NILIOA JINI NA KUZAA NAE
ONYO: Wakubwa tu, kuanzia Miaka 18, ndio wasome hii Hadithi
SEHEMU YA 11
ILIPOISHIA..
”Kama wewe ni Mtemi Wembe, mimi ni Banuna mwana wa Ziraili…mimi wa ukoo wa kifalme. Wewe huwezi kuniita mimi….”
“Nakwambia…..!” Mtemi wembe alitaka kusema lakini Banuna hakumpa nafasi.
“Una shida gani na mimi?” akaendelea kumuuliza kwa sauti yake kali na ya kiburi.
“Nataka kukutenganisha na Alfred, leo iwe mwisho wako kumfuata!” Mganga akamwambia kwa sauti kali.
Bananuna kwa jeuri alikishika kiuno chake akamwambia mganga.
“Nakwambia huniwezi! Alfred nitakuwa naye hadi kifo chake. Simuachi! Unasemaje?”
Hapo hapo mganga naye akapandisha jini lake.
“Shiit! Wewe nani Tanzania? Utakwenda tu!. Leo nitakuondoa kwa sababu umekosa adabu!” Jini wa mganga huyo akasema kwa ghadhabu.
SASA ENDELEA
Nikajiambia kimoyomoyo, leo patazuka balaa! Kabla sijamaliza kuwaza, Banuna alishavuta mkono, akamtandika Mtemi Wembe kibao cha shavu. Mtemi Wembe akaanguka chini. Hakuinuka tena. Povu likawa linamtoka mdomoni.
Kitendo hicho kilitufanya mimi, Juma na wasaidizi wa mganga huyo tukurupuke na kutimua mbio. Juma na mimi tulitimua mbio za ajabu. Kila mmoja alikimbilia upande wake. Tulikuja kukutana barabarani.
Kwa sekunde kadhaa tulikuwa tumesimama tukihema, hatukuweza kuzungumza lolote. Punde tu ikatokea daladala ikielekea mjini, nikaipungia mkono. Daladala hiyo iliposimama tukajipakia.
Humo ndani ya daladala pia hatukuzungumza kitu. Kila mtu aliyetuona alijua kuwa tumepatwa na jambo tena jambo kubwa.
Tulipofika stendi ya Tanga tulishuka. Mwili wangu ulikuwa bado ukutetemeka. Juma akanitazama kisha akatikisa kichwa kusikitika.
“Ni hatari!” akaniambia na kuongeza.
“Sikutarajia kuwa yatatokea mambo kama yale!”
“Mimi nilikuwa na mashaka tangu mapema”
“Yule msichana aliyekuja pale na kumpiga yule mzee ni nani?”
“Si ndiye huyo jini anayenifuata!”
“Kumbe jini mwenyewe ndiye yule, mkali namna ile!”
“Umemuona mwenyewe Juma!”
“Kwa uzuri ni mzuri sana lakini anatisha. Sijui kama yule mganga atapona!”
“Kama mganga mwenyewe amepigwa, je mimi mwenyewe itakuwaje!”
“Na ni mganga niliyemtegemea sana. Inaonesha tatizo lako ni kubwa sana”
“Sasa tufanyeje rafiki yangu?”
“Twende nyumbani, tutashauriana”
Tulipofika nyumbani kwa Juma, tulikaa na kuanza kujadiliana.
Juma aliniambia kuwa yule mganga ameshashindwa na haitakuwa na maana yoyote kurudi kwake tena. Na kama ni suala la pesa zetu tulizompa ndio zimeshapotea. Tusingeweza kwenda kumdai. Na pia hatukujua hali yake itakuwaje.
“Kwa jinsi hili tatizo lilivyo, mimi ningekushauri uende Pemba. Kule kuna waganga hodari sana wa majini”
“Hata mimi nimewahi kusikia hivyo”
“Nimesikia wanawafuga majini majumbani na kuwatuma”
Sikumjibu kitu. Nilikuwa nikiwaza jinsi nitakavyofika huko Pemba wakati sikuwa na akiba yoyote ya pesa.
