ROHO YAKE INADAI
ONYO: Wakubwa tu, kuanzia Miaka 18, ndio wasome hii Hadithi
Sehemu Ya 4
Binti huyo mdogo alikuwa anatazama hapo dirishani. Ni kama vile alikuwa anamwona Brian na pia anamfanyia mazingatio. Brian akamtazama vema binti huyo. Akili yake ikamwambia ndiye mtu aliyemwona kwenye ndoto siku ile. Akili yake ikamwambia kuwa binti yule ni Kecie!
.
.
Brian akafikicha macho yake kama mtu asiyesadiki. Alipotazama tena, bado akamwona binti yule! Alikuwa amesimama kama mstimu akimtazama, ila wanafunzi wengine walikuwa wanampita kana kwamba hamna kitu. Ina maana walikuwa hawamwoni!
.
.
“Kecie!” Brian akasema kwa kunong’ona. Ajabu binti yule akatikisa kichwa chake kuitikia, na taratibu akaanza kujongea kufuata dirisha alimo Brian.
.
.
Pale alipokuwa anakutana na wanafunzi wengine, Kecie akapita kana kwamba moshi ama kivuli. Macho yake yalikuwa yanatazama dirisha na macho ya Brian pekee. Hatua zake zilikuwa za taratibu ila zinazomfikisha kwa wepesi mno!
.
.
Brian akatoa macho.
.
.
“Kecie!” akanong’ona tena akiita. Moyo wake ulikuwa unapiga kwa kasi. Alisimama afuate dirisha kumtazama Kecie. Masikioni mwake alikuwa anasikia sauti ya kunong’ona, sauti ya kike, ikisema, “Niokoe, Brian … Niokoe, Brian.” Ila kabla hajafika dirishani, akashikwa mkono na kuvutwa.
.
.
“Brian!” alipotazama akakutana uso kwa uso na Dkt Hamill. Dkt alikuwa anamtazama kwa mshangao, na pia Georgina alikuwa ameduwaa kumwangalia.
.
.
“Nini shida?” Dkt Hamill akauliza. Brian akatazama kule dirishani, hakukuwa na mtu, hata wanafunzi walikuwa tayari wamesharudi kwenye madarasa yao.
.
.
Dkt Hamill akamtazama Georgina na kumwambia, “Naomba utupishe.” Georgina alipofanya hivyo, Dkt Hamill akamkalisha Brian kwenye kiti kisha na yeye akaketi mahala pake.
.
.
“Brian, niambie ulikuwa unaona nini dirishani?”
.
.
Brian akatazama tena dirishani, kulikuwa kweupe hamna jambo. Akaurudisha uso wake kwa Dkt na kumwambia kwa sauti ya chini, “Kitu cha ajabu!”
.
.
“Brian,” Dkt akaita. Akamtazama kwa macho ya udadisi na kumuuliza, “Kecie ni nani?”
.
.
Brian akanyamaza. Bado alikuwa kwenye ombwe la mawazo. Hakuwa anajua cha kusema.
.
.
“Brian, niambie kila kitu. Acha kunificha. Nitakusaidia.”
.
.
Brian akavuta kwanza pumzi ndefu. Akatazama chini akifikiri jambo kisha akaamua kukata shauri kusema kila kitu kwa Dkt Hamill. Basi asifiche kitu akaeleza kinaga ubaga. Simulizi yake ikamwacha Dkt akiwa ameachama.
.
.
“Brian, una kazi kubwa,” Dkt akasema na kisha akakuna kidevu chake. Akashusha pumzi ndefu na kupangilia vema maneno mdomoni.
.
.
“Kecie hajafa. Yupo mahali na anataka ukamwokoe.”
.
.
“Mahali gani?” Brian akauliza. Kabla Dkt Hamill hajajibu, akamwambia, “Brian, haitakuwa rahisi hata kidogo. Kecie sasa ni mali ya Helo!”
.
.
“Kivipi?”
.
.
“Michoro uliyoikuta kwa Faris kulikuwa na mwanaume kando yake, sio?”
.
.
“Ndio,” Brian akajibu.
.
.
“Maneno yale ambayo Faris ameyaandika kwenye kitanda ni yale aliyosema Helo pindi anakufa!”
.
.
“Kwahiyo ina maanisha nini?”
.
.
“Helo amerudi!” akasema Dkt Hamill. “Na ndiye huyo unayemwona akiwa anaongozana na Kecie.”
.
.
“Sasa tutafanyaje?” akauliza Brian kwa kimuhe.
.
.
“Bado sijajua, ila … kuna haja ya kwenda kuonana na Faris. Kuna mengi ya kujua toka kwake. Ni wazi yeye ndiye atakuwa daraja letu.”
.
.
Kukawa kimya kidogo. Dkt akasonya na kutikisa kichwa.
.
.
“Kwanini Helo hajaanza kuwamaliza watu wa mji huu?” akauliza akitazama dirishani. Hilo swali lilikuwa ni kubwa na lilimtafuna kichwa. Lazima kutakuwa kitu, aliamini.
.
.
.
**
.
.
Kesho yake majira saa sita mchana …
.
.
Watu kumi na wawili walikuwa makaburini wakiwa wamevalia nguo nyeusi. Walikuwa wameketi kwenye viti na mbele yao kukiwa na shimo refu lililofunikwa na jeneza.
.
.
Padri Alfonso akiwa amevalia nguo zake za kazi ndiye alikuwa anaendesha misa. Na alikuwa ukingoni. Alipomaliza jeneza lilishushwa chini na watu wakaanza kuweka udongo wakianza familia ya marehemu.
.
.
Wakatia pia maua na kisha watu wakaanza kuparanganyika kwenda majumbani mwao. Nyuma wakaachwa Mrs Garett, Olivia, Brian na mamaye.
.
.
Wageni wakawa wanateta kuwapoonza wafiwa. Wakatembea mpaka kufikia kwenye gari la Mrs Garett, hapo mama huyo akaomba kuonana na kuongea na Brian faragha. Kabla Mama Brian hajapisha, akamtazama mwanaye kisha akainamisha kichwa kuafiki. Akatangulia zake.
.
.
Brian akaingia kwenye gari la Mrs Garett akiketi viti vya mbele.
.
.
“Brian,” Mrs Garett akaita kisha akanyamaza kwa sekunde kadhaa. “Kuna kitu nataka kukuuliza na tafadhali naomba uwe mkweli.”
.
.
“Usijali, mama. Nitakuwa mkweli,” akasema Brian akianza kubuni kinachofuatia.
.
.
“Ushawahi kumwona Kecie?” mama akauliza. Kisha akamtazama Brian machoni.
.
.
“Kumwonaje, Mrs Garett?” Brian akauliza.
.
.
“Kwa vyovyote tu,” Mrs Garett akasema. “Tangu amepotea, ushawahi kumwona popote pale … akifanya lolote lile? Tafadhali naomba kuwa mwaminifu.”
.
.
Brian akanyamaza kidogo na kusema, “Nishawahi onana naye. Jana ilikuwa mara ya mwisho nikiwa shuleni.”
.
.
Jambo hili likaonekana kumshtua kidogo Mrs Garett, akauliza, “Unapomwona anakuambia nini? … kuna kitu chochote anakwambia?”
.
.
Brian akasita. “Kuna nini Mrs Garett?”
.
.
“Nataka tu kujua … niambie, Brian.”
.
.
Uso wa Mrs Garett ulionyesha mashaka ndani yake. Aidha kuna habari aliyokuwa anatarajia toka kwa Brian.
.
.
“Huwa ananiambia nimwokoe,” akajibu Brian. “Kila ninapomwona ananisihi nimwokoe.”
.
.
“Umwokoe?” Mrs Garett akastaajabu. Kwa akili yake alidhani Kecie atakuwa amemwambia Brian kuwa familia yake ndiyo imemuua. Hili swala la kuokolewa kwake lilikuwa jipya. Kecie anataka aokolewe na nini? Kutoka kwa nani?
.
.
“Umwokoe?” akauliza.
.
.
“Ndio,” Brian akajibu na kuongezea, “Pengine Kecie hajafa.”
Mrs Garett akatoa macho ya mshangao. “Brian, sikuelewi. Nini unasema?”
.
.
“Samahani, Mrs Garett. Ni simulizi ndefu kidogo na muda sina kwa sasa. Nakuahidi kuja kukuona baadae jioni. Kwa sasa kuna mahali natakiwa kwenda. Kuna mtu aningoja!”
.
.
Basi Brian akaaga na kwenda zake. Mpaka anayoyoma Mrs Garett akawa anamtazama kwa namna ya kubanwa na maswali. Brian alimtibua kabisa akili yake na kumwacha kwenye hamu kubwa ya kutaka kujua.
.
.
Hata bado hakumweleza kijana huyo ujumbe aliopewa na mumewe, Mr Garett, ya kwamba Kecie anawinda roho zao.
.
.
Mrs Garett akajikuta anaona mate ni mazito kuyameza.
.
Aliwasha gari na kutimka eneo la makaburini bado kichwa chake kikishindwa kabisa kuacha mawazo juu ya Brian. Alikuwa anahofia sana. Alikosa kabisa amani. Ni kivipi Kecie amwambie Brian amwokoe? Ni kwamba Kecie yupo hai au?
.
.
Mama huyu kwa muda akasahau kuhusu kifo cha mumewe. Hata kwa kiasi fulani akawa si mzingatiaji barabarani. Akiwa katika fikra zake hizo ni ghafula akamwona Kecie pembezoni mwa barabara! Haraka akaminya breki na kuangaza akiwa ametoa macho.
.
.
Breki yake kali ilisababisha nusura agongwe na gari lililokuwa nyuma. Dereva wa gari hilo alifoka kumtuhumu kwa ujinga huo. Lakini Mrs Garett hakuwa anajali. Pengine hakuwa hata anasikia kelele hizo. Alitazama kule alipomwona Kecie lakini ajabu hakuona kitu tena! Hakuwa Kecie bali mtoto fulani ambaye alikuwa anatembea ameshikwa mkono na mama yake.
.
.
Akashusha pumzi ndefu na kuendesha kujiondokea.
.
.
“Tushukie hapa,” alisema Dkt Hamill akizima gari. Alikuwa amevalia koti refu jeusi na kofia. Pembezoni mwake alikuwa ameketi Brian aliyekuwa anatazama huku na kule. Barabara ilikuwa pweke ikiwa imezingira na miti.
.
.
Hakukuwa sehemu ya kufurahisha hapa. Ni sehemu iliyojawa na misitu na ipo pweke. Miti yake ni mirefu na imefunga anga kujaza giza.
.
.
“Una uhakika?” akauliza Brian. Alihofia kushuka. Dkt Hamill alimtazama na kumtikisia kichwa alafu yeye akatangulia kushuka.
.
.
“Papweke na pakimya sana!” alisema Dkt Hamill akiwa anafunga vifungo kadhaa vya koti lake. Alimtazama Brian aliyekuwa anaufunga mlango wa gari, akamwambia, “Hapa palikuwa pamejawa na watu.” akamgoja Brian asogee karibu kisha akaendelea kueleza, “Kila mtu aliona ufahari kuwa karibu na Helo. Lakini habari ilipokuja kubadilika, wakamtenga. Na baada ya nyumba yake kuchomwa, watu wakahamishwa kupelekwa maeneo mengine …
.
.
Hapa pakabaki penyewe. Miti ikaota na kupazinga. Kukawa sehemu iliyosahaulika kabisa … sidhani kama kuna watu huja huku tena. Kufanya nini?”
.
.
Brian akiwa anatoatoa macho kuangaza, akauliza, “Iko wapi hiyo nyumba yake?”
.
.
Dkt Hamill akaonyeshea upande wao wa mashariki na kuanza kuufuata. Wakatembea kwa kama dakika tano, sasa wakaanza kuona mabaki ya nyumba fulani. Walipomalizia mwendo wao kwa dakika tatu, mbele yao sasa kukawa kumesimama nyumba kubwa ya ghorofa. Si nyumba, bali tuseme ghofu.
.
.
Lilikuwa bado lina makovu ya kuchomwa na kuungua. Lilikuwa limefichwafichwa na majani baadhi ya sehemu zake. Rangi yake ya kijivu, rangi ya kuungua, ilikuwa imegeuka na kuwa kijani kwasababu ya kutambaliwa na majani na matawi ya miti.
.
.
Lilikuwa ni ghofu kubwa. Na hivi halikuwa na watu na lipo misituni, lilikuwa laoghofya. Ni wazi ndani yake kutakuwa na wadudu ama wanyama ambao wangeweza kujeruhi mtu.
.
.
“Hapa ndipo alipokuwa anakaa,” akasema Dkt Hamill akitazama ghofu hili kila upande.
.
.
“Kumbe He –” kabla Brian hajamalizia, Dkt Hamill akamziba mdomo kwa kiganja chake. “Usitaje jina lake ukiwa hapa … sawa?”
.
.
Brian akatikisa kichwa kukubali. Dkt Hamill akatoa kiganja chake na kuendelea kutazama jengo lile.
.
.
“Kwanini?” Brian akauliza. “Kwanini tusitaje jina lake? Kuna shida yoyote?”
.
.
Dkt Hamill akamtazama Brian na kumwambia, “Shida ipo tena kubwa … simulizi zina kweli ndani yake kwamba ukitaja jina lake ukiwa hapa kwenye makazi yake, basi ataitikia wito wako na kujitokeza… sidhani kama ungelipenda hilo lijitokeze.”
.
.
Brian akanyamaza asitie neno. Basi wakalizunguka jengo hilo na kisha wakasimama mbele ya lango kuu la kuingilia.
.
.
“Tunaweza kuingia ndani kutazama?” akauliza Brian. Dkt Hamill akanyamaza kwa muda kidogo kabla hajasema, “Sidhani kama hilo ni wazo jema.”
.
.
“Ina maana tutaishia hapa baada ya kufunga safari yote hiyo?” Brian akatahamaki. Alikuwa ana hamu kubwa ya kuona na kutambua mapya. Basi Dkt Hamill kumtimizia haja yake, akamkumbalia, japo kishingo upande, wakaingia ndani.
.
.
Hakukuwa na kitu zaidi ya mabakimabaki tu. Majani yalikuwa yameota karibia kila sehemu pia tando za buibui zikiwa zimetalaki ndani ya eneo. Kulikuwa ni giza na pakimya sana.
.
.
“Nadhani inatosha, Brian,” akasema Dkt Hamill. “Twende sasa.” Lakini Brian hakuwa mwepesi kukubali. Ndiyo kwanza walikuwa wameishia sebuleni, kwanini wasitembelee kila eneo wakaona?
.
.
“Dkt Hamill kwanini unahofia?” Brian akauliza. “Kuna chochote ambacho hujanambia?”
.
.
“Hapana, ila sioni kama ni wazo zuri kuendelea kupekua nyumba hii,” akasema Dkt.
.
.
“Kwahiyo tulikuja kuishia nje tu?”
.
.
“Ndio. Si ulitaka kujua ilipo?”
.
.
Brian akanyamaza. Akaendelea kutazama huku na kule akitaka kujua zaidi.
.
.
“Brian, kama kuna namna ya kuepuka makubwa, basi tufanye hivyo. Hamna haja ya kuingia kwenye matatizo ya kujitakia, sawa? Mimi ni mzee sasa kuhangaikahangaika. Twende.”
.
Ila kabla Brian hajasema jambo, wakastaajabu mlango kufungwa! Wakatazamana kwa hofu. Dkt akarudia, “Twende! Twende, Brian!”
.
.
Wakaufuata mlango na kujaribu kuuvuta, haukufunguka! Wakahangaika sana pasipo mafanikio mwishowe wakaona wakatumie madirisha. Wakafuata dirisha la kwanza kabisa toka walipo, wakavunja mabaki ya fremuze na kutoka.
.
.
Ila wakati wanafanya vivyo, Dkt alijikata kidole chake cha mwisho. Kwakuwa hakukuwa na muda wa kungoja, walikuwa na haraka sana, Dkt Hamill hakujali. Muda si mrefu wakajikuta ndani ya gari na tayari ameshawasha watimke.
.
.
Baada ya mwendo wa dakika kadhaa, ndipo Brian akaona damu kwenye usukani. Dkt Hamill alikuwa anachuruza damu, na asioenakane kujali. Brian akatahamaki akimwambia,
.
.
“Unavuja damu!”
.
.
Dkt Hamill akatikisa kichwa chake asitie neno. Alionekana hayuko sawa. Sura yake alikuwa ameikunja kana kwamba anasikia maumivu na ana mawazo kwa wakati huohuo.
.
.
Brian akaona si vema akiendelea kumwongelesha. Akanyamaza lakini kila saa akiwa anamtazama Dkt na kile kidole chake kilichojeruhiwa.
.
.
**
.
.
Upepo ulipuliza kidogo na kukoma. Damu bado ilikuwapo pale dirishani na hata kwa pembeni yake. Haikuwa imekauka. Kwa mtu mwenye macho makali angeliiona na kama angeigusa basi angeliondoka na doa.
.
.
Baada ya upepo kukoma, kishindo cha miguu kilisikika kwa muda mfupi, na mara mtu mmoja ambaye hakuwa anaonekana kwa juu alijiri na kusogelea dirishani.
.
.
Mtu huyu alikuwa amevalia suruali nyeusi ngumu na chini akivalia viatu vyenye visigino vya kutesa sakafu na ncha butu. Kishindo chake kilionyesha ni mtu mzito mwenye kilo zake.
.
.
Alipofikia dirisha alisimama, akatia kidole chake kwenye matone ya damu yaliyokuwa yamedondoka kisha akapeleka kidole mdomoni kuyanyonya.
.
.
Alipofanya hivyo, matone yote ya damu yakapotea! Na dirisha lililokuwa limevunjika, likajirudi upya na kuwa kama lilivyokuwapo hapo awali.
.
.
“Dkt Hamill!” Brian aliita kwa hofu. Dkt alikuwa amechoka, macho yake yanarembua, mwili umekosa nguvu! Hakuweza kumudu gari. Brian akashikilia usukani na kufanya jitihada kusimamisha chombo hicho.
.
.
“Dkt Hamill!” Brian akaita. Akamtikisatikisa kichwa. “Dkt Hamill! Dkt Hamill!”
.
.
Dkt Hamill alikuwa amechoka mno. Macho yake yalikuwa mazito na mdomo ulikuwa wazi akihema kwa uzito. Brian akahofia sana. Akamtazama kidole cha Dkt Hamill, bado kilikuwa kinachuruza damu. Haraka akafanya jitihada za kumfunga kidole hicho na kisha akamhamisha kiti, akawasha gari na kutimka upesi.
.
.
Ni moja kwa moja akampeleka Dkt hospitalini. Akapokelewa na wahudumu na kuwekwa ndani kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
.
.
“Una uhakika?” Dokta akauliza.
.
.
“Ndio,” Brian akasema akitikisa kichwa. “Alijikata kidole tu, sikuona kingine zaidi ya hiko.”
.
.
Dokta akashusha pumzi na kwenda zake akimtaka Brian aendelee kungoja. Baada ya kama lisaa limoja, Dokta akamfuata Brian na kumtaka akaonane na mgonjwa kwani ameomba hivyo.
.
.
Brian aliyekuwa amepatwa na hofu, akanyanyuka na kwenda huko akisindikizwa na Daktari. Alipofika, daktari akaenda zake kuwapa faragha.
.
.
“Brian,” Dkt Hamill akaita. Sauti yake ilikuwa kavu isiyosikika vema. Brian akasonga karibu na kumtazama kwa macho ya huruma.
.
.
“Mimi sikuwa wa kuletwa hospitalini,” Dkt Hamill akasema kwa shida. Akageuza shingo yake kumtazama Brian. Akamtazama kwa sekunde kadhaa alafu ‘lips’ yake kavu ikasema, “Brian, sasa nitakuwa nimelaaniwa.”
.
.
“Na nani?” Brian akauliza kwa pupa. Dkt Hamill akakohoa kwanza kisha akatafuta hewa yake na kusema, “Nitakuwa nimelaaniwa na Helo … Brian, maisha yangu hayatakuwa sawa tena.”
Brian akashangazwa na maneno hayo. Akamuuliza Dkt Hamill kwanini anasema hivyo? Je kuvunja tu dirisha ndiyo imekuwa ya kupata laana?
.
.
“Hapana, Brian!” akasema Dkt Hamill kisha akakohoa kidogo. Ilikuwa ni ngumu kuamini kama ameletwa hospitali leo. Ungeweza kudhani ni mgonjwa wa muda.
.
.
“ … Ni damu. Ni damu yangu iliyobaki kule,” akasema Dkt kisha akatulia kama mtu anayeishiwa pumzi, sasa anaitafuta. “Nilijua toka nilipokuwa nimejakata pale. Hayakuwa mazingira ya kawaida. Lakini bado tulifanya busara kuondoka mapema. Huenda mambo yangekuwa mabaya zaidi.”
.
.
“Nisamehe, Dkt Hamill,” Brian akalia. “Kama isingalikuwa mimi yote haya yasingejiri. Laiti ningekusikiliza …”
.
.
“Ssshhh! …” Dkt Hamill akamnyamazisha Brian. “Huna haja ya kulia Brian. Hakuna kosa lolote ulilolifanya kwani kama mimi nisngetaka kwenda mule ndani basi nisingelikwenda.” akamshika Brian mkono na kumminya akimtazama kwa sura inayojitahidi kuumba tabasamu.
.
.
“Brian, wewe ni kijana mwerevu lakini pia shupavu sana. Nimefurahi mno kukutana na wewe. Si vijana wengi wako kama wewe. Una kitu ndani yako. Najua unataka kuyajua mengi sana. Ila …” akakohoa. “Tazama yasije yakakugharimu.”
.
.
Aliposema hayo akatulia kwa dakika moja, alikuwa anatazama chumba alicholaziwa kana kwamba ni kipya machoni. Aliporejesha macho yake kwa Brian, akasema, “Ni bora nikafa.”
.
.
Kauli hiyo ikamshtua Brian, “Kwanini unasema hivyo, Dkt Hamill? Tafadhali usiseme hivyo!”
.
.
Dkt akatabasamu. Akamtazama Brian aliyekuwa na sura ya hofu kisha akasema, “Brian, mimi ni mzee sasa. Si kama wewe. Wewe bado damu yako yazunguka, mwili wako una joto na hata akili yako inayoendelea kukua inafanya kazi upesi.
.
.
Hutonihitaji tena mimi, Brian. Niliyokupa yanatosha. Nashukuru sana kwa kuwa na mimi japo kwa kipindi kifupi, umenipa faraja na ‘kampani’ ya rafiki.”
.
.
Hapa ndipo Brian akajifunza ya kuwa Dkt Hamill hana familia. Yu mpweke sana na amekuwa akiishi hivyo kwa miaka mingi sasa. Mke na watoto wake wote walikufa lakini hakumwambia Brian nini kiliwaua.
.
.
Kauli yake ya mwisho alimwagiza Brian aende nyumbani kwake, akamwelekeza wapi atapata ufunguo, azame ndani na kumletea nyaraka zake tatu kwenye kabati.
.
.
Brian akitumia gari la Dkt Hamill, akaelekea huko, kulikuwa ni kingoni mwa mji wa Boston. Akaukuta ufunguo alipoelekezwa, akazama ndani na kunyookea kwenye kabati.
.
.
Ilikuwa ni nyumba kubwa yenye vyumba takribani vitano ila vyote vikifungwa isipokuwa kimoja tu alimokuwa anaishi Dkt Hamill mwenyewe. Nyumba hiyo ilikuwa kubwa na kimya sana. Pia pweke. Brian alishangazwa namna gani Dkt Hamill alikuwa anaweza kuishi mwenyewe hapo.
.
.
Asipeleleze sana, akarudi kwenye gari na kuanza safari ya kurudi hospitali. Alichukua takribani dakika kumi tu kutokana na mwendo wake wa kasi. Alipofika, ajabu hakumkuta Dkt Hamill. Dokta akamwambia tayari mzee huyo amekufa, amehifadhiwa mochwari.
.
.
Akashindwa kuzuia chozi. Akajihisi kuishiwa na nguvu. Aliketi kwenye benchi kama mtoto yatima akiwa na kujiona mpumbavu kwa namna alivyofanya mzee huyo akafariki. Alijiona muuaji. Alijiona mwenye makosa.
.
.
Macho yake yakiwa yamejawa na machozi yaliyomfanya asione vema, Dokta akamjia na kumgusa bega. Akamkabidhi karatasi fulani na kumwambia, “Ni ujumbe wako alinambia nikupatie punde utakaporudi hapa.”
.
.
Kabla Dokta hajaondoka akamshika Brian begani mara mbili kumpa pole.
.
.
Saa moja jioni …
.
.
Brian alikuwa amejifungia chumbani kwake, uso wake ukiwa mwekundu, macho yake bado yanachuruza machozi. Kitandani kulikuwa kuna zile nyaraka tatu ambazo Dkt Hamill alimwambia akazichukue, pamoja pia na ujumbe aliopewa na Dokta kule hospitalini.
.
.
Alitazama nyaraka zile na ule ujumbe. Sijui alikuwa anawaza nini kichwani mwake. Kwa muda kidogo hakuwa anajua cha kufanya ilhali kila kitu kipo bayana ya kwamba yampasa atazame vilivyomo ndani.
.
.
Baada ya kutulia kidogo ndipo akachukua ule ujumbe kwenye karatasi, akaanza kuusoma. Uso wake ulikuwa umepooza. Macho yake yalikuwa yanatia huruma.
.
.
Taratibu akawa anapitisha macho kwenye ujumbe uliokuwa unasomeka kama ifuatavyo,
.
.
