kujitambua na kuwatambua wengine, kwa kifupi napenda kufahamu kuhusu maisha tunayoishi.”
“Vizuri sana, ni nadra sana kuwaona vijana wadogo kama wewe wakijifunza mambo kama haya. Vipi unapenda kuwa tajiri?”
“Ndiyo, kwani kuna mtu asiyependa kuwa tajiri? Nimefundishwa kuwa nikiamua kuwa tajiri naweza, ni suala la kuamua tu.”
“Oooh vizuri sana, unajifunza tahajudi?” aliniuliza yule mwanamke, nikageuka na kumtazama kwani kwa ilivyoonesha, alikuwa na uelewa mkubwa kuhusu mambo yale.
“Ndiyo, mbona unaniuliza maswali mengi?”
“Kwani ni vibaya kukuuliza? Mbona unaonekana kama bado una hasira? Au hujanisamehe kwa kilichotokea?”
“Hapana, nimeshakusamehe, watu wengi huwa wanapenda kuhoji mambo kama hayo kwa kejeli.”
“Mh! Hivi unajua kwamba na mimi nilikuwa najifunza pale miaka mingi iliyopita? Hivi sasa nimeshafanikiwa sana kimaisha, namiliki nyumba nyingi nzuri, magari ya kifahari, fedha na chochote ninachokitaka,” alisema huku akiyazungusha macho yake makubwa kwa madaha, nilimtazama kwa sekunde kadhaa, nikajikuta nimevutiwa kkumtazama na kumsikiliza.
“Muda huu nimetokakwenye shughuli zangu na nnarudi nyumbani kwangu, wala usifikiria kama nina lengo la kukukejeli kwani hata mimi nilitokea hukohuko,” alisema. Nikashusha pumzindefu na kugeukia mbele. Safari iliendelea, yule mwanamke akawa anaendelea kunipigisha stori za hapa na pale.
Mwili mzima alikuwa amevaa vito vya dhahabu na almasi, pia alikuwa na simu zaidi ya tatu, zote za kisasa akiwa ameziweka kwenye dashboard ya gari lake.
Baada ya kufika Ubungo, niliona yule mwanamke ameanza kubadilisha mazungumo, akawa ananisihi niende naye mpaka nyumbani kwake kisha atanirudisha nyumbani na gari lake.
Kwa kuwa muda ulikuwa umeenda sana, nilimkatalia, nikamwambia kama alikuwa anataka nikapafahamu nyumbani kwake anitafute siku nyingine
“Una simu?” aliniuliza, nikatingisha kichwa kumkatalia. Sikutaka aione simu yangu ya kishamba niliyokuwa naimiliki. Akanipa kadi ya mawasiliano iliyokuwa na namba zake za simu na kuniambia nitakapofika nyumbani nimbipu kwa namba yoyote atanipigia.
Wakati akizungumza hayo, mkono mmoja alikuwa ameshika usukani wa gari lakini ule mwingine alikuwa akinioneshea ishara ambazo sikuzielewa. Pia kuna wakati alikuwa akijiziba jicho lake moja kwa mkono na kunitazama, nikabaki njia panda juu ya alichokuwa anakifanya.
Tulipofika Kimara Kona, alipunguza mwendo kisha akasimamisha gari, kwa makusudi kabisa nilimuona akiinyanyua sketi yake fupi aliyokuwa ameivaa na kuyafanya mapaja yake meupe yaonekane. Nilijikuta nikipata tama mbaya, nikajifanya sijaona chochote, nikateremka garini na kuagananaye, nikaanza kutembea harakaharaka kuelekea nyumbanai.
Baada ya kutembea hatua kadhaa, niligeuka na kuangalia nilikotoka, nikashangaa kumuona bado amesimamisha gari palepale aliponishusha, akawa ananitazama kama anayeniwazia jambo fulani. Alipoona nimegeuka kumtazama, alinipungia mkono kisha akawasha gari nakuondoka. Nilibaki na mswali mengi kichwani.
Nikatembea harakaharaka hadi nyumbani, ile nafika tu, nikakutana na baba mkubwa mlangoni.
“Ulikuwa wapi?” alinihoji kwa ukali.
“Shikamoo baba,” nilimsalimu kwa kubabaika.
