NI WEWE TU (ONLY YOU)
ONYO: Wakubwa tu, kuanzia Miaka 18, ndio wasome hii Hadithi
Sehemu Ya 8
Hawakujua kilichokuwa kikiendelea, haraka sana wakampakiza ndani ya gari. Kabla hawajaondoka, mzee Mwamanda akatoka ndani, akaanza kuwaangalia huku akionekana kushangaa.
“Kuna nini?” aliuliza mzee huyo.
“Ameanguka!” alijibu Jackline huku akianza kulia.
“Ameanguka?” aliuliza mzee huyo huku akiwasogelea, akamgusa Daniel, haraka sana akawaambia waondoke kuelekea hositalini kwani hali ya Daniel ilionekana si ya kawaida.
Ndani ya gari Jackline alikuwa akilia huku akiwa amekilaza kichwa cha Daniel mapajani mwake. Hakujua tatizo lilikuwa nini, alishangaa, ilikuwa ni ghafla sana mwanaume huyo kuwa kwenye hali hiyo.
Hakikuwa kifafa, kama kingekuwa chenyewe basi ilikuwa ni lazima kutokwa na mapovu. Kila alipokuwa akijifikiria tatizo lililokuwa limemsibu mpenzi wake, alikosa jibu.
“God! Don’t take him, please” (Mungu! Tafadhali naomba usimchukue) alisema Jackline huku machozi yakitiririka mashavuni mwake.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika katika Hospitali ya St. Marry iliyokuwa hapohapo Mbezi Beach. Haraka sana machela ikaletwa na mwanaume huyo kupakizwa kisha kuanza kusukumwa kuelekea ndani.
Jackline alikuwa akimsindikiza Daniel huku akilia, kwake, wakati mwingine alihisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa mpenzi wake huyo aliyejitolea kumpenda kwa hali na mali.
Alipofikishwa kwenye chumba cha matibabu, akalazwa na wao kutakiwa kusubiri kwa nje. Pale walipokuwa, wazazi wake walikuwa na kazi ya kumbembeleza Jackline aache kulia.
Hakubembelezeka, hakukuwa na kitu kilichokuwa kimemuuma kama kumuona mpenzi wake akiwa kwenye hali hiyo.
“Don’t cry my queen,” (usilie malkia wangu) alisema mzee Mwamanda huku akimbembeleza Jackline.
Madaktari walikuwa wakipishana kuingia ndani ya chumba kile. Mgonjwa alionekana kuwa na tatizo lililokuwa kubwa ambalo lilihitaji uchunguzi wa kina.
Waliendelea kusubiri mahali pale kwa saa mbili, hakukuwa na daktari yeyote ambaye alizungumza nao kwa lolote lile na hata walipokuwa wakiwauliza, hakukuwa na mtu aliyewapa majibu.
Baada ya saa moja, wazazi wake na Daniel wakafika hospitalini hapo kwani walipewa taarifa juu ya kile kilichokuwa kimetokea kwa mtoto wao.
Walipofika tu, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuulizia hali yake kama alikuwa mzima au la. Walipoambiwa kwamba alikuwa mzima, kidogo mioyo yao ikapoa.
Ilipofika majira ya saa sita usiku, daktari mmoja bingwa hospitalini hapo akawachukua na kuwapeleka katika ofisi yake kwani alikuwa na jambo muhimu alilotaka kuzungumza nao.
“Kuna nini? Amepatwa na nini? Amekufa?” alijikuta akiuliza Jackline huku akiyafuta machozi yake, daktari hakujibu, alibaki kimya huku akisubiri wafike ndani ya ofisi ile na kuwaambia kilichokuwa kikiendelea kwa Daniel.
Kabla daktari hakujibu kile kilichokuwa kikiendelea kwa Daniel, akabaki kimya, macho yake alikuwa akiwaangalia watu hao kama walikuwa na utayari wa kusikia kile kilichokuwa kimetokea.
Kichwa chake kilikuwa kikifikiria mengi, hakujua kama huo ungekuwa muda sahihi wa kuwaambia au haukuwa muda sahihi. Alibaki kimya kwa muda na kuanza kuzungumza.
“Ndugu yenu tumemkuta akiwa na tatizo kubwa,” alisema daktari huyo, huo haukuwa muda wa kuficha, ilikuwa ni lazima aseme ukweli kile kilichokuwa kikiendelea.
“Tatizo gani?” aliuliza mzee Mwamanda
“Ndugu yenu ana ugonjwa wa kansa ya damu,” alisema daktari huku akiwaangalia kila mmoja.
Walishtuka, hawakuamini kile walichokisikia, walimwangalia daktari mara mbilimbili, jibu lake lilionekana kutokuwa sawa na wakati mwingine walihisi kama walikuwa wakitaniwa.
Waliuliza mara nyingi lakini jibu lake lilikuwa lilelile kwamba Daniel alikuwa na ugonjwa wa kansa ya damu ambao kwa kitaalamu ulijulikana kama Eukemia.
Jackline akashindwa kuvumilia, hapohapo akaanza kulia, aliumia moyoni mwake, aliya jua magonjwa ya kansa, yalikuwa hatari ambayo yalipoteza maisha ya watu wengi duniani.
Hakutegemea kabisa kupokea jibu kama hilo. Kansa ya damu haukuwa na dawa, ulikuwa ni ugonjwa wa kutisha zaidi ya Ukimwi na kila mmoja aliyekuwa akiupata, mwisho wake ulikuwa ni kifo tu.
“Haiwezekani! Dokta, haiwezekani,” alisema alisema Jackline na kuanza kulia.
Huo ndiyo ukweli ulivyokuwa, majibu hayakubadilika, majibu yalisomeka kwamba Daniel alikuwa na ugonjwa wa kansa ya damu.
Walizungumza mengi na daktari na kuwaambia maneno ya kuwafariji kwamba kulikuwa na uwezekano mkubwa wa Daniel kupona kama tu wangechukua matibabu ya haraka.
Haikuwa kansa iliyokuwa imekomaa, ilikuwa imeanza na kama wangewahi tiba kwa haraka hata kabla ya miezi mitatu kukatika basi angeweza kupona kabisa.
Walizungumza mengi, walipomaliza, wakatoka na kwenda kumuona Daniel katika chumba alichokuwemo. Walipofika humo, Jackline akashindwa kuvumilia, akamsogelea mpenzi wake pale kitandani na kumkumbatia huku akilia.
Maneno ya daktari yakaanza kujirudia kichwani mwake, aliumia, alikuwa tayari kupoteza kila kitu katika maisha yake lakini si kumpoteza Daniel. Kwake, mwanaume huyo alikuwa kila kitu, furaha yake, tumaini lake na ni mtu ambaye alikaa vilivyo moyoni mwake.
“Jackline, usilie mpenzi,” alisema Daniel kwa sauti ya chini akbisa.
“Ninaumia mno! Why Mungu anafanya hivi?” aliuliza huku akilia.
“Yote ni MungU! Tumshukuru kwa kila jambo,” alisema Daniel kwa maneno ya kishujaa.
Kilichofuata ni kuanza matibabu. Kwanza akahamishwa katika hospitali hiyo na kupelekwa katika Hospitali ya Living Water iliyokuwa Upanga jijini Dar es Salaam.
Ilikuwa ni hospitali ya kisasa, ynye gharama kubwa mno. Kwa familia ya Daniel haikuweza kupambana na gharama kubwa bali mtu aliyeahidi kumsaidia alikuwa ni mzee Mwamanda.
Kila siku Jackline alikuwa akienda hospitalini hapo na wakati mwingine kulala hukohuko. Hakutaka kumuacha Daniel, alikuwa na hofu kwa kuhisi kwamba angeweza kufa hivyo alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha anakuwa naye karibu mno kwa kipindi hicho.
Mzee Mwamanda alitamani kuona Daniel akirudi katika hali yake ya kawaida. Alijua dhahiri kwamba kijana huyo alikuwa akipendwa sana na binti, na kitu kizuri ni kwamba alikuwa na baba wa mjukuu wake, hivyo kumpoteza yeye kilikuwa ni kitu kibaya mno.
Alichokifanya ni kuanza kuhangaikia matibabu yeye mwenyewe, ilikuwa ni lazima ahakikishe kwamba Daniel anapona kwani ndiyo ingekuwa furaha kwa binti yake, hivyo kaka baba hakutakiwa kulala usingizi.
Aliwasiliana na madaktari wengine na kuwaelezea kilichokuwa kikiendelea, wao wakamwambia kwamba alitakiwa kumsafirisha na kumpeleka nchini India katika hospitali ya Ganga ambapo kulikuwa na matibabu makubwa na mazuri zaidi.
Hakutaka kulichukulia jambo hilo kipeke yake, akamuita mkewe na kumwambia, akakubaliana naye, haikutosha, akamuita Jackline, naye akakubaliana naye na kuonyesha furaha aliyokuwanayo moyoni mwake, akamkumbatia baba yake na kumpiga mabusu mfululizo.
Baada ya hapo akawasiliana na wazazi wa Daniel na kuwaambia. Aliwaweka wazi kwamba hakutaka kuona kijana huyo akifariki kwani tayari alikuwa kama mwanafamilia hivyo ilikuwa ni lazima apambane kuhakikisha anayaokoa maisha yake.
Kwa wazazi hao ilikuwa ni furaha tele, wakakubaliana naye na wa mwisho kuambiwa alikuwa Daniel mwenyewe ambaye bila kupepesa macho alimwambia mzee huyo alikuwa tayari, si kwa India tu, popote pale alikuwa tayari kwenda kutibiwa.
Harakati za safari zikaanza kufanyika. Zilifanyika kwa kasi kubwa kwani ilikuwa ni lazima kuyaokoa maisha ya mwanaume huyo aliyekuwa muhimu mno.
Ndani ya siku mbili tayari walikuwa ndani ya ndege na kuanza kuelekea nchini India. Ndani ya ndege kila mmoja alionekana kuwa na furaha mno, Jackline alikuwa pembeni ya mpenzi wake, muda wote alikuwa akimwangalia, wakati mwingine alikuwa akitabasamu lakini wakati mwingine alionekana kuwa na huzuni kubwa.
Katika vitu ambavyo hakutaka kabisa kuona vikitokea ni kumpoteza mpenzi wake huyo. Ndege iliendelea kukata mawingu na baada ya saa kumi na sita ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Coimbatore.
Gari la wagonjwa kutoka katika Hospitali ya Ganga lilikuwa mahali hapo, baada ya abiria kuteremka, na wao wakateremka na kwenda kwenye magari maalumu yaliyofika mahali hapo kwa ajili ya kuwachukua.
Safari ikaanza na kuelekea katika hospitali hiyo. Njiani bado Jackline alikuwa akizungumza na mpenzi wake, alimtia moyo kwa kumwambia kwamba angepona na kuwa kama zamani.
Hawakutumia muda mwingi wakafika katika hospitali hiyo na hivyo Daniel kuchukuliwa na kuingizwa katika chumba cha mapumziko kabla ya kupewa matibabu.
Jopo la madaktari wanne wakakutana katika chumba cha mkutano na kuanza kuzungumza kuhusu ugonjwa uliokuwa ukimsumbua Daniel. Mikononi mwao walikuwa na ripoti ya Daniel ambayo ilitoka nchini Tanzania.
“Ni ugonjwa mbaya lakini kwa sababu ndiyo kwanza upo katika hatua ya kwanza, ninaamini tutafanikiwa,” alisema D. Patesh.
“Kweli! Ila kabla ya yote ni lazima kwanza tuchukue vipimo vingine kwa sababu ugonjwa mkubwa kama huu huwa unakuja na baadhi ya magonjwa, ni lazima tufanye uchunguzi wa damu yake kwa undani zaidi,” alisema daktari mwingine, wakakubaliana na hivyo kuanza kufanya uchunguzi kuhusu hali ya Daniel.
“Mungu atakuponya,” yalikuwa ni maneno machache yaliyokuwa yakisikika kichwani mwa Jackline.
***
Matibabu yalikuwa makubwa, yaliendelea kufanyika nchini India. Kila siku walikuwa ni watu wa kumuomba Mungu kuhakikisha kwamba Daniel anapona na kurudi katika hali yake kama kawaida.
Siku ziliendelea kukatika, madaktari hawakuchoka, kila siku kulikuwa na kazi ya kuhakikisha mwanaume huyo anarudiwa na afya yake kama ilivyokuwa zamani. Walibadilishana zamu, waliingia kwa zamu ndani ya chumba hicho na kuendelea kumtibu.
Walimpa dawa zenye nguvu, ilikuwa ni lazima kuiteketeza kansa hiyo hata kabla haijaanza kusambaa mwilini mwake. Hilo lilifanyika kwa nguvu kubwa na hatimaye baada ya mwezi akaruhusiwa kurudi nyumbani huku akipewa dawa ambazo alitakiwa kuzitumia kwa miezi sita.
“Baada ya hapo?” aliuliza mzee Mwamanda.
“Atakuwa mzima wa afya, cha kumshukuru Mungu ni kwamba tumeiwahi, vinginevyo mambo yangekuwa mabaya zaidi,” alijibu daktari.
Daniel akawa na furaha, alimshukuru mzee Mwamanda, alimuona mwanaume huyo kuwa na moyo wa kipekee, si kwa sababu alikuwa na uhusiano na mtoto wake na kumpa mimba, ila kujitoa kwa kiasi kikubwa namna ile ilikuwa ni upendo wa dhati.
Alikuwa na biashara zake, aliacha kila kitu kwa ajili yake, kila alipokuwa akifikiria hilo, aliona kabisa kwamba mzee huyo alistahili kumshukuru kwa yote aliyokuwa amemfanyia.
Siku moja kabla ya safari alikesha na Jackline katika chumba alichokuwa amelazwa, kila alipomwangalia msichana huyo, alikuwa mrembo mno, alimpenda kuliko kitu chochote kile katika dunia hii.
Hakuacha kumbusu, hakuacha kumshukuru kwa kuuruhusu moyo wake kumpenda. Alimtafuta mno, alilitafuta penzi la msichana huyo na hatimaye alifanikiwa kulipata, kubwa zaidi ni kwamba alimchukua kutoka kwa mwanaume mwingine kabisa.
Siku ya safari ilipowadia, wakapanda ndege na kurudi nchini Tanzania. Huko, waliendelea kupendana na hatimaye kuanza mipango mipya ya kuishi pamoja, hakukuwa na kitu walichokitamani kama hicho.