“Inabidi niende, Brian. Sidhani kama nitakuwa nimekuacha mpweke. Nimeenda kwenye ulimwengu wa pili. Ulimwengu ambao siujui moja wala kumi yake. Nimekamilisha maisha yangu huku duniani. Lakini nakusisitizia Brian, mimi nimekwenda. Ni hivyo tu. Endapo ukiniona tena muda wowote mahali popote, basi jua si mimi.
.
.
Kwenye hizo nyaraka tatu, tafuta muda usome kwa makini. Tafadhali usipuuze. Nakutakia kila la kheri ukatimize haja yako. Usiogope, Brian. Na usiache jitihada zako za kumwokoa Kecie. Huwezi jua utawaokoa na wakina nani pamoja naye.”
.
.
Ujumbe ulikwisha ukimwacha Brian akidondosha machozi. Kichwa kilikuwa kinamgonga na alijikuta anaumia sana moyoni. Anaumia mno. Alisaga meno yake kwanguvu akiangushia kichwa chake kitandani.
.
.
Hakukumbuka aliishia wapi kulia, usingizi ulimsomba kwa pupa sana kumpeleka kwenye ulimwengu wa kiza ila angalau wenye unafuu.
.
.
“Brian! Brian! Tih-tih!-tih!” alikuwa anaitwa na mlango unagongwa. Ni kama takribani dakika ishirini tangu alipozolewa na usingizi. Alihisi huenda anaota, ila ilikuwa ni uhalisia. Alikuwa anaitwa.
.
.
Mama yake alikuwa amesimama mlangoni akiwa ameshikilia kiuno chake kwa mkono wa kushoto, wa kulia akibondea mlango.
.
.
Mara punde mlango unafunguliwa Brian akiwa anafikicha macho yake. Alimtazama mamaye na kumuitikia kilevi.
.
.
“Uko sawa?” mama akauliza akifinyanga uso wake kwa hofu.
.
.
“Ndio … niko sawa!” Brian akaongea kivivu. Macho yake bado yalikuwa mekundu ila kwakuwa alitoka kulala, mama yake hakujali sana. Alishani ni usingizi.
.
.
“Mbona umelala pasipo kula?”
.
.
“Mama sisikii njaa.”
.
.
“Umekula wapi?”
.
.
Brian kimya. Mama akamtazama na kutaka kumuuliza tena kama yupo sawa, ila akasita. Akadaka kiuno chake kwa mikono yote alafu akamwambia, “Una mgeni wako sebuleni. Anataka kukuona hivi sasa.”
.
.
“Nani?”
.
.
“Mrs Garett. Fanya uje haraka.”
.
.
Mama aliposema hivyo akaenda zake kurudi sebuleni. Mama Kecie aliyekuwa ameongozana na Olivia walikuwa wameketi kwenye kochi la kwanza kabisa upande wa kulia wa mlango, akawaambia kuwa Brian yuaja muda si mrefu.
.
.
“Kweli hamtahitaji kitu?” mama Brian akauliza wageni huku akiwapatia tabasamu.
.
.
“Hapana,” Mrs Garett akasema akitikisa kichwa. “Tupo tu sawa, usijali.”
.
.
“Hata chai? Ni baridi jamani.”
.
.
“Sawa, tutashukuru.”
.
.
Mama Brian akaenda jikoni na kurejea na vikombe viwili vya chai, akawapatia Mrs Garett na Olivia. Taratibu wakawa wanavuta kimiminika hicho cha moto kumngoja Brian.
.
.
Punde Brian akafika sebuleni na kuwasalimu..
.
.
“Pole kwa usumbufu.,” Mrs Garett alisema akimtazama Brian. Kwa kumtazama tu mama huyu hakuwa sawa. Sauti yake ilikuwa ajabu na uso wake ulikuwa ulioganda. Hakuwa na lepe la furaha. Ungelitabiri vema hakukuwa na kitu kilichomfurahisha siku nzima ya leo.
.
.
“Usijali, Mrs Garett. Karibu.”
.
.
“Brian, nina shida sana. Nahisi maisha yangu yapo hatarini.”
.
.
Kauli hii ya upesi na iliyosikika vema ilimfanya Brian na mama yake wawe wasikivu zaidi.
.
.
“Baada ya mume wangu kufa, ni mimi ndiye yuaja. Naombeni mnisaidie.” Mrs Garett akaanza kububujikwa na machozi. “Kecie anataka kuniua kama alivyomuua baba yake. Anawinda roho yangu!”
.
.
Brian na mamaye wakatazama kwa puzo. “Kwanini Kecie akuue?” Briana akauliza. “Na kwanini alimuua baba yake?”
.
.
Mrs Garett kwa kujikaza, akasema kila kitu. Hakutaka yale ya mficha maradhi. Alikuwa anataka msaada haswa. Alipomaliza kueleza, akajikuta anatoa machozi zaidi na kupaliwa na kilio. Alikuwa anamwomba msamaha mwanaye.
.
.
Lakini kwanini alidhani Brian anaweza kumsaidia kwenye hilo?
.
.
“Ni wewe tu na sisi ndiyo hutokewa na Kecie. Lakini akija kwako hukuomba msaada. Akija kwetu hudai roho zetu,” alisema Mrs Garett akitoa macho yake mekundu. “Kama Kecie hukuskiza wewe, naomba utuombee msamaha, Brian!”
.
.
Mama Brian akamtazama mwanaye na kumuuliza, “Kecie, hukuomba umsaidie?”
.
.
“Ndio,” Brian akajibu na kuongezea, “Huniomba nimwokoe!”
.
.
“Umwokoe wapi? Kutoka kwa nani?”
.
.
Brian akamtazama mama yake na kumwambia, “Toka kwa Helo.”
.
.
“Ndiyo nani huyo?”
.
.
Kabla Brian hajajibu, akaona kitu dirishani.
.
.
Alikuwa ni mtoto akiwa amesimama na mwanaume mweusi asiyeonekana lakini wenziwe walipoangazia huko, hawakuona kitu! Kila kitu kilikuwa kimepotea katika kasi ya kufumba na kufumbua.
.
.
“Kuna nini, Brian?” Mama yake akauliza.
.
.
“Kulikuwa na mtoto akiwa amesimama pale na kando yake kuna mtu!” akasema Brian akinyooshea kidole kule dirishani. Ila hakukuwa tena na kitu! Na si kwamba watu hawakumwamini, la hasha. Ni kwamba tu hawakufanikiwa kushuhudia.
.
.
“Brian! Kecie atakuwa ananifuata mimi!” akasema Mrs Garett akijawa na woga. Aliangazaangaza huku na huko. Hakuwa na amani. Hofu aliyokuwa nayo ilikuwa ni ile iliyo kuu.
.
.
“Usijali, Mrs Garett!” Mama Brian akamfariji. “Leo utalala hapa wewe pamoja na Olivia. Nadhani msiba wa mumeo utakuwa umekuathiri.”
.
.
Mama hao wakakumbatiana. Mama Brian akaendea chai ya Brian na ya kwake wakaendelea kukaa hapo wakiteta. Lakini kila saa Mrs Garett akawa anamsisitizia Brian ya kwamba endapo Kecie akijiri basi amwambie ya kwamba anaomba msamaha. Ambakizie roho yake.
.
.
Usiku ukazidi kukua na mwishowe kabisa wakaenda kulala. Mrs Garett alienda kulala na Mama Brian huku Olivia na Brian kila mmoja akilala chumba chake.
.
.
Usiku huo wakati watu wakipambania kupata usingizi, Brian yeye akawa ndiyo anautumia huo muda kusoma zile nyaraka za Dkt Hamill. Zilikuwa ni za kuogopesha lakini hakuwa anataka kuzieka chini mpaka kumaliza. Haikuwa kazi nyepesi.
.
.
Basi na sehemu ya nyaraka hii yasomeka kama ifuatavyo …
.
.
“… Kifo kina wivu sana. Kinatutenga na wale tuwapendao. Kimeniacha na kidonda kikubwa sana kwani kichwa changu kimekuwa hakikomi kuwaza na kukumbuka matabasamu ya mke na watoto wangu. Waliniacha kipindi nawahitaji sana. Pengine waweza kuwa unanionea huruma, lakini utakapomaliza kusoma haya, labda utaniona mimi ni mkatili sana. Mtu asiyestahili huruma hata lepe.
.
.
Basi ningalikuwapo kijana nilikuwa mtanashati sana. Mwenye nguvu na kaliba ya kufanya kazi kwa bidii. Doa langu lilikuwa moja tu, nalo ni kupenda sana kujifunza na kujua. Sikuwa na jambo dogo, na niliamini kila lionekanalo kidole basi lina mwili mzima.
.
.
Kutokana na hulka yangu hiyo, nikawa napenda sana kujitenga na kujisomea. Lakini pia kuchangamana na watu kuwauliza mambo kedekede ambayo nilikuwa nataka kuyafahamu.
.
.
Baba yangu, Mr Lambert, alikuwa ni mtu mkorofi sana. Kwenye moja ya shamba lake la pamba alikuwa na watumwa weusi kumi na tano. Hakuwa anapenda kuniona nikichangamana na watumwa hao. Mara kadhaa alikuwa ananiadhibu kwa kunikuta nikiwa nakaa na kuongea nao, lakini sikuwa naskiza.
.
.
Watumwa hao walikuwa na simulizi tamu sana, haswa mwanamke mmoja mzee aliyekuwa anaita Jasmine. Yeye alikuwa akiniona anafurahi na kunikumbatia tofauti kabisa na mama yangu. Alikuwa ananipenda sana, na alikuwa anajua nini napenda pia.
.
.
Angeniweka kwenye mapaja yake na kuniambia simulizi mbalimbali, hata za kule Afrika. Lakini kwasababu ya umri wake, alikuwa ameona mengi. Alikuwa ni mkubwa kuliko hata baba yangu. Alinihadithia mambo mengi ya Boston ambayo hata baba yangu hakuwa anafahamu.
.
.
Ni yeye ndiye aliyenieleza juu ya familia ya Helo. Kipindi kile akiwa msichana , japo bado mtumwa, alikuwa anatoroka kwenda kwenye maonyesho ya bwana huyo. Japo ilikuwa hairuhusiwi kwenda, na hata huko kwenye vibanda, watu weusi walikuwa hawatakiwi, hakukoma kwenda kufurahisha nafsi yake.
.
.
Alikuwa ni jasiri. Mgongo wake ulijawa na makovu ya kupigwa, lakini hakuwa anaskiza. Alikuwa anaufuata moyo wake. Siku moja nilimuuliza, huoni kuwa mgongo wako unaisha kwa ukaidi? Basi akatabasamu na kunitazama na macho yake mekundu. Akanishika mashavu na kuniambia,
.
.
“Kuna furaha gani kwa mtumwa aliye ndani ya minyororo? … hata nikikaa hapa, bado nitaonekana mkaidi kwa maana mtumwa hupewa jina hilo tangu na uzao wake. Maisha yake ni mafupi na yanapokoma hukusanywa kama kiroba na kutupiwa shimoni.
.
.
Hamill, huoni kuna haja ya kuthubutu kutafuta tabasamu langu hata mara moja kwa miaka yote hiyo?”
.
.
Hakika alinitia moyo sana na alinifanya nifuate nikipendacho pasipo kujali nini kitanitokea. Ilimradi nina furaha, basi yatosha.
.
.
Lakini siku ile wakati Helo anachomwa moto baada ya kugundulikana kuwa ni mlozi, Jasmine alishuhudia kila kitu kwa macho yake. Alikuwa bado ni binti. Na kitu kile kilimuumiza sana. Hata alipokuja kunihadithia, japo ni miaka mingi ilipita, bado macho yake yalikuwa yanageuka kuwa mekundu. Na hakukoma kunihadithia hilo mara kwa mara.
.
.
Hatimaye tabasamu lake lilikuwa limekoma. Hakuwa na la kumfurahisha tena isipokuwa mateso ya kitumwa tu. Lakini katika hilo nilikuja kugundua kuwa Jasmine alikuwa na ratiba ya kwenda msituni mwenyewe, tena pasipo kumuaga mtu.
.
.
Mara kadhaa nilipokuwa namtafuta, hakuwa bandani wala shambani. Nilipomuuliza, hakuwa radhi kuniambia. Hivyo nikapanga kujua ni wapi huwa anaenda japo kwa siri. Niliwaza pengine atakuwa amepata kitu kingine cha kumfurahisha.
.
.
Siku hiyo wakati namfuatilia nikaenda naye mbali kuzama msituni. Hakuwa anajua kama mimi namtazama kwa mbali. Alienenda ndani kabisa mpaka kwenye ghofu fulani kubwa. Humo akazama ndani na kukaa kwa dakika kadhaa.
.
.
Sikujua alikuwa anafanya nini humo ndani. Nilitamani sana kujua. Ila kwa kuhofia kuonekana, ikabidi nikae mbali. Alipotoka nikakimbia upesi kurudi nyumbani.
Siku iliyofuata hakwenda tena kule. Nikamfuata na kumuuliza, wapi huwa anakwenda? Mbona kuna muda namtafuta, simwoni! Hakunijibu, bali akaniuliza akinitazama kwa macho ya kuumba, ‘Hamill haujui ninapokwenda?’ Nikapandisha mabega yangu juu nikisema, sijui.
.
.
Akatabasamu na kuendelea na kazi yake ya kufuma nguo. Nikadhani labda atakuwa aliniona nilivyokuwa namfuatilia, basi nikaona niwe mpole, nikamuuliza kule alikuwa ameenda kufanya nini?…”
.
.
Hapa ndipo Brian alikuwa ameishia kusoma kabla hajasikia kelele kali zilizomshtua. Alidhani pengine ni masikio yake, ila alipotulia vema akasikia sauti zingine. Hapo akaamini kuwa ni uhalisia! Kelele zote hizo usiku za nini?
.
.
Haraka akafungua mlango na kutoka nje. Akaenda chumbani kwa mama yake alipomkuta Mrs Garett akipiga makelele na mama yake akiwa anamtuliza. Akauliza nini kimejiri.
.
.
“Mrs Garett amemwona Kecie bafuni!” Mamaye akamjibu. Uso wake ulikuwa umeelemewa na usingizi, mshangao na woga.
.
.
“Yu kwapi Olivia?” Brian akauliza.
.
.
“Chumbani huko!” mama yake akajibu. Kwa haraka Brian akapata wazo la kwenda kumwona binti huyo. Alifungua mlango pasipo hata kubisha hodi, akatupa macho yake kitandani.
.
.
Olivia hakuwapo!
.
.
Akatafuta kwenye kabati, chini ya kitanda na nyuma ya mlango. Olivia hakuwapo! Haraka akarudi kule kwenye chumba cha mama na kuwaambia kuwa Olivia hayupo! Wakamtafuta nyumba nzima, kweli hakuwapo.
.
.
Wakiwa sebuleni, kwa mbali huko nje, Brian akamwona binti akiishilia na barabara! Akapayuka, “Yule kule!” haraka akafungua mlango na kumkimbilia binti huyo.
.
.
“Olivia! … Olivia!” alimwita lakini Olivia hakuitikia. Aliendelea kutembea akitazama mbele. Brian akamfikia na kumnyanyua juu, akamwita, “Olivia! Olivia!” akiwa anampigapiga makofi shavuni kumwamsha.
.
.
Macho ya Olivia yalikuwa yanatazama kule mbele alipokuwa anaenda. Kuna kitu alikuwa anaona. Akakinyooshea kidole. Lakini Brian alipotazama hakuona jambo.
.
.
“Kuna nini Olivia?”
.
.
Olivia hakuwa mtu anayejielewa. Bado macho yake yalikuwa yanaangazia kule mbele. Hakuonekana kama anasikia hata kile anachoambiwa.
.
.
Baada ya muda fulani ndipo akamtazama Brian. Macho yake yalikuwa yanatisha. Na Brian asifahamu kinachoendelea, akajikuta anadondoka chini na kupoteza fahamu!
Hewa inakuwa nzito sana. Hata harufu nayo pia inabadilika na kumfanya Brian apige chafya na kukurupuka. Hakuwa kwenye mazingira anayoyajua. Hapa chumba kilikuwa ni chembamba na kuta zake zilikuwa hafifu, kukuu.
.
.
Mwanga ulikuwa hafifu sana. Mwanga ulioshindwa kupambana na giza.
Brian akatazama kushoto na kulia. Hakumwona mtu. Alikuwa anatamani kunyanyuka, lakini mwili haukuwa na nguvu kabisa. Ni shingo tu ndiyo ilikuwa na uwezo wa kupeleka kichwa huku na kule.
.
.
Punde mlango ukafunguliwa, Brian akatazama huko. Akamwona Kecie na gauni lake. Mkononi alikuwa na mdoli. Binti huyo akamsogelea karibu na kumtazama machoni.
.
.
“Brian, naomba niokoe,” akasema kwa sauti ya upole.
.
.
“Nikuokoe na nini, Kecie?” Brian akauliza.
.
.
“Mimi ni mfungwa, Brian,” Kecie akasema. Mkono wake wa baridi ukamshika Brian. “Nipo kifungoni, nataka kutoka roho yangu iende kwa amani.”
.
.
“Nani amekufunga, Kecie?” Brian akauliza. Kecie akatazama mlangoni na kupanyooshea kidole pasipo kusema kitu. Ajabu, Brian akapata nguvu ya kunyanyuka. Akatoka kitandani na kuuendea mlango, akaufungua na kutazama nje.
.
.
Kulikuwa na korido ndefu sana. Sakafu yake haikuwa inaonekana kwani imetwaliwa na moshi. Kutani kulikuwa na fremu za picha na kwa mbali kulikuwa kunasikika sauti nzito ya mwanaume ikinena na hata kucheka.
.
Brian akapata shaka na walakini. Akatazama nyuma kumwangalia Kecie, Kecie akamnyooshea kidole huko huko mbele. Lakini Brian hakuwa anajua cha kufanya. Alinyanyua miguu yake kwenda mbele akiwa hafahamu anaenda kukutana na nani.
.
.
Sakafu ilikuwa ya baridi kupita kiasi. Ilimfanya atetemeke na akunjekunje vidole vyake kila alipokuwa anakanyaga. Kwenye kuta, zile picha zilizokuwa zimetundikwa, zikawa zinanyamaza na kumtazama Brian alipokuwa anapita.
.
Picha hizo zilikuwa ni za sherehe. Zilikuwa ni za vifijo cha kipindi kile ambapo Helo alikuwa anatumbuiza. Bado picha hizo zilikuwa hai. Watu walikuwa wanafurahia na kushangilia mazingaombwe ya Helo, lakini Brian akitazama zilikuwa zinaganda na kuwa picha kamili!
.
.
Brian akazitazama akisonga. Moyo wake ulikuwa unapiga kusema hofu iliyomtawala. Kadiri alivyokuwa anasonga kwenda mbele, ndivyo sauti ile aliyokuwa anaisikia kwa mbali ikawa inamjongea na hata kuleta maana.
.
.
Kuna muda ilikuwa ni wimbo waimba. Na kuna muda kulikuwa na sauti ya mwanaume ikifoka ama kuteta. Mwanaume huyo ni nani? Na wimbo huo – ngoja! Atakuwa ni Helo. Brian alikuwa na kikao kichwani mwake. Na huyo anayemfokea ni nani?
.
.
Hakukuwa na majibu zaidi ya yeye kusonga na kutazama kwa macho yake. Japo alikabwa na woga, hakika alitaka kujua. Alipofika kwenye mwisho wa korido, taratibu, akachomoza kichwa chake kuchungulia sebuleni.
.
.
Kwa macho yake akamwona mwanaume fulani mzito aliyekuwa amevalia kofia ndefu kichwani yenye michirizi mekundu kwenye kingo zake. Mwanaume huyo alikuwa amevalia nguo za sherehe, zinazometa na kuvutia.
.
.
Koti jeusi la kumbana, suruali iliyoshika mapaja na nyonga zake kisha kubwaga huko chini. Miguuni ana viatu vyenye visigino virefu na kuchongoka kwa mbele. Mikononi amevalia glovu nyeusi malighafi ya ngozi.
.
.
Vitu vyote hivyo ambavyo vimetajawa vilikuwa vyametameta kana kwamba nyota angani!
.
.
“Helo!” Brian akajikuta ananong’ona mwenyewe akistaajabu. Mbele ya macho yake alikuwapo mwanaume ambaye amekuwa akisikia tu simulizi zake. Mwanaume aliyewahi kutikisa Boston na Massachusetts nzima!
.
.
Bado mwanaume huyo alikuwa amevalia nguo zake alizokuwa anatumbuiza nazo, hata picha zake huko ukutani zilikuwa zamwonyesha hivyo.
.
.
Hakika alipendeza na basi ungetamani umwone akiwa anatumbuiza. Lakini endapo ungekumbuka kuwa mtu huyu ni mfu, ungepoteza hamu yote! Mtu aliyechomwa moto miaka iliyopita na hata nyumba yake kutiwa pia motoni, leo yu hai, mzima na anacheza!
.
.
Pembeni yake kulikuwa na santuri ya kale iliyokuwa inamimina muziki wa bluzi. Hakika muziki huu ulikuwa unamkonga moyo wake, alikuwa akiimba pamoja nao na muda mwingine akijikuta anapiga kelele kali za nguvu!
.
.
Lakini sura yake haikuwa inaonekana. Alikuwa amempa mgongo Brian. Kichwa chake anakitikisatikisa na mkono wake uliopo ndani ya glovu unatengeneza ala kwa vidole.
.
.
Brian atamfanya nini mtu huyu? Akatazama nyuma, akakutana uso kwa uso na Kecie. Kecie hakusema jambo, bali akaendelea kumnyooshea kidole huko mbele, yaani sebuleni. Brian alipotazama tena kule sebuleni, Helo hakuwapo! Kiti pekee kilikuwa kinachecheza.
.
.
Moyo wa Brian ukalipuka kwa woga sana. Akapepesa macho yake kule na kule, hakumwona Helo. Hakujua wapi ameenda, tena ‘hafla hivyo! Kurudisha uso kwa Kecie, hapo akamwona mwanaume mrefu akiwa amesimama! Mwanaume mzito aliyeshiba.
.
.
Uso wake haukuwa unaonekana kwa kufichwa na kivuli cha kofia. Nguo zake zilikuwa zametameta, zang’aa, kana kwamba vito vya almasi vimeshikiziwa kwenye shuka.
.
.
Alikuwa anatisha kwa urefu wake. Brian alitetemeka na akatamani kupiga kelele kwanguvu sana. Mwili ulimuisha nguvu. Mkojo ulimbana, maungio ya mwili yalipata ganzi!
.
.
Kecie alijificha nyuma ya mwili wa mwanaume huyo, naye pia akiwa na uso wa hofu kuu.
.
.
“Unafuata nini kwenye himaya ya walio wafu?” sauti nzito ikauliza.
.
.
Brian hajajibu, akazabwa kofi kali sana. Akapaa juu na kwenda kujikita ukutani na kupoteza fahamu papo hapo! Hakujua tena kilichoendelea. Alipokuja kufungua macho, hajui hata majira, akajiona yu sebuleni kwao. Kichwa kilikuwa kinamuuma sana, haswa upande wake wa kulia.
.
.
“Mama!” akaita.
.
.
“Brian!” mama yake akamjongea upesi kumtazama. “Brian, mwanangu. Unaendeleaje?”
.
.
“Kichwa kinaniuma sana …” Brian akatazama kushoto na kulia kwake, akamwona Mrs Garett na Olivia. Akaita, “… Olivia.” kabla hajaongeza neno, kichwa kikamgonga sana, akakunja uso wake kus’kizia.
.
.
“Pumzika, Brian,” mama yake akamsihi. “ulipoteza fahamu ghafla.”
.
.
“Mlikuta Olivia?” Brian akauliza.
.
.
“Ndio. Olivia alikuwa ndani. Tulistaajabu kukuona wewe ukikimbia kwenda huko nje.”
.
.
“Alikuwa ndani? Mbona sikumwona? Wote hatukumwona!”
.
.
“Sisi tulimwona, alikuwa amelala kitandani. Tulikuambia lakini hukutuelewa. Tulistaajabu unakimbilia nje. Tulipokufuata tulikukuta ukiwa umezirai, umelala barabarani!”
.
.
Brian akaduwazwa na hayo maelezo. Yule hakuwa Olivia? Mbona alimwona vivyo? Basi na ilikuwa ni njia ya Kecie kumpeleka kule kwenye ulimwengu mwingine. Ulimwengu ambao Helo aliuita wa wafu.
.
.
Hakuwa anaota. Ulimwengu huo ni wa dhati. Maumivu ya kofi zito alilozabwa, bado alikuwa anayasikia sana yakiathiri sikio lake la kulia. Akawaza, atamwokoaje Kecie kule? Na je baada ya yeye kuondoka huko, Helo atamfanya nini Kecie?
.
.
**
.
.
Saa nane mchana.
.
.
.
Hakukuwa na shule siku hiyo, wanafunzi wote pamoja na wafanyakazi wa shule walikuwa wamehudhuria msiba wa Dkt Hamill. Shule ilikuwa pweke. Makaburi ya Boston yalikuwa yamefurika watu waliovalia sare za wanafunzi.
.
.
Hakukuwa na ndugu, jamaa wala rafiki wa marehemu. Kwa heshima za wafanyakazi wenzake, shule ikiwa imesimamia kila jambo, Dkt Hamill akaagwa na kuzikwa.
.
.
Watu walipotawanyika, Brian akaenda nyumbani kwa Dkt Hamill moja kwa moja. Alikuwa ndiye mtu mwenye ufunguo wa nyumba hiyo, pamoja pia na wa gari yake.
.
.