“Sitaki salamu yako, nataka kujua ulikuwa wapi muda wote huo?”
“Nilikuwa Kariakoo kununua nguo.”
“Nguo gani unanunua siku nzima? Kwanza nguo zenyewe zipo wapi?”
“Nimeibiwa fedha zangu Kariakoo, nikawa najaribu kuwatafuta walioniibia ndiyo maana nimechelewa,” nilimdanganya baba mkubwa.”
‘Mwongo, unanidanganya?”
“Hapana baba sikudanganyi, kweli nimeibiwa fedha zangu zote,” nilisimamia uongo wangu kwa ngfuvu zote, nikawa najikamua ili machozi yanitoke. Nilifanikiwa kumrubuni baba mkubwa, akaanza kuniuliza kama nilipatwa na matatizo kwa nini sikumpigia simu na kwa nini kuna wakati nilikuwa sipatikani hewani?
Nilijiumauma kwa muda kwani ukweli ni kwamba sikwenda Kariakoo kama nilivyomwambia bali nilikuwa Chang’ombe kuhudhuria masomo ya utambuzi na nilizima simu kwani tuliambiwa tukiwa darasani ni marufuku kuacha simu zimewashwa ili kuepuka usumbufu.
Namshukuru Mungu baba mkubwa alinielewa, akanipa onyo kuwa siku nyingine niwe nampa taarifa ninapopatwa na tatizo. Ukweli ni kwamba baba mkubwa alikuwa mkali kuliko hata baba na huenda ndiyo sababu wazazi wangu walipoona naanza kutoka nje ya mstari kimaadili, waliamua kunileta kwa baba mkubwa.
Baada ya kumalizana, nilipitiliza mpaka chumbani kwangu, nikapumzika kwa muda kisha nikatoka na kwenda kuoga, nilipomaliza chakula cha jioni kilikuwa tayari. Tulikaa familia nzimana kupata chakula kisha nikawa wa kwanza kuinuka nakwenda chumbani kwangu.
Wote walidhani ni kwa sababu nina uchungu wa kuingizwa mjini na vibaka wa Kariakoo lakini haikuwa hivyo, nilitaka niwahi kupata muda wa kupumzika na kutafakari yote niliyojifunza siku ile.
Nilipofika chumbani kwangu, nilijifungia mlango kwa ndani na jambo la kwanza nililolifanya ilikuwa ni kuichukia ile kadi ya mawasiliano niliyopewa na yule mwanamke aliyenipa lifti wakati natoka Chang’ombe. Nilishika na kuanza kuitazama ile kadi kwa umakini.
Ni hapo ndipo nilipogundua kuwa kumbe jina lake alikuwa anaitwa Firyaal Kursi na alikuwa mkurugenzi wa kampuni ya mafuta ya Crystal Diesel iliyokuwa na makao makuu yake jijini Nairobi. Nilishusha pumzindefu kwani kwa jinsi ilivyoonesha, alikuwa mtu mzito.
Nilianza kujiuliza kuhsu maneno aliyokuwa annaiambia wakati tukiwa ndani ya gari, nikakumbuka swali aliloniuliza kama nataka utajiri au la. Nilijiuliza maswali mengi ambayo yote sikuyapatia majibu. Sikuelewa nimepitiwa na usingizi muda gani lakini nilikuja kuzinduka alfajiri, nikiwa bado nimeishika ile kadi ya mawasiliano ya yule mwanamke.
Niliamka na kujinyoosha kisha nikakaa sakafuni na kuanza kufanya meditation kama nilivyokuwa nimefundishwa kule Chang’ombe. Safari hii sikuwa nabahatisha kama mwanzo kwani tayari nilikuwa na uelewa wa kutosha kuhusu taratibu zote za namna ya kuifanya kikamilifu.
Sehemu Ya 12
Nilitulia kwa muda wa zaidi ya dakika ishirini, nikizingatia pumzi zangu na kuyatuliza mawazo yangu yote kwa ukamilifu. Nilipomaliza nilijihisi nikiwa kiumbe mpya kabisa, akili yangu ilikuwa mpya na nilijihisi mwili wote ukiwa mwepesi. Nikasimama na kwenda kuoga kisha nikarudi chumbani kwangu.