“Mimi nadhai Alfred uende Pemba” Juma akaendelea kuniambia.
“Ushauri wako ninaukubali, lakini sina pesa, nitakwendaje?”
“Hilo nalo ni tatizo jingine. Itabidi tusubiri mwisho wa mwezi nikupe mshahara wangu”
“Halafu wewe utatumia nini?”
“Usijali Alfred, nitakopa kopa hivyo hivyo”
Kwa kweli nilihuzunika sana lakini sikuwa na jinsi.
“Usihuzunike rafiki yangu. Yote yatakwisha. Hakuna lisilo na mwisho”. Juma akaniambia kwa moyo wa huruma.
Kutokana na hofu niliyokuwa nayo kuhusiana na Banuna, niliendelea kuishi kwa Juma nikisubiri mwisho wa mwezi ufike anipe mshahara wake niende Pemba kutafuta waganga. Lakini kutoka siku ile tuliyokwenda Amboni kwa yule mganga na kutokea lile tukio, sikumuona tena Banuna.
Usiku mmoja wa kuamkia ile siku ambayo Juma angepata mshahara wake na kunipa kama alivyoniahidi, lilitokea tokeo ambalo sitalisahau.
Usiku huo nilikuwa nimelala na Juma, nilishituka usingizini na kumuona Banuna amesimama kando ya kitanda upande ninaolala mimi. Alikuwa amevaa nguo nyeupe tupu. Ilikuwa ni hali ambayo ingenifanya nishituke na pengine kupiga kelele au kutoka mbio.
Lakini sikushituka wala sikupiga kelele wala sikutoka mbio. Nilikuwa kama zezeta. Nilijiona kama nilikuwa katika ndoto kwani akili hazikuwa zangu.
“Alfred!” Banuna akaniita alipoona nimeamka.
“Ndiyo Banuna!” nikamuitikia kwa sauti tulivu.
“Umeniona?” akaniuliza kama aliyekuwa ananisomesha.
“Ndiyo nimekuona, si Banuna wewe?”
“Nimekufuata twende kwetu”
“Kwenu wapi?”
“Kwetu baharini. Uko tayari twende?”
“Niko tayari” nikamjibu”
“Amka basi twende zetu”
Nikainuka na kushuka kitandani. Juma alikuwa amelala fofofo.
“Vaa nguo zako” akaniambia.
Nikavaa suruali, shati na viatu.
“Sasa twende”
Akanishika mkono.
Tukatoka mle chumbani. Akafungua mlango wa mbele na kuniambia nitangulie kutoka nje. Nilipotoka na yeye akafuatia.
Aliinama chini akachora msitari mbele yangu kisha akaniambia.
“Vuka huo msitari”
Nikiwa kama zezeta ambaye sikuwa na uwezo wa kuwaza chochote, nilitii alichoniambia, nikapiga hatua na kuvuka ule msitari. Kufumba na kufumbua nikajiona niko katika eneo jingine ufukweni mwa bahari. Banuna alikuwa amesimama kando yangu, akanishika mkono na kuniambia.
SEHEMU YA 12
“Twende kule”
Alinionesha kule baharini.
Tukawa tunatembea kwenye ufukwe kuelekea baharini. Sikuju tulikwa tunakwenda wapi. Ulikuwa usiku mwingi na kulikwa kunatisha lakini sikupata hofu yoyote.
Punde tu tukayafikia maji, sasa tukawa tunatembea kwenye maji huku nguo zetu zikitota. Tangu maji yalikuwa kwenye viwiko vya miguu hadi yakawa kwenye magoti. Tukaendelea kwenda hadi maji yakatufikia kifuani.
Sasa nikawa ninayumbishwa na maji. Ilibidi Banuna anishikilie ili maji yasinichukue.