Alipofika, akaitazama nyumba hiyo kana kwamba ni kitu anachokijua ila kilipotea kwa muda mrefu. Akaikagua sana kwa nje, kila kona, akajikuta anajawa na machozi machoni mwake. Aliingia ndani na kuendelea kupekua. Akatazama picha za Dkt Hamill na familia yake. Akapata maswali sana kichwani,.
.
.
Familia hii ilipotelea wapi? Kwanini Dkt Hamill amekufa akiwa mpweke. Hana ndugu wala rafiki? Ni maisha gani hayo aliyokuwa anaishi? Alitamani sana kujua.
.
.
Akiwa anaendelea kupekuapekua, akiwa kwenye ghorofa ya juu, kwa chini nje ya uzio, akamwona mwanaume mmoja akiwa amesimama … amesimama anamtazama!
.
.
Mwanaume huyo alikuwa amevalia koti refu jeusi. Kichwa chake amekihifadhi ndani ya kofia na mikono yake ameidumbuliza kwenye mifuko ya koti.
.
.
Brian akastaajabu kuwa mwanaume huyo amemwonaje akiwa juu huko? Na kwanini amesimama kana kwamba mnara akimtazama? Ni nani?
.
.
Alipotazama vema akagundua mwanaume huyo ni Brewster! Mwanaume kikongwe ndani ya mji wa Boston. Mzee huyo anafanya nini hapo? Brian alishangazwa na namna ambavyo Brewster amekuwa wa kumfuatilia.
.
.
Akashuka upesi toka ghorofani, akaendea geti na kutazama nje. Hakumkuta mtu! Brewster hakuwepo. Alikimbilia kaskazini mwa barabara na kusini lakini hakumwona mzee huyo. Haikujulikana wapi alielekea.
.
.
Basi Brian akaona shughuli imetiwa doa, akafunga kila kitu na kwenda zake nyumbani, akiwa na maswali juu ya Brewster.
.
.
Alipofika, kwakuwa alikuwa na njaa, akaendea jikoni na kupakua chakula. Alimkuta Olivia pekee sebuleni anatazama televisheni.
.
.
“Wapo wapi hawa?” akamuuliza akitafuna.
.
.
“Wametoka,” Olivia akamjibu kwa ufupi.
.
.
Hapa ndipo Brian akakumbukua kuwa gari halikuwapo nje.
.
.
“Wameenda wapi?”
.
.
Olivia akapandisha mabega juu pasipo kutia neno, hakuwa anamtazama Brian. Basi Brian akaendelea kula, lakini ghafla kuna kitu kikamjia kichwani. Hakujua kwanini, ila alijikuta akikumbuka tukio la ajali ya Mr Garett!
.
.
Aliyakumbuka yale maneno ya Mrs Garett kuwa bwana wake alimwambia kuwa Kecie anawinda roho yao kabla hajafariki, punde ndogo baada ya kupata ajali ya gari.
.
.
Basi Brian akajikuta anakosa amani. Hata chakula hakukimaliza, akakiweka kando.
.
.
“Wametoka muda mrefu?” Akauliza.
.
.
“Tangu asubuhi,” Olivia akajibu, bado akiwa anatazama televisheni. Ila sauti yake ilikuwa tofauti kidogo. Hili kwa kiasi likampa mashaka Brian. Akaita, “Olivia!”
.
.
Olivia akaitikia. Hakumtazama Brian. Uso wake ulikuwa umeng’ang’ania kutazama televisheni.
.
.
“Olivia, nitazame.”
.
.
Olivia akakaa kimya. Hakutikisika wala kupepesuka. Brian akarudia kumwambia akimtaka ageuke. Mara hii Olivia akajibu kwa swali, “Kwanini nigeuke?”
.
.
Sasa mara hii sauti yake ndiyo ilikuwa tofauti kabisa. Sauti nzito ya kiume! Brian akajikuta akishtuka mno
Moyo wake ukaenda mbio na mwili wake ukaanza kutetemeka kwa fujo! Kufumba na kufumbua, Olivia akageuza shingo yake kumtazama Brian! Lakini namna ambavyo alikuwa amegeuza kichwa hiko ilikuwa ni ya ajabu haswa! Mwili wake bado ulikuwa unatazama upande ilipo runinga, lakini uso wake ukiwa umegeuka nyuma kabisa!
Kwa mtu ambaye ni mzima, hawezi kufanya hivi, labda tu awe amevunjika ajalini. Macho yake yalikuwa meusi ti! Mdomo wake ulikuwa mkavu kana kwamba muhogo uliotelekezwa juani.
“Nini unataka kujua, Brian?” Olivia akauliza kwa sauti yake ya ajabu. Brian akabaki akiwa ametoa macho. Anahema kana kwamba mbwa aliyetoka kukimbizwa.
“Nini unaogopa? Si umetaka nigeuke?”
“Wewe ni nani?” Brian akauliza. Alikuwa amejiminyia kochini nusura atokee upande wa pili.
“Mimi? – wataka kunijua mimi?” Olivia akauliza. Kwa haraka mwili wake ukageuka kufuata uso wake, akasimama na kumtazama Brian huku shingo yake ikiwa inakunjikakunjika hovyo kupeleka kichwa huku na kule.
“Mimi ni mwenyeji wako, Brian! Hunijui?” Olivia akauliza. Brian akiwa anatweta kwa hofu kuu, akatikisa kichwa chake upesi. Paji lake la uso lilikuwa linatiririsha jasho.
“Sikujui!” akasema. “Sikujui wewe ni nani!”
Olivia akaangua kicheko na mara akakunja tena sura yake kwa hasira. Akamtazama Brian kiupande. “Mimi ni mwenyeji wako!” akamwambia kwa sauti yake ya mashine. Macho yake yaliyokoza uweusi yakiwa yametoka nje mithili ya balbu!
“Ulikuja kwenye himaya yangu kun’tembelea … Je nataka kumtorosha mwanangu?”
“Mimi hata simju-!” Brian hakumalizia kauli yake, akasombwa yeye pamoja na kiti. Ilikuwa ni nguvu ya ajabu. Alibamiziwa ukutani pasipo hata kuguswa, akaja kujikuta akiwa chini anagugumia na maumivu.
“Kamwe!” Akasema Olivia akipeperusha kidole chake kushoto na kulia. “Kamwe … kamwe … usije kuthubutu!”
Aliposema hayo akakunja ngumi ya mkono wake wa kuume, Brian akaanza kukabwa na mkono asiouona. Akadaka shingo yake akijitahidi kuhema. Mishipa ya shingo imemshupaa. Olivia akaendelea kuiminya ngumi yake. Brian akaendelea kuteseka maradufu, sasa hewa akiwa hapati! Jasho jingi lamchuruza. Macho yamemtoka nje! Alikuwa anaelekea kufa.
Uso wake ulibadili rangi kuwa mwekundu, na kila mshipa uliokuwapo kichwani ukasimama dede! Kwa sekunde tatu tu za mbele, kijana huyu alikuwa anaiacha dunia.
Kheri, huko nje sauti za watu zikajongea. Walikuwa ni watu wawili wanaongea na huku wakiwa mwendoni kufuata makazi ya wakina Brian. Hapa ghafla, Olivia akanyong’onyea na kudondoka chini akiwa hana fahamu! Hiyo ikawa ahueni ya Brian ya maisha yake yaliyokuwa yamebakia kwenye nyuzi nyembamba!
Punde mlango ukafunguliwa, akaingia Mama yake Brian pamoja na Mrs Garett.
“Mungu wangu!” Wakahamaki. Brian alikuwa ameegemea ukuta, yu hoi, na kwake pumzi ikiwa ni bidhaa yenye thamani kubwa akihangaika kuitafuta. Hata nguvu hakuwa nayo. Jasho limemvaa uso wake gubigubi. Anakohoa kwa pupa.
Olivia alikuwa hayupo hata kwenye ulimwengu huu.
“Brian, nini kimetokea?” Mama Brian akauliza akimkimbilia mwanaye upesi kumtazama. Mrs Garett naye akamsongea Olivia na kumpekua. “Amezirai!” akasema kwa mshangao. Baada ya muda kidogo, wakawa wamemweka Olivia juu ya kiti, na Brian naye amepumzishwa papo.
Nyuso za wanawake hawa zilikuwa na taharuki na hofu juu. Walikuwa na kiu kikubwa cha kufahamu nini kilichojiri.
Baada ya muda wa takribani dakika sita, Brian, akiwa ametulia na kurudi kwenye hali yake mbali na maumivu aliyokuwa anayahisi kwa mbali shingoni, akaelezea namna ambavyo mambo yalitokea. Habari hizo zikawashtua sana Mrs Garett na mama yake.
“Namna gani nitamwokoa mwanangu lakini?” akalia Mrs Garett. A;lijikuta anatamani hata kumwona huyo ‘mwanaume’ ambaye amemshikilia mtoto wake huko eneo ambako palikuwa panaitwa ulimwengu wa walio wafu.
Lakini Brian akamwonya. “Sidhani kama unataka kufika huko.” wakati Brian akisema haya, alikuwa ni mtulivu sana. Anajua anachokiongelea. Anajua kilichopo kule.
“Si mahali salama hata kidogo. Panatisha, na kuna uwezekano hafifu wa kurudi hai.”
Mrs Garett akakabwa na kilio cha gubi. Mama yake Brian akajitahidi kumpooza na kumtuliza. Punde kidogo Olivia akaamka. Hakuwa anajielewa. Aliambazaambaza macho yake huku na kule na kukutana macho kwa macho na Brian! Bado Brian alikuwa na hofu juu ya binti huyo.
“Olivia!” Mrs Garett akamkumbatia mwanawe. Akambusu kwenye paji la uso na kumuuliza wapi alipokuwa. Nini anachokumbuka. Hamna kitu! Olivia hakuwa anakumbuka chochote kile zaidi ya mara ya mwisho kusinzia baada ya kutazama runinga kwa muda mrefu.
Sehemu Ya 5
Saa tatu usiku …
Walikuwa sebuleni wanakula chakula cha usiku. Walikuwa wamekawia kula leo maana chakula kiliandaliwa kwa kuchelewa. Kulikuwa ni kimya mbali na sauti ya vijiko vikigonga sahani na midomo ikitafuna.
Brian alikuwa anamtaza Olivia mara kwa mara. Macho yake hayakukaa muda pasipo kuangukia kwa mtoto huyo. Bado alikuwa na hofu naye. Alidhani pengine aweza badilika kuwa kama alivyokuwa muda ule, lakini haikuwa hivyo mpaka wanaelekea kumaliza kula.
“Brian,” mama akaita. Yeye alikuwa ashamaliza kula. “Vipi msiba? Kila kitu kilienda sawa?”
Brian akatikisa kichwa pasipo kutia neno. Akaendelea kula.
“Tulitoka leo, kwenda nje kabisa ya mji. Ni kwasababu ya haya mambo yanayotokea, ila bahati haikuwa kwetu, hatukufanikisha!” mama alizungumza. Maongezi haya yakamvutia Brian, akamtazama mamaye na kumpa miamko yote impasayo mtu aliye makini.
“ … Tulienda kumtafuta mtaalamu wa mambo ya majini, ila hakuwapo. Inaonyesha ni mtu wa ratiba nyingi. Tungempata pengine angesaidia.”
Mama alipomaliza kusema hayo, Brian akaendelea kula. Hakuona kipya. Alikuwa anatafuna lakini asihisi ladha ya chakula. Mawazo yake hayakuwapo hapo kabisa. Mama akamtazama na kisha akasafisha koo lake, Brian akampatia macho.
“ … kwahiyo tukaona itakuwa kheri endapo tungetafuta namna nyingine, hivyo tukaenda kanisani kumwona padri aje kutusaidia kwa maombi.”
“Padri Alfonso?” Olivia akauliza kwa macho yalojawa woga. Mrs Garett akamtazama na kumtikisia kichwa kuafiki. Olivia akakunja uso wake na kulalama. “Simtaki padri Alfonso!” akarudia tena, “Simtaki padri Alfonso!” alafu akaangua kilio.
“Usijali, Olivia,” akasema Mrs Garett. “Kila kitu kitakuwa sawa!” akambeba binti huyo na kumweka mapajani mwake akimbembeleza. Brian hakutia neno, akaishia kutazama tu. Na alipomaliza kula, akaenda zake chumbani.
Alipojilaza, akatazama zile nyaraka tatu alizoachiwa na Dkt Hamill. Akainyaka ile ambayo alishaanza kuisoma. Akatafuta eneo alipoishia na kuendelea kuipitia taratibu …
“ … Jasmine kabla hajanieleza kule alienda kufuata nini, akatikisa kwanza kichwa chake,” Dkt Hamill aliendelea kuhadithia kwenye nyaraka. “ … alifuma mafundo matatu alafu akaniambia kama unataka kujua basi kesho tuongozane kwenda huko. Nilihofia. Japo nilikuwa nataka kujua nini kipo kule, bado nilikuwa na hofu kifuani mwangu. Basi hapo akawa amenikata hamu, na pasipo kuaga nikajiendea.
Kesho yake nikamfuatilia, hakwenda kule msituni. Wala keshokutwa, wala mtondogoo. Ila siku iliyofuata, majira ya jioni, akapotea nyumbani. Nilimtafuta kila kona pasipo mafanikio basi nikajua ya kuwa atakuwa ameenda kule msituni.
Nikaelekea huko. Na basi kama ilivyokuwa siku ile, alipotoka nikakimbia zangu kurudi nyumbani bado nikiwa sijui ni nini mtumwa huyo anafanya mule ndani. Siku hiyo, kwenye majira ya saa mbili usiku, Jasmine akaniita. Ilikuwa ni rahisi kwa maana nilikuwa nimejiketia nje.
Akaniambia, “Hamill, twende kule bandani kuna jambo nataka kukwambia!” Nikaongozana naye kwenda huko. Akaniketisha barazani na kuniuliza, “Unapenda mazingaombwe? Unafurahi kuyaona?”
“Ndio, napenda!” nikamjibu.
“Basi kesho twende kule msituni! Twende ukaone mazingaombwe ya kufurahisha!”
“Lakini mimi naogopa kwenda msituni!” nikamwambia nikimtazama kwa hofu. Akacheka. Akanidaka mkono na kunitazama machoni. “Hamna haja ya kuogopa, upo na mimi! Usijali, nyumbani hawatajua. Kwani mimi niendapo kuna yeyote ajuaye?”
Nikalala siku hiyo nikiwa na mawazo lakini pia hamu. Nilikuwa napenda sana kwenda kuyashuhudia mazingaombwe. Nilijiuliza kumbe Jasmine huenda kwenye lile ghofu kutazama mazingaombwe! Ni nani anayafanya mule?
Wasaa ulipowadia, nakumbuka ilikuwa ni kwenye majira ya jioni ya mapema, Jasmine akauteka mkono wangu na kutokomea nami msituni. Hakuna mtu aliyetuona. Hata watumwa wengine hawakuwa wanajua. Tukatembea upesi sana.
Njiani Jasmine akinieleza namna nitakavyofurahia mazingaombwe ninayoenda kuyaona!
.
Basi kwasababu ya mwendo wetu huo, tukawasili eneoni mapema. Ilikuwa ni kama baada ya dakika sita tu! Tayari jengo ghofu lilikuwa mbele yetu. Lakini kabla hatujaingia humo, ajabu nikasikia sauti kali ya risasi! Nilishtuka mno!
.
.
Sikuwahi nimewahi kusikia sauti kali kama hiyo. Huwa nasikia risasi ila si kwa ukaribu kiasi kile. Nilipotazama kando, nikamwona Jasmine akiwa hatamaniki kwa damu! Uso wake wote ulikuwa umefumuliwa na risasi! Haki sikuwahi kuona picha ya kinyama kama ile.
.
.
Tundu kubwa lililopasua kichwa cha Jamsmine na kutapanya uso wake lilikuwa linachuruza damu kedekede. Nikatazama, kwa hofu, wapi ilipotokea risasi ile. Macho yalikua yamenitoka na moyo wanienda kwa pupa sana.
.
.
“Hey Hamill!” nikasikia sauti kavu ikiniita. Kutazama upande wangu wa kulia, nyuma, hatua kama arobaini na mbili, nikamwona baba yangu. Mkononi alikuwa amebebelea gobore kubwa alilokuwa amelitua. Kumbe ndi’ yeye aliyemuua Jasmine.
.
.
“Upo sawa?” akaniuliza akijongea. Nilikosa cha kumjibu. Nilipandwa na hasira mno. Nilimtazama kwa ghafira nikitamani kummaliza. Lakini yeye hakuwa anajali. Aliposonga karibu nami, akani ‘patipati’ kichwani na kumtazama Jasmine aliyekuwa maiti. Akamtemea mate.
.
.
“Kufa wewe malaya!”
.
.
Kwa hasira nikajikuta namshika baba yangu pindo lake la suruali na kumuuliza, “Kwanini umemuua Jasmine?” mara machozi yakaanza kunivuja. Nilishindwa kuuweka mdomo wangu sawa, ulipinda kana kwamba upinde wa mshale.
.
.
“Unasemaje?” baba yangu akafoka. “Alikuwa anakupeleka wapi huyu malaya?” akaniuliza. Asingoje hata jibu, akasema, “Nilimkanya mara kadhaa akae mbali na familia yangu, hakusikia! Kwa maana mgongo wake hausikii tena mijeledi, ngoja na tuone kama kichwa chake kinaweza kuwa sugu mbele ya risasi!” aliposema hivyo akaguna akibinua mdomo.
.
.
Akanyanyua mwili wa Jasmine na kuupeleka ndani ya ghofu. Akautupia humo na kukung’uta mikono yake kwa kumaliza kazi. “Twende!” akaniamuru.
.
.
“Siendi popote!” nikamwambia. Na nisimngoje aniambie kitu, nikakimbia nisijue wapi naelekea. Nikakimbia tu kwenda mbali na baba yangu. Nilimchukia sana. Nilimwona ni mtu asiyefaa kabisa.
.
.
Nikakimbia kadiri ya uwezo wa miguu yangu. Nilipochoka, nikalala chini na kulia sana. Pale nilipokuwa nimelaza kichwa changu pakalowana kwa machozi.
Nilikaa huko mpaka giza lilipoanza kumeza uso wa nchi. Niliogopa sana kuwa msituni nyakati za usiku ila niliona ni kheri kuliko kwenda nyumbani. Basi nikajikunyata kwa baridi na kulazimisha usingizi unitwae.
.
.
Ila kila mara nikawa nashtuka. Wanyama wakikatiza ama matunda yakidondoka ama miti ikisogezwa na upepo, nilikuwa nafungua macho na kuangaza. Nilikuwa naogopa. Sikuweza kudhani usiku ule ungekuwaje.
.
.
Nikiwa sijapata usingizi, nahangaika kufumba na kufumbua macho, nikasikia jina langu likiitwa kwenye miti! Nikanyanyua uso wangu haraka na kuangaza. Ilikuwa ni sauti ya kike. Punde kidogo nikaona mwanga wa taa kwa mbali. Haraka nikanyanyuka na kwenda kufichama nyuma ya mti kuchungulia.
.
.
Nikaendelea kuitwa. Mara ya tatu nikatambua kuwa sauti hiyo ni ya mama yangu, nikaguswa moyoni. Nikaitikia na kukimbia kwenda kumkuta mama. Alikuwa mwenyewe katikati ya msitu. Mkono wake wa kushoto ulikuwa umebebelea taa, na ule wa kulia ukiwa umebebelea gongo kubwa kumlinda.
.
.
Aliponiona akafurahi sana. Akanikumbatia kwanguvu akitupia taa kando. Akanibusu na kunikumbatia tena kwanguvu.
.
.
“Twende nyumbani!” Akasema akinishika mkono. Alikuwa ni jasiri wa namna gani. Alikuja mwenyewe msituni kunitafuta, akimwacha baba peke yake nyumbani akivuta tumbaku. Asingeweza kulala ndani mimi nikiwa nje. Kuna muda nilikuwa najiuliza, ilikuaje mama yangu akaolewa na mwanaume katili kama baba yangu? Ila niliamini watu wadhalimu huitaji zaidi malaika kama mama yangu kuliko wawahitajivyo wadhalimu wenzao.
.
.
Tukafika nyumbani salama, naye baba asiseme jambo, mdomo wake ulikuwa umetingwa na shughuli kubwa ya kunyonya tumbaku na kutemea moshi nje.
.
.
Siku hiyo nikalala kwa maruweruwe sana. Jua liliponyanyuka, nikashukuru. Nikaomboleza kifo cha Jasmine na hata ile safari yetu ya kwenda kwenye mazingaombwe. Ningeenda na nani na yeye ashakufa? Niliogopa kwenda mwenyewe ingawa eneo nalifahamu.
.
.
Basi nikaachana na mpango huo. Na sasa nikadhani ya kuwa Jasmine atakuwa ameenda milele. Nisingemwona wala kumsikia tena. Hakuna mtu anayemkumbuka mtumwa. Hakuna anayejali wala kutunza tarehe yake ya kifo, labda wenzake.
.
.
Ila nilikuwa mwongofu. Nilikosea kuwaza hivyo. Roho ya Jasmine haikwenda, ilirejea kudai haki yake ya uhai. Ilirejea ikiwa si ya yule Jasmine nimjuaye, mwenye upendo, mpole na mkarimu. Ilirejea ikiwa ya muuaji asiye na chembe ya huruma. Aliyejawa na kisasi kikubwa!”
.
.
Brian akaishia hapa kusoma. Macho yalikuwa yamechoka sasa na hakuweza kuendelea tena. Akaweka nyaraka ile kando na kuchukua muda kidogo kuyawaza yale aliyoyasoma, Hakuchukua muda, usingizi ukamkwapua asiamke mpaka asubuhi.
.
.
Hakukuwa na shule hivyo hakuwa na sababu ya kuwahi. Akajibandua kitandani majira ya saa tatu asubuhi, akaoga na kuosha uso alafu akajivuta sebuleni. Huko akamkuta mama yake, Mrs Garett na Olivia. Walikwishaamka na tayari wamejipatia kifungua kinywa.
.
.
“Brian, leo ndiyo siku ambayo Padri atakuja hapa. Naomba uwapo mapema nyumbani,” mama akakumbushia. Brian asionyeshe muitikio wowote, akaenda jikoni na kutwaa chakula cha asubuhi. Baada ya hapo, hakukaa sana nyumbani. Hakuona shughuli ya kufanya papo. Alipata wazo la kwenda kwa Brewster, kwakuwa ni asubuhi, aliamini atamkuta mzee huyo.
.
.
Aliamini ana mambo kadhaa ya kuteta naye ingawa mlengwa wake hakuwa mtu wa kuunga mkono. Mkimya. Na kwa namna moja ama nyingine, anatisha.
.
.
Kuna kitu alihisi hakipo sawa na mzee yule. Brian aliamini. Na pia alihisi kuna mambo ambayo mzee yule anayajua ila mdomowe kautia gundi.
.
.
Akaendea stoo na kuchukua baiskeli yake, akakwea na kwenda moja kwa moja nyumbani kwa Brewster. Kama ilivyo ada nyumba hii ilikuwa imetulia haswa. Ni kama vile hakukuwa na mtu aishiye hapa. Kunguru walikuwa wametandia kwenye paa, wakitazama huku na kule, huku na kule.
.
.
Brian akasonga karibu. Akaugonga mlango na kuita. Hakukuwa na majibu. Akachungulia ndani, hakumwona mtu. Sebuleni kulikuwa na kiti kimoja cha kucheza. Mbali na kiti hicho hakukuwa na samani nyingine. Sebule ilikuwa pweke, hodi ikibishwa inasikika na mwangwi.
.
.
Brian akashusha pumzi na kujiuliza kwa sekunde kadhaa. Akakata shauri la kwenda nyuma ya nyumba hiyo. Huenda Mr. Brewster akaja kumkutia huko kama ilivyokuwa siku ile.
.
.
Napo huko akakaa kwa muda mrefu akimtazama nguruwe wa Brewster. Mzee huyo hakutokea. Akawaza kuondoka, ila kabla hajafanya hilo, akapata wazo. Vipi akizama ndani ya nyumba ya mzee huyo na kutazama? Kupekua kidogo?
.
.
Huenda nikagundua mambo ambayo hataki kuniambia, akawaza. Akili yake ikatumikisha viungo vyake vya mwili kutenda wazo hilo la kidhalimu. Akauendea mlango wa nyuma na kufanya namna kwa kuufungua kwa ndani baada ya kusukuma dirisha.
.
.
Taratibu akaurudishia mlango huo na akarusha macho yake kukagua nyumba hiyo. Ilikuwa imejawa na tando za buibui kwenye kona zake. Kuta zilikuwa na ukungu. Harufu iliyokuwamo ndani haikuwa ya kuridhisha.
.
.
Brian aliwaza ni namna gani mzee huyo anaishi humo. Alifika sebuleni, akakagua. Uso wake ulikuwa umeumba ndita kwa kutopenda anachonusa. Alipomaliza kutazama sebuleni, akaendea korido kwenda kukuta vyumba viwili vya nyumba hii.
.
.
Ila kadiri alivyokuwa anapiga hatua kwenda huko, nayo harufu ikawa inazidi maradufu. Hakujua ni nini inanuka. Ilikuwa ni harufu kali ya kitu kilichooza.
.
.
Alijaribu kuusukuma mlango wa kwanza, ukafunguka. Akachungulia humo ndani. Kulikuwa na kitanda chakavu chenye godoro lililotobokatoboka. Akaangaza huku na huko. Hakuona kitu zaidi ya tando za buibui, nguo zikiwa zimezagaa huku na kule.
.
.
Akaachana nacho na kwenda kwenye chumba cha pili. Akajaribu kukifungua, mlango ukakubali. Harufu ile aliyokuwa anaisikia, sasa ikazidi mara tatu yake! Ilikuwa ni kali mno kiasi cha kuwa ngumu kuvumilika.