Nilichomoa simu yangu kwenye chaji nilipokuwa nimeichomeka usiku uliopita na kuanza kusevu namba za simu za Firyaal. Nilisevu namba zote za mitandao mitatu alizokuwa anazitumia. Nilikuwa na shauku kubwa ya kuzungumza naye lakini kwa muda ule niliamini bado hajaamka. Nikasubiri mpaka kulipokucha kabisa.
“Haloo!”
‘Haloo! Nani mwenzangu.”
“Ni mimi Mkanwa tuliyekutana jana Chang’ombe ukanipa lifti kwenye gari lako,” nilijitambulisha, yule mwanamke akaonesha kuifurahia sana simu yangu. Tulizungumza mambo mawili matatu kisha akaniambia kama ningekuwa na nafasi, alitaka kunipeleka mahali anakosali kwani amegundua kuwa nina hamu kubwa ya maarifa ya utajiri.
Harakaharaka nilimjibu kuwa ningekuwa na nafasi, akaniambia atanipitia atanipitia saa tisa hivyo anikute namsubiri barabarani, pale aliponishusha jana yake. Nilimkubalia kisha nikakata simu.
Nikaanza kujiuliza jinsi nitakavyomuaga baba mkubwa. Kwa bahati nzuri, alikuwa na safari ya siku hiyo ya kuelekea Mlandizi na alisema angerudi kesho yake, kimoyomoyo nikafurahi sana kwani kumdanganya mama mkubwa haikuwa kazi kubwa.
Ilipofika saa nane, nilimdanganya mama mkubwa kuwa kuna chuo kinafundisha masomo ya kompyuta muda wa jioni hivyo nataka kwenda kujua utaratibu. Aliniruhusu lakini akaniambia nisichelewe kurudi. Nilifurahi sana, nikajiandaa harakaharaka na kuvaa nguo nzuri, nikatoka na kwenda barabarani kumsubiri Firyaal.
Saa tisa juu ya alama,gari jeusi la kisasa aina ya Murano lilisimama pembeni yangu, vioo vikashushwa taratibu, macho yangu na ya Firyaal yakagongana, wote tukatabasamu. Aliniambia kwa ishara kuwa nizunguke upande wa pili na kuingia ndani ya gari, nilifanya kama alivyonielekeza, nikaingiakwenye gari na kujifunga mkanda.
Nilimpa shikamoo lakini akaikwepa kijanja na badala yake, akanisalimia kama vijana wanavyosalimiana.
“Mambo!”
“Poa,” nilimjibu huku nikijihisi aibu. Alikuwa amependeza kuliko jana yake na alikuwa akinukia marashi mazuri sana. Nilijaribu kumuuliza tunaelekea wapi lakini hakunipa majibu ya kueleweka zaidi ya kuniambia nisubiri nitajionea mwenyewe. Akaondoa gari na tukaianza safari huku nikiwa na shauku kubwa ya kutaka kujua hilo kanisa lao linalotoa utajiri lipo sehemu gani.
Aliendesha gari mpaka Ubungo, tukasimama kwa dakika kadhaa kwenye mataa kisha safari ikaendelea. Tulienda moja kwa moja mpaka Posta, katikati ya Jiji la Dar es Salaam.
“Unalijua vizuri jiji?” aliniuliza huku akinitazama kwa macho yaliyojaa ujumbe.
“Hapana, mi bado mgeni.”
“Tukiwahi kumaliza nitakutembeza sehemu mbalimbali za jiji ili na wewe uwe mjanja.”
“Sawa nitashukuru,” nilimjibu wakati gari likizunguka kwenye mnara wa askari aliyekuwa ameshika bunduki,. Tuliivuka ile sanamu ma kusogea mpaka mbele, nikaona kibao kimeandikwa Sokoine Drive, akakata kona upande wa kushoto na kunyoosha na barabara, tukapita maghorofa mengi na hatimaye akasimamisha gari lkwenye jengo moja jeupe lililokuwa na maandishi yaliyosomeka: Wajenzi Huru Hall.
“Tumefika,” aliniambia huku akijifungua mkanda.