Wazazi waliposhirikishwa, hakukuwa na tatizo, wakakubaliana nao na hatimaye watu hao wawili kufunga ndoa takatifu kanisani. Wakawa mume na mke na baada ya miezi ya kujifungua ilipokamilika, Jackline akajifungua mtoto wa kike hospitali.
“Mke wangu!” aliita Daniel huku akionekana kuwa na furaha kupita kawaida.
“Ndiyo mpenzi!”
“Ninashukuru kwa zawadi hii, hakika ni zawadi kubwa ambayo nisingeweza kuipata sehemu yoyote ile,” alisema Daniel huku uso wake ukionyesha ni kwa jinsi gani moyoni mwake alikuwa na furaha kupita kawaida.
Maisha yakawa matamu, ya furaha, walionyesheana mapenzi kemkem, mtoto yule akawaunganisha na kuifanya mioyo yao kupendana kupita kawaida.
Daniel akawekwa katika kampuni moja ya mzee Mwamanda ambayo ilikuwa ikihusika na uchukuaji mizigo kutoka bandarini na kuisambaza sehemu nyingi jijini Dar es Salaam na nje ya nchi.
Alikuwa bosi, aliheshimika japokuwa alikuwa na umri mdogo. Alinyenyekewa, alipendwa na kuheshimiwa kila alipokuwa akipita.
Ofisi yake haikuwa bandarini, ilikuwa Posta Mpya katika Jengo la Mkapa. Ilikuwa moja ya ofisi nzuri ambapo ndani yake ilikuwa imezungukwa na vioo huku kiyoyozi kikipiga muda wote aliokuwa ofisini humo.
Mezani kulikuwa na kompyuta yake na pembeni kulikuwa na picha kadhaa za familia yake, kila alipokuwa akiziangalia, moyo wake ulikuwa na hamu ya kufanya kazi zaidi kwani aliamini kuwa kitu pekee kitakachoifanya familia yake kuishi maisha mazuri ni kufanya kazi kwa bidii tu.
“Samahani bosi,” alisema sekretari kupitia simu yake ya mezani.
“Ndiyo!”
“Kuna mgeni anakuulizia!”
“Nani? Adul?”
“Hapana! Amejitambulisha kwa jina la Felista!”
“Oh! Mwambie aingie!” alisema.
Ni ndani ya sekunde kadhaa mlango wa ofisi yake ukafunguliwa na msichana huyo kuingia. Alikuwa mweupe, mrefu kidogo, kifua saa sita, alipendeza kwa kuvaa sketi fupi ambayo iliiacha miguu yake wazi kwa kiasi kikubwa.
Alikuwa mzuri wa sura, hata kama hakuwa akiongea lolote, kwa mbali tabasamu lake lilikuwa likionekana. Alipoingia, Daniel alipomuona, kwanza akashtuka lakini akapiga moyo konde baada ya macho yake kuziona picha akiwa na familia yake.
“Karibu!” alimkaribisha huku akisimama, wakapeana mikono.
“Ahsante!” aliitikia msichana huyo na kukaa kwenye kochi.
Harufu yote ndani ya ofisi ikabadilika, harufu ya manukato ikatawala kila kona humo ndani. Pale alipokaa, Felista aliikunja miguu yake kwa staili ya nne, mapaja yakawa wazi lakini Daniel hakuonekana kushtuka kabisa.
Felista akaanza kumwambia kuhusu jambo lililomfanya kufika mahali hapo, alimwambia kwamba alikuwa na shida, alikuwa mfanyabiashara, alihitaji kupokea mizigo kutoka nchini Marekani lakini kwa bahati mbaya hakuwa na kampuni ambayo ingemuwezesha kusafirisha mizigo hiyo mpaka kulipokuwa na ofisi yake.
Hilo halikuwa tatizo kwa Daniel, hiyo ilikuwa kazi yake, ilikuwa ni pesa ambayo ilijileta. Akamwambia kwamba hakukuwa na shida, kama alihitaji msaada, kampuni yake ilijitolea kumsaidia kwa malipo ya kawaida kabisa.
Felista akafurahi, wakakubaliana kuhusu malipo, na baada ya hapo, akampa business namba yake na msichana huyo kusimama kwa lengo la kuondoka.
“Tutawasiliana bosi!” alisema Felista.
“Usijali!”
Akageuka na kuanza kuelekea mlangoni. Hapo ndipo kidogo Daniel akashtuka, alipomwangalia msichana huyo kwa nyuma, alijazia kidogo, umbo lake lilijigawa vilivyo, yaani ilikuwa ni sawa na kumuona mrembo wa Tanzania.
Hipsi zilipangwa na kupangika, kiwowo kidogo, miguu yake ilikuwa imejaa kidogo. Daniel akashindwa kuvumilia, akamfuata na kumfungulia mlango, kwa tabasamu pana, Felista akashukuru, akatoka, akamsindikiza kidogo na kisha kuondoka.
“Mmh! Mungu unajua kuumba,” alijisemea wakati msichana huyo akiifuata lifti kwa lengo la kuingia na kuondoka. Akashusha pumzi nzito na kurudi ofisini kwake.
Kichwa cha Daniel kilichanganyikiwa, hakuamini kama angeweza kumuona msichana mrembo kama alivyokuwa Felista. Alitokea kumpenda, kwa jinsi alivyovaa, alivyokuwa ameumbika kwake alionekana kuwa msichana wa ajabu kabisa.
Wakati mwingine alihisi kama Felista alikuwa ameshushwa, alipendeza machoni mwake na kila alipokumbuka jinsi alivyokuwa, ni kitu kimoja tu ndicho kilichokuja kichwani mwake, ngono.
Alikuwa na namba ya msichana huyo, alikumbuka kwamba alipewa business card hivyo haraka sana akaingiza mkono wake katika mfuko wa suruali na kuitoa kadi ile na kuanza kuiangalia, kadiri alivyokuwa akiitazama ndivyo alivyozidi kumuwaza msichana huyo.
“I must take her,” (ni lazima nimchukue) alijisemea.
“How can I win her? Should I make a call and ask her to meet me or?” (nitampataje? Nimpigie simu na kumbuomba aonane na mimi au?) alijiuliza.
Kichwani mwake hakumfikiria mke wake tena, mtu aliyekuwa ndani ya moyo wake alikuwa msichana huyo tu. Alijua dhahiri kwamba Jackline alikuwa na mtoto mdogo, alihitaji kuonyeshewa mapenzi motomoto lakini kwake akili yake ilibadilika kabisa na kitu pekee alichokihitaji alikuwa Felista tu.
Alijitahidi kukaa kimya siku hiyo, alijifanya kama kutotilia mkazo kuhusu kumpigia simu msichana yule lakini siku iliyofuata, akashindwa kuvumilia, haraka sana akampigia msichana huyo.
“Nimekumbumbuka Felista,” alisema Daniel huku akiangalia nje kupitia katika dirisha la kioo lililokuwa ofisini kwake.
“Naongea na nani?”
“Daniel!”
“Ooh! The big Boss!”
“Hahah! Hakuna buana! Mimi wa kawaida sana!” alijitetea.
“Sawa! Nimefurahi kuiona simu yako,” alisema Felista.
Daniel akatoa tabasamu pana kana kwamba msichana huyo alikuwa mahali hapo. Akabaki akizungumza naye, moyo wake ulikuwa na furaha kubwa kupita kawaida.
Alitokea kumpenda, alitamani kuwa naye, alimfikiria sana na muda huo ulikuwa ni wa kumwambia kwamba alitaka kuonana na kuzungumza naye kwani hakuona kama kungekuwa na msichana mwingine ambaye alitakiwa kuonana naye zaidi ya huyo.
Alizungumza naye kwa kujiamini, alichombeza kwa maneno matatu, alimsifia kwa kumwambia kwamba alikuwa mzuri wa sura, mpole, aliyependeza kwa kila mwanaume aliyekuwa akimwangalia.
Felista alifurahi, alipenda kusifiwa, alijiona mzuri hivyo alivyoambiwa maneno hayo moyo wake ukaridhika na kuona kabisa kwamba alistahili kwa kile alichokuwa akiambiwa.
“Ningependa kuonana nawe,” alisema Daniel.
“Leo?”
“Ndiyo! Kuna ugumu?”
“Wala hakuna!”
“Basi ningependa nikuone!” alisema.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, msichana huyo akakubaliana naye na hivyo kuahidi kuonana sehemu moja maalumu ambayo ilizoelewa kutembelewa na watu waliokuwa kwenye uhusiani wa kimapenzi.
Ilikuwa ni katika bustani ya Las Vegas iliyokuwa Masaki jijini Dar es Salaam. Walikutana mahali hapo na kuanza kuongea. Hawakuwa peke yao, walikuwepo watu wengine ambapo kila mmoja alionekana kuwa bize na mpenzi wake.
Daniel alipomwangalia Felista, msichana huyo alionekana kuwa mzuri zaidi ya jinsi alivyokuwa siku ile aliyokutana nayo. Alimwambia jinsi alivyopendeza, jinsi alivyouteka moyo wake kiasi kwamba hakuwa akijiweza kwa ajili yake.
“Kweli?”
“Ndiyo! Ninakupenda sana Felista! Wewe ni msichana wa kipekee sana moyoni mwangu, ninatamani kuwa nawe,” alisema Daniel huku akimwangalia msichana huyo.
Felista akanyamaza, hakuzungumza kitu, aliuinamisha uso wake chini, akashikwa na aibu za kike. Daniel akamsogelea na kumbusu shavuni mwake.
Kitendo hicho kikausisimua mwili wa msichana huyo, hakuamini kama mtu mwenye pesa kama Daniel angempenda msichana kama yeye ambaye alikuwa ameajiriwa sehemu akifanya kazi zake, tena za kutumwa kila siku.
“Sipendi kutembea na mume wa mtu!” alisema Felista huku akiangalia chini.
“Kwa nini? Tunauma?” aliuliza.
“Kwa sababu hamna malengo!”
“Felista! Nina malengo kwako!”
“Malengo gani? Kunioa? Hivi utaweza kumuacha mkeo kwa ajili yangu?” aliuliza Felista huku akimwangalia mwanaume huyo.
Daniel akabaki kimya, alichokizungumza msichana huyo kilikuwa kweli kabisa lakini hakutaka kuonekana kwamba hakuwa na malengo kwa Felista. Akamwambia mambo mengi lakini kusudi kubwa lilikuwa ni kukubaliwa ombi lake tu.
Kwa jinsi alivyokuwa akizungumza, alivyoonekana, alitia huruma kiasi kwamba ilikuwa vigumu kwa felista kuendeleza msimamo wake wa kumaktaa. Akakubaliana naye na hivyo kumbusu shavuni.
Moyo wake haukutaka kukumbuka kwamba alikuwa na mke nyumbani, tena aliyekuwa na mtoto mdogo kabisa, alikuwa bize na msichana huyo na kwa muda alitakiwa kumsahau mke wake.
Walikaa na kuzungumza mengi kisha kuingia ndani ya gari na kumpeleka msichana huyo nyumbani kwake maeneo ya Kijitonyama. Siku hiyo hawakufanya kitu chochote zaidi ya kubadilishana mate na kuondoka.
Njiani, kichwa chake kilivurugika, alijiahidi kwamba mara baada ya kumuoa Jackline asingeweza kutembea na mwanamke yeyote yule lakini kwa jinsi Felista alivyoonekana, hakuweza kuvumilia hata kidogo.
Ujanja aliokuwa akiutumia ni kwamba alihitaji kumuonyeshea Jackline mapenzi yakeyale, hakutakiwa kumuonyeshea utofauti wowote ule, kama alikuwa akimbusu kila siku alipokuwa akirudi, hata kipindi hicho ambacho moyo wake ulikuwa umechukuliwa na mwanamke mwingine, alitakiwa kufanya vilevile.
Alichangamka, Jackline hakugundua kitu chochote kile, hakubadilika, kama alivyokuwa siku nyingine ndivhyo alivyokuwa hata siku hiyo. Walizungumza mambo mengi lakini kichwa cha Jackline kilikuwa kikimfikiria Felista tu.
Waliachana kwa kipindi kifupi kilichopita lakini tayari mwanaume huyo alionekana kumkumbuka msichana huyo kupita kawaida, akatamani kumpigia simu na kuzungumza naye, alihitaji hata kuisikia sauti yake tu.
Akatafuta njia ya kumkimbia mke wake, apate nafasi ya kukaa peke yake na kumpigia simu ili hata amtakie usiku mwema.
Alichokifanya ni kumwambia mke wake kwamba alitaka kwenda kumfungulia mbwa kutoka kwenye banda lake. Hiyo haikuwa kazi yake, ilikuwa ni ya mlinzi lakini kwa kuwa alimwamini sana mume wake, hakutaka kumuuliza.
Akaelekea huko huku akiwa na simu yake, alipofika, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumpigia simu Felista na kuanza kuongea naye.
“Wewe! Humuogopi mke wako?” aliuliza msichana huyo.
“Hapana! Yupo chumbani!”
“Na wewe upo wapi?”
“Nimekuja kumfungulia mbwa!”
“Ehh! Huna mlinzi!”
“Nimezuga kufanya hivyo ili nije kuongea nawe, japo nikutakie usiku mwema,” alisema Daniel.
“Nashukuru kwa kunijali!”
“Usijali! Nakutakia usiku mwema mpenzi!”
“Na wewe pia!”
“Nakupenda!”
“Nakupenda pia!”
Moyo wake ukaridhika, akajisikia faraja kupita kawaida. Alipomaliza, akamfungulia mbwa na kurudi chumbani. Alipofika, akamsogelea mke wake pale alipokuwa na kumwambia alale kifuani mwake.
“Nakupenda mke wangu!” alisema huku mwanamke huyo akiwa kifuani.
“Nakupenda pia mume wangu,” alisema Jackline huku akifarijika, kwa jinsi walivyokuwa wakiishi na mapenzi aliyokuwa akionyeshewa, ilikuwa ni vigumu kuamini kama mume wake huyo alikuwa akimsaliti.
***
Japokuwa alikuwa na mwanamke mzuri lakini bado macho ya Daniel yalikuwa nje yakimwangalia mwanamke ambaye hakumfikia hata mke wake kwa uzuri. Alichanganyikiwa na kila wakati alipokuwa akimfikiria msichana Felista moyo wake ulikuwa kwenye presha kubwa.
Hakutaka kumuacha msichana huyo, alimpenda na kila wakati alikuwa akimfikiria. Kazi hazikufanyika kama ilivyotakiwa na hivyo kwa sababu ya msichana huyo.