.
.
Brian akabana pua yake kwanguvu. Akaangaza huku na kule chumbani. Hakukuwa na kitu! Chumba kilikuwa kitupu. Kimejawa na nzi na kina kiza kiasi kutokana na kutofunguliwa kwa pazia.
.
.
Ila kabla Brian hajakiacha chumba hiki, akaona mlango mdogo kwa sakafuni. Kulikuwa na andaki kwenye chumba hiki. Na Brian akawaza kuwa huko ndipo kwenye kitu kitoacho harufu.
.
.
Akabaki njia panda, aende kutazama, ama ajiondokee upesi kabla hajakutwa?
Akawaza kwa muda mchache, akaamua kwenda kutazama. Ila kabla hajatimiza adhma yake hiyo, akachungulia dirishani kukagua kama Brewster hayupo karibu. Alipojiona yu mwenyewe eneoni, akafungua mlango wa handaki na kutupia macho yake humo ndani.
.
.
Kulikuwa kuna giza hivyo basi hakuonekani. Brian hakuweza kuona chochote kile pasipo kujali namna gani alikodoa. Kutakuwa kuna namna, aliwaza. Akatazama huku na kule akitafuta taa ya kutazamia humo ndani. Juu ukutani akaona taa inaning’inia. Akaisongea na kuikwapua. Akaiwasha na kufungulia mlango wa handaki.
.
.Akanyooshea mkono wake ndani ya handaki. Kutazama akaona vitu kadha wa kadha vikiwa ndani ya mifuko ambayo imetandiwa na nzi. Handaki ilikuwa kubwa, asingeweza kuliona lote kwa juu.
.
.
Basi akashuka chini na kuendelea kuangaza. Kulikuwa na vitu vingi ambavyo vimefungashwa na kukalia hovyo. Vyote vilikuwa vinatoa harufu kali. Ndani humu kulikuwa na harufu na hewa nzito sana.
.
.
Brian akainama na kubinyabinya miongoni mwa mizigo iliyokuwamo humo. Akiwa anaangaza, mara akaona kichwa kikubwa cha mnyama. Akakisongea kukitazama vema. Kilikuwa ni kichwa cha mnyama paa. Kilikuwa kinaelekea kuoza sasa.
.
.
Ina maana kwenye mizigo yote ile kulikuwa na nyama za wanyama? Akajiuliza Brian. Ila bado roho yake haikuwa imeridhika. Alitaka kutazama kwenye mifuko ile mingine kulikuwa na nini pia.
.
.
Akatoboa mfuko mmoja. Kabla hajatazama vema, akasikia sauti ya kengele. Akashtuka. Kengele hii ilikuwa ni ya baiskeli! Nani amebofya baiskeli yake? Ina maana Brewster amefika? Akapatwa na maswali mengi lakini zaidi hofu sana!
.
.
Moyo wake ulianza kwenda mbio sana. Kichwa kiliwaka moto, je atoke upesi humo kwenye handaki ama abaki? Kwakweli hakuwa anajua cha kufanya. Alihisi kuchangayikiwa.
.
.
Haraka akapanda ngazi kuendea juu. Alipofika kwenye kamlango ka handaki, akasikia mlango unafunguliwa, na punde vishindo vya miguu! Akawaza upesi. Akitoka, humo chumbani hakuna mahali pa kujificha, itabidi aende chumba kingine. Ni wazi ataonekana.
.
.
Kwa upesi akawaza na kuamua kubakia humohumo ndani kwenye handaki. Akasimamisha masikio yake asikie kinachoendelea.
.
.
Brewster alisafisha koo lake na kuketi kitini. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea mfuko mweusi wenye kitu ndani. Alikuwa amechoka, lakini pia macho yake yalionyeshea mawazo fulani. Si makubwa. Hakuwa anahofia.
.
.
Kwenye koti lake akatoa kiko na kukiwasha. Akawa anavuta akiwa anachambua mawazo yake kichwani. Taratibu akawa anaenda mbele na kurudi nyuma, anaenda mbele na kurudi nyuma akibembea. Mdomo wake unanyonya kiko na kutemea moshi nje. Macho yake yanatazama dirisha, mlango, paa, korido, kila sehemu.
.
.
Baiskeli aliyoikuta nje. Nyayo za viatu. Mlango kuukuta wazi. Vyote vilikuwa vinatafuna kichwa chake kwa nafasi yake. Lakini ilikuwa ni ajabu kwani hakuonyesha hofu ambayo pengine mwanadamu mwengine angeonyeshea.
.
.
Alikuwa mtulivu.
.
.
Alipovuta kiko chake kwa dakika kumi pasipo kusikia jambo, akapaza sauti yake kusema, “Ni kheri ukaja sebuleni! Utakaa huko mpaka muda gani? Nimechagua amani badala ya shari na wewe.”
.
.
Sauti yake ilisikika kila eneo ndani ya nyumba yake. Alipolijua hilo, akaendelea kuvuta kiko chake akimpa muda mvamizi ajitokeze yeye mwenyewe. Akavuta tena kwa takribani dakika tano, bado kukawa kimya. Basi akazima kiko chake na kusimama.
.
.
“Kwakuwa umekuwa punda wa kulazimishwa kunywa maji ya mtoni, acha nikupe ukitakacho!” akasema kwa sauti kubwa. Akashika njia kuendea kile chumba chake cha kwanza. Mwendo wake ulikuwa wa kikakamavu mbali na umri wake. Bado alikuwa ana nguvu za kujisogeza, na hata kupambania maisha yake.
.
.
Alienenda kwa tahadhari na alipozama ndani ya chumba hicho, nyuma ya mlango akatoa gobore lake na kulitazama kama lina risasi humo ndani. Alipoliona li vema, akalikoki tayari kwa shambulizi.
.
.
“Toka na ujisalimishe kwa usalama wako!” Brewster akafoka. Akatoka kwenye chumba alichomo na kuendea kile chumba pekee kilichobakia. Bado alikuwa anatembea kwa tahadhari sana. Alipofika humo, akagundua ya kuwa, taa ile atumiayo kuzamia kwenye handaki haikuwapo!
.
.
Akatazama mlango wa handaki. Akapata sasa shaka kuwa mvamizi atakuwa humo ndani. Taratibu akauendea mlango huo, akafungua na kuonyeshea kinywa cha gobore humo.
.
.
Akajaribu kuangaza kwa macho yake ya kizee. Hakuwa anaona kitu! Ndani kulikuwa ni giza. Na pia kuingia humo pia ilikuwa ni hatari.
.
.
Brewster akawaza cha kufanya. Hakuwa mtu mwoga ila ilimlazimu achukue tahadhari hapa. Akafyatua risasi moja ndani ya handaki. Mwanga wa risasi ukalipuka na kuangaza humo. Kwa kiasi kidogo, Brewster akawa ameona sasa.
.
.
Akajiveka ujasiri na kuzama humo. Akashusha mguu kwa taratibu, akiwa anaangaza huku na huko ingawa haoni. Alipofika katikati ya ngazi, akafyatua tena risasi apate kuona lakini pia kumtisha mvamizi aliyekuwamo humo ndani.
.
.
Ila hakujua kuwa risasi hizo zilionyesha pia mahali yeye alipo.
.
.
Aliposonga hatua tatu, ghafla akastaajabu amedakwa mguu, akadondoka chini na kubiringita kwenye ngazi mpaka chini. Akapoteza fahamu kwa muda.
.
.
Haraka Brian akatoka ndani ya handaki, ndani ya nyumba, akajikwea kwenye baiskeli na kutokomea upesi akiwa na pupa sana! Hata hakuamini kama ametoka salama.
.
.
“Nadhani leo itakuwa vema tukipika mboga za majani!” Alipendekeza Mrs Garett baada ya kuulizwa na Mama yake Brian. Tangu amekuja kwenye nyumba hii, ni nyama tu ndiyo imekuwa ikitembelea jiko.
.
.
“Basi kama ni hivyo, sina haja ya kuanza kuandaa mapema,” akasema mama Brian kisha akaketi kochini. Hapo sebuleni walikuwa wote, hao wanawake pamoja pia na Olivia.
.
.
Baada ya Mrs Garett kutazama runinga kidogo, Mama Brian akamuuliza, “Ni nini mipango yako baada ya mumeo kufariki?”
.
.
Mrs Garett akaguna na kushusha pumzi ndefu. “Sijajua. Unajua sijapata muda wa kutulia tangu mume wangu afariki. Akili yangu inashindwa kuwaza mambo ya kujiendeleza, bali hofu hofu hofu tu!” aliposema hayo, akamtazama Olivia, alafu akapeleka sura yake kando na kusema kwa sauti ya chini.
.
.
“Likipita hili nitatuliza kichwa changu niangalie chakufanya sasa. Natumai kila kitu kitakuwa sawa.”
.
.
Mama Brian akamwekea mkono wake begani. “Kila kitu kitakuwa sawa, usijali.” Mrs Garett akatikisa kichwa chake kuitikia. “Hata wewe umewezaje kwenye hali hii?” akauliza. Mama Brian akatabasamu na kusema, “Nishazoea. Ni muda sasa nikiwa mwenyewe. Japokuwa mume wangu aliniacha na kiasi kidogo cha pesa, niliweza kukikuza.
.
.
Nilihangaika sana mwanzoni, kwa upweke na kwa kutokuwa na uzoefu. Ila kadiri na muda nikazoea. Niko sawa sasa,” akamalizia kwa kutabasamu. Mrs Garett naye akatabasamu.
.
.
“Nitashukuru sana mambo yatakapotulia.”
“Usijali. Kila kitu kitakuwa sawa. Ngoja padri Alfonso akija leo tuone nini kitatokea. Naamini atatusaidia.”
.
.
Mara mlango ukafunguliwa na Brian. Alikuwa anatiririsha jasho na anahema kwa pupa. Kila mtu akamshangaa kwa namna alivyokuwa. Hakusalimu, akaenda ndani upesi, ila mara akarudi na kusema, “Akija mtu yeyote kuniulizia, sipo!”
.
.
“Kuna nini Brian?” mama akauliza. Swali hilo lilimkutia Brian akiwa koridoni anazama ndani ya chumba chake. Alikuwa yu harakani mno. Mama hakuhangaika naye, wakaendelea na mambo yao.
.
.
Muda nao ukaenda mpaka kufikia jua kuzama na ilhali hakuna yeyote aliyekuja kumuulizia Brian. Ikiwa inaelekea majira ya saa mbili na nusu usiku, Padri Alfonso na dada Magdalena wakafika hapo nyumbani. Walikuwa wamekawia kwasababu ya kutingwa na shughuli fulani fulani za huduma huko kanisani.
.
.
Padri Alfonso alikuwa amevalia joho jeupe. Dada Magdalena amevalia gauni jeusi na kiremba cheupe, shingoni amebebelea rozari.
.
.
“Karibuni sana!” Mama Brian akasema kwa tabasamu pana akiwapa mkono wageni wake. “Nimefurahi sana mpo hapa. Najua mmeacha kazi zenu lukuki kuja kutuhudumia.” Hakika wanawake hawa wakafurahi sana. Ila si kwa Olivia. Yeye alikuwa ameketi kwa mbali, macho yake yakibeba hofu. Alikuwa anawatazama Padri Alfonso na dada Magdalena kana kwamba vinyago vitishavyo. Hakuwa na amani.
.
.
“Mngependelea chai?” akauliza Mama Brian.
.
.
“Hapana.” Padri Alfonso akatikisa kichwa. “Tunashukuru. Muda umeenda, nadhani tungeendelea tu na huduma yetu.”
.
.
“Olivia!” Mama Brian akaita. “Kamwite Brian aje sebuleni.”
.
.
Olivia akasimama na kwenda. Punde kidogo akarudi na Brian ambaye alisalimu na kisha kuketi. Aliketi karibu na Olivia, kochi moja.
.
.
Basi kidogo maongezi yakachukua nafasi mama akimtambulisha Brian na kutoa historia kidogo ya familia yake. Wakati huo Brian akatambua ya kuwa Olivia hakuwa sawa. Alikuwa anahofia. Macho yake yalikuwa yanamtazama padri Alfonso.
.
.
Brian akajaribu kutazama kile akitazamacho Olivia. Ilikuwa ni kwenye pindo la mfuko wa joho la padri. Hapo alipotazama vema, akaona kitu kama damu kwa ndani ya mfuko. Akapata shaka.
.
.
Akiwa kwenye hilo ombwe, mara mlango ukagongwa. Na sauti kavu ya kizee ikasema, “Hodi!”
.
Brian akatoa macho kwa mshangao. Aliogopa. Alihisi hiyo hodi haitomtendea jema.
.
.
“Brian, kafungue mlango,” mama akamwamuru. Brian akasita. Alimtazama mama yake kwa sekunde chache kisha akanyanyuka. Hata mama alihisi Brian hayupo sawa. Aliufungua mlango na uso kwa uso akakutana na Brewster!
.
.
Mzee huyo alikuwa amekodoa macho haswa. Kwenye paji lake la uso upande wa kulia alikuwa amevilia damu. Brian akamsalimu. Alikuwa anaogopa kwa namna ambavyo Brewster alivyokuwa anamtazama.
.
.
“Mama yako yupo?”
.
.
“Ndio, yupo. Karibu.”
.
.
Brewster aliingia ndani, akasalimu kila mtu. Kwakuwa kulikuwa na watu wengi humo, akaomba kuonana na mama Brian faragha. Basi Mama Brian akaomba radhi na kisha akaelekea nje pamoja na Brewster.
.
.
Huko wakakaa kwa muda wa kama dakika tano. Waliteta wakiwa hawasikiki na hata mmoja wa walioko ndani. Walipomaliza, Brewster hakurudi tena ndani hata kuaga, akaenda zake, Mama Brian akarudi ndani peke yake.
.
.
“Samahani kwa usumbufu.”
.
.
“Usijali,” akasem Padri Alfonso kisha akauliza Mama Brian akiwa anaketi kitini. “Unamjua yule mzee?”
.
.
“Aaahmm … ndio! Kiasi chake.”
.
.
Padri Alfonso akatikisa kichwa na kunyamaza asitie neno. Mama Brian akauliza, “Vipi kuna shida yoyote?”
.
.
“Ndio, ipo.”
.
.
“Ipi hiyo?”
.
.
“Watu wanasema si mtu mzuri. Hana marafiki wala mtu wa karibu. Ni mtu anayependa upweke. Mara kadhaa nimekuwa nikiletewa mashataka yake kanisani.”
.
.
“Umejuana naye lini?” Dada Magdalena akamuuliza mama Brian.
.
.
“Si muda mrefu sana.”
.
.
“Na tangu ulipojuana naye umemwona ni mtu wa namna gani? … Anakuletea habari gani?” Dada Magdalena akaendelea kuuliza. Kidogo Mama Brian akasita. Akamtazama Padri Alfonso na Dada Magdalena kisha na kusema, “Habari za kawaida tu. Hamna cha zaidi.”
.
.
“Hamna shida. Tulikuwa tuna hofu kutokana na historia yake. Nadhani sasa tunaweza kuendelea na huduma yetu,” akasema Padri Alfonso. Basi wote wakanyanyuka na kisha taa zikazimwa na kuwashwa mishumaa kwa maelekezo ya Padri.
.
.
Dada Magdalena akafukiza, na kumwagia maji maeneo mbalimbali ya nyumba. Maji ya baraka. Kisha wakafunga macho na sala ikaanza baada ya kuimba na kusema kwa pamoja vifungu kadhaa.
.
.
Wakasali kwa dakika sita mfululizo pasi na kukoma. Kwenye dakika ya saba, Brian akavutwa mkono wake wa kuume. Upesi akafungua macho na kutazama. Akamwona Olivia akiwa amejawa na hofu usoni. Macho yake yanatiririsha machozi.
.
.
“Nini, Olivia?” Brian akauliza kwa kunong’ona akitumia haswa uso wake kufikisha ujumbe. Olivia akaonyeshea koridoni. Brian kutazama hakuona kitu. “Kuna nini?” akauliza tena kwa mtindo uleule.
.
.
Olivia akatikisa kichwa. Kwa sura na mkono wake, akaonyeshea kulikuwa na kitu. Brian akamhimiza afunge macho, asitazame popote pale. Olivia akatazama tena kule koridoni kwa mashaka, kisha akafunga macho yake, Brian akafuatia.
.
.
Sala ikawa inaendelea. Baada tena ya dakika mbili, Olivia akamvuta Brian mkono. Brian akafungua macho yake kumtazama. Lakini kabla hajasema kitu, akaona mtu anaishia koridoni upesi. Olivia akanyooshea kule koridoni na kumwambia Brian kwa ishara ya kinywa, “Kuna mtu kule!” sasa hivi Brian hakuwa na haja ya kubisha kwani kwa macho yake alishuhudia.
.
.
Alikuwa nani yule?
.
.
“Kuna mtu kule!” Olivia alisema akiwa anachuruza machozi. Sauti yake ilikuwa inasikika kwa chini maana alikuwa ananong’ona. Basi Brian akatoka pale eneo la sala na kwenda koridoni kutazama. Alirusha macho yake, hakuona kitu! Ila mlango wa chumba chake ulikuwa wazi. Ulikuwa unachezacheza kuashiria umeguswa.
.
.
Akawaza. Mtu yule amekimbilia chumbani mwake? Basi akaanza kuchukua hatua kwenda huko kutazama. Olivia alikuwa anamtazama kwa hofu, ni kama vile alikuwa anataka kumzuia asifanye hilo.
.
.
Brian akasonga. Kulikuwa ni giza, ila kwakuwa nyumba za jirani na huko nje taa zilikuwa zinawaka, basi akaweza kuona akanyagapo. Taratibu akasonga na kusonga. Alipofikia mlangoni, akatazama ndani ya chumba chake. Hakuwa anaona jambo.
.
.
Akasonga kuzama ndani. Alikuwa ana hofu. Alikuwa anatembea kwa tahadhari macho yake akiyatupa kule na kule. Alipodumbukia kabisa ndani ya chumba, akasikia sauti ya kishindo cha mguu. Akapatwa na woga. Kutazama mlangoni alikuwa ni Olivia.
.
.
“Olivia, rudi sebuleni!” Brian akamwambia kwa kunong’ona. Olivia akatikisa kichwa na kusema, “yupo kule!”
.
.
“Wapi?” Brian akauliza.
.
.
“Jikoni!” Olivia akajibu akionyeshea kidole. Basi Brian, upesi, akatoka na kwenda jikoni akiongozana na Olivia. Walipofika huko hawakukuta kitu.
.
.
“Hamna kitu, Olivia.”
.
.
“Nilimwona! Alinichungulia na kisha akakimbilia huko!”
.
.
Brian akashusha pumzi ndefu. “Olivia, huyo mtu hataki tuwepo kwenye sala. Anatusumbua tusishiriki huduma. Turudi kwenye maombi na sasa tusitazame wala kuhangaika naye.”
.
.
Olivia akajibu kwa kumeza mate. Brian akautwaa mkono wake na kumrudisha sebuleni lakini binti huyo akitazamatazama huko nyuma, pembeni na kule aelekeapo.
.
.
Wakajiunga na sala. Wakafunga macho yao kwanguvu wakitulia. Kheri wale waliowaacha hawakutambua kama waliondoka. Au labda walitambua wakanyamaza.
.
.
Sala, kama walivyoiacha, ikaendelea. Sasa hivi wakadumu kwa dakika moja tu, na mara Brian akaanza kuhisi upepo kana kwamba wapo nje ya jengo. Akakunja uso wake kwa maulizo, ila hakufungua macho yake. Punde, sauti ya sala ikakoma!
.
.
Brian akiwa amefumba macho yake, yu gizani, akajitahidi kuskiza asisikie kitu. Muda kidogo akasikia sauti ya Olivia ikimwita! Akafungua macho kutazama, akamwona Olivia akiwa kando yake. Ila hawakuwa ndani bali nje! Kiza. Kimya.
.
.
“Olivia tuko wapi hapa?” Brian akauliza akitazama kila pande yake. Wote walikuwa wamejawa na hofu. Olivia alikuwa anachuruza machozi lukuki hata kunena hawezi.
.
.
Kutazama vema, wakagundua eneo walilopo ni la kanisa. Hapo palikuwa ni uwanjani. Hatua kama ishirini na nne mbele upande wao wa kaskazini kulikuwa na jengo kubwa la kanisa la Boston!
.
.
Wamefikaje hapa?
.
.
“Brian!” Olivia akaita. Akanyooshea kidole chake upande wa mashariki, huko, kwa mbali, Brian akamwona mtu akiwa amevalia nguo nyeupe. Mrefu, amesimama wima. Na kando ya mtu huyo, akamwona mwingine kama kivuli, ila kichwa chenye kiremba cheupe!
.
.
Punde watu hao wakaanza kuwasogelea! Mwendo wao ulikuwa ni kana kwamba watu wasio na maungio ama wamevunjika mifupa lakini wakitaka tu kutembea! Waliogofya. Na japo walikuwa mbali, macho yalikuwa yanang’aa kama taa ama paka awapo gizani.
.
.
“Kimbia!” Brian akaropoka. Upesi wakaanza kukimbia na Olivia kuelekea kule kanisani. Hawakuwa wanaona majengo mengine yoyote zaidi ya kanisa. Mbali na jengo hilo kulikuwa na misitu tu ikiwa imewazingira!
.
.
Wakakimbia kwa kasi na kukomea kwenye lango la kanisa. Wakajaribu kulifungua, haikuwezekana. Lilikuwa limetiwa ‘lock’, basi haraka wakaachana nalo na kuuendea mlango mwingine mdogo. Wakaujaribu, huo ukafunguka.
.
.
Wakazama ndani upesi na kuurejeshea. Wakiwa wanahema kwa pupa, macho yamewatoka, wakapata tulizo ya kuwa huenda sasa wakawa salama. Ila punde wakapata hisia tofauti! Ni kama baada ya sekunde sita tangu kuingia humo. Walihisi hawakuwa wenyewe, kuna watu wengine zaidi ya wao ndani ya jengo.
.
.
Kutazama kwenye ukumbi wa kanisa, vitini, kulikuwa na watu wameketi. Na walipotazama madhabauni, kulikuwa na padri, Padri Alfonso, akiongoza misa.
.
.
Nyuso za watu wote hawa hazikuwa za watu wa kawaida. Zilikuwa ni nyuso nyeupe zilizojawa na michirizi meusi kana kwamba vijito vya mito. Midomo meusi. Macho ya njano na nyekundu yaliyokuwa yanawatazama watu walioharibu misa yao, Brian na Olivia!
.
.
Kwa muda kidogo Brian akakosa la kufanya. Olivia akalia kwa hofu. Waliona huo ndiyo mwisho wa maisha yao. Waumini wote wakasimama na wakiongozwa na Padri Alfonso na Dada Magdalena wakawasogelea Brian na Olivia ambao hawakuwa na mahali pengine pa kukimbilia. Walijaribu kufungua mlango pasipo mafanikio.
.
.
Waliwapowasogelea kabisa, wakasimama wote na kusema kwa pamoja, “Unaona nini Brian?” kisha wakanyoosha mikono yao kuwadaka.
.
.
Brian na Olivia wakapiga kelele kali. Wakawashtua watu wote waliokuwepo kwenye sala. Wote wakakoma kusali na kuwatazama kwa mshangao.
.
.
“Brian! Olivia! Mmekumbwa na nini?” mama Brian akauliza. Brian kabla hajajibu kitu, akarusha macho yake kwa Padri Alfonso na Dada Magdalena. Dada Magdalena akatabasamu.
Brian akalipuka kwa hofu. Akamnyooshea kidole Dada Magdalena na kusema, “Ni mashetani!”
“Unasemaje Brian?” Mama akauliza akiduwaa.
“Ni mashetani!” Brian akalia. Aliwanyooshea kidole Padri Alfonso na Dada Magdalena. “Hawa ni mashetani! Mashetani! Tokeni nyumbani kwetu. Mashetani!”
Ikawa vurugu asitake kusikia wala kuambiwa kitu akaelewa. Aling’ang’ana Padri Alfonso na Dada Magdalena ni mashetani, watoke nyumbani kwao! Waende zao.
Basi sababu ya vurugu hii, Padri Alfonso na Dada Magdalena wakaaga waende zao. Mama Brian akawaomba radhi kwa yote yaliyotokea.
“Usijali,” Padri Alfonso akasema akiufuata mlango. Nyuma yake Dada Magdalena akimfuatia. Wakaenda zao na amani ikarejea kwa muda kwenye nyumba ya wakina Brian. Ila walezi wakiwa hawajui liendealo. Kwa namna moja wamechanganyikiwa, wamejawa na maswali pia hofu.
“Brian, Olivia, mnaweza mkatuambia nini shida?” mama aliuliza. Sebule ilikuwa imetulia tuli. Taa zimewashwa na hata madirisha yamefunguliwa.
“Ni mashetani!” Brian akasema akitazama chini kama mtu anayateswa na fikira. “Nimewaona kwa macho yangu. Tumewaona! Padri Alfonso na Dada Magdalena ni mashetani! Si watu wa dini!”
“Mmewaona wapi?” Mrs Garett akauliza.
“Kule kanisani!”
“Lini?”
“Leo! Leo wakati tunasali!”
Mrs Garett na Mama Brian wakatazamana. “Brian, ulienda kanisani muda gani na wakati ulikuwapo hapa?” waliwaona Brian na Olivia ni watu waliochanganyikiwa. Maelezo yao yalikuwa hayawaingii akilini. Yalikuwa ni ya kufikirika. Vitu visivyowezekana!