Aliteremka garini na kuja kunifungulia mlango upande wangu. Kwa mara yakwanza nikapata nafasi ya kulisanifu umbo lake. Japokuwa alikuwa mtu mzima, Firyaal alikuwa ameumbika haswaa. Kila kitu kilikuwa kimekamilika kwenye mwili wake.
Tuliongozana mpakakwenye lango la kuingilia ndani ya jengo lile, nikawa nageuka huku na kule kushangaa mandhari ya eneo lile. Tukatembea hatua fupifupi kuingia ndani, tulipokaribia sehemu ya kuingilia, Firyaal alinisogelea na kuniambia kuwa wanaume na wanawake huingia ndani ya jengo lile kwa kutumia milango tofauti.
“Wewe utaingilia kwenye mlango huu mkubwa wa mbele, mimii nazunguka upande wa nyuma kuna mlango mwingine,” alisema Firyaal kwa sauti ya chini. Nilitingisha kichwa kuashiria kukubalian anaye, tukaachana, yeye akakata kona upande wa kushoto na mimi nikanyoosha mpaka kwenye mlango mkubwa.
“Kwani na wewe ni mwanachama?”
“Mwanachama? Wa nini?”
“Hebu soma pale ukutani,” mwanaume mmoja wa makamo alinihoji huku akinionesha sehemu iliyoandikwa ‘Members Only’ ukutani. Akaniambia kuwa watu wasiokuwa
wanachama hawaruhusiwi kuingia ndani ya jengo lile.
“Lakini nimekuja kusali, mnawezaji kunizuia kuingia kusali?”
“Kama unataka kusali si uende kwenye makanisa au misikiti ? Hapa wanaingia wanachama tu, kama siyo mwanachama tafadhali ondoka,” alisema yule mwanaume huku akionesha kutokuwa na hata chembe ya masihara.
Niligeuka kumtazama Firyaal lakini tayari alishakuwa amepotelea ndani ya jengo lile kupitia mlango wa nyuma. Nilijaribu kumdadisi mzee yule namna ya kuwa mwanachama lakini hakuonesha ushirikiano wowote kwangu. Sikuwa na cha kufanya zaidi ya kugeuka nyuma na kuanza kuondoka huku kichwa nikiwa nimekiinamisha.
Nilitoka hadi kwenye geti , nikasimama na kuegamia ukuta, nikasikia mtu ananiita kwa nyuma.
“Haloo, huruhusiwi kusimama hapa, ingia ndani au toka nje kabisa, mimi nipo kazini,” alikuwa ni mlinzi wa kampuni moja ya ulinzi, akiwa amevalia sare maalum huku mkononi akiwa ameshika kirungu. Nilijisikia vibaya sana, ikabidi nitoke mpaka nje. Akanisogelea:
“Unaitwa nani?”
“Mkanwa.”
“Umefuata nini hapa?”
“Nimekuja na mwenyeji wangu lakini kwa bahati mbaya nimezuiliwa pale getini.”
“Ni utaratibu, wanachama pekee ndiyo wanaoruhusiwa kuingia.”
“Nawezaje kuwa mwanachama?”
“Mimi mwenyewe sijui, mi ni mlinzi tu na sijui chochote.”
“Kwani mle ndani kunafanyika shughuli gani?”
“Kwani mwenyeji wako alikwambiaje?”
“Aliniambia wanasali.”
“Basi hilo ndiyo jibu, maswali mengine utamuuliza huyo mwenyeji wako.”
“Kwani ni kweli kwamba wanaoingia humu wanamuabudu shetani?”
“Ni imani tu iliyojengeka kwenye akili za watu lakini mara kwa mara huwa nawasikia wakizungumza kuhusu kumuabudu Mungu, kupendana na kuishi kwa amani, hayo mengine siyajui.”
“Kwa hiyo siyo kweli kwamba hii ni dini ya shetani?”
“Kijana, nimekwambia sijui? Huwezi kuujua mti kwa undani mpaka utakapoamua kuwa mti.
Isitoshe umri wako bado mdogo, kwa nini usikazanie masomo ya shuleni badala ya kuumiza kichwa kwa mambo yasiyokuhusu?”
