AZIZA WA FACEBOOK
ONYO: Wakubwa tu, kuanzia Miaka 18, ndio wasome hii Hadithi
Sehemu ya 1
Najisikia nimechoka sana, nimechoka sana kwa sababu nilikuwa nimetoka
kucheza mpira uwanjani huku nikiwa nimechafuka kupita kawaida. Ninapofika
nyumbani, ninaoga na kisha kuchukua simu yangu kwa ajili ya kuangalia
updates za facebook, sikukuta hata meseji
moja zaidi ya notification tu, tena wala hazikuwa nyingi. Nilichokifanya ni kuanza
kuzugazuga hapa na pale na kisha kutulia. Mara ghafla nikaona namba moja
nyekundu kwenye sehemu ya meseji, kulikuwa na meseji imeingia,
nilichokifanya, nikaifungua na kuanza kuchati na mtu huyo huyo.
EDUADO: Mambo vipi Shahruk Khan.
MIMI: Hahahha! Poa. Inakuwaje wewe mtu.
EDUADO: Kama kawa. Nilikuwa nakusubiri sana hewani. Nilikuwa na mzuka na wewe ile mbaya.
MIMI: Duh! Mzuka na mimi! Kuna nini tena?
EDUADO: Kuna bonge la kazi hapa. Unataka?
MIMI: Kwa nini nisitake? Nipe mawasiliano yao niandike barua ya kuomba kazi fasta.
EDUADO: Hahahaha! Kaka unakosea. Niliposema kazi sikumaanisha hiyo.
MIMI: Wewe ulimaanisha ipi sasa?
EDUADO: Kazi moja hivi. Kazi ambayo watu wengi wameishindwa hasa masharobaro.
MIMI: Hahahaha! Itakuwa kubeba zege hiyo watoto wa mama hawaiwezi. Mimi naiweza, hebu niambie ni jengo gani.
EDUADO: Sio kazi ya kubeba zege. Kuna mtu nataka umfanyie kazi.
MIMI: Mtu gani?
EDUADO: Kuna mrembo fulani nipo nae hapa UDSM ni mkali ile mbaya. Yaani mkali
mpaka nashindwa kusema ukali wake unafanana na nini.
MIMI: Hebu acha masihala kaka. Kwa hiyo kama mkali mimi nifanyeje nini?
EDUADO: Huyu mrembo anaringa mbaya. Yaani mrembo ananata utafikiri akanyagi ardhi hii tunayochimbia vyoo.
MIMI: Ok! Wazuri wapo wengi na hata wenye maringo wapo wengi pia. Hebu niambie kuhusu huyo. Kwanza anaitwa nani. Nipe maelezo ya kujitosheleza na sio naanza kumtengeneza mrembo mkali kichwani mwangu ikawa ndivyo sivyo.
EDUADO: Huyu mrembo anaitwa Aziza Moody, anaishi Msasani, baba yake ni mfanyabiashara mkubwa sana aisee. Ni mrembo fulani pini…yaani ni pini sana.
MIMI: Hebu acha masihala. Sasa inakuwaje watoto wa kisharobaro wamemshindwa.
EDUADO: Huyu mrembo hafagilii muonekano, ni mrembo fulani ambaye anapenda mtu amfuate kama jinsi alivyo. Yaani kama wewe ni mtu wa chini, mfuate hivyo hivyo ila tatizo watoto wa hapa chuo wanapenda kumfuata kisharobaro kaka.
MIMI: Dah! Kwa hiyo kazi unayotaka kunipa ni ipi?
EDUADO: Umchukue huyu mtoto. Yaani ukifanikiwa, moyo wangu utakuwa mweupeeeeeee
kama theluji.
MIMI: Hahaha! Usitake kunichekesha EDUADO, hivi unamkumbuka Sikitu?
EDUADO: Sikitu yupi?
MIMI: Si yule mrembo wa mwaka jana ambaye ulikuwa unamsifia sanaaaaa kwamba
mkali kumbe wala hakuwa mkali kama ulivyokuwa ukimsifia, mbaya zaidi alikuwa anakaa mbali, Musomaaaaaa.
EDUADO: Acha na hayo, yule msahau kwani mimi mwenyewe alinitumia picha ambayo sio
yake. Ila kaka kiukweli Aziza ni mrembo mmoja mkali sana. Hapa chuo amekuwa
gumzo kila kona, vijana wengi wamechemka.
MIMI: Sasa kama wengine wamechemka mimi nitaweza vipi?
EDUADO: Hahahaha! Kaka ninakuamini sanaaaa, wewe mtu unaweza sana kuongea,
unaweza sana kuandika. Endapo kazi nikakupa na kisha ukashindwa, haki ya Mungu nitajua kweli
duniani kuna wasichana wagumu.
MIMI: Kwa hiyo kazi yako ina malipo au?
EDUADO: Ikitokea umempata, nitakupa zawadi kaka. Yaani ninachokitaka huyu mrembo
umchukue tu, basiiiiiiii. Anaringa sana, ananata sana, yaani sijui niseme vipi.
MIMI: Ila si anaringa kwa sababu mzuri?
EDUADO: Ndio. Ila yeye kazidi.
MIMI: Ila kwa sasa aisee nahisi nimepoteza kumbukumbu zangu za kuongea na hawa
watoto wa kike, sijui kama nitaweza.
EDUADO: Acha kunitania kaka. Nakuamini sana kwamba unaweza kuliko mtu yeyote
na ndio maana nikakufuata wewe. Hivi haujiulizi kwa nini sikumfuata Thomas? Thomas
kwenye kuongea mkali sana ila kwenye kuandika hakuna kitu, ila wewe, aisee una kipaji
kila kona, nafikiri hata ukimtokea kiziwi, hachomoiiiiiiiiii.