“Sijui huu mji unaelekea wapi? …” akasema Brian kwa sauti ya pole. Macho yake yalikuwa pole. Anatazama meza akiwandawanda mawazoni. “ … Naogopa sana. Sijui ni wangapi ni binadamu kama sisi, nyumba ngapi zimetwaliwa na kukaliwa na mashetani … Inatisha…”
Brian aliposema hayo, akanyanyuka akitaka kwenda zake chumbani.
“Ngoja, Brian,” mamaye akamshika mkono. “Ulimwona Brewster?” Brian kusikia hivyo, akaketi chini. “Ndio, nimemwona.”
“Alikuja kwa ajili yako.”
“Kukuambia kuwa nimevunja nyumba yake?”
“Umevunja nyumba yake?” Mama akashangaa. “Hapana, si hilo!”
“Amekuambia nini?” Brian akauliza akimtazama mamaye kwa mshangao.
“Amenipa onyo tu kama ilivyo kawaida yake … Brian, ulienda kwenye nyumba ya marehemu?”
“Marehemu?”
“Mkuu wenu wa shule aliyefariki majuzi!”
“Dkt Hamill! … Brewster amekuambia nini?”
“Jibu, ulienda huko?”
Brian akanyamaza kidogo.
“Ndiyo nilienda. Jana.”
“Ulienda kufanya nini huko na mwenyewe hayupo? Amekwishafariki!”
“Mama, Dkt Hamill alikufa mbele ya uwepo wangu. Nyakati zake za mwisho alikuwa na mimi. Kuna ubaya ga–?”
“Brian! … tafadhali unaweza ukakaa mbali na matatizo kwa muda?”
Brian akakuna kichwa chake akikitikisa. “Mama, nimechoshwa na hili! … ina maana umemweka Brewster awe ananifuatilia si ndio?”
“Mimi na wewe tunajua hilo haliwezekani. Umemsikia Padri Alfonso alivyokuwa anamwongelea Brewster. Sipendi kumwona, lakini haimaanishi nisimsikilize anachoniambia! Na ni kweli aniambiayo.”
“Kwanini ananifuatilia? Kwanini mimi?”
“Na hilo ndilo linalonipa hofu. Brian, kaa mbali na mambo ya ajabuajabu. Tafadhali.”
Brian akakaa kimya. Alikua anawaza kichwani mwake. Mbona Brewster anamfuatilia? Lakini zaidi, mbona hakumwambia mama yake kuwa amevunja nyumba yake kuingia ndani? Ina maana hajajua kuwa ni yeye?
Hapana. Kama anajua vitu ambavyo hudhani yu mwenyewe, ataacha kujua jambo kama hilo la kwenda kwake? Ilikuwa haiingii akilini.
Brian akanyanyuka na kwenda chumbani. Akatulia kitandani mwake akiwaza juu ya yale mambo aliyotoka kuyaona. Yalikuwa ni mambo mengi ya kumuumiza kichwa. Mengi ya kumuogopesha. Aliwaza nini yatakuwa mwisho wa yote hayo?
Alinyanyuka akaendea dirisha la chumba chake na kutazama nje. Alitazama nyumba za jirani zilizopo karibu mpaka zile zilizokuwapo mbali. Akawaza sana. Je katika nyumba hizo, kuna watu kama wakina ‘Padri Alfonso?’. Alipata hisia za kumwogopa kila mtu sasa, lakini zaidi Brewster. Kwanini mwanaume huyo anamfuatilia kiasi hiko? Na kule kwenye handaki lake ….
Sehemu Ya 6
Aliendelea kutazama nje kana kwamba mtu atazamaye runinga kisha akasombwa na mawazo. Alikaa hapo kwa takribani dakika tano, akashusha pumzi ndefu, na kugeukia kitanda chake. Akapiga hatua tatu kukifuata, ila kabla hajakifikia, akasikia dirisha linagongwa!
Haraka akageuza shingo yake kutazama. Hakuona kitu! Akasonga kulifuata dirisha na kutazama nje. Hakuona kitu. Akatikisa kichwa na kurudi kitandani. Akanyaka ile nyaraka ya Dkt Hamill ambayo bado hajaimaliza, akaiweka machoni apate kuendelea kuisoma.
Kabla hajaanza akasikia sauti ya dirisha likifunguka. Haraka akatupa macho yake kutazama. Akaona dirisha likiwa wazi, kioo kimefunguliwa. Akatazama kwa kama sekunde tano, hakuona jambo. Ila kidogo, akaanza kusikia sauti ya watoto.
Akaweka nyaraka yake pembeni na kunyanyuka taratibu kufuata dirisha atazame. Alipofika, akachomoza kichwa chake nje ya dirisha. Akatazama barabarani upande wa kushoto. Hakukuwa na kitu. Upande wa kulia. Hakukuwa na kitu!
Kabla hajarudisha kichwa chake ndani, mara kioo cha dirisha kikashuka chini na kukaba shingo yake. Akapapatika upesi kujinasua toka kwenye dirisha. Alipojinasua, akabaki anahema kwanguvu na kushika shingo yake kwa maumivu makali.
Hata mate aliona hayapiti kooni. Alipata woga, kila saa akitazama dirishani.
**
Baada ya kuzima bomba la maji mvua, Mrs Garett alitoka bafuni alimokuwa anaoga. Alifunga vema taulo lake kifuani na moja kwa moja akaendea sinki kwa ajili ya kusugua meno akamilishe zoezi lake la usafi.
Alitia dawa kwenye mswaki na kuanza kujisafisha. Hakuwa na hili wala lile. Macho yake yalikuwa yanatazama kioo muda wote akijikagua uso. Kumbe bado alikuwa kijana, alijiona. Kumbe bado anaweza kupata mwanaume mwingine na kuwa na familia, aliwaza kichwani.
Aliposafisha meno yake na kutema povu la dawa, akainua uso wake kutazama kioo. Ajabu akamwona Kecie nyuma yake! Akapiga kelele za woga macho yakiwa yamemtoka. Haraka akatazama nyuma, hakumwona mtu! Aliporudisha uso wake kwenye kioo, akakutana uso kwa uso na Kecie! Akapiga kelele kali za kumshtua kila mtu ndani ya nyumba.
Ndani ya dakika tatu, Mama Brian na Brian wakafika bafuni. Ila walikuwa wamechelewa. Mrs Garett alikuwa tayari amekwishakufa. Kichwa chake kilikuwa kimepondwapondwa kwenye sinki, sinki lote limekuwa jekundu kwa kujawa na damu!
“Mungu wangu!” Mama Brian akatahamaki akiwa ameziba mdomo wake. Muda si mrefu macho yake yakawa mekundu na kutiririsha machozi. Alimkumbatia mwanae na kuendelea kulia.
Brian akambembeleza mamaye akiwa anatazama mwili mfu wa Mrs Garett. Ila akiwa anatazama vema, akaona maandishi yakiwa yameandikwa kwa damu karibu na dirisha la bafuni! Alipoyafinya macho yake kutazama vema, akauona maandishi hayo yakisomeka, “Tazame vema mji wenu!”
**
Baada ya siku mbili tangu Mrs Garett azikwe … saa saba mchana.
Brewster akiwa amebebelea karatasi kadhaa mikononi mwake na mashine ya chuma ya kubania makaratasi hayo, alionekana akiwa anatembea kwa pole barabarani.
Alijongea kufuata mstimu mmoja pembezoni ya barabara, akabandika picha tatu tofauti za watoto waliopotea. Mmmoja alikuwa wa kike, wawili wa kiume. Alipofanya hivyo, akaendelea na mwendo wake wa taratibu kufuata mstimu mwingine kutimiza majukumu yake.
“Umeona matangazo ya wale watoto waliopotea?” aliuliza Mama Brian akiwa amesimama dirishani anamtazama Brewster akiishilia. Brian akanyanyuka upesi na kwenda dirishani kuangaza. Hakuona vema, akatoka kwenda nje kuufuata mstimu uliobandikiwa tangazo aone vema.
Akasoma matangazo yote hayo matatu na kugundua kuwa miongoni mwa wale waliopotea, mmoja wao anamfahamu fika. Alikuwa ni Silvia! Silvia rafiki yake mkubwa na Wayde. Wayde mtoto wa seneta wa Massachusetts!
Akaachama kwa mshangao. Nini kinaendelea?
.
Akarudi ndani na kumwambia mama yake kuwa mmoja wa wale waliopotea anamjua kwani wanasoma naye darasa moja. Na basi kutaka taarifa zaidi, akajipaki kwenye baiskeli yake, hakuweza kungoja, akaenda moja kwa moja kwa wakina Silvia.
.
.
Huko akamkuta Wayde akiwa ameketi kibarazani. Akamsalimu na kumuuliza nini kimejiri. Wayde alikuwa anachuruza machozi. Pua yake imekuwa nyekundu kwa kuifikicha.
.
.
“Silvia amepotea, Brian!” Wayde akalia. Akamkumbatia Brian na kuendelea kulia. Brian akapata kibarua cha kumbembeleza binti huyo kwa muda kidogo kabla hajatulia na kuendelea na maongezi yao.
.
.
“Ni jana tu, Brian!” akasema Wayde akiwa amebanwa na kwikwi. “Ni jana tu amepotea katika mazingira ya kutatanisha! Yaani siamini, Brian! Siamini kabisa! Nimejawa na hofu sana.”
.
.
“Ilikuwaje akapotea? Unaweza ukaniambia mazingira ya kupotea kwake?” Brian akauliza akimtazama Wayde usoni.
.
.
“Brian, usiku wa kuamkia juzi, wakati tukiwa tunaenda klabu, Silvia aliniuliza kuhusu ndoto za ajabu! Sikumwelewa, na sikutilia sana maanani. Najuta kwanini nilifanya hivyo. Aliniambia Wayde, nimeota naitwa usiku wa manane. Kuna mwanaume ananiita. Kuna mtoto ananiita. Watu hao wamesimama mlangoni, wamesimama dirishani!”
.
.
“Ni wakina nani? Aliwatambua?”
.
.
“Hapana. Aliniambia ni kama vivuli tu. Ajabu ni kwamba walikuwa wanamuitia kwenda kutazama mazingaombwe!”
.
.
“Ikawaje akanusurika siku hiyo?” Brian akadadisi.
.
.
“Wakati anatoka chumbani kwake, katika hali ya kutojielewa, akakutana na mama yake koridoni! Mama yake alimkurupusha na kumuuliza nini alikuwa anafanya, lakini hakuwa anajua kitu! Hakujua hata alifikaje pale koridoni. Kitu pekee alichoweza kumbuka ni kuitiwa kwenda kutazama mazingaombwe na wale watu!”
.
.
“Kwahiyo ndiyo haohao watakaokuwa wamemchukua?”
.
.
“Ni nani mwengine, Brian? … asubuhi ya leo, wazazi wake walikuta chumba chake kikiwa wazi, pia mlango wa sebuleni. Na skafu yake imeokotwa huko msituni.” machozi yakabubuja macho ya Wayde. “Silvia ametokomea huko!”
.
.
“Polisi wanasemaje?” Brian akauliza.
.
.
“Wamesaka msitu wote tangu asubuhi. Hakuna walichopata zaidi ya skafu yake.”
.
.
Brian akashusha pumzi na kushika tama akitazama barabara. “Brian, kuna lolote unajua?” Wayde aliuliza. Brian akatikisa kichwa akibinua mdomo. Akasema, “ni ajabu. Watu watatu wapotea ndani ya siku moja! Si jambo la kawaida hata kidogo.”
.
.
“Ni lazima kutakuwa na kitu,” Wayde akaunga mkono hoja. “Ngoja tuone ripoti ya polisi itasemaje. Ila …” Wayde akabinua mdomowe. “Sidhani kama kutakuwa na cha maana.”
.
.
“Kusipokuwa na cha maana utafanya nini?” Brian akamtazama Wayde. “Kuna kitu unaweza kufanya kwa ajili ya rafiki yako?”
.
.
“Chochote kile,” akasema Wayde akitikisa kichwa. “Kwanini unaniuliza hivyo Brian?”
.
.
“Nimetaka tu kujua,” Brian akajibu kisha akasimama na kumuaga Wayde. “Ningependa kukaa na wewe lakini unajua ku–”
.
.
“Unamwogopa baba yangu, sio?”
.
.
Brian hakutia neno.
.
.
“Usijali, Brian. Naelewa. Unaweza kwenda, lakini utakapopata kitu kuhusu Silvia, usisite kunijuza.”
.
.
“Ni mwanafunzi mwenzagu. Najali pia,” akasema Brian kabla hajajiweka kwenye baiskeli yake na kwenda zake.
.
.
.
**
.
.
Saa mbili usiku …
.
.
Baada ya ukimya mdogo wakiwa wanatazama runinga, Brian akamtazama mama yake na kumwita. Akamwambia kwa sauti ya chini, “Mama, Kecie ameanza kuua watu!”
.
.
“Kwanini unasema hivyo, Brian?”
.
.
“Nimekaa nikafikiri sana. Sasa ndiyo nimepata maana ya ujumbe ule ambao tuliukuta bafuni baada ya Mrs Garett kuuawa … unaukumbuka ujumbe ule?”
.
.
“Ndio.”
.
.
“Naona vitakuwa na mahusiano na huku kupotea kwa watu. Kwanini alituambia tutazame mji wetu?”
.
.
Mama akabaki kimya.
.
.
“Lakini kwanini muuaji huyo alituambia hivyo? Kwanini ametupa ujumbe huo baada ya Mrs Garett kuuawa?”
.
.
Hakuna aliyekuwa anajua. Walijawa na hofu. Hawakufahamu kama kupotea huko kwa watu kutakoma ama kutaendelea tena kesho yake. Lilikuwa ni swala la muda tu.
.
.
Basi baada ya muda kidogo, Brian akanyanyuka na kwenda zake chumbani. Alikuwa anataka kulala. Siku mbili za nyuma amekuwa akishughulika sana, haswa kutokana na msiba wa Mrs Garett, hivyo hakupata muda wa kupumzika vema.
.
.
Lakini basi kuvutia usingizi, akanyaka nyaraka ya Dkt Hamill aendelee kuisogeza karatasi kadhaa. Hakuwa ameipitia nyaraka hiyo tangu majuzi. Hakuwa na huo muda.
.
.
Alifungua alipoishia akaendelea kupekua kwa macho tangu pale ambapo mtumwa Jasmine alikuwa ameuawa na baba yake mzazi kisha kutupiwa ndani ya jengo ghofu la Helo.
.
.
“ … nakumbuka siku hiyo, ilikuwa ni usiku nikiwa chumbani mwangu, nikasikia sauti kali ya mama yangu. Haraka nikanyanyuka na kwenda chumbani kwake. Nilidhani ni baba ndiye anampiga mama, lakini nilipofika nikakuta habari tofauti. Mama alikuwa analia kwa woga wa kumwona mfu!
.
.
‘Kuna nini?’ nikamuuliza. Alikuwa amesimama kwenye kona ya chumba chake na bado sikuwa nimeona wapi baba alipo. Mama alikuwa anamimina machozi na ndita amezikunja haswa.
.
.
Akaninyooshea kidole nyuma yangu, yaani nyuma ya mlango. Nilipotazama nikauona mwili wa baba ukiwa umelala unachuruza damu nyingi mno. Nikaogopa haswa. Nikamuuliza mama nini kimemuua baba, akanijibu, ‘Jasmine!’
.
.
Nikastaajabu. Jasmine atakuwaje amemuua baba ingali amekufa?
.
.
‘Nimemwona kwa macho yangu!’ akasema mama akiwa ametoa macho ya woga. ‘Nimemwona Jasmine na amesema amerudi kulipa kisasi!’
.
.
Habari hizi zikaniogopesha kweli. Kesho na keshokutwa yake tukafanya utaratibu na baba akazikwa. Ila mambo bado yakaendelea kutokuwa shwari. Baada ya baba kufa, sasa watumwa wakaanza kupotea mmoja mmoja tukiambiwa ameelekea msituni! Ni kama mchezo, mwishowe wote wakapotea asibaki hata mmoja. Kwenye eneo zima, nyumba yote, tukabaki wawili tu mimi na mama yangu.
.
.
Hapo ndipo nilipogundua ya kuwa msitu ule umelaaniwa. Na aliyeulaani msitu ule ni yule ambaye anaishi humo. Helo. Kama vile alivyouawa kwa hatia, na kutupiwa huko, basi wote wale wanaouawa kwa hatia na kutupiwa humo msituni, huamka tena na kwenda kuwaangamiza wale waliosababisha vifo vyao.”
.
.
Brian alipofikia hapo, akafunga nyaraka na kujiuliza maswali juu ya hiko alichokisoma. Ina maana kile kilichotokea kwa Jasmine ndicho ambacho kinatokea kwa Kecie saa hii? Kama ilivyokuwa kwa Jasmine, Kecie aliuawa na kwenda kuzikiwa huko msituni. Kama pia ilivyokuwa kwa Jasmine, naye Kecie akawamaliza wazazi wake waliomuua.
.
.
Alafu kama ilivyokuwa kwa Jasmine, baada ya kumuua mtu aliyemuua, watumwa wenzake wakaanza kupotelea msituni, navyo kwa Kecie baada ya kuua wazazi wake, watu wameanza kupotelea msituni!! Ajabu. Ina maana Kecie alikuwa anajua kitakachofuatia baada ya yeye kummaliza mama yake? Ndio. Na ndiyo maana akaacha ujumbe wa kutazama mji?
.
.
Briana akapatwa na maswali haswa. Ina maana Kecie alikuwa anawatahadharisha? Kwanini afanye hivyo? Ina maana si yeye anayewapoteza hao watu msituni, bali Helo!
.
.
Helo anamtumikisha Kecie kufanya mambo yake ya kupoteza watu. Kecie hataki, na ndiyo maana anataka Brian amwokoe? Brian akajikuta anaketi akichakata mawazo haya. Sasa alipata picha kamili juu ya kinachoendelea. Ila bado hakuwa anajua cha kufanya. Atafanyaje kumwokoa Kecie?
.
.
Mara akasikia hodi mlangoni! Akashtuka haswa akikodoa macho.
.
.
“Nani?” Akauliza. Hakukuwa na majibu, akasita kwenda kufungua. Hodi ikapigwa tena. Akaamua kunyanyuka na kuusogelea mlango. “Nani?” akauliza tena. Hakukuwa na majibu. Brian akaamua kufungua mlango na kutazama nje.
.
.
Hamaki, kule sebuleni akauona mlango ukiwa wazi! Na kama haitoshi, akamwona Olivia akiwa anaishia, anaenda zake!
.
.
“Olivia!” Brian akapaza sauti. Haraka akatoka chumbani na kukimbilia nje.
Alimuwahi Olivia na kumsimamisha. Binti hakuwa anajitambua. Brian alijaribu kumwamsha toka usingizini pasipo mafanikio. Bado Olivia alikuwa anataka kwenda, anataka kusonga mbele! Macho yake yalikuwa yamepandisha kiini cheusi juu kupotea!
.
.
“Olivia, amka! Oliviaa!” Brian aliita akimtikisa Olivia kwanguvu. Akaita pasipo kuchoka, hatimaye Olivia akarejewa na fahamu! Alikuwa anahema kana kwamba ametoka kukimbizwa. Alitazama kando na kando akaitaajabu kwanini yupo hapo.
.
.
“Olivia, upo sawa?” Brian akauliza. Olivia akatikisa kichwa. Uso wake ulikuwa umejawa na woga. “Nipo wapi hapa Brian?” akauliza.
.
.
“Upo nje! Ulikuwa umetoka, unaondoka!” Brian akamjibu akimtazama mtoto huyo kwa matumaini. Lakini ghafla, Olivia akatazama nyuma ya Brian na kuduwaza macho. Akaachama mdomo na kumuuliza Brian, “Ni nani yule?”
.
.
Brian akageuza shingo kutazama. Ajabu akamwona mwanaume mrefu mweusi aliyekuwa anaongozana na mtoto akija kwa kasi kuwafuata. Moyo wake ukaruka pigo. Haraka akamnyakua Olivia na kuanza kukimbia naye haraka!
.
.
Alitupa miguu kadiri alivyokuwa anaweza. Kila alipotazama nyuma akaona mwanaume yule akimjongea kwa kasi ya ajabu. Alikuwa anakimbia kana kwamba upepo!
.
.
“Wanatufikiaa!” Olivia akapiga kelele. “Brian, wanatufikiaa!” Olivia akalia. Lakini nini afanye Brian? Alikuwa anakazana kadiri ya uwezo wake wa mwisho. Alikimbia haswa. Alikuwa amebakiza hatua chache tu kufikia mlango wa nyumbani, ila ajabu napo, mlango huo ukaanza kujifunga wenyewe taratibu!
.
.
Kwa mahesabu ya wazi, Brian asingeweza kuufikia mlango huo kabla haujajifunga.
.
.
“Tafadhali, usifunge!” Brian akalia. Hakuwa anaweza kuongeza tena kasi kwani hapo alikuwa tayari kwenye kikomo. Alichokifanya, alipoukaribia kidogo mlango, wazi akiona unaelekea kufunga, akaruka hewani kuuparamia.
.
.
Akadondokea chini kama mzigo, Olivia akiangukia upande mwingine. Lakini kabla hajaugulia maumivu, akaukita mlango kwa mguu wake wa kuume, mlango ukafunga! Haraka akanyanyuka na kuutia komeo kisha akasimama hapo akiskiza nini kitaendelea.
.
.
Punde akasikia kishindo cha mtu mlangoni. Mlango ukagongwa mara mbili na sauti ikanong’ona, “Heeeeeyy! … wataka kucheza?” Brian hakusema kitu. Alikuwa amesimama hapo kuugandamizia mlango akiwa amejawa na woga.
.
.
“Najua unataka kucheza, sivyo hivyo Brian?” sauti iliendelea kunong’ona. “Najua unapenda kucheza … njoo basi, twende tukacheze … eti?”
.
.
Brian hakusema kitu, akaendelea kuwa kimya. Naye Olivia alikuwa ametulia akimtazama Brian.
.
.
Wakasikia kishindo kile cha miguu kikisonga kwenda mbali na mlango na kisha kurudi karibu. Kwenda mbali na kisha kurudi karibu. Mara kikakoma. Alafu sauti ile ikauliza, “Brian, hutaki kumwona Silvia?”
.
.
Brian akakodoa kwa mshangao.
.
.
“Yupo wapi?” akaropoka kuuliza.
.
.
“Yupo kule, twende ukamwone!” sauti ikamjibu. “Twende upesi!”
.
.
“Anafanya nini huko?”
.
.
“Anatazama mazingaombwe! Hutaki na wewe kuona?”
.
.
“Sitaki!” Brian akafoka. “Sitaki kukuona maishani mwangu. Sitaki uje kwetu. Kaa mbali na sisi!” Brian alisema machozi yakiwa yanamtoka. Mara kukawa kimya kwa sekunde tano, hakuwa anasikia kitu. Alitega masikio yake vema akiwa anatazama madirishani.
.
.
Mara akasikia sauti ya kike, “Brian, niokoe! Niokoea tafadhali!”
.
.
Brian akagutuka. “Silvia!” akajikuta anaropoka. “Silviaa!”
.
.
“Ndio, Brian!” sauti ya kike ikamjibu. “Naomba uniokoe Brian!” sauti ikalia. “Naomba uniokoe, tafadhali!” ikaendelea kulia na kulia. Brian akatamani kufungua mlango. Alitazama kitasa akitaka kukiminya, Olivia akapaza sauti, “Hapana, Brian!”
.
.
Brian akamtazama Olivia.
.
.
“Usifungue, Brian. Usifungue! Sio Silvia huyo.”
.
.
Mara mlango ukaanza kupondwa kwanguvu! Nguvu ya kuponda ilikuwa kubwa sana. Ukuta ulikuwa unatikisika. Bawaba zilikuwa zinalegea. Olivia akaenda kumsaidia Brian kuminya mlango lakini haikusaidia chochote kwani mlango uliendelea kupondwa kwanguvu sana. Ukaanza kutia ufa kana kwamba gogo lililooza likikitwa na ncha ya shoka kali.
.
.
Mara,
.
.
“Briaaaan!” sauti ya kike ikaita. Brian alipotazama koridoni akamwona mama yake akiwa amesimama, anawatazama kwa mshangao mkuu. Ni ghafla pia mlango ukaacha kupondwa na kukawa kimya kabisa kana kwamba hakuna kilichotokea!
.
.
“Brian, kuna nini?” mama akauliza akijongea. Brian alikosa cha kusema akabaki kimya. Mama alisonga karibu akatazama mlango. Ulichora ufa haswa. Bawaba zilikuwa zimetema nati zake. Ukuta ulikuwa umechimba mistari!
.
.
**
.
.
Mama alifikicha macho yake kisha akamtazama Brian aliyekuwa ameketi kwenye kiti pamoja na Olivia. Akashusha pumzi ndefu na kukuna kichwa chake kilichojawa na nywele.
.
.
“Hili ni tatizo kubwa mno, kila siku linazidi kukua. Kama tusipochukua hatua za mapema, linaweza kutugharimu.”
.
.
Kukawa kimya Mama aliponyamaza. Vinywa vilikuwa vizito. Akili zilipoa. Ni kama vile walikuwa wamenyeshewa mvua.
.
.
“Nadhani inabidi turudi kule kwa mtaalamu demonolojia,” Mama akaendelea kuteta. “Bila shaka yule ndiye mtu pekee aliyebakia wa kutusaidia.”
.
.
“Tutaenda lini?” akauliza Brian.
.
.
“Jua litakapochomoza,” mama akajibu na kuongezea, “Jiandaeni kabisa maana umebaki muda mchache kwenda huko … nadhani tutalala hukohuko.”
.
.