“Tunakwenda hadi wapi?” nilimuuliza Banuna nilipoona maji yametufika shingoni.
“Tunakwenda kwetu” Banuna akanijibu.
“Kuna mji huku?”
“Ndio upo”
“Uko wapi?”
“Utauona, twende tu”
“Tutafika saa ngapi?”
“Usiwe na wasiwasi. Tutafika sasa hivi”
Banuna aliendelea kunipeleka hadi maji yakawa yananikosesha pumzi kwani mawimbi yalikuwa yanapiga kwenye uso wangu. Banuna akaniambia nipande kwenye mgongo wake.
“Panda ukae kwenye mabega yangu”
Banuna akanisaidia nikaweza kukaa kwenye mabega yake. Jambo la ajabu ni kuwa Banuna aliweza kunibeba na kutembea na mimi kwenye maji huku kichwa chake kikiwa kimeshazama baharini Sikuweza kujua alikuwa akipumua kwa namna gani.
Muda si muda niliona ananizamisha cihini ya bahari. Nikapiga kelele.
“Sasa tunakufa!”
“Usiogope, hutakufa” niliisikia sauti yake ikitokea ndani ya maji.
Licha ya kunitoa wasiwasi kuwa sitakufa, sikuamini. Nikizama chini ya bahari. nitapata wapi pumzi?
“Banuna sitaweza kupumua ndani ya maji!” nikamwambia Banuna kwa sauti ya kutetemeka.
“Utaweza. Mbona mimi ninaweza”
Banuna akazidi kunizamisha. Sasa maji yalikuwa kwenye shingo yangu. Nilikuwa nimefunga mdomo lakini ndani ya moyo wangu nilikuwa ninapiga kelele. “Nakufa…nakufa…nakufa…!”
Ghafla kichwa changu chote kikazama chini ya bahari. Nilikuwa nimetaharuki kwa hofu lakini niliona miujiza mikubwa. Vile ninazama tu chini ya bahari niliona tumetokea mahali kweupe kusiko na bahari.
Banuna akiwa amenibeba kwenye mabega yake alikuwa amesimama kwenye mnara mrefu ulioteremka chini. Huko chini kulikuwa na mji mkubwa uliokuwa unawaka taa. Kulikuwa na minara kadhaa iliyoonekana kila upande
Ulikuwa mji wa ajabu na mzuri usio na magari wala pikipiki isipokuwa watu wa ajabu walioonekana wakienda huku na huku kama vile ni mchana.
Kwa upande mmoja niliona kulikuwa na gulio. Watu walikuwa wamejazana wakinunua mahitaji.
Wengi wa watu niliowaona walikuwa wamevaa nguo zilizofanana na nguo zenyewe zilikuwa shuka, ama shuka nyeupe ama nyekundu. Wengine walikuwa wamechanganya shuka nyeupe na nyekundu. Baadhi ya watu hao walikuwa wamejifunga vilemba vikubwa kama waarabu.
Mbali ya watu hao, pia niliona punda wengi na farasi wa rangi mbalimbali.
Banuna akaniambia nishuke kutoka kwenye mabega yake. Huwezi kuamini kuwa msichana huyo aliweza kunibeba, labda kwa vile alikuwa ni jini kwani hata kwa uzito nilikuwa nimemzidi.
“Umeuona mji wetu?” Banuna akaniuliza.
“Nimeuona. Ndiyo mji wenu huu?”
“Ndio huo. Wale wote unaowaona chini ni majini!”
“Sasa huu mji ndio uko chini ya bahari?”
“Ndiyo. Na hapa tulipotokea ndio nyumbani kwetu”
“Huu mnara ndio nyumbani kwenu?”
“Hii ni ghorofa, imekwenda chini. Humu ndani kuna wazazi wangu”
Nikawa nimeshangaa.