Siku ziliendelea kwenda mbele huku mawasiliano yao yakiendelea kukua. Walikaa kwa wiki moja Daniel akamwambia Felista kwamba alimkumbuka na hivyo walitakiwa kuonana katika Hoteli ya Livingstone iliyokuwa Upanga kwa ajili ya kuzungumza.
Hilo halikuwa tatizo, wakaonana huko, wakazungumza sana katika mgahawa mmoja na baada ya hapo kwenda chumbani kutulia. Wakaanza kushikana huku na kule, baada ya hapo wakajifunika shuka na sauti ya kitanda kuanza kusikika.
Siku hiyo moyo wake ukaridhika, hakufikiria ni kwa kiasi gani moyo wa Jackline ungeumia kama tu angesikia kile kilichokuwa kimetokea.
Baada ya kumaliza, wakarudi tena kwenye mgahawa na kuanza kunywa kahawa kama kawaida. Hapo akakumbuka kwamba hakuwa amempigia simu mke wake kwa zaidi ya saa tatu, akaichukua na kumpigia na kuanza kuongea naye.
Walizungumza huku akimtania kama alivyozoea na kumwambia kwamba angerudi nyumbani mapema kabisa. Mkewe akaridhika na kukata simu.
Baada ya kuzungumza na msichana huyo, akaondoka kurudi nyumbani. Alipofika huko, akapokelewa kama kawaida, akakumbatiwa na kumwagiwa mabusu mfululizo shavuni na mdomoni na kuingia ndani.
Kitu cha kwanza kilikuwa ni kumuona mtoto wake, akacheza naye na baadaye kwenda kuoga. Muda wote Jackline alionekana kuwa na furaha tele, kila alipokuwa akimwangalia mume wake, uso wake ulikuwa na tabasamu pana kama mtu aliyeshinda mamilioni.
“Una furaha sana leo,” alisema Daniel huku akimwangalia mke wake.
“Nahisi baada ya mwaka nitakwenda kupata mtoto wa pili,” alisema Jackline.
“Hicho ndicho kinachokupa furaha?”
“Ndiyo! Napenda sana watoto. Nilishawahi kumwambia Mungu kwamba nitakapoanza kuzaa, nitazaa kama kuku,” alisema Jackline na kuanza kucheka.
Kitandani, walikuwa wakiongea mambo mengi, kila mmoja alionekana kuwa na furaha kupita kawaida jambo lililoashiria kwamba mapenzi yao yalikuwa makubwa kuliko mtu mwingine yeyote yule japokuwa katika upande wa pili, Daniel alichukua uamuzi mbaya wa kumsaliti mke wake huyo.
Sehemu Ya 9
“Ndiyo! Napenda sana watoto. Nilishawahi kumwambia Mungu kwamba nitakapoanza kuzaa, nitazaa kama kuku,” alisema Jackline na kuanza kucheka.
Kitandani, walikuwa wakiongea mambo mengi, kila mmoja alionekana kuwa na furaha kupita kawaida jambo lililoashiria kwamba mapenzi yao yalikuwa makubwa kuliko mtu mwingine yeyote yule japokuwa katika upande wa pili, Daniel alichukua uamuzi mbaya wa kumsaliti mke wake huyo.
***
“Shoga upo wapi?” ulikuwa ni ujumbe uliosomeka katika simu ya Jackline.
“Nyumbani! Kuna nini kwani?”
“Mume wako yupo wapi?”
“Kazini!”
“Eeh! Basi inawezekana huyu ninayemuona siyo yeye,” aliandika mwanamke huyo kutoka upande wa pili.
Moyo wa Jackline ukashtuka, hakuwa radhi mawasiliano hayo yaishie hapo, haraka sana akampigia simu mtu huyo na kuanza kuzungumza naye.
Alikuwa mwanamke aliyejulikana kwa jina la Pendo, alikuwa mwanamke mrembo ambaye alikuwa na urafiki wa dhati na Jackline. Walisoma wote kwa kipindi kirefu na kushirikiana kwenye mambo mengi mno.
Wakaanza kuongea. Pendo akamwambia Jackline kile kilichokuwa kikiendelea, alimwambia kuwa alimuona mume wake akiwa na mwanamke mwingine katika Hoteli ya Livingstone iliyokuwa Upanga.
Hilo lilimshtua mno Jackline na kuhisi kwamba inawezekana Upendo alikuwa amechanganya. Mwanamke huyo alimwambia kwamba hakuwa amechanganya ila alikuwa na uhakika kwamba mtu aliyekuwa akimuona mbele yake alikuwa Daniel.
“Hebu mpige picha.”
“Hakuna tatizo!”
Picha zikapigwa na kutumiwa Jackline, alipoziona, moyo wake ukawa kwenye maumivu makali, alikuwa mume wake. Alihisi kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake kupita kawaida lakini upande mwingine wa moyo wake ukamtoa hofu na kuhisi kwamba inawezekana msichana yule alikuwa wa kawaida tu.
“Wanaondoka, nadhani wanakwenda chumbani!” alisema Pendo.
“Nakuja!”
Haraka sana Jackline akaondoka nyumbani, alichanganyikiwa, hakuamini alichokuwa amekisikia, aliondoka kwa mwendo wa kasi mpaka katika hoteli hiyo, alilipaki gari lake mbali kabisa na hoteli hiyo, akateremka na kuelekea katika hoteli ile na kuonana na Pendo.
Mwanamke huyo alimwambia kwamba wawili hao waliondoka na kuelekea chumbani kupumzika. Hilo lilimuumiza mno Jackline, alitamani kutoka na kwenda kufumania lakini hakutaka iwe hivyo, hakutaka kugombana na mume wake kisa mwanamke mwingine, akavumilia.
Baada ya saa moja na nusu wawili hao wakatoka. Kila mmoja alionekana kuwa na furaha. Picha aliyokuwa akiiona Jackline ilimuumiza mno, kwa jinsi walivyoonekana, ilionyesha kabisa kwamba walikuwa wapenzi walioshibana na walitoka kufanya mapenzi.
Huku alipokaa kwa kujificha, alikuwa akilia, moyo wake ulikuwa na maumivu makali kupita kawaida. Baada ya dakika kadhaa, akashtukia simu yake ikianza kuita, alipoangalia kioo, alikuwa mume wake.
Kwanza akasita kuipokea, alichukia, moyo wake ulikuwa ukiwaka kwa hasira lakini mwisho wa siku akaona bora apokee na kuzungumza na mume wake huyo.
Hakutaka kuonyesha tofauti yoyote ile, alimuonyeshea furaha kama kawaida, walizungumza kwa dakika kama tano huku kila mmoja akionekana kumfurahia mwenzake.
“Upo wapi my prince?” aliuliza Jackline.
“Ofisini! Ila ndiyo nataka nijiandae nirudi nyumbani! Nimewakumbuka sana,” alisema Daniel bila kujua alikuwa akitazamwa.
“Tumekukumbuka pia! Nakusubiria mume wangu kipenzi,” alisema Jackline na kukata simu.
Alilia mno, hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea, wakati mwingine alihisi kama alikuwa akiota, hakuamini kama Daniel angeweza kufanya kitu kama kile. Alimwamini mno, alimuonyeshea mapenzi ya kila aina lakini mwisho wa siku akaanza kusalitiwa.
Alihisi kuwa na tatizo sehemu fulani, mtu kama Daniel asingeweza kumsaliti kama kungekuwa na tatizo sehemu fulani, na hili kufahamu tatizo lilipokuwa alitakiwa kuonyesha mapenzi kama ilivyokuwa siku za nyuma.
Hakutaka kukaa sana mahali hapo, akaondoka huku moyo wake ukiwa umejeruhiwa kupita kawaida. Katika muda ambao Daniela lirudi nyumbani, hakutaka kumuonyeshea tofauti yoyote ile, alimuonyeshea furaha ya ajabu ambayo hakuwahi kumuonyeshea katika kipindi chote.
Furaha ile ilificha maumivu makali yaliyokuwa moyoni mwake, uso ulitabasamu lakini moyo wake ulikuwa ukilia kwa ndani. Alijikaza, alijipa ujasiri wa kutokuyaonyesha maumivu yake mbele ya mume wake.
Usiku walikuwa wakizungumza, wakicheza lakini moyoni mwake hakuwa na furaha hata kidogo. Walifanya kila kitu na hata siku iliyofuatia, akamuaga na kwenda kazini.
Jackline akashindwa kuvumilia, mume wake alipoondoka, akajifungia chumbani na kuanza kulia kwa maumivu makali moyoni mwake. Alijiuliza juu ya kile kilichokuwa kikiendelea, kwa nini mume wake kipenzi aliamua kumsaliti kwa msichana ambaye aliamini kwamba hakuwa mzuri kama yeye zaidi ya makalio makubwa kidogo aliyokuwanayo?
Kila alichokuwa akijiuliza akakosa jibu lakini bado moyo wake ulikuwa na uhakika kwamba kulikuwa na tatizo mahali fulani kwani kwa jinsi alivyokuwa akimfahamu Daniel, namna alivyomuonyeshea mapenzi ya dhati, akilini mwake hakukuingia suala la usaliti hata kidogo.
“Kwa nini lakini? Nahisi kuna kitu, nitafuatilia nijue nini kinaaendelea,” alisema Jackline huku macho yake yakiwa mekundu mno kwa sababu ya kulia sana.
***
Jackline hakutaka kukurupuka, alitakiwa kuwa na ufundi mkubwa katika kumfuatilia mume wake. Alijua kabisa kwamba kama angefanya hayo kwa pupa asingeweza kufanikiwa kwani angeharibu kila kitu na kuonekana mbabaishaji.
Aliwajua wanaume, hawakuwa watu wa kuambiwa tu, walikuwa watu wa kushikwa huku wakiwa na mali mkononi, lakini pia pamoja na hilo alitakiwa kuhakikisha anamdaka huku akiwa na uhakika kwamba huyo alikuwa mpenzi wake vinginevyo angeambiwa kwamba ni rafiki yake tu.
Ili aucheze mchezo huo hakutakiwa kubaki nyumbani hapo, wazo lililokuja ni kwamba aondoke kurudi nyumbani kwa wazazi wake huku akiwa huko ndiyo aanze kucheza mchezo huo kwa lengo la kumtuliza mume wake.
Kumuaga halikuwa tatizo, aliamini kwamba atakapomwambia kuwa anataka kurudi nyumbani kwanza ampeleke mtoto kwa bibi na babu kusingekuwa na maswali mengi.
Usiku mume wake alivyorudi, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumwambia kile alichokuwa amekifikiria. Hilo halikuwa tatizo kwa Daniel, alimruhusu mke wake kumpeleka mtoto kwa babu na bibi yake.
Siku ya kuondoka, alimsindikiza hadi huko ambapo alimwambia kwamba angekaa kwa muda wa mwezi mmoja na kurudi nyumbani.
Kwa jinsi alivyokuwa akizungumza, Daniel hakuweza kugundua maumivu aliyokuwanayo mke wake moyoni mwake. Alitabasamu, walicheka pamoja huku wakitaniana lakini ndani kabisa ya moyo wake kulikuwa na mpasuko mkubwa mno.
Wakati akifikiria kuhusu mpango wake ndipo wazo jingine likamjia kichwani mwake, ilikuwa ni lazima amshirikishe rafiki yake aliyeitwa Pendo kwa lengo la kumpa ushauri juu ya kile alichotakiwa kufanya.
Haraka sana akampigia simu na kuanza kuzungumza. Akaomba kuonana naye na ndani ya dakika kadhaa msichana huyo alikuwa mahali hapo na kuanza kuzungumza.
Alichomwambia Pendo ni kwamba wao wawili walitakiwa kuhakikisha Daniel na Felista wanaachana kwa kuwachezea michezo mingi ambayo ingewafanya wasiwe na amani katika mapenzi yaliyokuwa yakiendelea.
“Ishu si kumuua yeyote, hapa ni lazima tuhakikishe kwamba wanaachana,” alisema Pendo huku akimwangalia Jackline.
“Sawa kabisa. Ni wazo zuri mno! Tunafanyaje sasa?”
“Ni rahisi! Una pesa?”
“Ninazo!”
“Basi tumkodi mwanaume mmoja, awe mzuri wa haja, halafu huyo ndiye ambaye atatumika, lakini pia tumuandae msichana mzuri wa haja, yaani hao ni kwa ajili ya kuwaachanisha wawili hao. Unaonaje?” alisema Pendo na kumalizia kwa swali.
“Wataweza?”
“Kwa nini washindwe! Yaani tujenge chuki kati yao, basi.”
“Sawa.”
Pendo ndiye alikuwa kila kitu, alijua kucheza na mambo kama hayo, katika kipindi ambacho mume wake alikuwa akichepuka na mwanamke mwingine alitumia njia ileile ambayo ndiyo alihitaji hata Jackline aitumie pasipo kushtukiwa.
Haraka sana akampigia simu mwanaume mmoja aliyeitwa kwa jina la Jackson na kumwambia kuhusu dili lililokuwa limewekwa mezani. Mwanaume huyo aliposikia, akafurahia kwani mbali na kupewa pesa, pia alikuwa na uhakika wa kufanya mapenzi na msichana mwingine mrembo.
“Naona unaniletea mpenzi mwingine! Safi sana,” alisema Jackson kwenye simu.
“Hebu tuonane kwanza na mhusika,” alisema Pendo.
Ndani ya saa moja, watatu hao wakakutana katika mgahawa wa Armando uliokuwa Kijitonyama. Jackline mwenyewe alipomuona Jackson akakiri kwamba kweli ingekuwa kazi nyepesi kwa msichana yeyote kudanganyika kutokana na uzuri wa sura aliokuwanao mwanaume huyo.
“Naitwa Jackson, mzee wa kazi,” alisema Jackson huku akimsalimia Jackline, kwa jinsi alivyokuwa akitabasamu, hata uzuri wake ukaongezeka.
“Naitwa Jackline!”
“Ooh! Kwa hiyo sisi ni JJ, safi sana,” alisema Jackson ambaye muda wote alikuwa mtu mwenye uchangamfu mkubwa.
Wakakaa na kuanza kuzungumza. Pendo akaanza kumwambia Jackson kila kitu kilichokuwa kikiendelea kwamba alitakiwa kumshawishi msichana fulani kimapenzi lakini pia angelipwa kiasi kikubwa cha pesa kama tu angekamilisha kile kilichotakiwa.
“Namba yake?”
“Hiyo si tatizo! Nilifanikiwa kuiiba,” alisema Jackline na kumpa namba ya simu.
“Sawa. Nyie niachieni! Si mnataka aachane na mumeo? Hiyo niachie mimi,” alisema Jackson na kuondoka mahali hapo.