Mama aliposema hayo akaenda zake. Kweli jua lilipochomoza wakajikwea kwenye gari wakiwa wamebebelea mahitaji kadhaa tayari kwa ajili ya safari. Brian aliona ni stara kubeba zile nyaraka tatu za Dkt Hamill, alizitia garini akilenga kuendelea kuzisoma safarini.
.
.
Wakafunga nyumba, safari ikaanza.
.
.
Wakatembea kwa muda wa masaa mawili. Wakaacha mji wote nyuma na kuzama katikati ya misitu. Mwendo ulikuwa wa upesi maana safari ilikuwa ndefu. Basi Brian, ambaye alikuwa ameketi nyuma peke yake, akawa ameegamishia kichwa chake kwenye kiti akitazama miti irudiyo nyuma.
.
.
Alikuwa ametulia haswa. Alikuwa anawaza mambo yake kichwani. Lakini ukimya wake huo haukudumu kwa muda mrefu. Akiwa hana hili wala lile, mara akaanza kusikia sauti nyembamba ikimnong’oneza masikioni … “Brian, unataka kucheza?” akashtuka kidogo na kutumbua macho. Akatazama kila pande akiwa amekunja ndita.
.
.
Sauti ile masikioni ikacheka ikiishilia … “Wataka kuniona?” ikanong’ona. “Wataka kuniona Brian?” mara Brian alipotazama kushoto kwake akamwona mtu aliyevalia nguo nyeupe akikatiza ghafla kana kwamba radi! Akatoa macho kushangaa!
.
.
Akakunja uso wake kuangaza. Alitupa macho kwenye kioo cha nyuma cha gari lakini hakumwona mtu. Alishusha vioo vyote vya nyuma, akatazama pasipo mafanikio.
.
.
Basi punde, upepo mkali ukapuliza. Sijui ulikuwa umetokea wapi. Ulizama ndani ya gari kwakuwa vioo vvya nyuma vilikuwa wazi. Ajabu ukasomba zile nyaraka za Dkt Hamill na kuzimwagia nje!
ukazipeperusha huku na huko kutawanyika.
.
.
“Mama, simamisha gari! Simamisha garii!” Brian akawaka akimpigapiga mama yake begani. Mama akasimamisha gari upesi, na kumtazama Brian kwa taharuki. “Vipi?” Brian alitoka kwenye gari upesi kukimbilia nyaraka zake. Zilikuwa zinapeperushwa upesi na upepo kuzama msituni!
.
.
Aliikimbiza mojawapo lakini upepo ulizidi kuitokomeza. Mwishowe alisimama akadaka magoti yake akihema kwanguvu. Hakuamini macho yake, nyaraka zilikuwa zimepotea mbele ya macho yake!
.
.
Basi akiwa hapo, sura imemvurugika kwa kuchoka na mawazo, akaona mojawapo ya nyaraka yake ikiwa pembezoni mwa mti mkubwa umbali wa kama hatua kumi toka alipo kwa upande wa mkono wake wa kushoto.
.
.
Akasimama na kutazama vema. Ni kweli alichokuwa anakiona. Nyaraka ilikuwa imetuama hapo. Basi akakata shauri kuifuata. Alipopiga hatua tatu, akastaajabu kuona mkono ukitokea nyuma ya mti, ukaivuta ile nyaraka upesi!
.
.
Akakimbia kutazama, hakukuta kitu! Akabaki akiduwaa. Mara akasikia sauti ya makaratasi nyuma yake yakifunguliwa na upepo! Akageuka kutazama. Uso kwa uso akakutana na kiumbe ambacho hakuwahi kukiona wala kuja kukikumbuka. Asijue kinachoendelea, akadondoka chini na kupoteza fahamu!
.
.
.
.
“Briaaaaan!” mama aliita akiangaza huku na kule. Kandokando yake alikuwa pia Olivia naye akirusha macho kumtafuta Brian ndani ya msitu huu mkubwa.
.
.
“Briaaan!” mama aliendelea kuita. Macho yake yalishaanza kuwa mekundu akitaka kulia. Alipotembea kwa muda kidogo, akaona alama za miburuzo kwenye majani! Akajikuta analalama akiziba mdomo, “Mungu wangu, Brian!”
.
.
Alitazama kufuatilia alama hiyo ya miburuzo, kwa mbali akamwona mtu fulani akiishilia akiwa anavuta mwili wa Brian!
“Ni Brian!” mama akaropoka kwa kuduwaa. Haraka akaanza kukimbia kumfuata Brian. Nyuma yake Olivia alikuwa anamfuata kwa kasi. Ajabu alipokimbia kwa muda fulani, akampoteza yule mtu anayemburuta Brian! Hakuwa anaonekana tena.
Akaangaza kushoto na kulia, kulia na kushoto, hakuona kitu! “Briaaan!” akaita. “Briaaaan!” machozi yakamshuka haswa akiwa anapoteza matumaini ya kumpata mwanae. Ila ghafla akiwa anaangaza, mara akauona mwili wa Brian kwa mbali ukiwa umelala.
Akausogelea upesi. Akiwa amebakiza hatua chache, akasimama na kuangaza. Alihisi hayupo mwenyewe. Alihisi kuna mtu anamtazama mahali. Akageuka na kumwita Olivia. Akamdaka mkono binti huyo na kisha akasonga naye mbele taratibu na kwa tahadhari.
“Brian!” mama akaita akimtazama Brian ambaye bado hakuwa na fahamu. Alipomkaribia, akamtikisatikisa akimwita. Punde Brian akaamka. Akatazama kando na kando, akauliza, “Nipo wapi?”
“Amka twende!” mama akamwambia akimnyanyua. Wakaanza kutembea kurudi kwenye gari lao. Wakatembea kwa kama dakika kumi na tano kwakuwa walitembea pole.
Walipofika barabarani, kuangaza, gari halikuwepo! “Mungu wangu! Mungu wangu!” mama akalalama. Akakimbia kwenda huku na huko, gari halikuonekana. Hakufahamu ni kwamba limepotea ama limeibwa!
“Sasa tutafanyaje pasipo gari?” mama akauliza akishika kichwa chake kwa mawazo. Hakukuwa na mwenye majibu. Kila mtu alikuwa ameduwaa wasijue cha kufanya.
Baada ya muda wakakata shauri kutembea kwa miguu. Endapo litatokea gari lolote, wataomba msaada. Basi wakatembea kwa muda wa karibia lisaa limoja pasipo kuona gari lolote. Walichoka ila hawakuwa na budi kuendelea na matembezi. Wasingependa usiku kuwakuta humo katikati ya miti.
Wakatembea kwa robo saa zaidi ndipo wakasikia honi ya gari nyuma yao. Wakashtuka na kuangaza kwa furaha. Waliamini msaada sasa umewadia. Kweli kutazama lilikuwa ni gari, wakalipungia mkono kuliomba msaada. Gari likasimama na upesi wakaliendea.
Vioo viliposhushwa, wakawaona Padri Alfonso na Dada Magdalena! Mioyo yao ikawashtuka.
“Habari zenu?” Padri Alfonso akasalimu kwa tabasamu.
“Njema,” akajibu Mama Brian.
“Vipi, mbona msituni muda huu?”
“Aaaahm ni simulizi ndefu kidogo … vipi? Nyie mwaenda wapi?”
“Tunaenda kwenye huduma ya pamoja ya Massachusetts! Bila shaka mnahitaji msaada.”
Kabla Mama Brian hajaitikia, akamtazama Brian na Olivia. Wote wakamtikisia kichwa kutoafiki. Mama akarejesha uso wake kwa Padri kisha akatabasamu. “Nashukuru. Nyie mnaweza kutangulia tu.”
“Kweli?” Dada Magdalena akauliza.
“Yah! Tangulieni tu hamna shida.”
Padri Alfonso akamtazama Mama Brian kwa sekunde kadhaa kisha akaatia moto chombo na kuondoka. Mama Brian na wanawe wakabaki kutazama gari hilo likiishilia. Japo walihitaji msaada, waliamua tu liende.
Wakaendelea kutembea kwa miguu. Ikapita dakika kumi, wakaona gari jingine. Wakalipungia mkono kulisimamisha.
“Samahani tunaomba mtusogeze!”
Lilikuwa ni gari lenye nafasi kubwa kwa nyuma, wakajipaki na safari ikaendelea. Wakatembea kwa muda wa kama dakika kumi na mbili wakipulizwa na upepo huko nyuma.
Ila ghafla, Brian akamshtua mama yake. “Mama, tazama!” alikuwa amenyooshea kidole chake mbele. Kutazama, Mama akaona gari lao likiwa limejiegesha kando.
Akiwa haamini, akakodoa lakini bado kitu kikiwa ni kilekile. Ni kweli lilikuwa gari linalowahusu. Basi wakawaomba wale waliowasaidia wasimamishe ili washuke.
“Hapa?” akauliza dereva akiwa anashangazwa kidogo na ombi hilo. Gari lilisimama, wakashuka. Wakalifuata gari lao na kulikagua vema. Ndilo lenyewe! Hakukuwa na mtu ndani. Ni tupu.
Mama akafungua mlango wakazama ndani, akaliwasha wakaendelea na safari. Ila nani aliyelileta gari hilo hapo? Na aliwezaje wakati funguo hakuwa nayo? Hayo yalikuwa ni maswali ambayo hayakuwa na majibu.
Wakatembea kwa muda wa lisaa limoja kamili. Walibakiza sehemu ndogo tu kumaliza msitu huu. Wakiwa wanatafuna sehemu hiyo ya mwisho, wakakutana na gari lile lililokuwa limewabebelea Padri Alfonso na Dada Magdalena!
Gari hilo lilikuwa limesimama kando, limeharibika. Padri Alfonso na Dada Magdalena walikuwa nje wakihangaika nalo. Lakini walipoliona gari la wakina Brian, wakaacha shughuli yao na kulipungia mkono kulisimamisha.
“Habari?” Mama Brian akasalimu akitazama gari lile lililogoma kwenda.
“Habari si nzuri, tumeharibikiwa na gari letu,” akasema Padri Alfonso. “Vipi mnaweza kutusogeza tuendako?” Padri akauliza. Mama Brian akawatazama wanawe, wote wakampatia nyuso ngumu kama ishara. “Sidhani kama mtaenea humu. Kuna baadhi ya mizigo.”
Padri akatazama kulikagua gari kisha akauliza, “Hawezi kuingia hata mmoja wetu basi?”
Mama Brian akabanwa. Akawatazama wanae kabla hajajibu kitu. Alikosa namna ya kumkatalia padri basi akasema, “kwa mmoja … aahm … tunaweza kwenda naye!”
Padri akatabasamu. Akamtazama Dada Magdalena na kumwambia aingie ndani ya gari, yeye atangoja lingine lijalo. Basi Dada Magdalena akazama ndani na safari ikang’oa nanga. Wakatembea kwenda kumalizia msitu ule waende zao kwa mtaalamu.
Safari ikaenda na kuenda. Ndani ya gari kulikuwa ni kimya. Hakukuwa na soga yoyote ile. Wakakata lisaa limoja. Wakakata lisaa la pili. Bado wapo ndani ya msitu usio na kikomo.
Lakini mama Brian alitwaliwa na shaka. Makadirio yake ya muda yalikuwa kinyume kabisa na alichokuwa anakiona. Kwa ufahamu wake safari iliyobakia haikuwa ya kuchukua masaa mawili kuimaliza. Alistaajabu! Kila alipokanyaga mafuta, ni miti tu ndiyo ilikuwa mbele na nyuma yake. Miti pasipo kikomo!
Akasimamisha gari.
“Nahisi nimepotea!” akasema.
“Kwani unaelekea wapi?” akauliza Dada Magdalena akitabasamu kwa ukarimu.
“Naenda mbele. Nashangaa msitu haukomi!”
Dada Magdalena akatabasamu. “Pengine ni macho yako tu. Mbona tunasogea?”
“Najua barabara hii! Hii si mara yangu ya kwanza kupita. Haikuwahi kuwa ndefu kiasi hiki!”
“Vipi tukatumia sjia fupi basi?” akauliza Dada Magdalena.
“Njia ipi?”
“Kuna njia ya vumbi naijua. Mngependa tupite?”
“Hapana!” Brian akawahi kujibu. “Tutatumia njia hiihii!”
“Mafuta yanaelekea kuisha,” mama akasema. “Endapo tukiendelea kuzunguka humu, basi muda si mrefu gari litazimika lisiamke tena!”
Kukawa kimya kidogo. Ni kama vile watu walikuwa wanategeana kuongea. Brian akauvunja ukimya. “Dada Magdalena,” Brian akaita akimtazama Dada huyo usoni. “Tumekukosea nini?” akamuuliza.
Dada Magdalena akakunja uso kwa mshangao.
“Usin’tazame hivyo. Unajua ninachokiongea. Tunajua kuwa wewe si mwenzetu. Wewe ni jini. Jini miongoni mwetu binadamu! … mnaweza mkatupa kipindi cha amani kidogo tafadhali?”
Dada Magdalena akamtazama Mama Brian. “Anasema nini huyu?” akauliza.
“Anasema wewe ni jini!” Olivia akadakia. Uso wake ulikuwa umefumwa kwa hasira zaidi kuliko woga. “Wewe na Padri Alfonso ni majini. Tumewakosea nini? Tuacheni!” Olivia akamalizia kwa sauti ya chini iliyokaribu na kulia.
Dada Magdalena akaziba mdomo wake kwa mshangao. Akafanya ishara ya msalaba na kukutanisha viganja vyake kana kwamba anataka kusali. Macho yake yalikuwa yanaelekea kuwa mekundu kwa kutaka kulia.
“Sijui nini mnaongelea. Kwanini mnanisemea hivyo? Kuna lolote baya nimewatendea?”
“Dada Magdalena,” Mama Brian akashika hatamu ya kunena. Aligeuza shingo yake vema kumtazama anayemwongelesha. “Tafadhali. Sipendi kwenda mbali kwa maneno ambayo aidha nami naweza kuja kuyajutia hapo mbeleni … naomba ushuke twendelee na safari yetu.”
“Lakini mtaniachaje msituni?” akauliza Dada Magdalea kwa uso wa huruma.
“Nimekuomba,” Mama Brian akamsisitizia. “Nimekuomba ushuke toka kwenye gari yangu!”
Dada Magdalena akamtazama Mama Brian kwa sekunde kadhaa pasipo kusema jambo. Mara akaanza kubadilika. Mwili wake ukawa mweupe ukichomozwa na michirizi meusi kana kwamba mizizi ya miti. Macho yake yakabadilika na kuwa ya paka. Mdomo wake ukawa mweusi, kucha kama chui, meno kama simba!
Ghafla akamnyaka Brian aliyekuwa amekaa naye nyuma, akamnyonga kwanguvu akipanua kinywa chake kipana! Brian akahangaika kujitetea. Upesi Mama akamkita Dada Magdalena kichwani kwa kutumia ‘fire extinguisher’, Dada Magdalena akapata maruweruwe.
Hajakaa vema, Brian akamkita teke zito. Mama alishafungua mlango. Dada Magdalena akajikuta chini, gari likatimka kwa kasi!
Wakati Dada Magdalena anajikusanya chini, mara miguu ya mwanaume ikamjongea na kukoma mbele yake. Alikuwa ni Padri Alfonso. Alitazama mbele gari la wakina Brian likitokomea.
.
Basi baada ya safari hii kudumu kwa muda fulani, Mama Brian akaweka gari kando mahali wapate kula na hata kutia mafuta garini. Walichukua kama dakika kumi na tano hapo. Wakajipakia tena kwenye gari na kuendelea na safari yao.
.
.
Wakadumu tena barabarani kwa muda wa kama lisaa, ndipo wakafika eneo walilokuwa wanaliendea, mji wa Northampton. Hapo wakatembea kwa dakika chache tu kabla hawajafika mbele ya nyumba fulani iliyo pweke. Mama Brian akazima gari na kusema. “Tumefika!”
.
.
“Ndiyo hapa?” Brian akauliza akiwa anaangaza macho yake. Punde wakamwona mwanaume aliyevalia suti nyeusi na kofia yake. Mdomoni alikuwa ameshikilia kiko chake kwa meno akijaribu kufunga mlango wake. Kuna mahali alikuwa anataka kwenda, hata mkononi mwake alikuwa amebebelea mkebe.
.
.
Mama Brian akashuka upesi na kuita, “Wisconsin!” mwanaume
yule akaacha shughuli yake na kumtazama. Ilikuwa ajabu kuwa hakumwona ilhali gari hilo lilikuwa limejiegesha karibu na makazi yake. Ila baada ya Mama Brian kujongea ndipo tukajifunza kuwa jicho lake moja la upande wa kushoto lilikuwa bovu. Yeye hutumia jicho moja tu, ambalo ameliveka miwani ya kioo kimoja.
.
.
“Hello mama!” Wisconsin akasalimu akivua kofia yake, kisha akaendelea na zoezi lake la kufunga mlango. “Samahani!” Mama Brian akasema akijitahidi kusonga karibu. Akadaka ngazi kupanda kwa upesi.
.
.
“Sisi ni wageni wako. Naomba utuskize!”
.
.
Wisconsin alipomaliza kufunga mlango wake. Akatazama jua na kisha akamtazama Mama Brian. “Samahani. Sina ratiba ya kufanya lolote leo hii, muda huu!”
.
.
“Hunikumbuki?” Mama Brian akauliza akiwa ametoa macho. Wisconsin, mwanaume mtanashati mwenye makamo ya umri wa miaka arubaini, akamtazama na kisha akabinua mdomo. “Hapana.”
.
.
“Oooh! Ndio. Tulipokuja mara ya kwanza hatukukuta … samahani, nina shida sana.”
.
.
Wisconsin akatabasamu. Akaweka mkebe wake kwenye kwapa alafu akasema kistaarabu. “Mama, mimi hufanya kazi kwa ratiba. Nina ratiba nyingine hivi sasa. Samahani sitaweza kukuhudumia.”
.
.
“Tumetoka mbali sana kuja kukuona.”
.
.
“Italia?”
.
.
“Boston!”
.
.
“Si mbali. Kama hutojali, naweza kwenda?”
.
.
“Tafadhali. Na –”
.
.
“Nazidi kukawia. Naomba niende.”
.
.
“Niambie basi muda wako. Lini unafanya kazi?”
.
.
“Keshokutwa kuanzia jua linapokuwa katikati mpaka kuzama.” Wisconsin aliposema hayo, akaenda zake. Mama Brian akabaki amesimama, anamtazama mwanaume huyo akiishilia.
.
.
“Amesemaje?” Brian akamuuliza. Yeye na Olivia walitoka ndani ya gari baada ya kumwona Wisconsin akiishilia. Mama alidaka kiuno chake akatikisa kichwa.
.
.
“Itabidi tulale huku hivi leo.”
.
.
Wakarejea kwenye gari na kutafuta ‘motel’ safi walipopata vyumba vizuri vya kulalia lakini pia huduma zinginezo zikiwa si haba. Huduma kama vile chakula na vinywaji. Moteli hii ilikuwa wazi masaa ishirini na nne kutokana na kwamba watu husafiri muda wote.
.
.
Basi baada ya kuona vyumba vyao, wakaendea mgahawa na kutulia hapo watete mawili matatu. Mezani kulikuwa na vinywaji laini, hususani sharubati.
.
.
Lakini wakiwa hapo wanateta juu ya mji ule wa Northampton, macho yao yakadakwa na taarifa runingani. Ilikuwa ni taarifa ya habari kutokea Boston.
.
.
“ … watoto nane wanaripotiwa kupotea leo katika mji wa Boston ukiwa mwendelezo wa matukio ya watoto kupotea kwa wingi kwa siku za karibuni. Sasa ndani ya siku tatu, takribani watoto kumi na tano wamekwishapotea huku karibia wote wakiripotiwa kuyoyomea ama kuonekana mara ya mwisho msituni!
.
.
Kamanda wa polisi wa mji wa Boston anathibitisha taarifa hiyo na kueleza kuwa wanaendelea kulifanyia kazi kiupelelezi zaidi. Hofu inazidi kuwatanda wazazi na vilio vinatawala majumbani.
.
.
John Bleach, KK tv!”
.
.
Mama Brian akatikisa kichwa, akasema kwa kuchoka, “wameendelea kupotea na leo.”
.
.
“Inabidi tufanye jambo haraka,” Brian akanguruma. Uso wake ulionyesha kuguswa na habari. Kwa muda kila mtu hakugusa bilauri yake ya sharubati. “La sivyo, watoto wote watatokomea. Mji mzima!”
.
.
Mama Brian akarusha macho yake nje ya vioo vya dirisha. Alikuwa anatafakuri. Japo macho yake yalikuwa yanatazama magari yakatizayo, akili yake ilikuwa inahaha ikimnyima amani.
.
.
Akasema, “Tunamhitaji sana Wisconsin.” sauti yake ilikuwa nzito kwasababu ya kubana koo lake kwa viganja vyake vyembamba ili ajipatie joto. Mhudumu akamtazama.
.
.
Alikuwa ni mwanamke mnene ndani ya sare. Mashavu yake makubwa yalikuwa mekundu yenye vidotidoti vingi rangi ya zambarau. Kidevu chake kilikuwa kimemezwa na shingo. Mdomo mdogo kana kwamba ndege.
.
.
“Umekuja kwa ajili ya Wisconsin?” mhudumu huyo akauliza. Mama Brian na wanawe wakamtazama.
.
.
“Mmekuja kwa ajili ya Wisconsin?” Mhudumu akarejea kuuliza. Mkononi alikuwa amebebelea kikombe cha udongo akikifuta kukikausha na maji.
.
.
“Ndio. Tumekuja kwa ajili yake,” Mama Brian akasema kwa kujiamini. Mhudumu yule akawatazama alafu akaendelea na kazi zake. Aliondoka pale ‘kaunta’ akaelekea ndani, jikoni. Akawaachia wageni maswali.
.
.
“Atakuwa na nini?” mama akauliza kiretorikali.
.
.
“Pengine anachakutuambia,” Brian akabashiri akiwa anatazama kule kaunta kama atamwona yule mhudumu. Kwa muda hakutokea. Alipotokea alikuwa ameshabadili sare zake, sasa amevalia nguo kama raia wa kawaida. Gauni jeusi pana.
.
.
“Tunaweza kuongea na wewe?” Mama Brian akamwomba. Mhudumu huyo akasimama akiwa anawatazama kwa mashaka. Akatikisa kichwa chake, mashavu yakacheza, kisha akaendelea zake na safari kuufuata mlango wa kutokea.
.
.
Mama Brian akanyanyuka kumfuata. Wakina Brian wakabaki wakimtazama mama yao akizungumza na yule mhudumu. Punde akarejea naye mezani.
.
.
“Hawa ni wanangu, huyu anaitwa Brian na huyu Olivia,” Mama akatambulisha kwa tabasamu. Mhudumu akaketi na kusema, “Mimi naitwa Keline.” alikuwa anaonyesha woga usoni mwake.
.
.
“Keline, kuna kitu chochote unataka kutuambia?” Mama akauliza akimtazama Keline kwa uso wa kudadisi. “… kumhusu Wisconsin. Chochote kile unachoweza kutuambia?”
.
.
Keline akatazama kwanza nje. Akarudisha macho yake madogo mezani na kisha akatazama chini. “Si mtu mwema,” akasema kwa sauti yake ndogo.
.
.
“Kwanini unasema hivyo?” Brian akauliza. “Kuna tabu yoyote?”
.
.
“Ndio … Wisconsin aliua wazazi wangu. Amenisababishia jeraha kubwa. Sitaweza kumsamehe kamwe!” macho yake yakaanza kujawa na machozi. Akavuta makamasi mepesi na kuendelea kunena, “Anasema kuwa anawasaidia watu dhidi ya nguvu za giza. Lakini yeye mwenyewe ni nguvu hizo, tena zaidi kwa maana amejiveka koti la kondoo.
.
.
Analaghai watu, na kila anayedai kumsaidia, hufa baada ya majuma matatu!”
.
.
Keline aliposema hayo akanyanyua uso wake na kumtazama Mama Brian. “Baba yangu alikufa majuma matatu baada ya kuonana naye. Naye mama ‘angu alipokwenda kumwomba msaada, naye akafa baada ya majuma matatu. Nisingependa mkapitia kwenye adha hiyo.”
.
.
Sasa Keline alikuwa anatiririsha machozi zaidi. Alitoa leso yake na kujipangusa. Akasimama na kuaga. Mama Brian na wanawe wakabaki wakimtazama mwanamke huyo akiishilia, anajifuta machozi na amebanwa na kwikwi za kilio.
.
.
Alipopotelea, Mama Brian akauliza, “Sasa tunafanyaje?” alionyesha kuchanganyikiwa.
.
.
“Tunaenda kumwona Wisconsin kesho kama tulivyokubaliana naye,” akasema Brian.
.
.
“Lakini umesikia habari zake?” Mama akauliza. Brian akatazama kwanza nyuma yake na kule mlangoni kisha akamwambia mama yake kuwa ana mashaka na Keline.
.
.
“Kwanini?” mama akauliza.
.
.
Brian akamtonya kuwa wakati Keline anaongea alifanikiwa kumtazama mkono wake wa kulia, akamwona akiwa na pete ambayo alimwona nayo Padri Alfonso wakati alipokuja kufanya sala nyumbani kwao. Hilo likamshangaza mama yake.
.
.
“Una uhakika?”
.
.
“Ndio, nina uhakika. Nimeona kwa macho yangu mwenyewe!”
.
.
Swala hilo likazua hofu miongoni mwao. Na pengine kwa kiasi fulani halikumkonga sana Mama kwenye kuliamini. Pete zi nyingi. Vipi kama ya Kelie haikuwa na mahusiano na Padri Alfonso? Aliwaza akiwa kitandani kwenye chumba cha peke yake.