“Biblia inasema tuyatafute maarifa nayo yatatuweka huru. Mimi nayatafuta maarifa,” nilimjibu yule mlinzi ambaye alionesha dhahiri kuchoshwa na maswali yangu. Nilisogea pembeni na kusimama kumsubiri Firyaal. Ningekuwa naifahamu njia ya
kurudia nyumbani, ningeondoka kwani nilikuwa nimebanwa na donge la hasira kooni kiasi cha kushindwa hata kumeza mate.
Nikiwa pale nje, nilishuhudia magari mbalimbali ya kifahari yakiwasili na kupaki pembeni ya jengo lile, watu wa mataifa mbalimbali wakawa wanashuka na kuingia ndani. Nilitamani sana siku moja na mimi niwe miongoni mwao. Baada ya kusubiri kwa muda mrefu, hatimaye niliwaona wakianza kutoka, nikasogea karibu na gari la
Firyaal ili nisipotezane naye.
Baada ya muda nikamuona akija, akionesha furaha ndani ya moyo wake lakini mimi nilikuwa tofauti. Macho yangu yalibadilika rangi na kuwa mekundu kwa hasira.
“Vipi, umejifunza kitu?” aliniuliza huku akinishika begani na kunifungulia mlango wa gari. Sikumjibu kitu, nikaingia ndani ya gari na kukaa kimya. Niliamini alinifanyia makusudi kwani kama taratibu za pale zilikuwa zinafahamika, kwa nini hakuniambia
mapema na badala yake kusababisha nidhalilike kiasi kile?
Na yeye aliingia na kukaa nyuma ya usukani, nadhani aligundua kuwa sipo sawa kwani hakunisemesha chochote, akawasha gari na tukaanza kuondoka. Tayari ilikuwa ni saa kumi na mbili za jioni, akaendesha gari kuelekea kwenye mitaa ya jiji ambayo sikuwa naifahamu, tukafika mahali nikaona bango kubwa lililoandikwa Ocean Road Cancer Institute, gari likakata kona upande wa kushoto na tukaendelea na safari.
Baada ya mita kadhaa, lilikata tena kona upande wa kushoto, nikaduwaa baada ya kuiona bahari upande wangu wa kulia.
“He, kumbe bahari ndiyo iko hivi?” nilijikuta nimeropoka kwani kiukweli sikuwahi kuiona bahari kwani kule kwetu Tukuyu hakukuwa na bahari zaidi ya mito midogomidogo.
Firyaal alinigeukia na kutabasamu, akapunguza mwendo na kusimama kandokando ya bahari, akanionesha kwa ishara kuwa niteremke ili tukapunge upepo. Nilifungua mkanda, na yeye akafungua wa kwake, tukateremka na kwenda kukaa kwenye mchanga wa bahari.
“Mbona umekasirika sana, kwani kumetokea nini?” aliniuliza Firyaal huku akizidi kunisogelea mwilini kiasi cha kuanza kulihisi joto la mwili wake. Ilibidi nimueleze kila kitu kilichotokea, akaonesha kusikitishwa sana, akanipa pole na kuupitisha mkono wake laini kwenye mabega yangu.
Nilijikuta nikisisimka mno kwani ukiachilia mbali ukweli kuwa sikuwahi kumjua mwanamke katika maisha yangu, nilikuwa nimekamilika. Mapigo yangu ya moyo yalianza kunienda kasi kutokana na hisia zilizokuwa zinatembea kwa kasi kwenye mwili wangu, nikamgeukia Firyaal na yeye akanigeukia, tukawa tunatazamana.
“Naomba nikubusu.”
“Mh! Hapana, naogopa.”
“Unaogopa nini?”
“Mumeo akijua je? Kwanza mi sijawahi.”
“Mi sina mume Mkanwa, naishi peke yangu, kama huamini leo tukitoka hapa twende ukajionee mwenyewe.”
“Leo siwezi kwenda, muda utakuwa umeenda sana, isitoshe baba mkubwa ni
mkali sana.”
“Basi tutapanga siku nyingine, hata kesho. Au unasemaje?” Firyaal aliniuliza huku akiyarembua macho yake makubwa na meupe kama aliyekula kungu. Nilishindwa kumjibu kwani hata mimi sikuelewa nilichokuwa nakitaka. Ni kweli alikuwa amenizidi sana kiumri lakini nilivutiwa na jinsi alivyokuwa anajiweka nadhifu.