MIMI: Hahaha! Hebu acha kunipamba. Hebu niambie, huyo mrembo yupo Facebook?
EDUADO: Amejaa teleeee…yaani kajaa teleeee. Anajiita Aziza M Aziza. Ni mrembo mkali sana.
Hebu mcheki kwanza.
MIMI: Sawa.
Sehemu ya 2
Sikutaka kuchelewa, tayari kichwa changu kikaanza kujazwa na sura nyingi za wasichana
wazuri huku nikianza kuzigawanya kimakundi kwamba huyu alikuwa Aziza mwenyewe
huyu hakuwa mwenyewe. Nilikuwa namfahamu EDUADO toka tupo katika shule ya
sekondari, alipokuwa akisema msichana fulani ni mzuri, mzuri kweli japokuwa kwa
Sikitu alikuwa ameniingiza choo cha kike. Sikutaka kuremba, mara baada ya kuona
majina kadhaa, nikamfuata Eduado inbox.
MIMI: Oyaa Akshey.
EDUADO: Vipi ushampata?
MIMI: Wamekuja wakina Aziza wengi hao, mpaka wengine wanakaa India.
EDUADO: Hebu subiri.
Sikujua alikuwa akifanya nini, kwa sababu aliniambia kwamba nisubiri,
wala sikuwa na presha, nikamsubiri nione angeniambia kitu gani baada ya hapo.
Nilimsubiri kwa kipindi kama cha dakika moja hivi, akanijia tena inbox.
EDUADO: Umeiona hiyo picha yenye mdoli wa Barbie?
MIMI: Yeah!
EDUADO: Ndiye yeye huyo. Ibra huyo ni mrembo mkali ambaye sijawahi kuona.
MIMI: Acha utani.
EDUADO: Shua. Unamkumbuka Silvia tuliyesoma nae? Sasa Silvia haingii kwa Aziza.
MIMI: Acha utani kaka. Silvia haingii?
EDUADO: Kweli tena. Tena hagusi hata robo.
MIMI: Sasa mbona hajaweka picha yake, nitamjua vipi kama ni mkali.
Hebu nipe sifa kwanza manake naona picha zake kazipiga pini watu wasio
marafiki zake wasizione.
EDUADO: Kwanza mrembo ni pini sana, mrembo kwao wana mahela ya kumwaga,
chuo anakuja na gari, Verrosa moja nyeusi, mtoto anamiliki laptop aina ya
Apple ile inaayouzwa milioni tatu, mtoto anamiliki anamiliki iPhone
5 huku akisema kwamba iPhone 6 ikianza kuuzwa atataka kuanza kuitumia
kwani anapenda kwenda na wakati.
MIMI: Kaka utakuwa unanitania tu.
EDUADO: Kweli tena. Halafu kuna cha zaidi.
MIMI: Kipi?
EDUADO: Otea.
MIMI: Hebu niambie kipi?
EDUADO: Ugonjwa wako.
MIMI:Unamaanisha nini?
EDUADO: Mtoto Mpemba.
MIMI: Hahahaha! Kaka acha utani, utanifanya nimfuate sasa hivi.
EDUADO: Ndio hivyo. Mtoto ni pini sana, pini ile iliyosimama.
MIMI: Hahaha! Pini kama ya Blackberry vile.
EDUADO: Acha kaka. Mtoto ni pini zaidi ya zile za Blackberry.
Kwanza ukimuona tu, mtoto utampenda. Mavazi yake sasa…weeeeeee.
MIMI: Hebu nipe sifa zake kwa ujumla.
EDUADO: Nisikilize. Mtoto ni wa kipemba.
Ana nywele ndefu zinazomfikia chini ya mabega yake,
mtoto ana hipsi zilizopangika, hapa mashavuni mwake ana vijishimo viwili,
lipsi lainiiiii kila wakati zinang’aaaaa.
MIMI: Kingine?
EDUADO: Mtoto ana sura nyembamba, masikio hayaonekani sana,
ifuani hapa kumesimama vizuri sana, mavazi yake huwa ni suruali za jinsi kwa sana.
MIMI: Umesema anaishi wapi?
EDUADO: Anaishi Masaki.
MIMI: Halafu mimi naishi uswahilini Tandale. Umesema anamiliki simu gani?
EDUADO: Anamiliki iPhone 5.
MIMI: Halafu mimi namiliki Nokia ya Tochi. Umesema baba yake ana gari?
EDUADO: Yeah! Yeye mwenyewe analo.
MIMI: Mimi sina gari na baba yangu hana hata gari.
EDUADO: Acha kujizarau Ibra. Mtoto unang’oa huyu.
MIMI: Usijali. Ushawahi kufika kwao?
EDUADO: Yeah kaka. Kwanza hiyo nyumba yao….duh! Kuna watu wanakufuru. Kwanza bonge la nyumba. Limezungushiwa ukuta, jumba lina fensi kwa juu, ndani kuna kamera, nyumba vigae, ukiingia ndani unakutana na bwawa la kuogelea. Kuna ungo wa Dstv, kuna bustani kali ya maua mbalimbali, kuna walinzi wawili ambao wanalinda kwa bunduki kutoka Knight. Yaani wapo full.
MIMI: Ok! Mimi naishi Tandale. Nyumba yetu ndogo, haina ukuta wala fensi, haina mlinzi na kama kuogea, tunaogea bafuni na si kwenye bwawa. Mpaka hapo, nimeshamkosa.