.
.Ila kule dirishani, kivuli cha mtu kikakatiza. Mtu mwenye mwili mpana.
.
Mama Brian hakuwa na hili wala lile. Alikuwa anaendelea kuwaza mambo yake hayo kichwani. Lakini mtu yule aliyekuwa anakatiza dirishani, akasimama na akageuza uso wake kutazama dirishani.
.
.
Akajongea karibu na karibu. Sasa akawa karibu kabisa na dirisha kiasi kwamba mtu aliyekuwepo ndani akahisi kufifia kwa mwanga! Mama Brian akageuza shingo yake kutazama. Hakuna kitu! Akapata shaka kidogo ila mwishowe akapuuzia na kulaza kichwa chake kitandani.
.
.
Basi taratibu usingizi ukaanza kumnyemelea. Macho yakawa yanafumba pasipo ruhusa. Akaona si stara kulala pasipo kuoga. Akanyanyuka afanye jitihada za kuoga upesi kisha arejee kitandani. Punde akawa bafuni akikoga akiimba na kuburudika na maji ya moto yaliyompa faraja dhidi ya hali ya baridi.
.
.
Akiwa anaoga huko, akahisi kuna mtu ndani. Akajawa na shaka. Alitulia askize vema, akahisi kishindo cha mtu kikikatiza chumbani. Na mara akahisi mtu huyo akinong’ona huko. Basi haraka akatoka bafuni na kwenda kutazama. Hakuona mtu.
.
.
Alitazama huku na huko pasipo mafanikio. Mwishowe akarejea bafuni aendelee kuoga. Akamaliza salama na kutoka akijifuta maji. Akiwa anaendea kitanda chake, akagundua kuwa kuna nyayo za miguu kwenye sakafu.
.
.
Nyayo hizo zilikuwa zimetwaliwa na mabaki ya maji. Na alipozifuatilia, akagundua zimetokea kwa nje! Haraka akatazama mlango kama umefungwa. Akaukuta ukiwa salama, umetiwa ‘lock’. Sasa mbona nyayo za mtu ndani?
.
.
Akarejea kuketi kitandani akiwa amejawa na hofu. Akawa amepata mawazo maradufu. Akiwa bado yupo hapo, kama baada tu ya dakika tatu, taa zikaanza kufinyafinya. Mara umeme nao ukakatika! Akaduwaa.
.
.
Sauti yake ya kuhema ikawa inasikika vema sasa. Kulikuwa ni kimya, kimya ya tuli. Hata mende angepita ukutani, basi ungemsikia.
.
.
Mama Brian akatulia tuli kana kwamba maji mtungini. Alitumai umeme utarejea muda si mrefu. Na kama usiporejea basi atakuwa kwenye hali mbaya maana alikuwa anahofia juu ya yule mtu aliyeacha chapa za nyayo chumbani.
.
.
Kila alipomuwaza mtu huyo akahisi baridi kali. Moyo wamwenda mbio. Kichwa nacho chamgonga ‘alarm’ titi! titi! titi!
.
.
Ikapita kama dakika moja. Bado kulikuwa kimya. Ila mara Mama Brian akaanza kuhisi kuna mtu chumbani, hayuko mwenyewe! Alihisi kabisa uwepo wa mtu mule ndani. Vinyweleo vilimsimama na baridi likamzidi mwilini.
.
.
Kama haitoshi, punde akaanza kusikia mtu akikanyaga sakafu taratibu. Alipiga hatua zake kila baada ya sekunde mbili kisha kukoma. Sekunde mbili kisha kukoma. Mama Brian akapata wazo la kuliendea dirisha afungue mwanga uingie ndani.
.
.
Haraka akasonga. Kwakuwa dirisha alikuwa anajua lilipo, hakuhitaji mwanga kulitambua. Akanyoosha mkono wake na kupapasa. Akapapasa na kupapasa. Akapapasa chini … akapapasa juu … hakuhisi dirisha!
.
.
Akaona atumie mikono miwili kupapasia, hakuwa anaaamini anachohisi kwani ilikuwa kinyume na matarajio yake, lakini napo akapapasa pasipo kushika kitu isipokuwa ukuta pekee!
.
.
Sasa akawa anahema kwanguvu sana. Pumzi ya hofu. Alipata mashaka juu ya uhai wake akajikuta anatamani kupiga kelele kali sana za kuomba msaada.
.
.
Akajikunyata. Kichwa chake kiligoma kabisa kuwaza cha kufanya. Yaani hakuwa anajua kabisa afanye nini kwa muda huo. Ulikuwa ni wakati mgumu sana kwake.
.
.
Basi akiwa ametulia, amejikunyata akitazamia nini kitatokea, akaanza kuhisi mtu anapanda kitandani. Godoro lilibonyea na kitanda kikatoa mlio. Hapa ndiyo Mama Brian akaona ni muda stahiki wa kupiga kelele. Hakuwa amepanga hata hivyo, alijikuta akipanua kinywa apige yowe kali.
.
.
Kwanguvu zote akafanya hivyo, ila ajabu sauti haikutoka hata punje! Kilichosikika ni ile sauti ya pumzi tu mtu apumuapo. Mama Brian akajaribu tena na tena kupiga kelele. Kazi bure. Sauti haikuwa inatoka. Ilikuwa imekaua kabisa kooni!
.
.
Hapa akakutana uso kwa uso na kifo kwenye kona. Hakuwa na pakukimbilia wala cha kujitetea nacho. Punde kidogo akavamiwa na mtu asiyemjua, akaanza kumkaba akimminyia kwenye godoro!
.
.
Akapapatika kudai roho yake. Akagahangaika haswa akipambana kwa nguvu zake zote, hakufua dafu! Akiwa anatetea uhai wake, akajikuta akipiga teke chupa iliyokuwa imesimama kwenye droo ya kitanda. Ilikuwa ni chupa ya kioo yenye sharubati ndani yake kwa nusu ujazo. Ikadondoka na kusababisha kelele kali!
.
.
Kwakuwa mazingira yalikuwa tulivu, sauti hiyo ya chupa ilisikika moteli nzima.
.
.
“Ni muda wako wa kufa!” mnyongaji akasema kwa kunong’ona. Mikono yake ya baridi ilikuwa imeminya shingo ya Mama Brian kwanguvu kiasi cha kumfanya mwanamke huyo atoe macho na ulimi nje. “Huwezi kushindana … sawa? … huwezi kushindana …” akaendelea kunong’ona akiwa na uhakika na kazi yake.
.
.
Ila ghafla, mlango ukagongwa. Muda tu kidogo ukavunjwa kwanguvu, Brian akaingia na kuangaza mule kizani ambapo sasa mwanga angalau ulipenya kutokana na mlango kuwa wazi.
.
.
“Mama!” Brian akaita akiwa na uso uliopaliwa na woga. Akamsikia mama yake akikohoa kitandani, akamsongea upesi na kumtazama amjulie hali. Umeme ukarejea. Mama alikuwa amedaka shingo yake akikohoa na kuhangaika kupata hewa.
.
.
“Nini kimetokea?” Brian akauliza. Kabla hajajibiwa akaongezea lingine, “Uko sawa?”
.
.
Maswali yote hayo mama hakuweza kumjibu kutokana na hali aliyomo. Alikuwa ametoka kukabwa ikibaki sekunde kadhaa tu akate pumzi. Shingo yake haikuwa sawa, haswa koo. Na pia hata kichwa kilikuwa kinamgonga sana kutoka na kubanwa kwa mishipa ya fahamu kwanguvu, kwa muda mrefu.
.
.
Basi mama akachukua kama dakika sita kukaa angalau sawa. Kabla hajanena kitu, akakagua chumba kwa macho yake yalikuwa yamegeuka kuwa mekundu, akatazama kila kona, kila eneo. Punde wakafika walinzi wa motel, mmoja alikuwa amebebelea bunduki aina ya gobore mwenzake akiwa amebebelea fimbo iliyosanifiwa vema kiulinzi.
.
.
“Kuna shida yoyote?” mmoja akauliza wakiwa wanatazama kwa macho juujuu. Brian akafoka, “nyie mnaona vitu vipo sawa? Walinzi wa aina gani ninyi mteja anakumbwa na kadhia kwa muda wote huo pasipo msaada?” sauti ya Brian ilikuwa kubwa na ilisikika moteli nzima.
.
.
Walinzi wakaomba radhi. Hawakukaa sana hapo wakaenda zao. Mama Brian akatoka kwenye chumba chake na kwenda kulala pamoja na watoto chumba kimoja.
.
.
“Nina uhakika kabisa atakuwa ni yule mhudumu,” alisema Brian. “Padri Alfonso bado anatufuatilia hata sasa.”
.
.
Mama alikuwa ameketi ametulia. Hakuwa na nguvu ya kuzozana wala kuteta. Hata hamu hakuwa nayo. Alikuwa amezubaa kana kwamba kuku mgonjwa. Kwake ilikuwa ni miujiza muda huo kuwa hai.
Sehemu Ya 7
Asubuhi ya saa moja na nusu …
.
.
“Naomba kahawa pekee,” alisema Mama Brian kwa sauti ya chini akimwambia mhudumu baada ya watoto kuagiza vifungua kinywa. Muda si mrefu mhudumu akarejea akiwa amebebelea hitaji la kila mmoja wao, akawapatia.
.
.
Mhudumu huyu alikuwa ni mwanamke mrefu mwenye nywele nyekundu. Uso wa kiukarimu na mkakamavu. Hakuwa mnyimi wa tabasamu.
.
.
“Samahani, dada,” Mama Brian akanena akimtazama mhudumu. “Keline yupo?”
.
.
Mhudumu akakunja sura. “Keline?”
.
.
“Ndio, Keline. Ni mhudumu wa hapa. Alituhudumia jana,” Mama akadadavua.
.
.
“Anaitwa Keline?”
.
.
“Ndio, Keline! Ni mnene mfupi.”
.
.
Mhudumu akabetua mdomo. “Simfahamu.” akatikisa kichwa chake. “Hamna mtu anayeitwa Keline hapa.” Mama Brian akamtazama mwanaye pasipo kutia neno.
.
.
“Vipi, kuna tatizo lolote?” Mhudumu akauliza.
.
.
“Hapana, nashukuru,” Mama akajibu akiigiza tabasamu.
.
.
“Una uhakika?”
.
.
“Ndio. Hamna shida, ahsante.”
.
.
Mhudumu akaenda zake.
.
.
“Ulikuwa sahihi,” Mama akasema akimtazama Brian kisha akanyanyua kikombe chake cha kahawa na kujipasha mwili. Walipomaliza, wakiwa wamechukua kama robo saa tu hapo mgahawani, wakaendea gari lao na kufunga safari ya kwenda kuonana na Wisconsin.
.
.
Mwanaume aliyewafanya wafunge safari iliyojawa na mashaka na mateso.
Walipowasili, baada tu ya kuegesha usafiri wao, wakaendea mlango na kugonga hapo mara tatu. Punde mlango ukafunguliwa na mwanamke mwembamba mzee. Akawasalimu kwa tabasamu na kuwauliza shida yao.
“Tunahitaji kuonana na Wisconsin,” Mama Brian akaeleza. Mlango ukafunguliwa kwa upana, wakakaribishwa kuingia ndani. Wakaketi sebuleni, na yule mwanamke mzee akaelekea ndani. Muda si mrefu, akaja Wisconsin na kuketi miongoni mwao.
“Naona mmetunza muda.”
“Ndio. Pengine utakuwa umeelewa kuwa tuna shida,” Mama Brian akasema akimtazama Wisconsin usoni.
“Naam, niambieni basi shida yenu, nami nitawasaidia kwa kadiri ya uwezo wangu.”
Mama akamtazama Brian na kumpa ishara ya kichwa, basi kijana huyo akaanza kueleza yale yote anayoyajua. Tangu Kecie alivyopotea, anavyojiri mpaka watu kupotea katika mji wa Boston. Wisconsin alipoyasikia hayo akashangazwa hata naye. Alikuwa anamfahamu vizuri Helo, simulizi zake alishawahi kuzisikia hapo kitambo.
Basi akasema, “Ningojeni kwa dakika kadhaa.” yeye akaelekea kwenye chumba kimoja kilichokuwa katikati ya vyumba vinne. Akadumu huko kwa muda wa dakika kumi kisha akarejea sebuleni.
“Nifuateni!”
Akaongozana na wakina Brian mpaka kwenye kile chumba, wakazama humo. Kilikuwa ni chumba kipana kilichopakawa rangi nyekundu ukutani. Katikati yake kulikuwa na viti vitano vikiwa vimeizunguka meza moja ndogo.
Hapo wakaketi na kukiacha kiti kimoja kikiwa wazi. Yule mwanamke mzee akaja akiwa amebebelea taa. Ulikuwa ni mshumaa ndani ya chupa kubwa kiasi mithili ya ile ya taa ya chemli. Akaiweka juu ya meza kisha akaendea mfuko fulani mweusi aliokuja nao na kuuweka karibu na Wisconsin alafu akazima taa.
Sasa chumba kizima kikawa kinaangaziwa na mwanga wa mshumaa. Wisconsin akatia mkono wake kwenye ule mfuko alioletewa, humo akatoa mashine fulani mbili, akaziweka mezani. Akapekua tena mfuko wake na kutoa chombo fulani cha chuma, kilikuwa mithili ya sahani ila kikiwa na mguu wake.
Baada ya hapo akachoma maani fulani aliyoyatia kwenye kile chombo. Harufu ya kunukia, moshi mweupe, ukatawala ndani ya chumba. Akachukua mashine moja na kui ‘set’ kwa mkono alafu akaiweka mezani. Ikawa inatoa sauti kubwa kiasi mithili ya mshale wa dakika.
Sasa alipoona kila kitu kipo sawa, akamtazama Brian na kumwambia.
“Kama Kecie huwa anakufuata kukuomba umsaidie, basi utakutana naye. Muulize kila unachotaka kukijua …” Lakini pia akamtahadharisha, “Kuwa makini sawa?”
Basi baada ya hapo akamtaka Brian afunge macho yake kisha azingatie sauti ile inayotoka kwenye mashine. Wote wakashikana mikono na kuwa kimya. Sauti tu ya mshine … tap!-tap!-tap!-tap! … ikiwa inasikika chumba kizima.
Basi Brian akiwa amefunga macho yake kwanguvu, baada ya dakika kadhaa, masikio yake yakaanza kupoteza uwezo wake wa kusikia ule mlio wa mashine. Punde kidogo akawa hausikii tena! Kulikuwa ni kimya kabisa masikioni mwake kiasi kwamba akaanza kustaajabu kama amekuwa kiziwi.
Ila muda si mrefu sana, kwa mbaali akaanza sikia wimbo ambao hakuwa anaujua. Alichosikia ilikuwa ni sauti nyembamba ya mwanamke iliyokuwa inatetemesha na kuimba kwa maringo.
Zaidi ya hapo, mwili wake ukaanza kuhisi baridi kali. Alijikuta anajikunyata na kung’ata meno Alihisi upepo unamtafuna kwa namna ulivyokuwa wa baridi haswa. Akastaajabu ni wapi alipo? Chumbani na baridi lote hilo? Akafungua macho yake kuangaza. Ajabu akajikuta kwenye ulimwengu wa tofauti!
Alikuwa yu mwenyewe nje. Ni giza na kuna upepo mkali. Mbele yake kuna nyumba kubwa sana ambayo ipo kwenye mwanga hafifu. Nyumba hiyo ni ya zamani. Alipotazama vema aligundua nyumba hiyo ni ile ya bwana Helo!
Basi akatazama kushoto na kulia kwake. Hakukuwa na msitu bali giza tu, hata kuona njia ilikuwa ni tabu. Lakini ndani ya nyumba ile iliyopo mbele yake, kulikuwa na mwanga hafifu waonekana madirishani. Mwanga mithili ya ule wa vibatari.
Akiwa anaduwaa,
“Brian!” Sauti ikamwita. Kutazama akamwona Kecie akiwa amesimama kandokando yake. Alikuwa ndani ya gaunile na mdoli wake mkononi. Brian akamjongea, “Kecie!”
Kecie akamwonyeshea ile nyumba na kusema, “Nenda kule. Nenda kanikomboe!”
Lakini kabla Brian hajaenda, akamuuliza, “Naendaje huko? N’tawezaje kumkabili mtu wa ajabu vile?”
Kecie akamjongea na kumshika mkono. “Brian, kammalize. Kammalize niende zangu salama!”
“Uende wapi?”
“Brian, roho yangu ilishakwisha kufa. Nashindwa kupumzika kwa amani kwasababu ya Helo. Yeye hunirudisha tena duniani kumfanyia kazi yake. Nimekwisha kumaliza yangu.”
“Kazi yako ilikuwa ipi?”
“Kuwamaliza wale watesi wangu.”
“Unamaanisha wazazi wako?”
“Ndio, hao waliofanya nikaja huku … Brian, nilipatwa na hasira sana kuona nimesalitiwa na wazazi wangu. Nilishindwa kabisa kuwasamehe. Na pale Helo aliponiuliza ni nini ada yangu nikatende kazi yake, nikamwambia ni kuwamaliza watesi wangu.
Akanikubalia. Akawa ananirejesha duniani nikaitende kazi hiyo. Sasa nimemaliza, ni zamu yangu kufanya kazi yake. Kuitesa Boston. Kuchukua watoto wote walipo ndani ya mji huo kisha Massachusetts nzima.”
Kecie akaweka kwanza kituo, akatazama jengo la Helo kisha akaendelea kumsemesha Brian.
“Inabidi Helo atoke kwenye ulimwengu huu, la sivyo Boston haitakuwa salama. Huu ni ulimwengu wa watu ambao roho zao bado hazijaenda, watu waliotendewa maovu, watu wenye visasi na vinyongo na wale walio hai uko duniani.
Kadiri mtu awavyo hapa, anakuwa karibu na dunia. Anaweza kuitembelea na kuwaadhibu watesi wake. Inabidi Helo atoke hapa, akitoka hapa roho yangu na za wengine alizozifungia nazo zitaenda.”
“Lakini kwanini ameweza kuwakamata na kuwatawala ingali wote miliuawa kama yeye?” Brian akadadisi. Kecie hakuwa na jibu. Zaidi alisisitizia tu ya kwamba Helo ana nguvu kupita kiasi. Ni kama vile amekuwa mtawala kwenye anga yao.
“Inabidi afe tena kwenye huu ulimwengu. Unaweza kumuua Brian.”
“Mimi? Nitawezaje Kecie? Sina nguvu kama yeye! Yeye si binadamu kama mimi? Nawezaje?”
“Brian, mtu pekee anayeweza kumwangamiza Helo ni wa kutoka duniani. Hakuna yeyote aliyeko huku akamshinda yeye … tafadhali, jaribu. Najua unaweza. Najua utanikomboa rafiki yako …”
Lakini Brian alikuwa na woga kifuani mwake. Alikuwa anaogopa kukumbana na marehemu uso kwa uso. Alistaajabu kwanini msalaba huu umemwangukia yeye.
“Kwanini mimi?” akamuuliza Kecie.
“Wewe ni rafiki yangu. Au sivyo hivyo Brian?” Kecie akauliza akimtazama machoni.
“Lakini,”Brian akaeendelea kueleza shaka yake. “Ni lazima Helo afe au ni muhimu tu kwako kujiendea?”
“Vyote ni muhimu,” akajibu Kecie. “Amezifungia nafsi zetu kwenye ghala lake kama watumwa, funguo anazo yeye mwenyewe muda wote zikiwa karibu … Brian, hata kama ukizipata funguo hizo nikawa huru, bado Helo atarejea kuisumbua Boston kwa kutumia watu wengine. Bado halitakuwa komo lake.”
Basi Brian akawa hana lingine la kuuliza, akaanza kupiga hatua zake kuendea mlango wa jengo. Kabla hajaufungua, akachungulia ndani. Hakukuwa na mtu. Kiti kilikuwa peke yake, runinga inawaka.
“Tumia mlango wa nyuma,” Kecie akashauri. Alikuwa tayari ameshafika kandokando ya Brian.
Nyumba hii ilikuwa kubwa. Kuizunguka ilikuwa inachukua muda kidogo. Brian allipofika huko nyuma, akafungua mlango na kuzama ndani. Ajabu kulikuwa kiza. Ukutani, kulikuwa kuna taa inayoning’inia, akaikwapua na kutumia kuangazia hatua zake kwenye korido hili jeusi.
Akatembea kwa hatua nne, akasikia kishindo kizito cha miguu ya mtu. Akasimama upesi akiwa amekodoa macho. Akaanza kutetemeka. Akatetemeka zaidi alipohisi kuna mtu nyuma yake, mpaka taa ikaanza kutikisika!
Moyo ukamwenda mbio. Maungio yake ya miguu yakaanza kukosa nguvu.
Baada ya sekunde kadhaa, kule chumbani, Wisconsin pamoja na wageni wake wakaanza kuona mwili wa Brian ukiwa unahangaika kitini. Brian, akiwa bado amefunga macho yake, alikuwa anapapatika haswa akiwa ameshikilia koo lake. Mdomo aliachama, ulimi ulimtoka nje!
Mama Brian akamtazama Wisconsin kwa mshangao, akamuuliza, “Ana nini?”
“Atakuwa anakabwa!” Wisconsin akamjibu.
“Mwokoe basi!” Mama Brian akaropoka akiwa amelowana hofu.
Basi upesi Wisconsin akafanya jitihada za kumwamsha Brian kwa kumfukizia moshi zaidi, akapiga chafya kali na kufungua macho yake aliyoyatumbua kwa upana wote. Alikuwa anahema kwanguvu. Jasho lilikuwa linamchuruza. Anahema kana kwamba mbwa aliyekimbizwa.
“Brian, uko sawa?” Mama akawahi kumuuliza. Brian akakohoa kwanza mara tatu kisha akavuta pumzi ndefu na kutikisa kichwa chake pasipo kutia neno.
“Nini umeona huko?” Wisconsin akamuuliza. Brian alipoka vema akaeleza kila jambo, yale aliiyoyauliza toka kwa Kecie na yale aliyoyashuhudia yeye mwenyewe. Wisconsin akatikisa kichwa chake na kusema, “Basi kazi ni kubwa.”
“Kwanini?” Brian akawahi kuuliza.
“Kwa maelezo aliyokupatia Kecie, ni lazima mzizi wa nguvu za Helo zitakuwa duniani na si kwenye ulimwengu wa wafu. Inabidi mizizi hiyo ikatwe kwanza kabla ya kwenda kumkabili. Na hiyo ndiyo sababu wafu wenziwe hawawezi kummudu, yeye yu kwenye ulimwengu wa aina mbili, ule wa wafu na walio hai.”
“Kivipi?” Brian alihisi kuchanganywa na maelezo hayo. Wisconsin kabla hajaeleza zaidi, akawataka watoke ndani ya chumba hicho kwani walishamaliza zoezi lao kwa muda huo. Waende wakapate chochote kitu tumboni na kuliwaza akili zao alafu, kama kutakuwa kuna haja, watarejea na kuendelea.
Wakaenda zao sebuleni na yule mzee aliyewakarimu akaleta chakula kidogo cha kupasha matumbo yao. Wakiwa wanaendelea kula, Wisconsin akawa anawapa historia za mji huo wa kihistoria na tamaduni. Mambo aliyokuwa anayaongea hayakuenda na umri wake. Alionekana mdogo ukilinganisha na simulizi zake za kale.
“Umezaliwa mwaka gani?” Mama Brian akamuuliza. Alitabasamu kwanza alafu akasema, “Nashangaza na habari zangu, sio?” Mama Brian akatabasamu pasipo kutia neno.
“Uso wangu unaendana na umri wangu. Mimi si wa zamani sana, lakini nayapata kuyajua mengi sababu ya kukutana na watu kila uchwao, watu wa umri mbalimbali, watoto, wazee kwa vijana. Nao wananieleza mengi … mengine yakufurahisha, yakutisha na hata kuhuzunisha.”
“Ulianza kazi hii lini?” Mama akaongezea swali.
“Muda mrefu,” Wisconsin akajibu. “Tangu ujana wangu.” kisha aliposema hivyo akamtazama Mama Brian. “Nilitamani sana kuwa daktari nisaidie shida za watu za kimwili. Lakini nikiwa nasoma, nilikuja kugundua ni lheri ya shida za kimwili, zaweza kuonekana na kuthibitishwa kiwepesi, lakini vipi kuhusu zile za kiroho, ambazo haziwezi kuthibitishwa maabara? … watu wakihisi miili yao haipo sawa, huenda hospitali, lakini vipi si kama miili bali ni hisia ndizo huwasumbua, ni wale waliokufa, majini ama waliolaaniwa?” Wisconsin akaweka kituo. Macho yake yalikuwa yametuama kama mtu anayefakiri jambo. Mama Brian akamuuliza, “Ni hilo ndilo likakufanya uende kwneye taaluma hii?”
“Ndio,” Wisconsin akajibu. “Haswa baada ya rafiki yangu mkubwa, Thompson, kukumbwa na tatizo hilo. Nilishuhudia namna alivyokuwa anateseka. Kila siku akiniambia anakabwa usingizini, anamwona mpenzi wake aliyefariki njiani kila asubuhi ajapo shule. Niliumia maana sikuweza kumsaidia. Sikutaka mtu mwingine ayapitie yale ambayo Thompson aliyapitia.”
“Yuko wapi hivi sasa huyo Thompson?”
“Amefariki.”
“Aliuawa na huyo mpenzi wake?”