“Hii ni nyumba kabisa. Tutaingia na utaiona” Manuna akaniambia.
Mnara huo wa mawe ulikuwa na matundu kama madirisha na kulikuwa na sehemu yenye uwazi mrefu kama mlango. Banuna akaniambia nimfuate.
Akatangulia kuingia kwenye ule uwazi na mimi nikamfuata nyuma. Kulikuwa na kiza sana. Nilikuwa sioni.
“Nishike bega twende” Banuna akaniambia.
Nikanyoosha mkono wangu wa kulia na kumshika bega.
Kulikuwa na ngazi. Tukashuka taratibu. Tulikuwa kama tunaoshuka kwenye shimo. Kila tulivyozidi kushuka ndio kiza kilivyozidi.
“Huoni kabisa?” Banuna akaniuliza baada ya ukimya mrefu.
“Sioni!”
“Mimi naona. Tunapita katika kuta za mawe, karibuni tutafika”
“Sasa mnaishije kwenye kiza namna hii?”
“Tunapokuwa kwenye mwanga, mboni zetu za macho zinakuwa
Ndogo lakini tukiwa kwenye kiza mboni zinakuwa kubwa na kutuwezesha kuona”
“Kwa hiyo mimi sitaweza kuona”
“Tutatokea kwenye mwanga muda si mrefu”
“Kiza hiki kinatisha sana bora mngeweka taa”
“Usijali, utazoea tu”
Mara nikasikia Banuna akisemeshana na mwenzake mwenye sauti ya kiume ambaye sikuweza kumuona kutokana na kiza. Lugha waliyozungumza haikuwa ya Kiswahili.
Hapo hapo nikaona mlango unafunguliwa. Nikaona mwanga mzuri mweupe umetokea.
“Tuingie” Banuna akaniambia.
SEHEMU YA 13
Tukaingia mle ndani. Kwa vile sasa kulikuwa na mwanga niliondoa mkono wangu kwenye bega la Banuna. Licha ya kuuona ule mwanga sikuweza kujua ni kitu gani kilichokuwa kinatoa mwanaga huo.
Tulikuwa tumetokea katika ukumbi mpana uliokuwa umetandikwa mazulia mazuri na wenye hewa safi lakini ulikuwa mtupu usio na kitu chochote.
Ulikuwa na milango mitatu iliyoingia ndani ambayo ilikuwa imezibwa kwa mapazia mazito ya hariri. Banuna alinipeleka katika mlango uliokuwa katikati, tukaingia.
Tulitokea katika ukumbi mwingine mdogo uliokuwa na ngazi za kupanda. Tukapanda ngazi hadi juu kidogo, tukaingia kwenye mlango mwingine ambao pia ulizibwa kwa pazia. Tulipoingia katika mlango huo tulitokea katika ukumbi mwingine uliokuwa kama sebule iliyokuwa ina meremeta.
Ulikuwa na fanicha zilizotengezwa kwa madini. Fanicha hizo zilikuwa zikitoa rangi mbalimbali za kupendeza. Muundo wa fanicha hizo sikuwahi kuuona popote. Nikabaki ninakikodolea macho kila kitu ninachokiona kwani kilikuwa
cha ajabu kwangu. Mbali na vitu hivyo, harufu iliyokuwa inasikika humo ndani ilikuwa ni ya marashi na udi wa Ajemi.
“Kaa hapo chini” Banuna akaniambia.
“Nikae chini wapi?” nikamuuliza.
“Kaa popote tu, sisi huku tunakaa chini”
Nikakaa chini huku nikiendelea kuikodolea macho ile sebule. Kila kitu nilichokiona kilikuwa kigeni kwangu.
“Sasa nisubiri nikamuite mama yangu, aje muonane” Banuna akaniambia na kupotea kwenye pazia lililokuwa mbele yake.