EDUADO: Ibra. Usiniangushe. Yaani mimi lengo langu umchukue huyu mtoto tu.
MIMI: Una namba zake za simu?
EDUADO: Hapana.
MIMI: Basi ngoja nifanye mishe halafu nione itakuwaje. Ila wasiwasi wangu ule ule tu, itakuwa kama Sikitu.
EDUADO: Usijali kaka. Huyu sio kama Sikitu. Kwanza yule demu mwenyewe alinitaka nikaamua kukurushia wewe. Mimi na mrembo wa mkoa wapi na wapi. Ishi Dar tuwe tunamalizana, mambo ya mikoani haya, tigo pesa zinatumika sanaaaa. Hapa hapa Bongo ndio kuzuri, ukimtaka tu,
nauli yako sh 400 kwenda, 400 kurudi. 600 soda yako, 600 soda yake. Mwisho wa siku kwa
gharama zote ukitoa buku tano, michenji inarudi mingi mpaka mfuko unaomba poo kwa kuzidiwa uzito.
MIMI: Hahaha! Umeonaeeeee. Hakuna gharama kabisa. Ila poa, usijali. Ngoja nimtumie friend request halafu nianze kumfanyia uninja. Ila niandalie zawadi yangu.
EDUADO: Usijali kaka. Wewe fanya yako, ukimaliza, niache nami nifanye yangu. Au sio?
MIMI: Poa. Mia mia. Ngoja nianze kazi.
EDUADO: Shwari. Ngoja nifanye yangu. Nataka nimfuate mtoto Magreth hapa.
MIMI: Ndio yupi huyo?
EDUADO: Si yule wa facebook wa kipindi kileeeee.
MIMI: Kwani ushang’oa?
EDUADO: Chezea mimi wewe. Mimi noma…kama ni wembe basi Gilette.
MIMI: Sasa mbona hujamkata Aziza kama ni Gilette.
EDUADO: Aziza ana chembechembe za chuma. Ningemkataje? Huyo nakuachia kama wewe mwenye yale maji ya kuyeyushia vyuma ndio utakwenda nae sawa.
MIMI: Basi poa. Acha nikufanyie kazi yako mkurugenzi. Kazi hii niliachana nayo zamani sana ila kwa ajili yako, navaa gwanda nikukamilishie halafu nisepetue.
EDUADO: Mia mia.
Sehemu ya 3
Hapo nikatulia kwanza. Nikaanza kujifikiria ni kwa jinsi gani nilitakiwa kuanza kumfuata msichana Aziza. Kitu ambacho kilikuwa kikiniumiza kichwa changu kwa wakati huo ni kwamba hata Aziza mwenyewe sikuwahi kumuona kwa hiyo niliogopa kuuziwa mbuzi kwenye kiroba kama ilivyokuwa kwa Sikitu. Ngoja nikupe kijistori changu na huyu Sikitu.
Eduado alinifuata inbox na kuniambia kuhusu Sikitu, alimsifia na kumpamba sana, alinifanya nivutiwe nae sana na yeye alitaka nimchukue, nikasema poa. Mzee nikaanza mishemishe zangu kama Michael Scotfield wa Prison Break na kweli ndani ya wiki mbili, mtoto akawa mikononi mwangu. Unajua jinsi mtu anavyokwambia kwamba msichana mzuri hata kama wewe mwenyewe haujamuona unaanza kumtengeneza msichana wako kichwani, hivyo ndivyo nilivyofanya kwa Sikitu. Nikamtengeneza Sikitu wangu kichwani, kumbe nilikuwa namuumba Sikitu wa tofauti bila kujua. Siku aliponitumia picha yake inbox niione mara baada ya kumlazimisha sanaaa, akanitumia. Alikuwa mrembo lakini hakuwa na urembo kama ambao Eduado aliniambia. Nikaachana nae.
Sikitu hakukoma, chating zangu nzuri za inbox za maneno ya hapa na pale alikuwa akizipenda sana, hivyo alitaka tuendelee kuchati. Haikuwezekana tena, nilimkatia maguu mara baada ya kuniambia kwamba anaishi Musoma, mbaya zaidi huku Dar hakuwa hata na ndugu kwa hiyo hakuwa na ndoto za kuja Dar, sasa mimi ningeonania nae wapi? Yaani nisafiri mpaka Musoma kwa ajili yake? Niliona kuwa suala gumu sana kufanyika. Basi ndio hivyo, tukapotezana potezana na hatimae mapenzi kutoweka, siku hizi simuoni, bila shaka, kaniblock.
Baada ya miezi miwili, leo Eduado kaja na mpya, kaja na mrembo mpya ambaye wala sijawahi kumuona, huyu anaitwa Aziza. Sikutaka kufanya vitu kwa presha sana, nilichokifanya ni kumuomba urafiki na kisha kuanza kusubiria majibu. Kila siku nilipokuwa naingia facebook, hakuwa amenikubalia, sikuwa na shaka, niliendelea kusubiria zaidi na zaidi na baada ya siku mbili, akakubali kuwa rafiki yangu, furaha iliyoje? Hapo ndipo nilipoamua kuuanza mchezo wangu, mchezo ule ule ambao ulimfanya Sikitu kuchanganyikiwa kwangu, ila kwa hapa, kutokana na sifa ambazo niliambiwa na Eduado, ilinipasa nitumie mbinu kubwa zaidi, mbinu ambazo zingeendana na uzuri wake, mtoto wa kipemba bwana, hakutakiwa kufuatwa kikawaida, nami nikaanza kumfuata kipemba kipemba na mapenzi ya Kihindi….mtu mzima nikawa najiona kama Shahruk Khan vile.