“Halo! Mambo vipi!”
“Safi! Naongea na nani?”
“Jackson Edward!”
“Nikusaidie nini?”
“Nilikuwa nahitaji kuonana nawe, sijui una muda?”
“Mimi? Kwanza namba yangu uliipata wapi?”
“Eeh! Yaani hukumbuki mtu unayempa namba yako?”
“Nilikupa namba yangu?”
“Ndiyo! Niliagiza gari, ukanipa business yako.”
“Mmh! Sikumbuki!”
“Nahisi tukionana utanikumbuka! Upo ofisini kesho?”
“Yeah!”
“Nitakuja!”
“Sawa.”
Yalikuwa ni mazungumzo mafupi baina ya Jackson na msichana Felista. Walizungumza kwa kidogo sana na mwanaume huyo kutaka kuonana na msichana huyo mrembo.
Hakutaka kuwapa taarifa akina Jackline mpaka pale mambo ambapo yangekuwa motomoto. Siku iliyofuata, akaondoka na kuelekea mahali ilipokuwa ofisi ya akina Felista na kuonana naye huko.
Felista alipomuona mwanaume huyo na kujitambulisha kwake alionekana kuwa mgeni, hakuwa amemuona kabla na hata aliposisitiza kwamba alikuwa akifahamiana naye moyo wake ulikataa vilivyo.
Alipenda kuwa na wanaume wazuri, kwa jinsi Jackson alivyokuwa, kwake ingekuwa vigumu sana kutokumkariri kwani kila siku katika maisha yake alipenda kutembea na wanaume wa aina hiyo.
Pale ofisini, si yeye tu, kila mtu alikuwa akimwangalia Jackson kwa macho ya mshangao. Ni kweli waliwahi kukutana na wanaume wazuri lakini kwa kijana huyo, alikuwa mzuri kupita kawaida.
Muda wote tabasamu lilikuwa usoni mwake, alipenda kufurahia na hata alipokuwa akiongea alichanganya na Kingereza cha Mmarekani mweusi kitu kilichowapagawisha wasichana wengi.
“You look so stunning,” (umependeza sana) alisema Jackson huku akimsalimia Felista, tena alikuwa akimwangalia kuanzia chini hadi juu.
Walikaa na kuzungumza kidogo na kumwambia kwamba alitaka kuagiza gari lake hivyo alihitaji kufahamu gharama zenyewe. Kwa Felista halikuwa tatizo, akampa gharama hizo na baada kumwambia kwamba lingekuwa jambo zuri kama wangeonana baadaye.
“Hakuna shida! Nitakushtua,” alisema Felista huku akionekana kuingia kwenye penzi la mtu ambaye ndiyo kwanza alimuona siku hiyo.
“Nashukuru sana malkia!” alisema Jackson, akaachia tabasamu pana, kali lililokuwa la kumuulia adui wake, tabasamu hilo likazidi kumchanganya Felista, akaukuta moyo wake ukianza kuburuzwa vilivyo.
***
Felista alidata na wanaume wenye pesa lakini kwa Jackson hakuweza kupindua kwa sababu mwanaume huyo alikuwa mzuri wa sura. Waliagana na kuondoka.
Picha ya Jackson ikaganda kichwani mwake, hakuelewa kama alikutana na jini au binadamu wa kawaida kama alivyokuwa yeye. Alilikumbuka tabasamu lake, aliikumbuka sauti yake, alikumbuka namna alivyokuwa akizichezesha lipsi zake kila alipoongea, moyo wake ulichanganyikiwa mno.
Hakutaka kusikia kitu chochote kipindi hicho zaidi ya kuwa mpenzi wa mwanaume huyo. Kila alipokuwa akimfikiria mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kupita kawaida.
Aliporudi nyumbani, akatulia kitandani na kuanza kumfikiria mwanaume huyo, alihitaji kuwa naye lakini wakati mwingine alikuwa na hofu kwamba inawezekana Daniel akagundua na hivyo kumuacha.
Moyo wake ukagawanyika, upande mmoja ulikuwa ukifikiria mapenzi lakini upande mwingine ulikuwa ukifikiria pesa. Vilikuwa vitu viwili vilivyokuwa vikishindana, hakujua ni upande gani ungeibuka na ushindi mkubwa.
Nyumbani hapo, tena akiwa kitandani akachukua simu yake na kumpigia Jackson na kuanza kuongea naye. Sauti yake alipoisikia, mapigo yake ya moyo yakaongezeka kiasi kwamba akahisi kabisa moyo wake ungeweza hata kuchoma.
“Jackson!” aliita kwa sauti ndogo, nyororo iliyofanana na ile ya kumtoa nyoka pangoni.
“Niambie malkia,” alisema Jackson, Felista akazidi kuchanganyikiwa.
“Ulifika salama?”
“Ndiyo! Nimekukumbuka, ninatamani hata niwe na wewe au nije kwenu,” alisema Jackson na kutoa kicheko cha chini kilichompagawisha Felista kishenzi.
“Nimekukumbuka pia! Gari lako linafika lini?” aliuliza felista.
Jackson hakutaka kujivunga, alimwambia ukweli kwamba hakuwa na gari lakini kitu alichokihitaji kutoka moyoni mwake ni kuweka ukaribu naye kwani siku ya kwanza kumuona, alijisikia tofauti moyoni mwake na ndiyo maana aliamua kumfuatilia.
Felista alivyosikia hivyo, kama kawaida ya msichana yeyote yule wa Kitanzania, akaanza kuringa na kunata lakini moyo wake ulikuwa ukimuomba Mungu mwanaume huyo asibadilishe mawazo na kuachana naye.
Aliringa lakini hakutaka kukaza, kila alichoambiwa alikubali kwa kuwa moyo wake ulitokea kumpenda Jackson kupita kawaida. Wakazungumza mambo mengi mno usiku huo, Jackson alijitahidi kutokumpenda msichana huyo lakini mwenyewe akawa amefika, haambiwa wala hasikii lolote lile.
Baada ya kumaliza, Daniel akapiga simu na kumwambia kwamba sasa alikuwa huru kwani mke wake, Jackline hakuwa nyumbani, aliondoka kuelekea kwa wazazi wake kwa kuwa walihitaji kumuona mjukuu wao.
Kwa jinsi alivyoongea Daniel, alionekana kuwa na furaha tele, alimpenda felista, kwake, msichana huyo alionekana kuwa kila kitu, yaani pumzi yake, kituo chake na mwisho wa moyo wake.
“Ni kweli kaenda nyumbani au kakuzuga?” aliuliza Felista.
“Amekwenda. Mke wangu hajui chochote kile, usiogope,” alisema Daniel huku akionekana kuwa na furaha tena.
Wakati hayo yakiendelea, ili kumpa urahisi wa kumkamata mume wake, Pendo alimkutanisha Jackline na msichana aliyekuwa katika kitengo cha huduma kwa wateja cha mtandao aliokuwa akiutumia mume wake na kumuunganishia namba yake ili kila meseji aliyokuwa akitumiwa, ilipitia kwake na kila siku iliyokuwa ikipigwa, na kwake ilifika.
Daniel aliwasiliana na Felista huku mke wake akifuatilia kila kitu. Aliumia mno, alilia kupita kawaida, bado hakuamini kama mume wake yule aliyekuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati angeweza kubadilika kiasi hicho.
Pamoja na kufanya ujinga wote huo lakini bado Daniel hakutaka kumuonyeshea mke wake tofauti yoyote ile, kila siku aliwasiliana naye na kwenda nyumbani kwake na kuzungumza naye.
Alimwambia kwamba alimkumbuka na alitamani sana muda ufike ili arudi nyumbani kwani upweke ulitawala nyumbani hapo na alihitaji sana kumuona akirudi.
Alijua kwamba mume wake alikuwa akimsaliti lakini kwa mapenzi ambayo aliendelea kumuonyeshea bila kubadilika yalimuonyeshea kabisa kwamba hakuwa mwanaume wa kawaida na inawezekana kabisa kwamba alitembea na felista kwa tamaa ya mwili lakini si kwa mapenzi.
“Nakupenda mke wangu!” alisema Daniel huku akimwangalia mwanamke huyo.
“Nakupenda pia!”
“Nataka niende nawe nikale chakula cha usiku na wewe halafu nitakurudisha, upo tayari?” aliuliza Daniel.
Hilo halikuwa na tatizo hata kidogo, Jackline akakubaliana naye na kwenda naye kula chakula cha usiku pamoja. Njiani kama kawaida yao waliendelea kutaniana, walicheka pamoja kiasi kwamba mpaka wakati mwingine Jackline alihisi kwamba zile meseji alizokuwa akizisoma hazikuwa za mume wake, inawezekana hata ile sauti aliyokuwa akiisikia ikizungumza na Felista ilikuwa ni ya mtu mwingine kabisa.
Walikwenda huko na kula pamoja, walipomaliza, Daniel akamrudisha nyumbani na yeye kurudi kulala. Alipofika nyumbani, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu Felista na kuanza kuzungumza naye, alimpenda msichana huyo kwa sura lakini kila alipokuwa akilikumbuka umbo lake matata la nyuma, tamaa ilimuingia.
“Naomba nije nikuone, mke wangu hayupo hivyo hata nikilala nje hakuna atakayeniuliza,” alisema Daniel huku akionekana kuwa na mhemko kupita kawaida.
“Sasa hivi?”
“Ndiyo! Mbona saa nne mapema sana!”
“Hapana! Nimepumzika bebi!”
“Jamaniii! Halafu unaongea kwa sauti ndogo, upo nyumbani kweli?” aliuliza Daniel alionekana kuwa na wasiwasi kwani kwa sauti aliyokuwa akiitumia Felista kuzungumza ilikuwa tofauti kabisa na siku hiyo.
“Ndiyo! Mama amekuja kunitembelea, yaani ulipopiga simu, nikatoka chumbani,” alisema Felista.
“Kumbe mama yupo?”
“Ndiyo!”
“Basi nitakucheki kesho. Nakupenda bebi!”
“Nakupenda pia!”
Upande wa pili felista alikuwa nyumbani kwake. Alimwambia Daniel kwamba mama yake alikuwa nyumbani lakini ukweli ni kwamba mtu huyo hakuwepo bali alikuwa Jackson ambaye alikwenda kumtembelea na kulala naye usiku mzima.
Wakati msichana huyo alipotoka kwenda nje kuzungumza kwa simu, Jackson alikuwa akifuatilia, alijua ni mtu gani alikuwa akienda kuongea naye hivyo hakuonekana kujali kwani hakuwa kwenye mapenzi ya dhati na msichana huyo bali alichokihitaji ni kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha kwamba msichana huyo anaachana na Daniel.
“Ulikwenda wapi bebi?” aliuliza Jackson mara baada ya Felista kurudi chumbani.
“Nilikwenda kuongea na shoga yangu! Ananidai nikawa nakwenda kumpiga maneno kidogo,” alisema Felista huku akitoa tabasamu ambalo aliamini lingemfanya Jackson kumwamini.
“Ooh! Kumbe nimepata mchumba mjanja sana, hivyo ndivyo unavyotakiwa kufanya,” alisema Jackson pasipo kuonyesha wivu wowote ule, akamvuta msichana huyo, akampiga mabusu mfululizo na kisha kulala naye kwa kujifunika kwenye shuka, kilichosikika baada ya hapo ni sauti ya kitanda hicho tu.
“Kwichiiii…kwichiii…kwichiiii…”
Maisha ya mapenzi yakamteka Felista, moyo wake ulichanganyikiwa kwa Jackson, ni kweli aliwahi kukutana na wanaume wengi waliokuwa na uwezo mkubwa kitandani lakini kwa mwanaume ambaye alikutana naye kipindi hicho alikuwa na uwezo mkubwa kupita kawaida.
Akachanganyikiwa, moyo wake ukatokea kumpenda kuliko mwanaume yeyote yule, kila siku alikuwa akimpigia simu na kumsisitizia kwamba alikuwa akimpenda kupita kawaida.
Kwa Jackson, hakutaka kuuruhusu moyo wake uwe kwa msichana huyo, hakumpenda kutoka moyoni mwake bali kila kitu alichokuwa akikifanya, alifanya kwa kuwa alitumwa, yaani alifanya kwa sababu kulikuwa na kazi aliyokuwa akiifanya.
Aliendelea na maisha ya maigizo, kila siku alikuwa akikutana na msichana huyo na kumuigizia kwamba alikuwa akimpenda kupita kawaida.
Kwa upande wa pili, Daniel hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea. Moyo wake ulimpenda sana Felista na hakuona kama kungekuwa na mwanamke ambaye angeweza kuutoa moyo wake kutoka kwa msichana huyo.
Alimpa kila kitu alichokitaka na hakuhisi kabisa kama Felista angeweza kumsaliti kwani hata walipokuwa wakikutana na kuzungumza, msichana huyo alizungumza naye kwa mapenzi ya dhati kiasi kwamba Daniel alichanganyikiwa zaidi.
Siku zikaendelea kukatika kama kawaida. Mara kwa mara wawili hao walikuwa wakikutana lakini kwa kipindi hiki hali ilionekana kuwa tofauti na si kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma.
Yule Felista hakuwa na furaha kama kipindi cha nyuma, kila alipokuwa akikutana na Daniel alionyesha mabadiliko fulani ambayo yalionekana kuanza kumtia hofu Daniel.
Hakujua kulikuwa na kitu gani kilichokuwa kikiendelea, alijaribu kumuuliza kulikuwa na nini lakini msichana huyo alikuwa akimdanganya kwamba hakukuwa na kitu chochote kile, mambo yote yalikuwa supa kabisa.
Hilo halikuaminika kwa Daniel lakini hakuwa na jinsi, alijifanya kumwamini lakini upande wa pili moyo wake ulikata katakata kukubaliana na kile alichokuwa akimjibu kila alipokuwa akimuuliza.
Felista alibadilika kwa kiasi kikubwa, kilichombadilisha si kitu kingine zaidi ya Jackson ambaye aliingia kwa kasi moyoni mwake. Mabadiliko hayo makubwa yakampelekea kumuona sana Daniel kwamba kila watakapokuwa wakifanya mapenzi ilikuwa ni lazima kutumia mpira.
“Kwa nini?” aliuliza Daniel huku akionekana kushtuka.
“Ni maamuzi!”
“Yaani imekuwaje? Mbona yamekuja ghafla sana?” aliuliza Daniel, kuambiwa vile kulimchanganya kwani hakutegemea kama Felista angemwambia jambo hilo.