Baada ya muda kidogo niliona pazia likipenuliwa akatokea tena Banuna na mwanamke mmoja mzee. Alikuwa mfupi aliyevaa shuka nyeupe. Alikuwa na nywele ndefu nyeupe zizilizomteremka kwenye mabega. Hata hivyo alikuwa amefunga kilemba cheupe kichwani. Licha ya kumtazama kwa makini bibi huyo, sikuweza kutambua alikuwa muarabu au muhindi.
Bibi huyo wa kijini alikuja hadi pale nilipokuwa nimeketi. Nikayaona macho yake ya kijivu, yalikuwa na mboni zilizosimama kama mboni za paka. Hata Banuna anapokasirika mboni zake hubadilika na kuwa hivyo..
Jambo la ajabu ni kuwa sikutishika kukaa na viumbe hao waliokuwa na maumbile tofauti na mimi.
Yule bibi aliketi karibu yangu akakunja miguu yake kisha akaniambia.
“Asalaam alaykum”
“Alaykumu salaam” nikamjibu.
Banuna naye akaketi palepale.
“Alfred, huyu ni mama yangu. Anaitwa Ummi Mariam” Banuna akaniambia.
“Nimefurahi kumuona” nikamwambia Banuna.
Banuna akamtazama mama yake na kumwambia.
“Maa, huyu ndiye yule kijana niliyekuwa ninakwambia. Leo nimekuja naye umuone”
Yule bibi akanitazama na kuniuliza.
“Mmekubaliana nini na Banuna?”
Swali hilo lilinishitua kidogo. Hata hivyo nilibetua mabega yangu na kumjibu.
“Hatukukubaliana chochote!”
“Alipokwambia mje huku alikwambia manakuja kufanya nini?”
“Hakuniambia kitu”
“Amekuleta tu!”
“Aliniambia twende kwetu”
Yule mama akamtazama Banuna.
“Mbona mwenyewe hajui amekuja kufanya nini huku?”
“Anajua” Banuna akasema kisha akabadili lugha na kusema kwa kiarabu, lakini sikuelewa alisema nini.
Mama yake akanitazama mimi tena.
“Eti mmekubaliana kuwa mnakuja huku kuoana?” akaniuliza.
“Hatukukubaliana kuwa tunakuja kuoana” nikamjibu.
“Na wala hakuwahi kukueleza jambo hilo?”
“Aliwahi kunieleza”
“Je ulikubali kwa hiyari yako?”
“Hapana, sikukubali”
“Alikuwa anakutisha?”
Hapo nikanyamaza. Sikutaka kusema ukweli kuwa alikuwa ananitishia maisha.
Yule mama alitambua mawazo yangu, akaniambia.
“Sema usifiche”
“Ndiyo alikuwa ananitisha” nikamwambia.
Banuna akanitazama kwa uso wa tadhaa.
“Alfred sema ukweli, nimekutisha mimi? Si tumekubaliana tuoane, uliniambia kuwa umenipenda?” Banuna akaniambia lakini sauti yake haikuwa na nguvu kwa vile maneno aliyosema yalikuwa ya uongo.
SEHEMU YA 14
Sikumjibu chochote. Nilikuwa nimeinamisha kichwa changu chini. Sikutaka kutazamana na macho yake.
Mama mtu akakasirika.
“Banuna, wewe muongo. Umekuja kunidanganya hapa!”
Banuna akamjibu kwa kiarabu. Pengine hakutaka nisikie uongo wake. Lakini mama yake aliendelea kuchachamaa. Wakawa wanajibizana kwa kiarabu.
Mwisho Banuna alinyanyuka kwa hasira. Sikujua aliambiwa nini. Mama yake naye akanyanyuka. Banuna alitamka neno lililomuudhi yule mama, akampiga kibao Banuna.
“Ondoka hapa fedhuli mkubwa!” Mwanamke huyo wa kijini alimwambia Banuna kwa ukali kisha akaongeza.