****
Mtu mzima nikaingia kazini kwa ajili ya kuanza kazi yangu ambayo nilikuwa nimepewa ya kuhakikisha kwamba mtoto wa Kipemba, Aziza anakuwa wangu. Ni kweli kwa mambo ambayo alikuwa amenieleza Eduado yalikuwa yamekwishanitenga kwa kiasi kikubwa sana kutoka kwa Aziza lakini ilitakiwa pia nifanye yangu katika kipindi hicho.
Kitendo cha Aziza kuukubali urafiki pamoja nami kilionekana kuwa kitu kizuri sana, kwa hiyo nilichokifanya nikajifanya bonge la bwege, nikamfuata kwa wall yake na kuandika ‘Asante A’ na kisha kusikilizia.
Kweli, kama alivyosema Eduado ilikuwa vile vile, mrembo hakuiLIKE asante yangu wala kuitolea comment, nikaona poa, vyote hivi ni mwanzo wa kumbukumbu zangu nitakazompa hapo baadae. Kwa upande wa Eduado, hakutaka kujishika, kila siku alikuwa akinisumbua tu kwa inbox.
EDUADO: Kaka vipi?
MIMI: Kuhusu nini?
EDUADO: Mtoto. Hujaniambia chochote kile. Umefanikiwa au?
MIMI: Wewe umeniambia mambo mengi kuhusiana na huyu mrembo, unadhani ningeweza kumamilisha ndani ya siku tatu?
EDUADO: Hapana. Nilikuwa nauliza manake nimeona hapa sasa hivi u rafiki yake.
MIMI: Yeah! Ni rafiki yangu ila kila kitu kinatakiwa kufanywa kimahesabu.
EDUADO: Usiniangushe basi Sharukh Khan.
MIMI: Hilo usijali.
Katika kipindi hicho nilikuwa nafikiria mambo mengi sana, huyu mtoto kwangu alionekana kuwa na pozi ajabu, yaani nilikuwa nikizipitia post za kizushi alizokuwa akiziweka, watu walikuwa wakicomment halafu yeye hatokei. Hata kama kaweka picha ya mdoli, watu walikuwa wakicomment halafu yeye hatokei na mbaya zaidi kulikuwa na watu wengi wanaolike na kucomment jambo lililonifanya kugundua kwamba kuna siku huyu msichana alikwishawahi kuweka picha na hivyo wanaume kujua ni mzuri na kisha kuzitoa.
Bado kiu yangu ilikuwa ni kuwasiliana na Aziza tu ambaye alionekana kuwa mtu wa mapozi sana. Sikujua ningeanzia wapi ila nilichokifanya ni kuanza kumtumia meseji nione kama angeijibu au kuipotezea.
2
MIMI: Mambo!
Niliituma meseji hiyo, siku ya kwanza, ya pili, ya tatu mpaka wiki hadi mwezi lakini meseji ile moja haikujibiwa, mbaya zaidi nilikuwa namuona yupo hewani. Sikukoma kidume mimi, bado nilikuwa nikimtumia meseji za kumsalimia lakini hali ilikuwa vile vile, hakujibu.
Mtu mzima nikaona naumbuka, kama nilikuwa naitwa Sharukh Khan basi ilibidi niwaonyeshe watu kwamba hawakukosea kuniita jina hilo, nilitaka kuwaonyeshea dhahiri kwamba mama yangu alikuwa mtu wa Tanga, kule ambapo mapenzi yalikuwa yamenogeshwa kwa kuwekewa makorokocho. Nilichoanza kukifanya ni kuanza kumtag picha. Hapa ni lazima ugundue, picha ambazo nilikuwa nikimtag ni zile ambazo zilikuwa na muonekano wa kimapenzi tu. Picha ambazo zilikuwa zikiwaonyesha wapenzi wakibusiana na kukumbatiana, ndizo ambazo nilikuwa nikimtag, tena yeye peke yake.
Hahaha! Ule ukaonekana kama ujinga vile kumbe kwa wakati huo nilikuwa na target zangu kichwani. Niliendelea na mtindo ule ule mpaka siku ambayo akaonekana kuchoka na kukasirika, kwa mara ya kwanza akaja inbox, ila sio kiamani kama nilivyotaka, alikuja kibifu.
AZIZA: Naomba usiwe unanitag mapicha yako.
Niliisoma meseji ile. Kwanza nikacheka, kilichonifanya kucheka ni kwa kumuona kwamba alikuwa msichana mjinga sana, kitendo cha yeye kuniandikia meseji kilionekana kuwa kama kosa kubwa sana, nilichokifanya, nikaanza kuandika meseji ndefu, meseji ambayo ingemfanya kunijibu, meseji ambayo isingemfanya kubaki kimya.
MIMI: Kuna vitu kadhaa Aziza itakupasa uelewe na ninatumaini vitakuongoza katika maisha yako yote. Jitahidi kuishi lakini kamwe usiwe mbinafsi. Unapopata kitu, usitake kukaa nacho, jaribu kuchangia pamoja na wenzako. Unapopata chakula, jaribu kumwangalia yule asiye na chakula na kumgawia, milele atakushukuru kwa ulichomfanyia siku moja tu alipokuwa na njaa. Unapomuona mtu hana nguo, mgawie nguo na ataendelea kukushukuru maisha yake yote. Unaniona mimi, mimi si mbinafsi hata mara moja, katika maisha yangu nimekuwa nikiwapa watu vitu fulani vitu ambavyo hawana katika maisha yao, nikakuangalia wewe, nikakuona kwamba u masikini sana, ukijiangalia, unajiona kuwa tajiri, mwenye fedha labda, lakini bado ni masikini, masikini wa kitu kimoja ambacho ulihitaji mtu mwenye kitu hicho akusaidie, nikakusaidia lakini unaonekana kuukataa msaada wangu. Kuwa makini Aziza, mara nyingine msaada huja mara moja na kupotea, unapoutafuta, inawezekana usiuone tena.