“Hapana, aliamua kujiua mwenyewe. Alishindwa kuvumilia. Alinyonga kitanzi na kujitundika apate kujinusuru toka kwenye maisha ya tabu aliyokuwa anaishi.” Wisconsin alinywea sana akiyasema hayo. Japo kitu hicho kilitokea muda mwingi ulopita, bado lilimbakizia kovu kubwa moyoni mwake. Bado akilieleza ni kama vile limetukia jana tu.
Akashusha pumzi ndefu na kukuna kichwa chake. Akanywa mafundo mawili ya kahawa alafu akamtazama Brian aliyekuwa ametuama muda wote huo, akamuuliza, “Ulikuwa rafiki mkubwa sana wa Kecie, sio?”
Brian akatikisa kichwa na kusema, “sasa ndo’ nalijua hilo.”
“Kwanini? Ulikuwa hujui toka kitambo?”
“Sikuwa najua kwa namna hiyo. Kecie alikuwa ni rafiki yangu, rafiki mpenzi, ila nahisi kulikuwa na mwingine ambaye ndiye alikuwa rafiki yake mkubwa.”
“Nani huyo?”
“Faris. Anaitwa Faris. Hata wakati Kecie anapotea msituni, aliyemwona ni Faris.”
“Faris?”
“Ndio.”
“Ni nani huyo? Yupo wapi kwa sasa?”
“Alikuwa ni jirani yake pia rafiki yake. Tangu Kecie alipopotea, Faris amekuwa bubu, haongei chochote akaeleweka. Anaishi maisha ya ajabu sana. Ni kama vile mnyama maana hufungiwa chumbani akiwa ndani ya kamba.”
“Mbona hukuniambia hilo hapo awali?” Wisconsin akastaajabu, akauliza, “anaishi wapi huyo Faris?”
“Nje kidogo ya mji wa Boston, yeye na familia yake.”
“Inabidi tukaonane nae. Ni muhimu!”
“Kwanini?” Mama Brian akauliza upesi kisha akaongezea, “Sidhani kama wazazi wake hupenda kuwaona watu wakiwa wanawatembelea.”
“Itabidi tufanye kila namna tuonane naye,” Wisconsin akasisitiza. “Faris atakuwa na jambo litakalotusaidia kumshida Helo. Yeye alikuwa mtu wa mwisho kumwona Kecie. Kuwa kwake bubu kunamaanisha kuna kiu hatakiwi kusema. Kuna jambo lililofanya akafumbwa mdomo. Inabidi tulijua jambo hilo.”
“Tutalijuaje na yeye ni bubu?” Mama akaongezea swali lingine. Wisconsin akamtoa shaka. “Tutajua tu.” akasema pasipo kutoa maelezo yoyote ya ziada.
“Tutafunga safari kumwendea punde jua litakaposimama katikati ya anga,” akasema na kisha akaenda zake chumbani akiwaacha wageni wake mezani.
**
Saa nane ya mchana …
Wisconsin aliweka mkoba wake mweusi kwenye buti la gari kisha akajiweka ndani ya chombo hicho tayari kwa ajili ya safari. Dereva, Mama Brian, alikuwa tayari ameshakaa kwenye kiti chake. Kwenye viti vya nyuma walikaa watoto, Brian na Olivia.
Chombo kikatiwa moto, wakahepa zao kushika barabara. Hawakutumia tena njia waliyokuja nayo bali ya ziada ambayo Wisconsin aliwaelekeza. Wakadumu kwenye gari kwa takribani masaa mawili kuelekea matatu kasoro tu dakika chache, wakawa wamefika mbele ya nyumba ya wakina Faris. Nyumba iliyojitenga na kuzingirwa na miti mirefu.
Kulikuwa kimya. Giza lilikuwa limeshaanza kuingia, ila bado taa hazikuwa zimewashwa. Ni kama vile hakukuwa na mtu hapa. Mazingira yake hayakuwa yakuvutia.
“Ndiyo hapa,” akasema Brian. Wakasongea mlango na kuugonga mara tatu, hakukuwa na majibu. Brian alitazama ndani hakuona kitu, taa zilikuwa hazijawashwa hivyo ilikuwa ngumu kuona.
“Nadhani hawapo,” akasema Brian. Punde wakaona gari aina ya ‘pickup’ likiwa linasonga kuja eneo walilopo. Lilikuwa ni pickup ya zamani, iliyochoka. Taa yake moja tu ndiyo ilikuwa inawaka. Likaegeshwa, toka ndani akashuka bwana York na mkewe, wazazi wa Faris.
Bwana York alikuwa amebebelea gobore akiwa amelishikilia katika namna ya kujilinda. “Ni wakina nani nyie?” akapaza sauti yake kavu. Hakuwa anaona vema. Alikuwa amekodoa haswa na kufanya uso wake utishe.
“Ni sisi, majirani zako!” Mama Brian akajitambulisha.
“Majirani? Majirani zetu ni miti tu! Ninyi ni wakina nani?” Bwana York akafoka. Mkewe ndiyo akamwambia kuwa ni familia ya wakina Brian, hivyo aweke silaha yake chini.
“Mmekuja kufuata nini hapa?” Bwana York akauliza. Bado silaha yake alikuwa akiielekezea kule kwa wageni.
“Tuna maongezi kidogo, tafadhali tunaomba mtuskize.”
Mke wa bwana York akamtaka mumewe atulize munkari wawakaribishe wageni kwani wametoka mbali, si bure kuna jambo lililowafungisha safari.
“Wanataka nini lakini?” bwana York akawaka. “Tulihama kwenye ule ulimwengu kuja kutafuta amani huku msituni, kwanini bado wanatufuata?”
Mama Brian akamsogelea bwana York na kumweleza, “Tumekuja na mtaalamu. Anaweza kumsaidia Faris endapo wakimpa nafasi.”
Bwana York akamtazama Mama Brian. Angalau sasa macho yake ya kizee yaliweza kumwona. Akamwambia akiwa amekunja uso wake, “Faris hayupo hapa.”
“Yupo wapi?” Mama Brian akauliza.
“Ameshakufa,” bwana York akamjibu kisha akatembea zake kwenda ndani. Mama Brian akamtazama mama yake Faris kwa mshangao, akamuuliza, “Ni kweli?”
Mwanamke huyo akamtikisia kichwa. “Ndio. Ni kweli.” mara macho yake yakaanza kuwa mekundu, uso wake ukionyesha kulia.
**
.
Akaongozana na wageni wake mpaka ndani alipowaketisha na kuwapatia vikombe vya kahawa kisha akawaeleza kilichomsibu Faris.
.
.
“Hali yake ilikuwa mbaya zaidi. Alikuwa anadhoofika siku baada ya siku. Alikuwa anapiga kelele sana usiku na hakuwa anataka kumwona mtu yeyote,” Mrs York akaweka kituo na kufuta kwanza machozi yaliyokuwa yanammiminika. Pua yake ilikuwa nyekundu na mdomo wake mkavu.
.
.
“Kila siku baba yake alikuwa ananisihi anataka kumuua lakini mimi nikiwa namkataza. Japo alikuwa vile bado sikutaka aondoke. Bado nilikuwa na matumaini huenda akaja kupita jaribu lake hilo, ila kila siku matumaini yalikuwa yanafifia. Hakuonyesha dalili yoyote. Kila siku ilikuwa ni mbaya zaidi ya iliyopita.
.
.
Alikuwa anachanganyikiwa maradufu. Ndipo baba yake akalazimisha kuwa ampumzishe …” Hapa Mrs York akakabwa na kilio kwa muda. Ilimchukua kama sekunde tano kuendelea kuongea tena, “Alimpiga risasi mbili zilizomlaza mfu kisha tukaenda kumzika. Sasa akiwa amelala kwa amani.”
.
.
Mrs York akiwa amebanwa na kwikwi, akaendelea kupambana na mito ya machozi. Roho yake ilikuwa inamuuma. Angalau alikuwa ameyasahau haya.
.
.
“Tunaweza kuona mlipomzikia?” Brian akauliza. Pasi na hiyana, Mrs York akaongozana nao mpaka nyuma ya nyumba, huko wakalikuta kaburi la Faris. Wakaomboleza hapo,
.
.
“Aliishi maisha ya tabu sana,” Mrs York akasema. “Maisha yake yalijawa na majeraha, kilio, hofu, masumbuko na mateso. Ni kheri hata akiwa amekufa kuliko maisha yale.”
.
.Mama Brian akamtazama Wisconsin na kumuuliza, “Sasa tutafanyaje na tuliyemfuata hayupo?”
.
.
“Labda kuna mengine yanaweza kutusaidia,” akasema Brian
akiwatazama mama yake na Wisconsin, kisha akamtazama Mrs York na kumuuliza, “Kwenye chumba cha Brian kuna chochote mlichobadili?”
.
.
Mrs York akatikisa kichwa chake. “Tangu alipokufa, chumba chake tulikifunga na kufuli.”
.
.
Basi wakaenda huko chumbani, Brian akimwambia Wisconsin kuwa Faris alikuwa akichora michoro kadha wa kadha kwenye mbao ya kitanda. Pengine picha hizo akizitazama, ataweza kugundua jambo.
.
.
Wisconsin akachukua kioo cha kukuzia toka kwenye mkebe wake, kisha wakaelekea kwenye chumba hicho na kuanza kupembua kwa macho kingo zote za kitanda. Na hata kule ukutani ambapo Faris alikuwa amechorachora ama kuandika vitu ambavyo havijulikana maana zake.
.
.
Wisconsin alinakili kwenye kijitabu chake kila jambo aliloliona, baada ya dakika kumi, akawa amemaliza zoezi lake hilo wakarejea sebuleni. Wisconsin akatoka tena kuuendea mkoba wake, akatoa kitabu fulani kikubwa na kuja nacho ndani.
.
.
Akatumia karibu nusu saa kutazama kile kilichopo kwenye kijitabu chake na kufananishia na yale yaliyopo kwenye kitabu chake kikubwa alichotoa garini. Alipomaliza, sasa akawa amepata maana kamili.
.
.
“Faris alikuwa anajua mambo mengi, ni ajabu hatukuyajua kabla ya kufa kwake. Alitamani kuyasema, lakini haikuwa inawezekana. Hata alipotumia alama, bado mlishindwa kuyajua.”
.
.
Wisconsin akafungua ukurasa wa kwanza kabisa wa kijitabu chake kidogo, akaonyeshea ule mchoro wa msichana na mwanaume pembeni yake. Msichana na mwanaume njiti. Msichana akiwa ameshikilia mdoli wake mkononi.
.
.
“Huu ndiyo ulikuwa mchoro wake wa kwanza kabisa. Mchoro wa kitu cha mwisho alichokiona pindi akiwa timamu. Huyu ni Kecie na hawa wanaume wawili, mmoja ni Helo, mwingine ni yule mwanaume aliyeuawa na familia ya Mrs Garett kwa ajili ya kuficha siri. Kwahiyo Faris alikuwa anamfahamu Helo. Alimwona kwa macho yake.
.
.
Na huu ujumbe ambao umewekwa hapa kwenye huu mchoro ni ushahidi tosha kuwa Helo alimtaka Faris aungane nae kama ilivyokuwa kwa Kecie. Ujumbe huu umeandikwa kwa lugha ya kilatini ukimaanisha ‘kuwa wangu.’ kwahiyo Helo alijaribu kumshawishi Faris aende naye.”
.
.
“Mbona sasa akabakia? Tena akiwa hawezi kuongea?” Brian akauliza kwa pupa.
.
.
“Kwasababu aliweka agano na Kecie,” akajibu Wisconsin akionyeshea michoro kadhaa aliyoinakili toka kwa Faris. “Kwenye michoro hii ukiitazama vema utaona maneno ya kilatini yakimpa Faris kikomo. Helo aliweka agano na Kecie kuwa Faris atakuwa hai, ila akiwa salama zaidi kwake, ndiyo maana Faris alikuwa bubu.”
.
.
“Na hiyo michoro mengine?” Mama Brian akauliza.
.
.
“Kecie alikuwa anamtembelea Faris mara kwa mara. Unaweza kuona hapa … hapa … na hapa, na hata lile la watoto kupotea, Faris alikwishalifahamu, unaweza kuona mchoro huu, watoto wakiwa wamesimama na mwanaume yule mrefu.”
.
.
“Aliyajuaje?” Mrs York akauliza. Wisconsin akamtazama Brian na kumuuliza, “Haujawahi kupata ishara yoyote toka kwa Kecie?”
.
.
Brian akafikiri kidogo, mara akasema, “Nadhani nilikuwa napata ishara! Mara ya kwanza kabisa kabla watu hawajaanza kupotea, tuliona maneno fulani ya damu ukutani tukiambiwa tutazame mji wetu. Nakumbuka pia wakati Olivia anaondoka kuelekea msituni, nilisikia mtu anagonga mlango! Nilipoenda kutazama sikuona mtu bali nilihamaki Olivia akiishia!”
.
.
“Hivyo tu?” Wisconsin akauliza. Brian akaendelea kusema, “nakumbuka tena jana, wakati mama akiwa amevamiwa na kukabwa, kabla ya kusikia chupa ikipasuka, nilisikia mtu akigonga dirishani mwangu mara tatu! Simjui mtu huyu ni nani, ila kila baada ya hapo napata kushuhudia jambo.”
.
.
“Ni Kecie!” akasema Wisconsin. “Alikuwa anawatumia ninyi wote kuwapa ishara ya kile kilichokuwa kinatokea.”
.
.
“Sasa kwanini Kecie hakumwambia Faris amwokoe? Badala yake Brian?” Mama Brian akauliza.
.
.
“Kwasababu Faris asingeweza kumwokoa tena Kecie kwasababu ya agano waliloweka. Faris alibakiziwa uhai, kumbuka, kwasababu ya Kecie. Asingeweza tena kwenda kumwokoa, la sivyo agano lingetenguliwa!”
.
.
“Sasa tunafanyaje?” akauliza Brian. “Tutamalizaje Helo?”
.
.
“Unakumbuka nilikuambia kuwa nguvu za Helo hutokana na mihimili iliyokuwapo duniani?” Wisconsin akauliza, kabla hajajibiwa akaendelea, “Hata hilo Faris alikuwa analitambua.”
.
.
“Ni mihimili gani hiyo?” Brian akawahi kuuliza kwa pupa. Wisconsin akaonyeshea kidole chake kwenye moja ya mchoro wa Faris. “Unaona huu mchoro, huyu mwanaume aliyesimama katikati ni Helo, unaweza kumtambua kwa namna ambavyo Faris amekuwa akimchora. Na hawa wawili kushoto na kulia kwake, ndiyo mihimili yake.”
.
.
Brian na wenzake wakatazama hao watu wawili wakijaribu kuwang’amua. Mmoja wao Brian akamtambua upesi. “Huyu atakuwa ni padri Alfonso!” Kwenye mchoro mtu huyo alikuwa ana alama ya msalaba kichwani.
.
.
“Na vipi kuhusu huyu?” Wisconsin akauliza akionyeshea ule mchoro wa mwanaume mwingine.
.
.
“Huyu sijajua atakuwa ni nani,” akasema Brian. “Ila huyu Padri Alfonso hawezi kutusaidia kumpata huyo mwingine?”
.
.
“Si rahisi kihivyo,” akasema Wisconsin. “Kumaliza hii mihimili haitakuwa kazi rahisi hata kidogo lakini kuwatambua ni nusu ya kumaliza kazi hiyo.”
.
.
Basi walipomaliza zoezi lao hilo, wageni wakaaga wanaenda zao. Kwakuwa Mr York alikuwa chumbani amejifungia, Mrs York akawasindikiza wageni wao mpaka kwenye gari. Wakajipaki na kwenda zao. Yalikuwa ni majira ya saa tatu usiku sasa.
.
.
Wakiwa kwenye gari wakawa wanakata misitu kwenda Boston. Walitembea kwa muda wa nusu saa. Kulikuwa kimya msituni lakini pia kiza.
.
.
“Itabidi unipatie hifadhi kwa muda wote huo wa kazi,” Wisconsin alimwambia Mama Brian. Wote walikuwa wamekaa mbele, watoto wapo nyuma.
.
.
“Ondoa shaka,” Mama Brian akamwambia. “Utakaa mpaka utakaponiambia tatizo limekwisha.”
.
.
Mama Brian alipomaliza kusema hayo, mara gari likatikisika kana kwamba limekanyaga kitu. Mara kidogo taa zikaanza kufifia pamoja pia na mwendo. Mara likazima na kusimama!
.
.
Ilikuwa ni katikati ya msitu. Mbele ni miti na nyuma ni miti!
.
.
“Hapana! Hapana!” Mama Brian akalalama akipiga usukani. Hakuwa anaamini macho yake. Gari lazima msituni tena usiku kama ule, hatari iliyoje.
.
.
“Sasa tunafanyaje?” akauliza.
.
Wisconsin na Brian walishuka toka kwenye gari na kuanza kulipekua gari wajue limepata shida gani. Matairi yalikuwa sawa, injini nayo ilikuwa sawa na hata kila kitu kilichokuwa kinaonekana kwa macho kwa wepesi vilikuwa sawa.
.
.
Basi Wisconsin akalala na kutazama huko chini. Akisaidiwa na kurunzi akapekua huku na huko, hakuwa anaona jambo lolote. Akiwa anaendelea kuangaza, mara akaona miguu ya mtu ikiwa imesimama kwa upande wa pili! Hii haikuwa ya Brian. Ilikuwa ni miguu meupe pe. Miguu mipana na iliyokomaa.
.
.
Wisconsin akastaajabu. Haraka akatoa uso wake chini atazame huko alipoona hiyo miguu, ajabu hakuona kitu. Brian akamuuliza, “Vipi?”
.
.
Wisconsin akiwa ametoa macho akamuuliza, “Haukuona mtu yeyote hapo?” Brian akatikisa kichwa kukataa. Hakumwona mtu. Basi Wisconsin akadhani pengine ni macho yake. Akalala tena chini na kuendelea kutazama kama ataona hitilafu ya gari.
.
.
Akiwa anaendelea kutazama, akaona tena miguu ya mtu! Mara hii haikuwa imesimama, bali inakimbia. Haraka akanyanyuka na kuangaza. Hamna mtu.
.
.
“Haujaona mtu akikimbia?” akamuuliza Brian. “Hapana, sijaona!” Brian akajibu akirusha macho huku na kule. “Vipi, kuna nini?” Brian akauliza.
Wisconsin kabla ya kujibu, akatazama kwanza pande zake zote, karibu na mbali. Hakuona chochote. Akamtazama Brian na kumwambia, “Nimeona mtu.” Brian akashtuka,
.
.
“Yuko wapi?”
.
.
“Nimemwona wakati nikiwa chini. Ajabu nikiamka, simwoni!”
.
.
“Una uhakika?”
.
.
“Ndio … Brian, turudi ndani ya gari.”
.
.
Basi upesi wakarejea kwenye viti vyao.
.
.
“Hamna shida,” akasema Wisconsin. “Gari lipo sawa.”
.
.
“Sasa nini tatizo, mbona limezima?” akauliza Mama Brian kwa hamaki.
.
.
“Nadhani tatizo litakuwa ni mambo mengine,” akasema Wisconsin. “Ila kwa upande wa gari, hamna tatizo.”
.
.
Basi wakakaa hapo kwa muda wakiwaza namna ya kufanya. Hawawezi kulala ndani ya gari msituni. Muda ukazidi kwenda wasipate la kufanya. Wakakubaliana endapo wakiliona gari linakuja walisimamishe na kuomba msaada.
.
.
Nusu saa ikapita, bado kimya. Kila mtu alikuwa ameegesha kichwa chake kwenye kiti kwa uchovu. Waliposikia sauti wakaangaza barabarani, hakuna kitu. Ni upepo tu ukicheza na matawi ya miti.
.
.
Lisaa likapita, bado kimya. Sasa wakaanza kusinzia. Macho yalikuwa mazito. Walikuwa wamechoka mno na hakukuwa na soga za kuwafanya wakodoe.
.
.
Wakiwa wamelala, baada ya muda fulani, Brian akajikuta akiwa amefumbua macho. Akatupa macho yake kutazama huku na huko ndani ya gari. Amah! Akastaajabu Olivia aliyekuwa amekaa naye pembeni hakuwapo! Nao mlango wa nyuma wa upande aliokuwa amekaa Olivia ulikuwa wazi.
.
.
Akarusha macho yake kutazama. Hamaki akamwona Olivia akiwa anaishia msituni! Haraka akamshtua mama yake na Wisconsin waamke. Ajabu hawakuamka! Aliwasukumasukuma, aliwaita kwanguvu lakini waapi! Hawakuamka wala kushtuka. Ni kama vile walikula madawa ya kulevya! Kila Brian alipotazama msituni, Olivia aliendelea kuishia.
.
.
Basi akatoka ndani ya gari na kukimbia upesi kwenda kumwokoa Olivia. Alimuita kwanguvu akiwa anamkimbilia. Olivia hakuwa anasikia, alikuwa anaendelea kutembea tena akiwa amefumba macho. Alikuwa umbali wa kama hatua thelathini na tano toka Brian alipo.
.
.
Brian akakazana kukimbia. Alipomkaribia akamnyaka na kumkumbatia.
.
.
“Olivia, uko sawa?”
.
.
Ila aligundua Olivia ni wa baridi sana. Ni kama vile ni maiti na si binadamu. Akamtazama usoni, binti alikuwa amefumba macho. Akajaribu kumwamsha, haikuwezekana. Akaweka sikio lake kifuani mwa mtoto huyo, hakuwa anasikia mapigo yoyote yale! Akastaajabu.
.
.
Aliporudisha macho yake usoni mwa Olivia, akastaabu mtoto huyo amefumbua macho! Macho yake yalikuwa meusi ti, na uso wake mweupe ulianza kuchipuka michirizi meusi.
.
.
Brian akashtuka, Olivia akatabasamu. Nayo meno yake yalikuwa kana kwamba mkaa kwa uweusi, na yote yakiwa chonge. Kabla Olivia hajasema jambo, mdomo wake ukaanza kuchuruza udenda mweusi, na mara akanyanyua mkono wake wa kuume akitaka kumnyaka Brian.
.
.
“Olivia, amka!” Brian akapayuka akiwa anasonga kurudi nyuma. Olivia akaongeza kasi ya miguu yake kumfuata.
.
.
“Amka! Olivia, amka!” Brian akaendelea kuita lakini Olivia hakuwa anajali hata kidogo. Bado alikuwa anamsogelea Brian huku akiwa amenyoosha mkono wake wa kuume akitaka kumnyaka. Mwishowe Brian akajigota kwenye mti, Olivia sasa akamkaribia!
.
.
“Hapana, Olivia! Hapana! Hapanaa!” mara Brian akapiga kelele kali sana, kule ndani ya gari Wisconsin akaisikia na kukurupuka. Kutazama nyuma, mlango ulikuwa wazi, na Brian hayupo! Olivia pekee ndiye kalala kwenye kiti.
.
.
Upesi akamwamsha Mama Brian.
.
.
“Brian ameondoka!”
.
.
Basi haraka wakatoka na kwenda kumtafuta. Mama Brian akabebelea kurunzi, Wisconsin akibebebelea gongo kubwa. Wakawa wanaangaza huku na kule, wakijongea kwa woga na tahadhari.
.
.
Mara wakasikia tena sauti ya Brian kwa mbali. Wakakimbilia huko upesi, wakamkuta Brian akiwa amelala chini pamoja na Olivia! Wakastaajabu. Mbona walikuwa wamemwacha Olivia kwenye gari!
.
.
Mama akamnyakua Brian na kumweka kwapani, wakabaki wanamtazama Olivia.
.
.
“Wewe ni nani?” Wisconsin akauliza akiwa ameshikilia gongo lake vema kwa tahadhari. Olivia hakujibu, bado alikuwa yu katika hali ya kutokuwa na fahamu. Wisconsin, akiwa amejikaza kisabuni, akamgusa Olivia kwa gongo lake. Mara akaanza kuonyesha ishara ya kuamka.
.
.
Ila kabla hajatengemaa, Brian akawa amerejewa na fahamu zake kamili. Alipotazama na kumwona Olivia, akashtuka sana. Akasema akinyooshea kidole, “Huyo si Olivia! Si Olivia!” Wisconsin na Mama wakasonga nyuma kwa tahadhari.
.
.
Olivia akanyanyua uso wake na kuwatazama. Alikuwa na uso wa Olivia tumjuae. Macho yake yalikuwa ya binadamu, pia uso wake mwekundu wenye kutia huruma.
.
.
Akaita kwa sauti ya upole,
.
.
“Brian.”
.
.
Watu wote walikuwa wamekaa mbali wakimtazama kwa mashaka. Wisconsin alikwisha andaa rungu kwa kazi ya ziada.
.
.
“Mbona nipo hapa?” Akauliza. “Tunafanya nini hapa?” uso wake ulikuwa umejawa na ndita za hofu na kukanganyikiwa. Macho yake punde yalianza kulowana maji.
.
.
Brian akasema, “wewe si Olivia!” huku akitikisa kichwa. Alipomalizia kauli yake hiyo, wakasikia sauti ya honi barabarani! Honi ilipigwa mara tatu! Wakatazamana. Walidhani ni gari la msaada. Haraka wakaanza kukimbia kwenda kule barabarani. Olivia naye hakubakia nyuma, akaongozana nao akikimbia kadiri ya uwezo wake.
.
.
Walipofika, hawakuona gari jingine isipokuwa la kwao. Ajabu lilikuwa limewaka taa na fyagio zake za kioo zikienda kushoto na kulia. Wakashangaa, “limewaka!”
.
.
“Nani kaliwasha?” Mama Brian akauliza. Haraka wakaliendea na kutazama ndani kupitia madirisha, wakamwona Olivia! Alikuwa ameketi kwenye kiti cha dereva akitazama mbele kana kwamba anaendesha.
INAENDELEA