Pia nilitaka kumtumia kama daraja la mimi kujiunga na dini yao kama ambavyo mwenyewe aliniahidi. Nilijikuta nikibaki njia panda, nikazama kwenye dimbwi la mawazo. Nilikuja kushtuka baada ya kugundua Firyaal amenibusu bila idhini yangu, nilijifanya kumtoa mwilini mwangu lakini kiukweli hata mimi nilisisimka na kutamani kumwambia arudie tena.
Baada ya kukaa kwa zaidi ya dakika arobaini ufukweni pale, nilimwambia Firyaal aniwahishe nyumbani kwani nilikuwa namhofia baba mkubwa. Kweli alikubali na tukaingia ndani ya gari, safari ikaanza. Tukiwa njiani nilimuuliza maswali mengi Firyaal kuhusu kanisa lao lakini cha ajabu ni kwamba hakuwa akinijibu moja kwa moja zaidi ya kunitolea mafumbo.
“Kwani ni kweli kwamba dini yenu inamuabudu shetani?”
“Mbona nilishawahi kukujibu swali hilo? Huwezi kuujua mti mpaka utakapoamua
kuwa mti.”
“Vipi kuhusu kutoa kafara za damu?”
“Hakuna kitu kama hicho, hizo ni propaganda zilizoandaliwa na wapinga ukweli ambao walisambaza uzushi dunia nzima dini hii ionekane ni ya kishetani.”
“Kwa hiyo siyo kweli kwamba mnamuabudu shetani?”
“Nikujibu mara ngapi? Nguzo kuuza dini yetu ni upendo wa kindugu, kuamini uwepo wa Mungu na kuwasaidia wengine. Hakuna mahali panapoeleza kuwa tumchukie Mungu na kumuabudu shetani… hii siyo dini ya shetani.”
“Sasa mbona kuna masharti makali ukitaka kuingia sehemu yenu ya kuabudia?”
“Hata kwenye vyama vya siasa au taasisi yoyote lazima kuna masharti ya namna ya kujiunga, huwezi kuingia kama unavyoingia msalani.”
“Kwa hiyo inawezekana ukawa unasali pamoja nanyi lakini ukawa unaendelea kwenda msikitini au kanisani?”
“Ni uamuzi wako! Kwani ukiipenda Arsenal ya Uingereza huruhusiwi kuishabikia Simba ya Tanzania? Uamuzi ni wako.”
“Ni kweli kwamba wote wanaosali pale ni matajiri?”
“Haina maana kwamba ukijiunga nasi basi utapata utajiri wa ghafla lakini ukweli
ni kwamba utapata maarifa ya namna ya kujichagulia aina ya maisha unayoyataka
ndiyo maana siku ya kwanza nilikuuliza kama unataka utajiri.”
“Sasa nikikubali kuwa tajiri halafu nikaambiwa nimtoe kafara mama yangu itakuwaje?”
“Nani aliyekwambia maneno hayo? Najua umelishwa sumu ambayo itachukua muda mrefu sana kutoka ndani ya mawazo yako, nakuhakikishia hakuna kitu kama hicho na yote uliyowahi kuyasikia ni uzushi.”
“Vipi kuhusu digrii thelathini na tatu?”
“Safi sana, hayo ndiyo maswali niliyotegemea kuyasikia kutoka kwako. Inaonesha una uelewa wa kutosha kuhusu wajenzi huru. Ni hivi, kama ilivyo kwenye mfumo wa elimu wa nchi yoyote, lazima kuna madaraja, mtu anayeanza kujifunza leo hawezi kuwa sawa na aliyeanza kujifunza miaka kumi na tano iliyopita.
“Ili mtu akamilike kuitwa mjenzi huru, lazima asome madaraja 33 ambayo ndiyo huitwa digrii za wajenzi huru,” Firyaal alinijibu huku akikaa vizuri nyuma ya usukani.
Mazungumzo yetu yalikolea kiasi cha kufanya nisielewe tumefika wapi, nilikuja kushtuka baada ya gari kusimama nyuma ya taa za kuongozea magari, nikamuuliza Firyaal ambapo aliniambia kuwa tayari tumefika Ubungo.
INAENDELEA