Kwanza nikashusha pumzi nzito, nikaiangalia meseji ile na kisha kuirudia rudia mara nyingi nyingi na kisha kuituma. Niliiona kuwa meseji kali ambayo isingemfanya kubaki kimya kwa kutaka kujua ni kitu gani ambacho alikuwa amekosa katika maisha yake, kilichonifurahisha, akatuma meseji. Kuna nini tena? Meseji ya pili hiyo, hakujua kwamba ndio mwanzo wa chating yetu.
AZIZA: Umemaanisha nini?
MIMI: Nimemaanisha kwamba wewe ni masikini. Tena yule fukara kabisa. Hiyo ndio maana yangu.
AZIZA: Sijakuelewa.
MIMI: Hebu isome vizuri hiyo meseji, utaielewa tu.
AZIZA: Nimeirudia zaidi ya mara tano, sijaielewa, naomba uniambie umemaanisha nini.
MIMI: Nikuulize kitu kimoja?
AZIZA: Niulize.
MIMI: Unaweza kugundua ni umasikini wa aina gani umekuwa nao?
AZIZA: Hapana na ndio maana nikauliza.
MIMI: Inawezekana ukawa na magari, nyumba na fedha ila bado ukawa masikini, unakubaliana nami?
AZIZA: Hapana.
MIMI: Kwa sababu gani?
AZIZA: Mtu ana kila kitu, atakuwaje masikini.
MIMI: Hahahah! Aziza. Ukisema hivyo unakosea. Kuwa na kila kitu haimaanishi kwamba wewe si masikini. Unaniruhusu nikuulize kitu?
AZIZA: Niulize
MIMI: Unaamini katika fedha?
AZIZA: Yeah!
MIMI: Fedha inaweza kukupa kila ukitakacho?
AZIZA: Yeah!
MIMI: Unakosea sana Aziza.
AZIZA: Unapokuwa na fedha unanunua gari ulitakalo, unanunua chakula, unanunua nyumba na mambo mengine. Kwani nimekosea?
MIMI: Umepatia. Ila unavyoona kila mtu mwenye fedha huwa na furaha?
AZIZA: Inawezekana.
MIMI: Umekosea. Umekwishawahi kuwasikia wale matajiri wanaojiua?
AZIZA: Yeah!
MMI: Sasa wamekosa nini wale katika maisha yao? Wana fedha, wanaweza kununua kila kitu, wana magari, wanaweza kwenda sehemu yoyote ile. Ila swali linakuja kwa sababu gani wanajiua?
AZIZA: Mmmh! Sijui.
MIMI: Hahaha! Jibu rahisi sana. Walikosa furaha, amani, wakakosa mapenzi na mambo mengine. Unapokuwa na fedha, utanunua gari ila kumbuka hautoweza kununua furaha, unapokuwa na fedha utaweza kumnunua msichana mtaani lakini ukashindwa kununua mapenzi. Umenipata hapo?
AZIZA: Kidogoooo.
MIMI: Yeah! Kila mtu hunipata kidogo, ila tukiendelea kuchati, utanipata sana tu. Utaniruhusu niwe nachati nawe kwa ajili ya kukuambia mengi usiyoyajua?
AZIZA: Yeah! Ila huwa siwi hewani muda wote.
MIMI: Hilo si tatizo. Unachotakiwa ni kunishtua kila unapokuwa hewani. Utakwenda kufahamu mengi ambayo haujayajua. Kwani unaishi wapi?
AZIZA: Nipo Masaki Dar es Salaam.
MIMI: Ndio maana.
AZIZA: Kwa nini?
MIMI: Usijali. Mtaa unaokaa ndio nitakaoanza nao siku tukianza kuchati. Kwa sasa nahitaji kusoma, naomba uniruhusu niondoke.
AZIZA: Ila pleeeaseeee naomba uniambie.
MIMI: Sijakataa. Nitakwambia tu wala usijali. Wewe ni rafiki yangu, pamoja kuwa na kila kitu, yakupasa kupata vitu vingine ambavyo haupaswi kuvinunua. Nitakwambia namna ya kuvipata na inawezekana hata marafiki zako wakakushangaa.
AZIZA: Mmmh!
MIMI: Usigune. Huo ndio ukweli. Usiku mwema Aziza.
AZIZA: Nawe pia.
Sehemu ya 4
Kuna nini tena? Nilichokifanya ni kutoka hewani mpaka saa sita ndio nikaingia tena, Aziza hakuwepo, nikamtafuta Eduado, nikamuona, hata kabla sijamtumia meseji, akaniwahi.
EDUADO: Vipi Sharukh Khan. Imekuwaje au bado?
MIMI: Kwisha habari yake. Anacheza na mwanasaikolojia nini.
EDUADO: Imekuwaje tena?
MIMI: Wewe usijali. Cha msingi andaa zawadi yangu.
EDUADO: Umeanza kufanikisha?
MIMI: Ndio maana yake. Unajua ukimjua mpinzani inakuwa rahisi sana.