“Mrudishe kijana wa watu kule ulikomchukua. Mrudishe sasa hivi halafu ukome kumfuatafuata tena!”
Banuna alipopigwa kibao aliondoka huku maneno yakimtoka mdomoni.
“Sitamuacha hata ukunipiga. Nimeshampenda. Nitaendelea naye hivyo hivyo!” akamjibu mama yake na kutokomea kwenye pazia.
Yule mama alikuwa akumfuata nyuma huku akijibishana naye kwa kiarabu. Na yeye aliingia kwenye pazia hilo hilo. Sauti zao za kujibizana zikawa zinasikika kwa ndani. Baadaye kukawa kimya.
Nikajikuta nimeachwa peke yangu mahali hapo. Kwa mara ya kwanza nilianza kusikia uoga hasa vile ambavyo mwenyeji wangu aliyeambiwa anirudishe, amenikimbia kwa hasira.
Nilijua kuwa nilikuwa nimemuudhi kwa kumkana mbele ya mama yake ambaye ingawa alikuwa jini, alikuwa muadilifu sana.
Alipoambiwa na Banuna kuwa anataka kuoana na mimi, alitaka uthibitisho kutoka kwangu. Nilipopinga jambo hilo aliamua kumuonya Banuna asinifuate tena, lakini Banuna alikuwa kisoi.
Niliendelea kukaa pale kwa muda kidogo kabla ya kumuona jini mwingine mwanaume aliyenifuata na kuniambia.
“Mama ameniambia nikurudishe kwako kwa usalama, sasa inuka twende”
Niliponyanyuka akaniambia.
“ Nifuate”
Nikamfuata. Tulipita katika njia ileile tuliyopita na Banuna mpaka tukatokea ile sehemu yenye kiza. Jini huyo hakuniambia nimshike bega, hivyo ikanibidi niwe karibu naye sana ili tusipoteane. Tukaenda mpaka tukatokea kule juu ya mnara.
Yule jini akachutama na kuniambia.
“Kaa kwenye mabega yangu”
Nikakaa. Akanibeba na kuniambia nifumbe macho, nikafumba macho. Vile ananyanyuka tu, nikahisi tunaibuka juu ya bahari!
Nilifumbua macho yangu bila kuambiwa. Ilikuwa miujiza mikubwa ambayo sikupata kuiona maishani mwangu.
Yule jini alinipeleka hadi ufukweni mwa bahari, akachutama na kuniambia nishuke. Nikashuka.
Niliposhuka alichora msitari kwenye tope, akaniambia.
“Fumba macho yako halafu vuka msitari huu. Ukishavuka fumbua macho yako”
Nikaenda nyuma ya ule msitari, nikafumba macho yangu na kuinua hatua kuvuka ule msitari. Nilipofumba na nilifumbua macho na kujikuta nipo mbele ya mlango wa nyumba ninayoishi Makorora.
Niliangalia kila upande ili kujiridhisha kuwa kweli nilikuwa nyumbani ninakoishi. Nikaona ni kweli. Macho yangu hayakunidanganya.
Ilikuwa bado usiku. Na kitu kingine cha ajabu ni kuwa nguo zangu zilikuwa kavu kabisa. Nilisimama kwa muda mbele ya huo mlango nikifikiria kati ya kubisha mlango niingie ndani, au nirudi kwa Juma.
Kwa vile ilikuwa usiku, kubisha mlango ilikuwa ni vyema zaidi ila nilipata shaka kuwa naweza kuingia chumbani mwangu na kukutana na Banuna mwenye hasira.
Wazo hilo lilinifanya niamue kwenda kwa Juma. Ilikuwa ni hatari usiku ule kutembea nikiwa peke yangu lakini nilijikaza kiume. Nikatembea haraka haraka kuelekea mtaa wa pili.