Akawa na hofu kwamba inawekana msichana huyo alikuwa ameathirika na hivyo kwenda kupima. Alipofika huko, afya yake ilionekana kuwa safi kabisa.
Alijiuliza zaidi kuhusu uamuzi wa msichana huyo lakini hakupata majibu yoyote yale. Hakutaka kuwa na hofu, hakutaka kujipa presha hivyo akakubaliana naye kwa kila kitu na maisha kusonga mbele.
Kadiri siku zilivyosonga ndivyo msichana huyo akaanza kuonekana kupunguza mapenzi kwake. Alitumia kiasi kikubwa cha pesa kuyarudisha mapenzi ya msichana huyo lakini alishindwa kabisa.
Katika kipindi hicho akahisi kabisa kwamba Felista alikuwa na mwanaume mwingine. Alihisi hicho, zikawa hisia zilizokuwa zikimuumiza kupita kawaida. Alikaa chumbani kwake huku akihuzunika, kila alipokuwa akimpigia simu msichana huyo, aliipokea na jibu moja tu ndilo alilokuwa akimpa “Nipo bize sana”.
Neno hilo liligeuka kama msumali wa moto moyoni mwake, hakutaka kuamini kama msichana yule ambaye alitumia muda wake mwingi, pesa zake mwisho wa siku angemwambia maneno kama hayo.
Alijiamini kwa sababu alikuwa na pesa hivyo kuanza kumpeleleza mpenzi wake huyo. Siku alipokutana naye, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuchukua simu yake, akaifungua na kukutana na meseji za kimapenzi alizokuwa amewasiliana na Jackson.
Moyo wa Daniel ukawaka kwa hasira, wivu mkali ukamkamata na kumuumiza kupita kawaida. Alimwangalia msichana huyo huku macho yake yakionyesha kuwa na hasira kupita kawaida. Alitamani kumpiga lakini mapenzi aliyokuwanayo yalikuwa makubwa na mbaya zaidi hakutamani kabisa kumkasirisha msichana huyo.
“Kwa nini Felista?” aliuliza Daniel huku machozi yakitiririka mashavuni mwake, alijishangaa kwani hata kwa mke wake hakuwahi kulia kiasi hicho.
“Daniel! Una mke, si ndiyo?” aliuliza Felista swali ambalo lilimshtua mno Daniel.
“Unasemaje?”
“Wewe si una mke?”
“Ndiyo!”
“Kwa hiyo hutaki mimi niolewe?” aliuliza Felista.
Swali hilo likamfanya Daniel kubaki kimya. Hakutegemea kusikia swali kama hilo akiulizwa na msichana huyo. Alimwangalia mara mbilimbili, swali lake lilikuwa la msingi sana lakini hakutaka kulijibu kwa haraka, ilihitajika hekima ya zaidi kulijibu swali hilo.
“Hutaki niolewe?” aliuliza Felista huku akimwangalia Daniel machoni.
“Si kwamba sitaki!”
“Kumbe?”
“Ninaumia moyoni!” alijibu.
“Kwa hiyo mimi siumii kila siku unavyolala na mkeo?” aliuliza Felista.
Daniel akanyamaza, akayatuliza macho usoni mwa Felista. Aliona jinsi msichana huyo alivyokuwa na maumivu moyoni mwake lakini pia alimuona jinsi alivyokuwa na wivu mkali uliokuwa ukiutesa moyo wake.
“Daniel!” aliita Felista.
“Naam!”
“I am pregnant?”(nina mimba) alisema Felista, moyo wa Daniel ukapiga paa.
“Unasemaje?” aliuliza.
“Nina mimba!” alirudia jibu lake.
Daniel akanyamaza, akaelekea pembeni, akatulia na kumwangalia Felista. Moyo wake ulishtuka, hakuamini kile alichokisikia kutoka kwa msichana huyo.
Picha ya mke wake ikamjia kichwani mwake, hakuona kama lilikuwa jambo jema kumfanyia mkewe, moyo wake ulimuuma mno na kitu ambacho kilikuja moyoni mwake ni kumshawishi msichana huyo aitoe mimba yake.
“Felista! Hapana! Ni mapema mno mimi kuzaa na wewe!” alisema Daniel huku kijasho kikimtoka.
“Kwa hiyo nisizae!”
“Ikiwezekana hata kutoa mimba mpenzi!” alisema Daniel bila hofu yoyote ile.
“Yaani nitoe damu yako?”
“Kwani kuna tatizo?”
“Mbona hukumwambia mkeo atoe mimba ya mtoto wako?” aliuliza felista swali lililomuumiza Daniel lakini hakuwa na jinsi kwani kile alichoulizwa, kilikuwa ni ukweli mtupu.
Hakujua ni lipi alitakiwa kujibu, alitulia na kuamua kuondoka huku akiwa amechanganyikiwa. Felista alibaki akicheka tu, aliamini kwamba mimba haikuwa ya Daniel, alipewa mimba hiyo na Jackson ambaye alifika kwake huku akiwa hana hata mapenzi.
Lakini mbali na hilo akagundua kwamba Daniel hakuwa na mapenzi ya dhati kwake kwani kama kweli alikuwa na mapenzi ya dhati asingeweza kumwambia aitoe mimba hiyo na wakati alijua kwamba ilikuwa yake.
Nyumbani Daniel alikuwa na mawazo tele, moyo wake ulimuuma, alichanganyikiwa. Alimpenda felista lakini kitendo cha kubeba mimba aliyohisi kwamba ni yake kilimuumiza mno.
Kitu pekee kilichokuja kichwani mwake kilikuwa ni kuitoa mimba hiyo kinguvu. Yaani amuite ofisini mwake kwa lengo la kuzungumza naye na kumpa kahawa ambayo ndani ingekuwa na dawa ya kutoa mimba na kusafisha kabisa.
Hilo wazo likapita kichwani mwake, hakutaka kujiuliza, kilichotakiwa kufuata ni utekelezaji wa kile alichotakiwa kufanya. Kwa hali aliyokutana nayo, hakutakiwa kuwa na huruma tena, iwe isiwe ilikuwa ni lazima mimba ya Felista itoke.
Sehemu Ya 10
Kitu pekee kilichokuja kichwani mwake kilikuwa ni kuitoa mimba hiyo kinguvu. Yaani amuite ofisini mwake kwa lengo la kuzungumza naye na kumpa kahawa ambayo ndani ingekuwa na dawa ya kutoa mimba na kusafisha kabisa.
Hilo wazo likapita kichwani mwake, hakutaka kujiuliza, kilichotakiwa kufuata ni utekelezaji wa kile alichotakiwa kufanya. Kwa hali aliyokutana nayo, hakutakiwa kuwa na huruma tena, iwe isiwe ilikuwa ni lazima mimba ya Felista itoke.
***
Jackson alikuwa akipambana kwa nguvu zote, alionyeshewa mapenzi yote na Felista lakini moyo wake haukutaka kukubali kuwa na msichana huyo.
Walifanya mapenzi lakini mwisho wa siku alikumbuka kabisa kwamba huyo alikuwa kama rafiki yake ambaye alikuwa akifanya kazi fulani kwa ajili ya mtu fulani.
Walikuwa wakitoka na kwenda sehemu mbalimbali, walistarehe huku muda mwingi wakiwa wanapigiana simu. Lengo kubwa la kufanya hivyo lilikuwa ni kumsahaulisha msichana huyo na Daniel kitu ambacho kwa kiasi fulani kilionekana kuanza kufanikiwa.
Huku akiwa bize na Felista, kitu cha kushangaza moyo wake ukaanza kuzama kwa msichana huyo. Hakutaka kuona hilo likitokea, alijikaza mno, alifanya kila liwezekanalo kuhakikisha kwamba haangukii kwenye penzi la Felista lakini kikafika kipindi kila kitu kikaonekana kuanza kubadilika.
Kila alipokaa, alimkumbuka msichana huyo, kila alipokuwa akifanya hiki na kile ni picha ya Felista tu ndiyo iliyokuwa ikija kichwani mwake. Alikasirika, alichukia lakini moyo wake ndiyo ulianza kubadilika taratibu kiasi kwamba kila alipokuwa akikaa kimya pasipo kuwasiliana na msichana huyo, moyo wake ulijisikia tofauti kabisa.
Siku zikaendelea kukatika, penzi likaanza kuunyemelea moyo wake na mwisho wa siku kuanza kusikia wivu kila alipokumbuka kwamba Felista alikuwa akitoka kimapenzi na Daniel.
Alitamani kumwambia ukweli kuwa alitakiwa kuachana na mwanaume huyo lakini alishindwa kabisa kwani kama angefanya hivyo ilikuwa ni lazima kuharibu mambo kabisa kitu ambacho hakikutakiwa kutokea hata siku moja.
Alichokifanya ni kuanza kumpa ubize mwingi wa kuwa naye, hakutaka kuona msichana huyo akiwasiliana na Daniel kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma, alimbana na hata wakati mwingine kuichukua simu ile na kukaa nayo.
Hakutaka kuona akichukuliwa msichana huyo, alitokea kumpenda na kila alipokuwa akienda kazini, alihakikisha jioni anakwenda kumchukua hukohuko kazini.
Penzi likanoga, Felista alichanganyikiwa na kuona kabisa kwamba moyo wake ulitekwa na Jackson na kitu pekee alichokuwa akikihitaji ni kuzaa na mwanaume huyo tu.
Wakati akifikiria hilo ndipo akagundua kwamba alikuwa na mimba. Ilikuwa ni ya Jackson, moyo wake uliridhika mno na aliona kabisa hiyo ndiyo ilikuwa nafasi ya kuachana na Daniel hivyo kumwambia kwamba alikuwa na mimba.
Hakutaka kumwambia kama ilikuwa yake au la. Alihitaji kukaa kwa siku kadhaa ndipo amwambia kwamba haikuwa mimba yake, ilikuwa ya mwanaume mwingine hivyo alitakiwa kumuacha na kuendelea na maisha yake.
Wakati hayo yote yakiendelea, hakutaka kujificha, alichokifanya ni kumwambia Jackson kwamba alikuwa na mimba yake hivyo alitakiwa kulifahamu hilo.
Jackson akashtuka, hakuamini alichokisikia, moyo wake ulikuwa na furaha tele, alipenda kuwa na mtoto na ndiyo ilikuwa furaha yake katika maisha yake yote.
Akamsogelea Felista pale alipokuwa, akamsimamisha na kumkumbatia kwani katika vitu ambavyo alitamani sana kuwa navyo, cha kwanza kilikuwa ni mtoto.
“Nimefurahi kuniambia hivyo,” alisema Jackson huku akiwa amemkumbatia.
“Nashukuru kwa kunipa kitu nilichokuwa nakihitaji sana,” alisema msichana huyo na kisha kukumbatiana kwa kung’ang’aniana sana.
Wawili hao walifurahia, mapenzi waliyokuwanayo yakazidi kuongezeka pasipo kujua kwamba upande wa pili Daniel alikuwa akipanga jambo lake. Hakutaka kuona Felista akijifungua kwa kuamini kwamba hiyo ilikuwa mimba yake, kama mwanaume alitakiwa kupambana mpaka kuhakikisha kwamba mimba hiyo inaharibika hata kabla ya kujifungua.
Siku iliyofuata akaamka asubuhi, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu mke wake na kumsalimia, alizungumza naye kwa dakika kadhaa kisha kujiandaa kwa ajili ya kwenda kazini.
Kichwa chake kikaanza kumfikiria Felista, moyo wake ulimuuma mno, hakuamini kama kutembea nje ya ndoa kungemfanya kumpa mimba msichana fulani. Aliona kabisa ndoa yake ilikuwa ikienda kuvunjika kama tu angemucha msichana huyo ajifungue.
Ilikuwa ni lazima kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha mimba hiyo inaharibika. Kabla ya kufika ofisini, akapitia katika duka la dawa ambapo akaulizia dawa iliyokuwa na uwezo wa kutoa mimba ya msichana na kumsafisha kabisa.
“Ipo lakini huwa hatuuzi mpaka uwe na cheti kutoka kwa daktari,” alisema msichana aliyekuwa akiuza dawa.
“Kwa hiyo mpaka niwe na cheti cha daktari?” aliuliza Daniel.
“Ndiyo!”
Daniel akanyamaza, kichwa chake kikaanza kufikiria kitu kingine kabisa. Alijua kwamba hakuruhusiwa kununua dawa hizo kama tu hakuwa na cheki maalumu kutoka kwa daktari lakini aliamini kwamba kwa kutumia pesa angeweza kuzinunua dawa hizo bila tatizo lolote lile.
Hicho ndicho alichokifanya, akachukua noti tano za shilingi elfu kumi na kumgawia msichana huyo na kumwambia kwamba alihitaji sana hizo dawa kwa kuwa hakutaka kupata mtoto na wakati mtoto wake hakuwa ametimiza hata mwaka mmoja.
Msichana huyo hakuwa na jinsi, alizitamani pesa zile na asingeweza kuziacha hata kidogo. Akazichukua dawa hizo na kumpa Daniel dawa zilizoitwa Misoprosol ambazo mhusika alitakiwa kumeza vidonge viwili na baada ya saa sabini na mbili alitakiwa kumeza vidonge vinne.
“Nashukuru sana!” alisema Daniel na kuondoka mahali hapo.
Kidogo moyo wake ukafarijika, akawa na furaha kwamba hatimaye alikuwa akienda kufanikiwa kile alichokuwa akikitaka. Hakuchukua muda mrefu, akafika ofisini ambapo akateremka na kuingia ndani.
Alipofika, akajiachia kwenye kiti na kuendelea kufanya kazi zake kama kawaida. Moyo wake muda wote ulikuwa na mawazo tele, hakujua ni kitu gani kingetokea kama tu asingefanikiwa kwa kile alichokuwa amekikusudia.
Baada ya saa moja, akachukua simu yake na kumpigia Felista na kumwambia kwamba kama alikuwa na muda aende ofisini kwake kwani kulikuwa na vitu kadhaa alitaka kuzungumza naye, hususani mtoto ambaye alitarajiwa kuzwaliwa baada ya miezi tisa.
Hilo halikuwa tatizo, baada ya saa moja, akapigiwa simu na kuambiwa kwamba Felista alikuwa kwa sekretari hivyo kilichohitajika ni ruhusa yake. Kabla ya kuruhusu, haraka sana akaelekea kwenye meza ndogo iliyokuwa na chupa ya chai, akachukua vidonge vinne badala ya viwili, akavisaga na kuviweka katika kikombe ambacho ndicho alichotakiwa kummiminia chai msichana huyo.