EDUADO: Dah! Wewe noma kaka. Yaani hii kazi nimewapa watu saba, naona wengine wanambwela tu, wananiambia kila wakimtumia meseji dogo hajibu.
MIMI: Hahahaha! Hata mimi ilikuwa hivyo hivyo. Nilivyoona anashindwa kujibu, nikatumia plan B. Hapo ndipo nilipompoteza na kuchati nae sana.
EDUADO: Kwa hiyo ulichati nae?
MIMI: Yeah! Tena mimi ndiye nimemkatisha. Chezea mimi wewe.
EDUADO: Hahahah! Ebwana wewe nomaaaaa….sasa hata kukutambulisha kwa mrembo wangu mwingine naogopa.
MIMI: Wewe si ulinipa kazi kaka? Hakuna tatizo. Kazi inafanyika taratibu.
EDUADO: Duh! Kaka nashukuru sana kwa kunisikiliza. Natumaini mtoto ataeleweka tu.
MIMI: Amekwishaeleweka. Dogo amekwishaeleweka.
EDUADO: Hahahah! Basi poa sana, nimefurahi sana.
MIMI: Usijali kaka…hug.
EDUADO: Poa.
Kila kitu kikaonekana kuwa juu ya mstari, meseji moja ambayo alikuwa amenitumia ikaonekana kubadilisha kila kitu. Ile meseji ndio ambayo nilikuwa nikiitaka kuiona na kweli aliituma. Chatting zikawa zimeanza, kwa Aziza, nilihitajika kuwa makini sana kupita kawaida kwani kwa kufanya vile nilikuwa na uhakika wa kumchukua ili kumuonyeshea Eduado kwamba nilikuwa Sharukh Khan.
****
Sikutaka kuleta shobo tena kwani tayari nilimuona kuku kuwa wangu kwa hiyo sikutakiwa kumshikia manati kwa kuamini kwamba jioni ikifika mwenyewe atarudi bandani. Nilipoingia hewani siku iliyofuatia, msichana Aziza alikuwepo, kajaa tele ila mtu mzima nikaamua kuchuna. Katika hili ngoja nikwambie kitu kimoja rafiki yangu hasa mwanaume kama mimi. Unapoona kwamba kuna msichana fulani unampigia sana misele facebook, hautakiwi kila wakati umuanze wewe tu, sometimes unamchunia uone je ataweza kukutumia meseji au la. Ukiona kwamba kakutumia, basi jua kwamba anautambua mchango wako na hata kwenye ile mishemishe yako anaonekana kuifurahia. Ila ukiona nae anakaa kimya, mtu mzima poteza kwani si unajua warembo wapo wengi! Inawezekana haujapangiwa kuwa na huyo.
Nilipomuona Aziza hewani, nikamchunia kana kwamba sijamuona huku nikiamini kwamba yeye ndiye alipaswa kunitumia meseji. Ila katika kipindi hiki hasa siku ya leo, meseji zilikuwa zikiingia nyingi nyingi hasa kutoka kwa marafiki zangu wengine, bahati nzuri nilikuwa natumia kompyuta hivyo ilikuwa rahisi kuwajibu.
IBRA: Mambo vipi kaka!
MIMI: Poa. Ni aje mkuu?
IBRA: Kama kawa. Upo wapi?
MIMI: Nipo gheto aiseee nimesizi tu si unajua kijimvua nje kinazingua.
IBRA: Yeah! Hilo kweli kaka. Hivi unamuona mtu wangu hapo hewani?
MIMI: Nani?
IBRA: Tina.
MIMI: Dah! Hapa namuona kwa kuotea, mara anakuja mara anatoka. Kama vipi mcheki kwa whatsapp.
IBRA: Kwani yupo huko?
MIMI: Yeah!
IBRA: Dah! Basi nafikiri kule atakuwa kaniblock mtu mzima. Simuoni kabisa.
MIMI: Hahahah! Kaka pole sana. Umeblockiwa…hahaha! Tatizo lako uliremba sana kwa kujifanya umeoa, full mauhakika.
IBRA: Unajua nini kaka, kila siku naamini kwamba mwenda pole ndiye mla nyama.
MIMI: Usitake kuniambia hivyo. Wahenga wengine walikuwa wakizingua tu, kidogo naweza kumuamini yule aliyesema chelewa chelewa utakuta mwana si wako. Si kwamba unamuona kinyonga anatembea taratibu ukajua hata yeye anajua kwamba anatembea taratibu, mwenzako pale anajiona anakimbia kwa kasi sana. Hahahaha! Na bado…atakublock mpaka whatsapp.
IBRA: Akiniblock na huko tena, nitamuona katili sana kaka.
Huku nikiendelea kupiga stori na Ibra, mara Emmanuel Solo nae akaingia kwa inbox yangu. Sikuwa na jinsi, nilikuwa nachati nao huku nikimuona Aziza hewani ila nami nilikuwa nimemlia pini tu.
SOLO: Kaka.
MIMI: Niambie.
SOLO Upo wapi?
MIMI: Nipo gheto. Wewe upo wapi?
SOLO: Nipo Morogoro kama kawaida yangu.
MIMI: Duh! Wewe noma. Ndani ya wiki moja umetembea mikoa mitatu. Big Up mkuu.
SOLO: Kutafuta kaka. Maisha kutafuta. Si unamuona hata Ndimanga Hassan, anatembea zaidi ya mikoa kumi kwa mwezi, hatutakiwi kukaa sehemu moja. Hadithi imeishia wapi?