Mwili ulikuwa unanisisimka kila nilipokumbuka nilivyopelekwa ujinini. Sasa niligundua kuwa Banuna alipokuja kunichukua, sikuwa na akili yangu. Nilikuwa kama niko kwenye ndoto. Lakini kwa muda ule niliorudishwa nilijiona niko sawa.
Niseme ukweli kama ningekuwa na akili yangu timamu wakati Banuna anakuja kunichukua, nisingekubali. Tungebishana sana na ningekimbia. Na yeye kwa kujua hilo ndio maana alinizuga akili.
Nilipofika nyumbani kwa Juma nilijaribu kufungua mlango, kwa vile nilipoondoka na Banuna hatukuufunga. Lakini nikaukuta umefungwa.
Nikaenda kwenye dirisha la chumba cha Juma, nikamgongea huku nikimuita.
“Juma! Juma!”
Mara moja Juma alizinduka na kuuliza.
“Wewe nani?”
“Mimi Alfred”
“Alfred?” Juma alionekana kushituka, akauliza. “Alfred si yumo humu ndani?”
“Ni mimi. Nilikuwa nimetoka, wewe ukiwa umelala”
Mara nikaona taa inawashwa.
“Alfred ulitoka saa ngapi, mbona mlango umefungwa kwa ndani?” Sauti ya Juma ikauliza kutoka ndani.
“Nifungulie, nitakueleza”
Baada ya ukimya wa dakika mbili hivi, Juma akafungua mlango wa nje.
“Ulitokaje humu ndani?”
“Tuingie ndani nikueleza”
Tukaingia ukumbini. Juma akaufunga mlango wa nje kisha tukaingia chumbani. Mimi nilikaa kwenye kiti, Juma akakaa kwenye kitanda.
SEHEMU YA 15
“Juma utashangaa nikikueleza kuwa Banuna alikuja kunichukua huu usiku na kunipeleka kwao ujinini chini ya bahari!” nikamwambia Juma.
“Unasema kweli Alfred?”
“Huwezi kuamini Juma lakini hivi ninavyokwambia ninatoka ujinini”
“Alikuja kukuchukua saa ngapi?”
“Sijui ilikuwa saa ngapi lakini alinipeleka baharini, tukazama chini ya bahari na kukuta mji wao”
“Acha bwana!. Mji uko chini ya bahari!”
Hapo nikamueleza Juma jinsi nilivyoondoka na Banuna, tulivyozama chini ya bahari na kutokea katika mji wa majini. Pia nilimuelezea yale yaliyotokea wakati tulipokuwa ndani ya jumba la majini hao lenye mnara mrefu.
“Mama yake amekataa msioane?” Juma akaniuliza baada ya kumueleza kisa kizima.
“Amekataa. Nafikiri yule mama alitaka nikubali mwenyewe na sio kulazimishwa kama anavyotaka Banuna”
“Sasa itakuwaje, kwa maana kesho ndio napata mshahara ambao tumepanga nikupe uende Zanzibar?”
“Banuna alipokatazwa asinifuate, alisema kwa kiburi kuwa atanifuata. Sasa sijui itakuwaje!”
“Kama mama yake amemkataza, unadhani anaweza kuendelea kukufuata kweli?”
“Amesema ataendelea”
“Labda amesema kwa hasira tu”
“Siwezi kujua. Na hata alipoambiwa anirudishe huku alikataa. Nimerudishwa na jini mwingine”
“Sasa unaweza kwenda Zanzibar kesho lakini Banuna akawa hana shughuli na wewe tena. Hapo ni sawa na kuharibu pesa bure. Au unaweza usiende lakini keshokutwa ukaona amekufuata”
“Hapo ndipo penye utata”
“Sasa tusubirishe kwanza tuangalie. Kama atakutokea tena utakwenda”
“Sawa”
Nikaendelea kuzungumza na Juma hadi asubuhi kwani hatukulala tena.
Kutoka siku ile ulipita mwezi mzima sikumuona Banuna. Hapo nikapata uhakika kuwa Banuna alishaamua kuachana na mimi kwa sababu haikuwa kawaida yake kupitisha hata wiki moja bila kunitokea.