Baada ya kuona kila kitu kipo sawa, akaruhusu msichana huyo aelekee ofisini kwake ambapo akaingia na kuelekea kwenye kiti kimoja na kutulia.
Wakaanza kuongea, muda wote Daniel alionekana kuwa na furaha, alimchangamkia Felista kana kwamba hakukuwa na kitu kibaya. Walikuwa wakiongea huku wakati mwingine wakigongesheana mikononi.
Felista alionekana kuwa na furaha tele na hakujua nini kingetokea kama mwanaume huyo angejua siku moja kwamba ile mimba haikuwa yake.
Baada ya kuzungumza kwa dakika kumi huku kiyoyozi kikipiga, Daniel akasimama na kumwambia amuekee chai ili awe anakunywa huku wakiendelea na mazungumzo yao.
“Nitashukuru!” alisema Felista.
Akaenda kwenye kile kimeza na kumimina chai vikombe viwili. Kile ambacho alitakiwa kunywa Felista kilikuwa upande wa kulia na kingine upande wa kushoto na kumpelekea.
Alihakikisha kile alichotakiwa kunywa msichana yule anampa na yeye kuchukua kile kingine na kukaa, wakaendelea na maongezi yao.
Felista alitaka kunywa chai ile lakini alishindwa kwa kuwa ilikuwa ya moto sana, Daniel alilijua hilo hivyo kumwambia kwamba hakutakiwa kuwa na wasi, asubiri kwanza ipoe ndiyo aenze kunywa.
Maongezi yaliendelea, baada ya sekunde kadhaa, Daniel akapigiwa simu na sekretari wake na kuambiwa kwamba kulikuwa na wageni walihitaji kumuona mara moja.
“Niwaambie waingie?”aliuliza sekretari.
“Hapana! Nakuja hapohapo!”
Hakutaka kubaki ndani, akamuaga Felista na kumwambia kwamba angerudi baada ya dakika kadhaa kwani kulikuwa na watu alitaka kuzungumza nao.
Akatoka na kukutana na watu hao. Walikuwa ni watu kutoka katika Kampuni ya Vodacom ambao walihitaji kuzungumza naye. Walikuwa watu muhimu, aliwakalisha hapo kwa sekretari na kuzungumza nao kwa dakika kumi kisha kurudi ofisini kwake ambapo akamkuta Felista akiendelea kunywa chai yake baada ya kupoa.
Moyo wake ukafurahi, alionekana kufanikisha kile alichokihitaji. Wakaendelea kupiga stori kama kawaida huku akimwambia kuwa alikuwa tayari kumlea mtoto wake kwa nguvu zote kwani aliamini kuwa mtoto ni baraka kutoka kwa Mungu.
“Nitamlea kwa nguvu zote. Ninapenda sana watoto, kama ni uwezo wangu, nitahitaji niwe na watoto zaidi ya watano,” alisema Daniel huku akionekana kuwa na furaha mno.
“Kweli mpenzi?”
“Niamini! Ninapenda sana watoto,” alisema Daniel huku akiwa na uhakika kwamba ile mimba ingetoka kwani tayari msichana huyo alikunywa chai iliyokuwa na dawa ile ya kutoa mimba ambayo ingeanza kufanya kazi baada ya saa kadhaa.
***
Daniel alizungumza sana na Felista na alipomaliza, msichana huyo akaondoka kurudi nyumbani kwake. Huku nyuma mwanaume huyo alikuwa na furaha tele, hakuamini kama alifanikisha mpango wake na muda wowote ule mimba aliyokuwanayo Felista ingetoka na hivyo kuachana naye huku msichana huyo akiwa hana cha kujidaia.
Alikaa ofisini na baada ya muda fulani akaondoka kurudi nyumbani. Njiani, alikuwa na furaha tele, moyo wake ulifarijika kwa kile alichokuwa amekifanya, alimpenda Felista lakini moyo wake haukutaka kupata mtoto kwa msichana huyo kwa sababu alikuwa na mke.
Alimchukulia kama msichana wa starehe ambaye alikutana naye pale alipotaka kutimiza haja za mwili wake na ndiyo maana hakuacha kumpenda mke wake ambaye aliamini kwamba ndiye Mungu aliyekuwa amemchagua na kuishi naye.
Kabla ya kufika nyumbani, akapata wazo la kwenda kumsalimia mke wake. Akachukua simu na kumpigia, ilipopokelewa, akamwambia kwamba angefika huko muda si mrefu.
Akaelekea huko na kuonana naye. Alipomuona, moyo wake ukafurahi, tabasamu pana likaonekana usoni mwake na kuona kwamba alikutana na mwanamke mrembo kupita wote katika dunia hii.
Kwa jinsi alivyokuwa akiishi na mke wake, ilikuwa ni vigumu kugundua kwamba aluwa akitembea nje ya ndoa, hakuonyesha mabadiliko yoyote yale kiasi kwamba hata wakati mwingine Jackline alijiona kufanya makosa kuhisi kama mume wake huyo alikuwa akitembea nje ya ndoa.
“Kazi vipi?” aliuliza Jackline huku akimwangalia mume wake.
“Ni nzuri! Nimechoka, nimekukumbuka sana mke wangu, nyumba nayo imekukumbuka, vyombo, mbwa wetu na kila kitu ndani ya nyumba kimekukumbuka,” alisema Daniel huku akimwangalia mke wake huyo.
“Tumewakumbuka pia, natumaini nitarudi baada ya siku kadhaa!” alisema Jackline.
“Kweli?”
“Ndiyo! Wala usijali mume wangu!” alisema Jackline.
Alikaa huko kwa zaidi ya dakika arobaini na tano kisha kuaga na kuondoka mahali hapo. Njiani, kichwa chake kikaanza kumfikiria tena Felista, msichana huyo alimkaa kichwani lakini hakutaka kumuendekeza sana kwani alitarajia kuachana naye wakati mimba hiyo itakapokuwa imetoka kabisa.
Alipofika nyumbani, simu yake ikaanza kuita, alipoangalia kioo, akakuta ni Felista, kwanza akahisi kwamba tayari mambo yalikubali na hivyo msichana huyo alikuwa akitaka kumpa taarifa kuhusu kuchomoka kwa mimba hiyo.
Akaipokea huku uso wake ukiwa na tabasamu pana, alikuwa akifarijika moyoni mwake kwani alikuwa na uhakika simu hiyo ingeufanya moyo wake kufurahia kupita kawaida.
“Niambie bebi!” alisema Daniel.
“Safi tu! Nimekaa na kitumbo changu hapa. Hivi tukipata mtoto wa kiume ungependa tumuite nani?” aliuliza msichana huyo.
Kwanza Daniel akabaki kimya, kile alichokuwa akikitegemea si kile alichokisikia. Alichokitegemea ni kwamba angepewa taarifa mbaya kuhusu kutoka kwa mimba hiyo lakini kitu cha ajabu kabisa alikuwa akipewa taarifa kuhusu jina la mtoto.
“Tumuite Dylan,” alisema Daniel huku akionekana kutokuwa na furaha.
“Kwa hiyo jina lake lianze na D kama baba yake?”
“Ndiyo hivyo! Ninayapenda majina ya D sana, yaani kama langu!” alisema Daniel huku akitamani hata kumuuliza msichana huyo kama alianza kusikia maumivu ya tumbo.
Walizungumza mengi, baada ya dakika kadhaa, akakata simu na kujipa uhakika kwamba kama si siku hiyo basi siku yoyote ile angepigiwa simu na msichana huyo kupewa taarifa kwamba mimba ilikuwa imetokea.
Siku ziliendelea kukatika, upande wa pili Jackson alikuwa akiendelea kuonyesha mapenzi yake kwa Felista, alimpenda msichana huyo na kila wakati alipokuwa naye alipenda kulishika tumbo la Felista na kujifanya akimsikiliza mtoto wake.
Moyo wake haukumpenda Daniel, alikuwa amepewa kazi kuhakikisha wawili hao wanaachana lakini kilichotokea ni kwamba akajikuta akitumbukia katika penzi na msichana huyo.
Hakutaka kumuacha peke yake, mara kwa mara alikuwa akimchukua na kwenda naye sehemu, walikuwa wakiyafurahia maisha na baada ya saa kadhaa kurudi na kuendelea na mambo mengine.
Kwa kile kilichokuwa kikiendelea, Jackson akashindwa kuvumilia, alihitaji wale watu waliomtuma wajue kila kitu, akachukua simu yake na kumpigia Pendo, msichana huyo alipopokea, akaanza kuzungumza naye.
Hakutaka kumficha, alimwambia ukweli kwamba kutumwa kwake kulimfanya kumpenda msichana huyo na mbaya zaidi alimpa mimba hivyo alitegemea kupata mtoto baada ya miezi tisa.
Pendo alivyosikia hivyo, alishangaa, hawakumtuma kijana huyo kwenda kumpa mimba Felista bali walimtuma kumuachanisha na Daniel. Ila hilo hakulilaumu sana kwani aliamini kwa kuwa alimpa mimba basi ilikuwa kazi nyepesi kuwaachanisha wawili hao kama walivyokuwa wamepanga.
Walizungumza kwa dakika kadhaa, baada ya kukata simu, Pendo akampigia Jackline na kuanza kuzungumza naye. Alimwambia kila kitu alichoambiwa na Jackson, kama alivyoona kwamba hilo lilikuwa jambo jema, naye akaungana naye na kuamua kumpigia simu kijana huyo ili asikie kwa masikio yake kile alichoambiwa.
“Nimesikia umempa mimba!” alisema Jackline.
“Ndiyo! Halafu huwezi kuamini, nimetokea kumpenda sana Felista, tena kwa moyo wangu wote!” alisema Jackson.
“Mmh! Wanaume nyie mmeshindikana!”
“Hahaha! Kweli tena! Yaani sikutaka kabisa hilo litokee lakini imeshindikana, moyo wangu umetekwa na sisikii la mtu yeyote yule,” alisema Jackson na kuanza kucheka.
Wiki ya kwanza ilikatika, wiki ya pili kuingia lakini Daniel hakupigiwa simu na Felista kuambiwa kama mimba ilitoka au la. Moyo wake ulihuzunika, muda wote alikuwa akijiuliza nini kilitokea lakini alishindwa kupata jibu kabisa.
Hakutaka kusubiri, alipoona wiki hizo zimekatika bila kupewa taarifa ya kuharibika kwa mimba, akampigia simu msichana huyo na kutaka kuonana naye.
Kwa felista ilikuwa vigumu kwa sababu muda wote alikuwa na Jackson, na hakutaka kumficha, alimwambia kwamba muda huo alikuwa na mpenzi wake hivyo hakutaka usumbufu kabisa.
“Na mimba?” aliuliza.
“Inaendelea vizuri kabisa. Nilikwenda kuangalia, nikaambiwa ni mtoto wa kike, ungependa tumpe jina gani?” aliuliza Felista huku akitoa tabasamu kana kwamba alikuwa akionana na Daniel.
“Jina? Jina? Daah! Hebu subiri kwanza,” alisema Daniel na kukata simu.
Alichanganyikiwa, moyo wake ulikuwa na presha kupita kawaida. Kwa usalama wa ndoa yake ilikuwa ni lazima mimba hiyo itoke kwa vyovyote vile. Hakutaka kuona msichana huyo akijifungua kwa kuamini kwamba kuna siku angempeleka mtoto huyo nyumbani kwake na hivyo kuzua kizaazaa.
Baada ya kuona hilo halikufanikiwa, moyo wake ukamwambia ni lazima awasiliane na dada wa lile duka alilomuuzia ili apate kujua kama kweli dawa ile aliyoinunua ilikuwa yenyewe au la, na kama ilikuwa yenyewe, kwa nini mpaka kipindi hicho mimba ya Felista haikuwa imetoka?
Sehemu Ya 11
“Jina? Jina? Daah! Hebu subiri kwanza,” alisema Daniel na kukata simu.
Alichanganyikiwa, moyo wake ulikuwa na presha kupita kawaida. Kwa usalama wa ndoa yake ilikuwa ni lazima mimba hiyo itoke kwa vyovyote vile. Hakutaka kuona msichana huyo akijifungua kwa kuamini kwamba kuna siku angempeleka mtoto huyo nyumbani kwake na hivyo kuzua kizaazaa.
Baada ya kuona hilo halikufanikiwa, moyo wake ukamwambia ni lazima awasiliane na dada wa lile duka alilomuuzia ili apate kujua kama kweli dawa ile aliyoinunua ilikuwa yenyewe au la, na kama ilikuwa yenyewe, kwa nini mpaka kipindi hicho mimba ya Felista haikuwa imetoka?
Hakutaka kubaki ofisini, haraka sana akaondoka mpaka kwenye lile duka, alipofika akaanza kuzungumza na msichana yule. Alimkumbuka vizuri sana, Daniel akamuuliza kuhusu zile dawa alizokuwa amezinunua.
“Kwani zimefanyaje?”aliuliza dada huyo.
“Nilimuwekea mke wangu, lakini mpaka leo naona haumwi tumbo, linazidi kukua tu, yaani tuna wasiwasi,” alisema Daniel huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Ulimuwekea kwenye chai kama nilivyokwambia?”
“Ndiyo!”
“Vidonge viwili?”
“Hapana! Niliweka vinne, yaani niliongeza dozi!” alisema Daniel.
“Na umesema mpaka leo mimba ya mkeo haijatoka?”
“Ndiyo! Yaani nimechanganyikiwa. Na haya maisha kupata mtoto mwingine ambaye hatujapanga, sijui itakuwaje!” alisema Daniel.
“Na chai alikunywa?”
“Ndiyo! Alikunywa! Tena tulikunywa wote,” alisema Daniel.
Kwa jinsi alivyokuwa akionekana tu ilikuwa ni rahisi kugundua kama mwanaume huyo hakuwa sawa, alichanganyikiwa kiasi kwamba kila kitu alichokuwa akikifikiria ni picha ya Felista ndiyo iliyomjia kichwani mwake.
Dada huyo akazungumza naye kwa kumridhisha kwamba hakutakiwa kukata tamaa kwani kuna siku angepewa taarifa kwamba mimba hiyo ilikuwa imeharibika kwani wakati mwingine huchukua hata mwezi lakini majibu ni lazima yapatikane.
***
Felista alikuwa ofisini kwa Daniel, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele kuhusu mimba ile. Alijua dhahiri kwamba haikuwa ya mwanaume huyo lakini aliamini kwamba kama angemwambia ukweli ingekuwa vigumu kuja kupata pesa tena.