MIMI: Ipi? Zipo nyingi tu.
SOLO: Ile ya yule msichana mwimbaji wa kwaya aliyekuwa amepanga mauaji kwa mvulana ambaye alikuwa amemkataa kanisani na kuamua kutaka kumuua nchini Zambia.
MIMI: Bila shaka unaizungumzia HER HIDDEN FACE, si ndio?
SOLO: Yeah!
MIMI: Ile ipo sehemu ya tano. Inaendelea kama kawa.
SOLO: Basi poa. Ngoja niitafute niendelee kuisoma.
EDUADO: Kaka
MIMI: Niambie kijana.
EDUADO: Mtoto leo kaja chuo aisee kapendezaje!
MIMI: Acha utani.
EDUADO: Sure. Mtoto ni noma kaka. Mtoto mrembo mpaka anajishangaa. Namuona hewani, ushatupia mambo?
MIMI: Hapana. Nangoja anianze, asiponianza nampotezea tu kwani si lazima kivile kuchati nae na kumshobokea.
EDUADO: Ila kaka fanya mambo bhana. Huyu mrembo sitaki umkose kabisa.
MIMI: Usijali kaka. Huyu mdogo mdogo mwisho wa siku utamkuta gheto kapumzika. Chezea Tandale wewe.
EDUADO: Hahaha!
AZIZA: Mambo!
MIMIl Mabaya.
AZIZA: Ubaya wake?
MIMI: Naumwa.
AZIZA: Nini tena jamani?
MIMI: Maralia. Yaani mbu mmoja tu jana chumbani kwangu ndio alisababisha majanga yote haya.
AZIZA: umekunywa dawa?
MIMI: Hapana.
AZIZA: Kwa nini sasa jamani?
MIMI: Naogopa sana dawa Aziza. Labda uje uninyweshe kinguvu.
AZIZA: Dah! Pole sana Ibra. Nitakuombea kwa Mungu akuponye.
MIMI: Asante sana. Nitafurahi sana.
AZIZA: Aya nishakushtua. Hebu niambie kuhusu vitu ulivyokuwa ukiniambia.
MIMI: Tatizo lako unajiamini sana Aziza halafu unafanya makosa sana kila unapoona kwamba fedha ndio kila kitu. Yaani haujifikirii kama kuna watoto wa matajiri ambao wanaumwa sana mpaka wanakufa, kama fedha ni kila kitu si wangepona.
AZIZA: Nafahamu.
MIMI: Basi kama unafahamu, fahamu pia kuna kitu ambacho ni kila kitu na si fedha kama unavyofikiria.
AZIZA: Kipi tena.
MIMI: Mungu ndiye kila kitu katika maisha yetu. Bila Mungu, huwezi kuwa na furaha hata kama una fedha, bila Mungu huwezi kupona ugonjwa wako hata kama una fedha na kutibiwa na madaktari wakubwa duniani. Umenipata?
AZIZA: Ndio nimekupata.
MIMI: Au hadi hapo unataka kubishana tena?
AZIZA: Hapana. Ila unaonekana kuwa na hekima sana Ibra.
MIMI: Yeah! Unajua wakati mwingine yatupasa kuutambua ukweli. Hatutakiwi kuamini sana katika fedha. Ila achana na hayo. Wewe ni mama wa nyumbani, mwanafunzi wa sekondari au mwanafunzi wa chuo?
AZIZA: Naonekaje?
MIMI: Profile picha yako ni ya mdoli, sasa nitajua unaonekanaje?
AZIZA: Hahaha! Usijali. Mimi ni mwanachuo.
MIMI: Unasoma wapi?
AZIZA: Mlimani
MIMI: Unasomea nini?
AZIZA: Sheria.
MIMI: Afadhali.
AZIZA: Afadhali ya nini tena?
MIMI: Uje kuwa mwanasheria wangu baadae katika kampuni yangu.
AZIZA: Hahahah! Utaweza kunilipa?
MIMI: Kwa nini nisiweze? Nitakuwa na fedha mbayaaaaaaa….nitamiliki magari ya kifahari na majumba makubwa sana….lol
AZIZA: Yote ni mipango ya Mungu ila napenda ulivyoongea kwa sababu unaonekana una imani ya kupata hivyo, cha msingi yakupasa kujituma tu na kumtanguliza Allah kwa kila kitu. Naomba nikuulize swali.
MIMI: Usijali. Uliza.
AZIZA: Unaishi wapi?
MIMI: Tandale kwa Mtogole.
AZIZA: Kule kwenye wezi wengi na wakabaji?
MIMI: Si wezi wengi tu, kule kunapodharaulika na watu wenye fedha kama nyie.
AZIZA: Hahaha! Usiseme hivyo bwana. Ila mbona umedanganya?
MIMI: Nimedanganya nini?
AZIZA: Kwenye profile lako. Umeandika unaishi Romania. Ulikuwa unataka kujipaisha nini upate wanawake?
MIMI: Hapana Aziza. Hiyo imekuja yenyewe tu.
AZIZA: Kivipi?
MIMI: Nilikuwa nataka kupatambulisha kama home kwetu ni Tandale. Ila nilipokuwa nikiandika Tandale, haikuwa ikitambulika kama ilivyokuwa sehemu nyingine. Matokeo yao wao kama facebook wakaniletea Tandalesti mji fulani kutoka Romania, nikaona sio kesi, nikakubaliana nao, ila ukiangalia kwa makini, Tandale imetokeza katika jina hilo.
AZIZA: Yeah! Nimeona. Hebu naomba uniambie mengi kuhusu Tandale.