Ile hofu niliyokuwa nayo ya kupata vitisho vya Banuna, sasa ikaniondoka. Nikaamua kurudi chumbani kwangu.
Maisha sasa yakawa ya utulivu na ya amani. Siku moja nilipata barua ya kuitwa katika kampuni moja ya ulinzi ambako nilikuwa nimeomba kazi. Nikaenda. Nilifanyiwa usaili na baadaye niliambiwa niende kesho yake kuanza kazi.
Siku iliyofuata nilipokwenda niliajiriwa kazi ya ulinzi. Nilipewa sare za kampuni nikavaa a kupelekwa kwenye duka la muasia mmoja kuanza kazi ya ulinzi wa duka hilo.
Nilikuwa naingia kazini saa mbili asubuhi na kutoka saa kumi jioni. Nikishakunywa chai asubuhi ndiyo nashinda hadi saa kumi jioni ninapotoka na kurudi nyumbani. Kuanzia saa kumi anaingia mlinzi mwingine ambaye anaendelea hadi asubuhi ya siku ya pili.
Zamu hizo zilikuwa zinabadilika kwa wiki. Anayeingia mchana anabadilishiwa zamu na kuingia usiku.
Katika juma lile la kwanza nilikuwa nimepangiwa zamu ya mchana. Hii ilikuwa nzuri kwani iliniwezesha kulala nyumbani kuliko zamu ya usiku ambapo unalazimika kukesha macho usiku kucha.
Siku tatu baada ya kuanza kazi yangu alikuja msichana mmoja wa kiarabu pale dukani. Akanunua vitu vingi. Alipokuwa anatoka nikamsaidia boksi moja na kumpelekea kwenye gari lake. Akanishukuru kisha akanipa shilingi elfu ishirini kama bahashishi yangu.
Kwanza sikuelewa pesa hizo alizonipa zilikuwa za nini. Nikawa nimeduwaa na kumuangalia ili aniambie pesa hizo zilikuwa za nini.
“Ni zako. Nimekupa kwa msaada wako” akaniambia huku akifungua mlango wa gari hilo na kujipakia.
Kwa kweli nilimshangaa msichana huyo kwa kunipa pesa zote hizo kwa msaada mdogo tu. Hata hivyo nilishukuru na kuzitia mfukoni. Msichana huyo akaliwasha gari na kuondoka.
Nikarudi kwenye kiti changu kilichokuwa kando ya mlango wa duka hilo, nikaendelea na kazi yangu. Kabla ya wiki ile kumalizika yule msichana alikuja tena pale dukani. Kwa bahati mbaya vitu alivyotaka kununua havikuwepo. Alipotoka akanipa tena shilingi elfu ishirini kisha akaenda kwenye gari lake na kuondoka.
Siku nyingine tena wakati niko katika zamu ya mchana, msichana huyo akaja tena Nakumbuka ilikuwa saa kumi wakati nabadilishana zanu na mlinzi mwenzangu. Msichana huyo hakushuka kwenye gari. Alisubiri mpaka wakati naondoka akanifuata na gari na kusimama karibu yangu. Na mimi nikasimama.
Msichana huyo alitoa kichwa kwenye dirisha la gari na kuniambia.
“Kijana hujambo?”
“Sijambo. Habari yako?”
“Nzuri. Unarudi nyumbani?”
“Ndiyo,ninarudi nyumbani”
“Ingia garini nikupeleke. Nina mazungumzo na wewe!”
“Una mazungumzo na mimi?” nilimuuliza kama vile sikumsikia vizuri.
“Mbona umeshituka?”
“Hapana, sikushituka”
“Basi ingia garini”
Nikafungua mlango wa upande wa pili wa dereva na kujipakia. Msichana akalindoa gari.
INAENDELEA