Alipokorogewa chai na mwanaume huyo kwenda nje, alibaki mule ofisini huku akitaka kunywa chai ile. Alipoonja kidogo sana akagundua kwamba ilikuwa na majani mengi mno kiasi cha kumfanya hata kupata matatizo katika ujauzito aliokuwanao hivyo alichokifanya ni kulifuata sinki la maji, akaimwaga na kuchukua maji mengine, akamimina na kuweka majani kidogo na kurudi kwenye kiti kile.
Alitulia hapo na kuisubiria ipoe kwanza, ilipopoa, akaanza kunywa kama alivyotaka. Daniel aliporudi ndani ya ofisi hiyo, akamkuta msichana huyo akinywa chai ile, hakuwa na wasiwasi, aliamini kwamba chai ile aliyokuwa akinywa ilikuwa ileile aliyomuwekea hivyo kuanza kupiga stori huku akiwa na uhakika wa mimba ya msichana huyo kutoka.
Hakujua kama ile chai aliyokuwa amemuwekea aliimwaga na hivyo kuchukua maji mengine na kuweka majani ya chai kidogo kwa ajili ya afya yake.
***
Kile alichokuwa akikiamini Daniel hakikuweza kutokea, mimba ambayo aliamini kwamba ingetoka haikuweza kutoka tena. Alimwambia Felista kwamba anahitaji kumuona, alitaka kuzungumza naye lakini msichana huyo hakutaka kukubali tena kwa sababu alikuwa beneti na mpenzi wake, Jackson hivyo ilikuwa ni vigumu kuonana naye tena.
Walikuwa wakiwasiliana kwenye simu tu na muda mwingi Daniel aliogopa kwani alijua dhahiri kwamba mara baada ya mtoto kuzaliwa ilikuwa ni lazima msichana huyo aende nyumbani kwake na kumbwaga mtoto na kama siyo hivyo basi kitu kingine chochote ambacho kingeiweka ndoa yake katika hali mbaya.
Hakutaka kuona hilo likitokea, alijitahidi kwa nguvu kubwa kuhakikisha analimaliza suala hilo hata kabla mke wake hajagundua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.
Kwa sababu ilikuwa vigumu kuonana na msichana huyo, alichokipanga kilikuwa ni kuwatafuta watu kwa ajili ya kuifanya kazi yake. Hakutaka kuona akishindwa, kwake, ilikuwa ni afadhali jambo lolote lile limtokee msichana huyo lakini si kuona akipata mtoto kwake.
Wazo moja ambalo lilimjia kichwani mwake ilikuwa ni kumteka Felista. Alijua kwamba alikuwa akienda kufanya jambo la hatari mno lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima kupambana kwa ajili ya familia yake.
Hakujua ni kwa namna gani angeweza kuwapata watu wa kumfanyia kazi yake. Hakuwa akiwafahamu, hakujua walikuwa wakiishi wapi lakini aliamini kwamba kama kweli alidhamiria kuwatafuta, asingeshindwa kwa lolote lile.
Akawaulizia matajiri wenzake ambao hao ndiyo waliomwambia kwamba kulikuwa na kundi moja lililokuwa likiishi Manzese Darajani lililoitwa Cobra ambalo lilikuwa likifanya kazi hiyo bila tatizo lolote lile.
Kidogo akafurahia na kuona kabisa kwamba alikuwa akienda kufanikisha kile alichokitaka. Akatafuta mawasiliano yao, alipoyapata, haraka sana akawasiliana nao na kuwaambia kile alichohitaji kuona kikifanyika.
“Hilo si tatizo,” ilisikika sauti kutoka kwa mwanaume aliyekuwa upande wa pili.
Akawapa maelekezo yote kuhusu mahali alipokuwa akiishi msichana huyo, muonekano wake na kila kitu kilichokuwa kikihitajika. Alipomaliza, akawatumia kiasi cha pesa walichokuwa wakikihitaji na kuwatakia kazi njema.
Kundi hilo likaanza kupanga mipango kuhakikisha kazi hiyo inafanyika haraka sana. Hawakutaka kupoteza muda, walijua kabisa kwamba walilipwa vizuri hivyo ilikuwa ni lazima kuhakikisha wanaifanya kazi hiyo.
Baada ya siku moja, vijana wa kundi hilo la Cobra wakaanza kufanya kazi yao. Ilikuwa ni lazima waifanikishe ndani ya muda hivyo walichokifanya ni kwenda katika nyumba aliyokuwa akiishi Felista kwa lengo la kumteka.
Walihitaji kumteka katika kipindi ambacho alichokuwa akitoka nyumbani kwa na kuelekea kliniki. Waliamini kwamba wangefanikiwa katika hilo kwani kama mwanamke mjauzito ilikuwa ni lazima kwenda huko.
Ilipofika majira ya saa 5:10, Bajaj moja ikaanza kusogea katika geti la nyumba hiyo na kusimama, walijua dhahiri kwamba ilikuja kumchukua msichana huyo na kwenda naye kliniki.
Wala hazikupita dakika nyingi, wakamuona Felista akitoka ndani ya nyumba ile na kuingia ndani ya Bajaj na kuondoka mahali hapo. Hawakutaka kubaki, walichokifanya ni kuanza kuifuatilia kwa gari lao.
Kwa kuwa mitaa hiyo ilikuwa kimya kabisa, hawakutaka kuwafikisha barabarani bali ni kuwawahi na kwenda kwa mbele na kulisimamisha gari lao.
Hilo ndilo walilolifanya, wakalisimamisha gari hilo mbele ya Bajaj ile na wanaume wawili waliokuwa na bastola kuteremka.
Kila mmoja aliyekuwa ndani ya Bajaj ile akaogopa, bastola zile ziliwatisha na kuona kwamba walikuwa wakienda kuuawa kinyama mahali pale.
Wakawasogelea, hawakutaka kumjeruhi mtu yeyote, wakamwambia Felista ateremke ili waondoke naye. Huku akiwa na kitumbo chake, Felista akatereka, alikuwa akitetemeka kwa hofu, hakuamini kama watu wale walimfuata yeye kwa lengo la kumteka.
“Jamani msiniue…jamani msiniue,” alisema Felista huku akitetemeka, na kilio juu.
Akachukuliwa na kuingizwa ndani ya gari lile na kuondoka mahali hapo. Humo garini alikuwa akilia, aliomba msamaha pasipo kujua kosa alilokuwa amelifanya.
Hakuwa na ugomvi na mtu, hakuwahi kulumbana na mtu yeyote yule, alimheshimu kila mmoja, kila alipojiuliza kuhusu utekaji ule alishindwa kupata jibu na wakati mwingine alihisi kwamba watu hao walikosea na kumteka mtu ambaye hakuwa tageti yao.
“Jamani naomba msiniue, naomba msiniue,” alisema Felista huku akilia.
“Usijali Felista! Hutokufa, ila ukiongea sana, kulia sana, tutakuua,” alisema mwanaume mmoja.
Kitendo cha kutajwa jina lake kikamfanya kugundua kwamba watu wale hawakukosea kumteka mhusika, alihitajika yeye na ndiyo maana walimfuata na kumteka.
Hakujua kosa alilokuwa amelifanya, aliomba msamaha lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa akijali. Akafungwa kitambaa usoni huku gari kuendelea na safari.
Alibaki akimuomba Mungu tu, hakujua ni kitu gani kilikuwa kikienda kutokea huko. Moyo wake ulimuuma na muda wote alikuwa akiomba sala yake ya mwisho kwani muda wowote ule angeweza kuuawa kinyama.
Safai iliendelea kwa dakika kumi na tano ndipo gari likasimama ndani ya jumba moja kubwa lililokuwa uswahilini. Akateremshwa na kuingizwa ndani huku akiwa amefungwa kitambaa machoni mwake.
Akapelekwa mpaka katika chumba kimoja na kutolewa kitambaa kile. Mandhari ya chumba kile ilimtisha kupita kawaida. Kulikuwa na michirizi ya damu, kiti kilichokuwa na uwazi mkubwa sehemu ya kukalia.
Kulikuwa na nyaya za umeme, pasi ya umeme na vitu vingine ambavyo vyote hivyo vilikuwa na kazi ya kuwatesa watu waliokuwa wakiingizwa humo.
Moyo wake ukaogopa, hofu kubwa ikautawala moyo wake na kujipa uhakika kwamba hakutakiwa kutoka salama ndani ya chumba hicho. Kilio chake kikaanza upya, akaanza kulia kwa maumivu makali, alimlilia Jackson, alikililia kiumbe chake kilichokuwa tumboni, kwa kifupi, hakuwa na uhakika wa kutoka salama.
“Mpigie simu bosi,” alisema mwanaume mmoja maneno ambayo yalisikika vema masikioni mwa Felitsa.
Haraka sana simu ikapigwa na baada ya sekunde kadhaa kijana huyo akawa anazungumza na mwanaume kutoka upande wa pili, alikuwa ni Daniel.
Alichokihitaji yeye si kuuawa kwa Felista bali kitu alichokihitaji ni kingine kabisa. Alimwambia kijana huyo kwamba lengo lake lilikuwa ni kuhakikisha mimba hiyo inatoka kwani hakuwa na mpango wa kuwa na mtoto wa nje hata kidogo.
Aliwaambia waende kwenye duka la dawa ambapo huko wangenunua vidonge viitwavyo Misoprosol na kwenda kumnywesha msichana huyo.
“Hakuna shida bosi.”
“Ila hakikisheni mnapewa Misoprosol, tena vidonge vyote inabidi anyweshwe kwa mkupuo!”
“Sawa bosi!”
Baada ya kuzungumza na Daniel, kilichofuata kilikuwa ni kuwaambia wenzake kile alichoambiwa. Hakuongea kwa sauti ya chini kama siri, aliongea kwa sauti ya kawaida ambayo iliweza kusikika mpaka kwa Felista aliyekuwa chumbani.
“Kwa hiyo lengo lake ni kuitoa mimba hiyo?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Ndiyo! Yaani kwa kifupi ni kwamba hataki mtoto wa nje ya ndoa,” alisema jamaa aliyeongea kwenye simu.
“Basi sawa! Hilo si tatizo, ila kwa tumbo lake lile, tukimpa hivyo vidonge si atakufa?”
“Nahisi itakuwa hivyo! Ila hatuna jinsi, jamaa katupa hela nyingi hivyo tufanyeni kama anavyotaka, ngoja nifuate vidonge,” alisema kijana huyo aliyeitwa Ramadhani na kwenda kununua vidonge hivyo.
Mule ndani alipokuwa Felista hakuamini alichokisikia, moyo wake ulimuuma baada ya kugundua kwamba mtu aliyekuwa nyuma ya kila kitu ni Daniel.
Alilia mno, alijuta kuwa na mwanaume huyo, alijuta kumdanganya kwamba mimba ilikuwa yake. Hakuona kama angefanikiwa kutoka salama humo kama tu angenyweshwa dawa hizo za kutoa mimba.
Mimba yake ilitimiza miezi saba kwa maana hiyo ilikuwa ni lazima afe tu kama tu angekunywa dawa alizokuwa akitakiwa kupewa.
Alibaki akimuomba Mungu, hakuona tumaini kama angeweza kupona kutoka katika mikono ya watu hao salama. Alisali kila sala aliyokuwa akiifahamu kwani alijua baada ya muda fulani tu angenyweshwa dawa za kuondoa mimba ambazo ilikuwa ni lazima zimuue.
Ndani ya dakika ishirini, kijana aliyekuwa ametumwa kununua dawa hizo, Ramadhani akarudi huku akiwa na dawa hizo mikononi mwake. Mwenzake akazichukua na kusoma kiboksi chake, ziliandikwa Misoprosol.
“Safi sana!” alisema mwanaume huyo.
Hakukuwa na sababu ya kupoteza muda, haraka sana maji yakaletwa yakiwa kwenye glasi, akafumbuliwa mdomo na kuanza kunyweshwa vidonge hivyo.
Felista alikuwa akinywa huku akilia, alijua kabisa kilichokuwa kikifuata baada ya dakika chache ni kufariki dunia. Wanaume hao wakahakikisha mpaka dawa hizo amezinywa zote na kumtoa nje ambapo wakamwambia aondoke kwani hawakutaka msichana huyo afie mikononi mwao ndani ya chumba hicho.
Felista akaondoka, alikuwa analia, aliamini kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake. Hakujua alikuwa wapi, alitembea kwa dakika kama tano, akahisi mwili wake ukiishiwa nguvu, hakuweza kupiga hatua zaidi, akaanza kuona giza, hapohapo akaanguka chini na kutulia.
***
Fred ndiye ambaye alitumwa kwenda kununua dawa ya Misoprosol kwa ajili ya kutoa mimba ya Felista. Aliondoka mahali hapo huku akiwa na mawazo tele.
Hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea, kila siku alikuwa akifanya kazi na kundi lake hilo, alikuwa muuaji ambaye alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile. Siku hiyo ambayo walikwenda kumteka Felista, moyo wake ulimuuma mno.
Hakuamini kama walitakiwa kumuua mwanamke aliyekuwa na ujauzito, kila alipokuwa akimwangalia msichana yule jinsi alivyokuwa akilia, tumbo lake moyo wake ulimuuma kupita kawaida.
Hakutaka kumuua, hakutaka kuona msichana huyo akifa, kwake, hakumfikiria zaidi yeye bali alifikiria kile kiumbe kilichokuwa tumboni. Alijua kabisa watoto wengi wanaozaliwa katika mazingira hayo, nje ya ndoa ndiyo wanakuwa maisha mazuri hapo baadaye, alikumbuka kuhusu mfalme Daudi, jinsi alivyomtamani mke wa askari wake na kuamua kumuua vitani ili amchukue mkewe.
Mtoto aliyezaliwa kwenye dhambi hiyo ndiye alikuja kuwa mfalme Suleimani ambaye alibarikiwa kuliko wafalme wote katika dunia hii. Alijua kabisa kwamba Mungu alikuwa na mipango na mtoto huyo na ndiyo maana hakutaka kabisa kushiriki dhambi kubwa namna hiyo.
Alielekezwa mpaka kwenye duka la dawa na kwenda huko, alipofika, akamuuliza muuzaji vidonge ambavyo isingekuwa hatari kwa mwanamke mjauzito kunywa, yaani hata akinywa, asife.
“Ninahitaji vidonge vya malaria kwa ajili ya mjauzito,” alisema Fred huku akimwangalia dada aliyekuwa akiuza.
“Vipi?”
“Wewe una vipi?”
“Vipo vya aina nyingi.”