MIMI: Kama yapi unataka kufahamu?
AZIZA: Mazingira, watu wa huko na mambo mengine.
MIMI: Tandale kama Tandale mazingira yake mazuri sana, watu full kuyafurahia maisha kama kawa. Kuna watoto wazuri, watoto ambao wanajitambua wao ni nani na kipi cha kufanya maishani mwao. Kuna mambo ya Rusha Roho usiku, yaani kwa kifupi kuhusu maisha, huku tunakula sana bata kuliko kwenu pa kulala saa moja.
AZIZA: Hahaha! Kwani huko kwenu huwa mnalala saa ngapi?
MIMI: Huwa nikiwa mgonjwa sana, nawahi kulala kama saa saba hivi.
AZIZA: Saa saba?
MIMI: Yeah! Ila nikiwa si mgonjwa, mpaka adhana iadhiniwe. Watu tunatransform usiku kuwa mchana na maisha yanasonga.
AZIZA: U must be kidding me Ibra.
MIMI: Huo ndio ukweli Aziza. Siwezi kukutania.
Unaona jinsi mawasiliano yetu yalivyokuwa yakienda? Hapo ndipo nilipokuwa napataka sasa. Nilikuwa namletea sana ucheshi lakini mwisho wa siku kuna kitu nilikuwa nakihitaji kutoka kwake, namba ya simu tu. Unajua katika maisha ya kuchati facebook huwa yanachosha sana, kuna kipindi fulani automatically unatokea kummisi mtu fulani na ungependa sana awe hewani lakini hayupo hewani, unapokuwa na namba ya simu, inakupa wakati mzuri wa kumsikia na kumjulia hali katika kipindi chochote ambacho ungependa kumsikia.
Ucheshi ndio ulikuwa kawaida yangu ila katika kipindi hiki nilikuwa nataka kuuleta ucheshi mpaka katika maandishi. Aziza akaonekana kulifurahia hilo, akaonekana kuanza kunikubali japokuwa hatujawahi kuonana hata siku moja. Nilikuwa bize na chatting na Aziza, sikutaka kuwasiliana na mtu mwingine katika kipindi hicho japokuwa nilimuona Eduado, Ibra Akilimia na Emmanuel Solo walikuwa wamenitumia meseji.
Nilikuwa nikijitahidi sana kumuingiza Aziza kwenye himaya yangu, yaani aingie bila kupenda na mwisho wa siku kila kitu kiwe poa sana. Sikujali alikuwa akiishi wapi, sikujali na mimi nilikuwa nikiishi wapi, kitu ambacho nilikuwa nikikiamini ni kwamba mapenzi wala hayakuwa na hiyana, yalikuwa hayabagui watu kama tulivyo wanadamu.
AZIZA: Nikuulize kitu.
MIMI: Niulize tu.
AZIZA: Unasoma?
MIMI: Hapana.
AZIZA: Unafanya kazi?
MIMI: Hapana.
AZIZA: Sasa unafanya nini?
MIMI: Nipo nipo nyumbani. Nilisoma kidato cha kwanza, sikuwa na fedha za kuniendesha kielimu, nikaachana nayo mpaka sasa hivi. Kuna kipindi nilipata vijisenti mara baada ya kubeba sana mizigo Tandale sokoni, nikaenda kusoma English Course.
AZIZA: Kwa hiyo haufanyi kazi?
MIMI: Yeah! Sifanyi kazi.
AZIZA: Unafanya kitu gani kingine?
MIMI: Sifanyi chochote kile.
AZIZA: Ila niliona kama unaandika hadithi! Au majina yamefanana?
MIMI: Yeah! Huwa ninazipost tu.
AZIZA: Hadithi zile huwa unaandika wewe?
MIMI: Hapana.
AZIZA: Sasa huwa anaandika nani?
MIMI: Anaandika baba na kisha mimi kuzichukua na kuziweka facebook.
AZIZA: Unanidanganya Ibra.
MIMI: Nikudanganye ili iweje? Kuna tuzo ya uongo wanapewa waongo? Huo ndio ukweli.
AZIZA: Mmmh! Basi mpe hongera baba yako.
Mimi: Zimefika.
Wakati mwingine haitakiwi kuwa mkweli kwa kila kitu. Tayari nilikwishaona kwamba kagundua kwamba sisi ni watu tunaoishi sehemu mbili tofauti, madaraja mawili tofauti na katika kichwa chake aliamini kwamba Tandale wanaishi watu masikini japo haikuwa hivyo. Nilichokuwa nikikifanya ni kuendana na akili yake alivyokuwa ameiweka, nami nikaanza kujifanya masikini ambaye sikubahatika kusoma kwa kuwa sikuwa na fedha ya kuniendeleza kielimu. Nikafanikiwa, kwa kiasi fulani aina ya maisha ambayo nilimpa yalimfanya kuamini kwamba kweli nilikuwa mtoto wa uswahilini, nilijivunia kuishi Tandale katika uwepo wake.
Maisha yalikuwa yakiendelea kama kawaida, kuhusu Aziza, wala sikuwa na wasiwasi kwa kuamini kwamba piga ua huyu mtoto ni lazima ningemchukua bila tatizo lolote lile. Kila siku nilikuwa nikiwasiliana nae, alikuwa akionekana kunikubali sana, chatting zangu zilizokuwa zikitabasamu zikaonekana kuuteka moyo wake. Nilikuwa na marafiki wengi facebook lakini nikikaa bila kuchati na Aziza sikuwa nikijisikia furaha kabisa.
INAENDELEA