“Naomba ambavyo ni vizuri,” alisema Fred na msichana huyo kumpa vidonge vilivyoitwa Clindamycin.
Akamuelekeza jinsi ilivyotakiwa kutumika, ilikuwa kwenye kiboksi kilichokuwa na dawa sita. Fred aliyasikiliza maelezo vizuri na kisha kuondoka mahali hapo huku akiomba kikaratasi kingine cha akiba kwa ajili ya kuwekewa dawa.
Alipofika njiani, akapitia dukani na kuandika kwenye kikaratasi kile Misoprosol na kuondoka kurudi katika jumba lile walilomuhifadhi Felista.
Alipofika, akawaonyeshea wenzake dawa zile ambapo wakachukua na kumnywesha Felista vidonge vitatu kwa kuamini kwamba vingefanya kazi na kumuondoa mahali hapo.
Moyo wa Fred ukaridhika japokuwa alijua kabisa alitakiwa kumfuatilia msichana huyo ili hata kama angepata tatizo njiani basi amsaidie. Alipowaambia wenzake kwamba alitakiwa kuondoka, walimkatalia kwani bado walikuwa na mambo mengine waliyotakiwa kufanya, hivyo akabaki na kumuomba Mungu amlinde Felista kule alipokuwa.
Felista alishtuka na kujikuta akiwa kitandani. Mkononi mwake kulichomwa sindano ambayo ilikwenda moja kwa moja mpaka kwenye dripu ya maji iliyokuwa imening’inizwa kwa juu.
Hakutaka kujiuliza mahali hapo palikuwa wapi, alijua kabisa kwamba palikuwa ni hospitalini, swali ambalo lilikuja kichwani mwake ni jinsi alivyofika hospitalini humo.
Akajiinua na kuangalia huku na kule, ndani ya chumba kile alikuwa peke yake. Kumbukumbu za kile kilichotokea zikaanza kumjia kichwani mwake, alikumbuka jinsi alivyotekwa na watu wale kisha kupelekwa ndani ya nyumba moja na kunyweshwa dawa.
Hapo, pia akakumbuka kuhusu maneno yao, moyo wake ulimuuma baada ya kugundua kwamba mtu aliyekuwa amefanya hayo hakuwa mwingine bali Daniel ambaye kila siku alimwamini na kumdanganya kwamba alikuwa na mimba yake, ili mwanaume huyo kuhakikisha hapati mtoto nje ya ndoa, akaamua kuwatuma watu wamteke na kumnywesha dawa ili mimba itoke.
Akabaki akilia kwa uchungu, moyo wake ulimuuma mno, hakuamini kama mwanaume huyo ndiye aliyefanya hilo huku akiwa na lengo la kumuua yeye na mtoto wake wa tumboni.
Alilia sana lakini hakuwa na jinsi, baada ya dakika kadhaa nesi akaingia ndani ya chumba hicho na kumjulia hali, alimwambia kwamba alipelekwa mahali hapo na wasamaria wema ambao walimuokota alipokuwa ameanguka barabarani na alifanyiwa vipi kukaonekana hakuwa na tatizo lolote lile.
Alimshukuru Mungu, akaomba simu na kumpigia Jackson ambaye baada ya dakika kadhaa akafika hospitalini hapo. Alishangaa kumkuta mpenzi wake hospitalini huku akionekana kuwa na tatizo fulani, akauliza kilichotokea, akaambiwa jambo lililomshtua yeye mwenyewe.
“Hebu niambie kuna nini?” aliuliza Jackson aliyeonekana kujiuliza sana juu ya kile kilichokuwa kimetokea.
“Nilitekwa!”
“Na nani?”
“Sijajua! Ila lengo lao lilikuwa ni kutoa mimba yangu, kwa maana hiyo ningeweza kufa,” alijibu Felista.
Alipoambiwa hivyo tu, Jackson akahisi kwamba aliyefanya jambo hilo alikuwa Daniel hivyo kutoka ndani ya chumba hicho na kumpigia simu Jackline na kuanza kuzungumza naye.
Mwanamke huyo alishtuka, hakuamini kama mume wake angeweza kufanya jambo kama hilo hivyo kumwambia waonane.
“Mumeo awe makini, nitaweza kumuua,” alisema Jackson huku akionekana kumaanisha alichokisema.
“Hebu tuonane kwanza!”
“Sawa.”
Jackson akamuaga Felista na kuondoka mahali hapo huku lengo likiwa ni kuonana na Jackline, baada ya dakika kadhaa, akaonana na mwanamke huyo katika Hoteli ya Wanyama na kuanza kuongea.
Alimwambia kilichotokea na alikuwa na uhakika kwamba Daniel ndiye aliyekuwa amesababisha hayo yote kwa kuhisi kwamba mimba ilikuwa yake kitu ambacho hakikuwa kweli kabisa.
“Kwa hiyo!”
“Tumtumie huyuhuyu Felista! Nataka tuchukue chumba, Felista amuite kuzungumza naye, wakati huo wewe na mimi tunakuwa chooni, akija, tunatokea na kuzungumza naye,” alisema Jackson.
Wakakubaliana na kuwasiliana na Pendo, siku hiyo naye alitakiwa kuwepo kwani walihitaji kufanya kitu ambacho Daniel asingejua kama nyuma ya hicho walikuwepo wao.
Hilo halikuwa tatizo, Jackson akaondoka na kurudi hospitali ambapo akaanza kuzungumza na Felista na kumwambia kuhusu mpango waliokuwanao.
Felista alishtuka, hakuamini kama Jackson alikuwa akifahamu kila kitu kilichotokea. Hakuwa na jinsi, akakubaliana naye na hivyo baada ya kutoka hospitali, siku iliyofuata akachukua simu na kumpigia Daniel huku nyuma tayari watu watatu, Jackson, Jackline na Pendo walikuwa ndani ya chumba namba 27 katika Hoteli ya Pacifician Royal iliyokuwa Mikocheni B.
***
Daniel alikuwa na uhakika kwamba vijana wale walifanya kazi kama alivyotaka ifanyike, moyo wake ulikuwa na furaha baada ya kupigiwa simu na kuambiwa kwamba kila kitu kilifanyika kwa mafanikio makubwa na hivyo ajiandae kusikia taarifa za kifo chake kwani kwa jinsi mimba ile ilivyokuwa kubwa, lisingekuwa jambo la kawaida kufa mtoto na mama kupona.
Alikaa na presha nzito, kwake, kuua halikuwa tatizo tena, alifanya kila liwezekanalo kuhakikisha kwamba Felista anakufa hivyo alichokuwa akisubiri ni taarifa kuhusu kifo cha msichana huyo.
Siku iliyofuata, majira ya saa 4 asubuhi, huku akiwa ofisini kwake akapigiwa simu na Felista ambaye aliomba kuonana naye. Kwanza hakuamini kuisikia sauti ya msichana huyo, alichoamini ni kwamba alikufa baada ya kunywa vidonge, sasa ilikuwaje ampigie simu na kumwambia kwamba alitaka kuonana naye.
Kwa jinsi alivyokuwa akizungumza kwa kilio, akahisi kwamba alitaka kumpa taarifa ya kutoka kwa mimba yake hivyo alivyoambiwa kuonana naye, hakutaka kuchelewa, akaelekea katika hoteli hiyo kwa lengo la kumuona msichana huyo.
Alipofika, haraka sana akateremka na kwenda mpaka mapokezini ambapo akaomba kuonana na msichana aliyekuwa katika chumba namba 27. Simu ikapigwa mpaka huko, Felista akathibitisha kumfahamu mwanaume huyo na hivyo kuruhusiwa kwenda huko.
Alipofika, akaingia kwa kujiamini, alimuona Felista amekaa kwenye kiti huku akionekana kuwa na huzuni tele, kitendo cha kumuona vile tu, Daniel akawa na uhakika kwamba kila kitu kilikuwa poa.
“Kuna nini mpenzi? Mbona unalia?” aliuliza Daniel huku akimsogelea msichana huyo.
Akamshika na kumvutia kwake, alitaka kuona kama mimba ilikuwepo, alipoliangalia tumbo, lilikuwa vilevile kiasi kwamba ilionekana kumshangaza kupita kawaida, alitamani kuuliza lakini alikosa jibu kabisa.
“Umefurahi mimi kubeba mimba yako?” aliuliza Felista huku akimwangalia mwanaume huyo.
“Nani? Mimi? Kwa nini nichukie sasa?” aliuliza Daniel huku akimwangalia msichana huyo.
“Sasa kwa nini ulituma watu waniteke na kutaka kuniua kwa kuninywesha vidonge?” aliuliza felista.
Swali hilo lilimshtua Daniel, alimwangalia msichana huyo huku akionyesha mshtuko aliokuwa ameupata. Hakutegemea swali kama hilo, hakutegemea kuona msichana huyo akifahamu kile kilichotokea, sasa nani alimwambia?
“Eti! Kwa nini ulitaka kuniua na mtoto wangu?” aliuliza Felista huku akianza kulia.
“Felista! Ulichokisikia si kweli, naanzaje kumuua mtoto wangu?” aliuliza Daniel huku akionekana kutokujiamini.
“Ulitaka kuniua, kwa nini?”
“Mpenzi…”
“Nijibu kwanza!”
Daniel akabaki kimya kama mtu aliyekuwa akijifikiria kitu fulani. Wakati akiwa kwenye hali hiyo, mara mlango wa chooni ukafunguliwa na Jackson kutoka.
Daniel alipigwa na mshangao, hakumfahamu mwanaume huyo alikuwa nani na kwa nini alikuwa ndani ya chumba hicho. Akasimama na kuanza kumfuata.
“Kwa hiyo ulitaka kumuua mtoto wangu?” aliuliza Jackson swali lililomfanya Daniel kusimama kwanza, akayarudisha macho yake kwa Felista.
“Daniel! Kwa nini ulitaka kumuua mtoto wa mwanaume mwenzako?” aliuliza Felista huku naye akisimama na kumwangalia mwanaume huyo.
“Felista! Yaani ulikuwa ukinisaliti?” aliuliza Daniel.
“Nilikwambia kwamba nina mpenzi!”
“Sasa ndiyo unisaliti! Wewe wa kunifanyia hivi kweli?”
“Mbona hata wewe ulimsaliti mkeo, au umesahau?”
Daniel akabaki kimya, alionekana kuwa na hasira kupita kawaida, alitamani amfuate Jackson na kupigana naye kwani hakutamani kabisa kuona Felista akichukuliwa na mwanaume mwingine.
Wakati akijifikiria kumvamia Jackson, mara mlango wa chooni ukafunguliwa na mkewe kutoka. Moyo wa Daniel ukapiga paa! Hakuamini alichokuwa akikiona, macho yake yakatua kwa Jackline ambaye alikuwa akilia tu.
Akaishiwa nguvu za miguu na kujikuta akikaa kitandani, machozi yakaanza kumlenga kwani hakuamini kama Jackline alikiona kile kilichokuwa kimetokea.
Alihuzunika, moyo wake ukaanza kujutia kile alichokuwa amekifanya. Kukaa kimya haikusaidia, kama mwanaume alitakiwa kuzungumza neno lolote lile hata kumuomba msamaha mke wake kwa kile kilichotokea.
Akasimama na kumsogelea Jackline, alipofika karibu naye, akapiga magoti na kumshika miguu yake. Alishindwa kuzungumza kitu chochote kile, alibaki akilia tu, moyo wake ulimuuma, mwanamke mzuri kabisa ambaye alimwambia kuwa alimpenda kwa mapenzi ya dhati leo hii alikuwa akimsaliti kwa msichana mwingine.
“Mke wangu! Naomba unisamehe!” alisema Daniel huku akimwangalia mke wake, tena huku akiwa amepiga magoti.
“Daniel! Ulikosa kitu gani kwangu?” aliuliza Jackline huku akilia.
“Sikukosa kitu chochote kile!”
“Kwa nini ulikuwa unanisaliti? Kwa nini umeamua kuniumiza kwa namna hii?” aliuliza Jackline huku akimwangalia mume wake huyo.
Alishindwa kuzungumza lolote lile, kila swali alilokuwa akiulizwa lilikuwa gumu kujibika, hakujitetea zaidi ya kuomba msamaha tu kwani kwa kile alichokifanya kilikuwa ni cha aibu mno.
Alilia kupita kawaida, hakuangalia kama alikuwa mbele ya mwanamke mwingine, hiyo ilikuwa nafasi yake ya kuinusuru ndoa yake. Hakuangalia suti yake, alikuwa akilia huku akiwa amepiga magoti.
Jackline hakuwa na kinyongo, alijua kwamba mume wake alianguka na kamwe hakutaka kuzaa nje ya ndoa na ndiyo maana aliamua kuchukua uamuzi mgumu wa kutaka kuua mtoto.
Alimpenda, pamoja na kugundua kwamba mume wake alikuwa akisaliti, hakutaka kuonyesha kinyongo chochote kile, kama alivyokosewa alijua kabisa kwamba kuna siku naye angeweza kumkosea mwanaume huyo kwa kuwa moyo wa binadamu haukukamilika hata kidogo.
Akaamua kumsamehe kwa kuamini kwamba hilo lilikuwa onyo kubwa na tishio kuliko hata kama angeamua kuondoka na kurudi nyumbani kwao na kuwa mwisho wake kuwa naye.
Akamnyanyua na kumkumbatia. Wote hawakuamini, waliamini kwamba Jackline angechukua uamuzi mgumu lakini matokeo yake aliwaonyeshea kwamba kwenye mahusiano ya ndoa, kuna msamaha, kitu ambacho kila mwanandoa alitakiwa kukifanya kwa mtu wake.
“Nimekusamehe!” alisema Jackline, kila mmoja mahali pale akashusha pumzi ndefu.
Hilo likawa kama fundisho kwa Daniel, hakutaka kumsaliti tena mke wake, hakujiamini, kila msichana mzuri ambaye alipita mbele yake kumbukumbu zake zilirudi kwa Felista aliyesababisha kuonekana kuwa msaliti.
Penzi lake kwa mke wake likaongezeka, kwa kile kilichokuwa kimetokea, kilimpa fundisho. Kwa kuwa alifumaniwa pasipo kufanywa kitu chochote kile, hilo likamfanya kutokuthubutu kufanya kitu chochote nje ya ndoa.
Kwa upande wa Felista, msichana huyo akafanikiwa kujifungua mtoto wa kike na kumuita jina la Love yaani likimaanisha upendo mkubwa aliokuwanao kwa mpenzi wake huyo ambaye baadaye wote kwa pamoja wakaamua kuoana na kuishi pamoja.
MWISHO

